Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 47

Je, Utaendelea Kurekebishwa Upya?

Je, Utaendelea Kurekebishwa Upya?

“Mwishowe, akina ndugu, endeleeni kushangilia, kurekebishwa upya.”—2 KOR. 13:11.

WIMBO 54 “Hii Ndiyo Njia”

MUHTASARI *

1. Kulingana na Mathayo 7:13, 14, kwa nini tunaweza kusema kwamba tupo safarini?

SISI sote tuko safarini. Mahali tunakoelekea, au lengo letu, ni kuishi katika ulimwengu mpya chini ya utawala wenye upendo wa Yehova. Kila siku tunajitahidi kufuata njia inayoongoza kwenye uhai. Lakini kama Yesu alivyosema, barabara hiyo ina nafasi ndogo na nyakati nyingine si rahisi kuifuata. (Soma Mathayo 7:13, 14.) Sisi si wakamilifu na ni rahisi kwetu kuiacha barabara hiyo.—Gal. 6:1.

2. Tutachunguza nini katika makala hii? (Tazama pia sanduku “ Unyenyekevu Hutusaidia Kurekebisha Upya Hatua Zetu.”)

2 Ili tuendelee kubaki kwenye barabara yenye nafasi ndogo inayoongoza kwenye uzima, ni lazima tuwe tayari kurekebisha upya njia yetu ya kufikiri, mtazamo wetu, na matendo yetu. Mtume Paulo aliwatia moyo Wakristo waliokuwa wakiishi Korintho waendelee “kurekebishwa upya.” (2 Kor. 13:11) Ushauri huo unatuhusu sisi pia. Katika makala hii, tutazungumzia jinsi Biblia inavyoweza kutusaidia kurekebisha upya hatua zetu, na jinsi Wakristo wenzetu wakomavu wanavyoweza kutusaidia tubaki katika njia ya uzima. Pia, tutachunguza mambo yanayoweza kufanya isiwe rahisi kufuata mwongozo tunaopewa na tengenezo la Yehova. Tutaona jinsi unyenyekevu unavyoweza kutusaidia kufanya mabadiliko bila kupoteza shangwe yetu ya kumtumikia Yehova.

LIRUHUSU NENO LA MUNGU LIKUREKEBISHE

3. Neno la Mungu linaweza kukusaidiaje?

3 Tunapojitahidi kuchunguza mawazo na hisia zetu, tunakabili changamoto. Moyo wetu ni wenye hila, na hilo linaweza kufanya iwe vigumu kwetu kujua utatuongoza kufanya nini. (Yer. 17:9) Ni rahisi kwetu kujidanganya kwa “mawazo ya uwongo.” (Yak. 1:22) Hivyo, ni lazima tutumie Neno la Mungu kujichunguza. Neno la Mungu linafunua jinsi tulivyo kwa ndani, “fikira na makusudio” yaliyo ndani kabisa ya moyo wetu. (Ebr. 4:12, 13) Kwa njia ya mfano, Neno la Mungu ni kama mashine ya eksirei inayotuwezesha kuona kilicho ndani ya moyo wetu. Lakini ni lazima tuwe wanyenyekevu ikiwa tunataka kunufaika kutokana na ushauri tunaopata katika Biblia au kutoka kwa wawakilishi wa Mungu.

4. Ni Jambo gani linaloonyesha kwamba Mfalme Sauli alikuja kuwa na kiburi?

4 Mfano wa Mfalme Sauli unaonyesha kile kinachoweza kutokea ikiwa tutakosa unyenyekevu. Sauli alikuwa na kiburi sana hivi kwamba hangekubali, hata ndani ya moyo wake mwenyewe, kwamba mawazo na matendo yake yalihitaji kurekebishwa. (Zab. 36:1, 2; Hab. 2:4) Jambo hilo lilionekana wazi Yehova alipompa Sauli maagizo hususa kuhusu mambo aliyopaswa kufanya baada ya kuwashinda Waamaleki. Hata hivyo, Sauli hakumtii Yehova. Na nabii Samweli alipomwambia kuhusu kosa lake, Sauli hakukubali kwamba amekosea. Badala yake, alijaribu kujitetea kwa kupunguza uzito wa kosa lake la kutotii na kuwatupia wengine lawama. (1 Sam. 15:13-24) Mapema, Sauli alikuwa ameonyesha mtazamo kama huo. (1 Sam. 13:10-14) Inasikitisha kwamba Sauli aliruhusu moyo wake uwe na kiburi. Hakurekebisha njia yake ya kufikiri, hivyo Yehova alimkaripia na kumkataa.

5. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Sauli?

5 Ili tujifunze kutokana na mfano wa Sauli, ni vema tukajiuliza maswali haya: ‘Ninaposoma shauri kutoka katika Neno la Mungu, je, ninatafuta visingizio vya kutotumia shauri hilo? Je, ninapunguza uzito wa kosa ninalofanya? Je, ninamtupia lawama mtu mwingine?’ Ikiwa jibu letu ni ndiyo kwa swali lolote kati ya hayo, ni lazima turekebishe njia yetu ya kufikiri na mtazamo wetu. La sivyo, moyo wetu unaweza kuwa na kiburi sana hivi kwamba Yehova atakataa tusiwe rafiki zake.—Yak. 4:6.

6. Fafanua tofauti iliyopo kati ya Mfalme Sauli na Mfalme Daudi.

6 Ona tofauti iliyopo kati ya Mfalme Sauli na mrithi wake, Mfalme Daudi, mwanamume aliyependezwa na “sheria ya Yehova.” (Zab. 1:1-3) Daudi alijua kwamba Yehova huwaokoa walio wanyenyekevu lakini huwapinga wenye kiburi. (2 Sam. 22:28) Hivyo, Daudi aliruhusu sheria ya Mungu irekebishe njia yake ya kufikiri. Aliandika hivi: “Nitamsifu Yehova, ambaye amenipa ushauri. Hata wakati wa usiku, mawazo yangu ya ndani kabisa hunirekebisha.”—Zab. 16:7.

NENO LA MUNGU

Neno la Mungu hutuonya tunapokengeuka na kuiacha njia. Ikiwa sisi ni wanyenyekevu, tutaruhusu Neno la Mungu lirekebishe njia yetu ya kufikiri iliyopotoka (Tazama fungu la 7)

7. Tutafanya nini ikiwa sisi ni wanyenyekevu?

7 Ikiwa sisi ni wanyenyekevu tutaruhusu Neno la Mungu lirekebishe mawazo yetu mabaya kabla hayajatuongoza kufanya mambo mabaya. Neno la Mungu litakuwa kama sauti inayotuambia: “Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake.” Itatuonya tutakapokuwa tumetoka kwenye njia, iwe tumeenda kushoto au kulia. (Isa. 30:21) Tukimsikiliza Yehova tutajinufaisha kwa njia mbalimbali. (Isa. 48:17) Kwa mfano, tutaepuka aibu ya kusahihishwa na mtu mwingine. Na tutamkaribia zaidi Yehova kwa sababu tunatambua kwamba anatutendea kama watoto wapendwa.—Ebr. 12:7.

8. Kama inavyotajwa kwenye Yakobo 1:22-25, tunaweza kutumiaje Neno la Mungu kama kioo?

8 Tunaweza kutumia Neno la Mungu kama kioo. (Soma Yakobo 1:22-25.) Wengi wetu tunatumia kioo kila asubuhi kabla ya kuondoka nyumbani. Hivyo, tunaweza kuona marekebisho tunayohitaji kufanya kabla wengine hawajayaona. Vivyo hivyo, tunaposoma Neno la Mungu kila siku tutaona namna mbalimbali tunazoweza kurekebisha njia yetu ya kufikiri na mtazamo wetu. Wengi wanaona inafaa kusoma andiko la siku kila asubuhi kabla hawajaondoka nyumbani. Wanaruhusu mambo wanayosoma yarekebishe njia yao ya kufikiri. Kisha siku hiyo nzima, wanatafuta njia ambazo wanaweza kutumia shauri walilopata katika Neno la Mungu. Zaidi ya hilo, ni lazima tuwe na ratiba ya kujifunza inayotia ndani kusoma na kutafakari Neno la Mungu kila siku. Huenda hilo likaonekana kuwa jambo rahisi, lakini ni mojawapo ya mambo muhimu zaidi tunayoweza kufanya ili tuendelee kubaki katika barabara yenye nafasi ndogo inayoongoza kwenye uzima.

WASIKILIZE WAKRISTO WAKOMAVU

WAKRISTO WAKOMAVU

Huenda Mkristo mwenzetu aliye mkomavu akatuonya kwa fadhili. Je, tunashukuru kwamba rafiki yetu alikuwa na ujasiri wa kuzungumza nasi waziwazi? (Tazama fungu la 9)

9. Ni wakati gani ambapo huenda rafiki yako akahitaji kukurekebisha?

9 Je, umewahi kutembea kwenye njia iliyokuwa inakupeleka mbali na Yehova? (Zab. 73:2, 3) Ikiwa rafiki yako au Mkristo mkomavu alipata ujasiri wa kukurekebisha, je, ulimsikiliza na kutumia ushauri wake? Ikiwa ndivyo, ulifanya jambo linalofaa, na bila shaka unashukuru sana kwamba rafiki yako alikuonya.—Met. 1:5.

10. Unapaswa kuitikiaje ikiwa rafiki yako atakurekebisha?

10 Neno la Mungu linatukumbusha hivi: “Majeraha yanayosababishwa na rafiki ni ya uaminifu.” (Met. 27:6) Maneno hayo yanamaanisha nini? Fikiria mfano huu: Wazia kwamba unataka kuvuka barabara yenye magari mengi na kisha simu inakukengeusha. Unaanza kuvuka barabara bila kutazama magari. Halafu ghafla, rafiki yako anakushika mkono na kukuvuta nyuma. Anakushika kwa nguvu hivi kwamba anakuumiza mkono; lakini kwa kufanya hivyo anakuokoa usigongwe na gari. Hata kama utakuwa na maumivu kwa siku kadhaa, je, utakasirika kwa sababu rafiki yako alikuvuta kwa nguvu? Bila shaka la! Utathamini sana msaada wake. Vivyo hivyo, ikiwa rafiki yako atakuonya kwamba maneno au matendo yako hayapatani na viwango vya uadilifu vya Mungu, mwanzoni unaweza kuumia. Hata hivyo, usikasirike au kukwazika kwa sababu alikushauri. Huo utakuwa ujinga. (Mhu. 7:9) Badala yake, shukuru kwamba rafiki yako alikuwa na ujasiri wa kuzungumza nawe.

11. Kwa nini mtu anaweza kukataa shauri zuri kutoka kwa rafiki yake?

11 Kwa nini mtu anaweza kukataa shauri zuri kutoka kwa rafiki mwenye upendo? Kwa sababu ya kiburi. Watu wenye kiburi hupenda “masikio yao yafurahishwe. [Wanaacha] kuisikiliza ile kweli.” (2 Tim. 4:3, 4) Wanajiona kuwa bora kuliko wengine na wanaona maoni yao ndiyo ya maana zaidi. Hata hivyo, mtume Paulo aliandika hivi: “Mtu akifikiri yeye ni kitu wakati yeye si kitu, anajidanganya mwenyewe.” (Gal. 6:3) Mfalme Sulemani alifafanua jambo hilo vizuri sana. Aliandika hivi: “Ni afadhali mtoto maskini lakini mwenye hekima kuliko mfalme mzee lakini mpumbavu, ambaye hana tena ufahamu wa kutosha wa kutii onyo.”—Mhu. 4:13.

12. Tunajifunza nini kutokana na mfano uliwekwa na mtume Petro, kama inavyotajwa kwenye Wagalatia 2:11-14?

12 Fikiria mfano ambao mtume Petro alituwekea aliporekebishwa na mtume Paulo mbele za watu. (Soma Wagalatia 2:11-14.) Petro angeweza kumkasirikia Paulo ikiwa angekazia njia na mahali ambapo Paulo alitoa shauri hilo. Lakini Petro alikuwa na hekima. Alikubali shauri na hakuweka kinyongo dhidi ya Paulo. Isitoshe, baadaye Petro alimwita Paulo ‘ndugu mpendwa.’—2 Pet. 3:15.

13. Tunapaswa kuzingatia mambo gani tunapotoa shauri?

13 Ikiwa pindi fulani utahisi kwamba unahitaji kumshauri rafiki yako, unapaswa kukumbuka mambo gani? Kabla ya kuzungumza na rafiki yako, jiulize, ‘Je, mimi ni “mwadilifu kupita kiasi”?’ (Mhu. 7:16) Mtu aliye mwadilifu kupita kiasi anawahukumu wengine si kulingana na viwango vya Yehova, bali kulingana na viwango vyake mwenyewe, na huenda asiwe na rehema. Ikiwa baada ya kujichunguza unaona bado unahitaji kuzungumza na rafiki yako, mwonyeshe waziwazi tatizo na utumie maswali ya maoni ili kumsaidia atambue kosa lake. Hakikisha kwamba yale unayosema yanategemea Maandiko, ukikumbuka kwamba rafiki yako atatoa hesabu kwa Yehova na si kwako. (Rom. 14:10) Tegemea hekima inayopatikana katika Neno la Mungu, na unapotoa shauri, iga huruma ya Yesu. (Met. 3:5; Mt. 12:20) Kwa nini? Kwa sababu Yehova atashughulika nasi kwa njia ileile tunayoshughulika na wengine.—Yak. 2:13.

FUATA MWONGOZO UNAOTOLEWA NA TENGENEZO LA MUNGU

TENGENEZO LA YEHOVA

Tengenezo la Mungu linatuandalia machapisho, video, na mikutano inayotusaidia kutumia mashauri yaliyo katika Neno la Mungu. Nyakati nyingine, Baraza Linaloongoza hubadili jinsi kazi yetu inavyopangwa (Tazama fungu la 14)

14. Tengenezo la Mungu linatuandalia nini?

14 Yehova anatuongoza katika barabara ya uzima kupitia sehemu ya kidunia ya tengenezo lake ambalo linaandaa video, machapisho, na mikutano inayotusaidia sisi sote kutumia shauri linalopatikana katika Neno la Mungu. Mambo hayo yanategemea kabisa Maandiko. Baraza Linaloongoza linategemea roho takatifu linapoamua njia bora zaidi ya kutimiza kazi ya kuhubiri. Hata hivyo, mara kwa mara Baraza Linaloongoza hupitia tena maamuzi yake kuhusu jinsi kazi ya kuhubiri inavyofanywa. Kwa nini? Kwa sababu “tamasha ya ulimwengu huu inabadilika,” na ni lazima tengenezo la Mungu libadilike kulingana na hali mpya.—1 Kor. 7:31.

15. Baadhi ya wahubiri wamekabili changamoto gani?

15 Bila shaka, sisi huwa tayari kufuata mwongozo unaotegemea Biblia tunaopokea kuhusu mafundisho na viwango vya maadili. Lakini tunaitikiaje wakati tengenezo la Mungu linapofanya mabadiliko yanayoathiri sehemu nyingine za maisha yetu? Kwa mfano, katika miaka ya karibuni, gharama za kujenga na kudumisha sehemu za ibada zimeongezeka sana. Hivyo, Baraza Linaloongoza limeelekeza kwamba Majumba ya Ufalme yatumike kikamili. Kutokana na marekebisho hayo baadhi ya makutaniko yameunganishwa na Majumba ya Ufalme kuuzwa. Pesa zinazopatikana zinasaidia kujenga majumba katika maeneo ambayo yana uhitaji mkubwa zaidi. Ikiwa unaishi eneo ambalo Majumba ya Ufalme yanauzwa na makutaniko yanaunganishwa, huenda ikawa vigumu kuzoea hali hiyo mpya. Sasa, baadhi ya wahubiri wanahitaji kusafiri umbali mrefu zaidi ili kuhudhuria mikutano. Huenda wengine ambao walifanya kazi kwa bidii ili kujenga au kudumisha Jumba la Ufalme wakashangaa kwa nini jumba hilo linauzwa. Huenda wakahisi kwamba muda na jitihada zao zimepotea bure. Licha ya hayo, wanaunga mkono mpango huo mpya na wanapaswa kupongezwa.

16. Kutumia shauri linalopatikana kwenye Wakolosai 3:23, 24 kutatusaidiaje kudumisha shangwe yetu?

16 Tutadumisha shangwe yetu ikiwa tunakumbuka kwamba kazi yote tunayofanya ni kwa ajili ya Yehova na kwamba yeye ndiye anayeongoza tengenezo lake. (Soma Wakolosai 3:23, 24.) Mfalme Daudi alituwekea mfano mzuri alipotoa mchango ili kujenga hekalu. Alisema hivi: “Mimi ni nani na watu wangu ni nani hivi kwamba tukutolee matoleo haya ya hiari? Kwa maana kila kitu kinatoka kwako, nasi tumekupa vitu vinavyotoka mkononi mwako mwenyewe.” (1 Nya. 29:14) Tunapotoa mchango, sisi pia tunampa Yehova vitu vinavyotoka mkononi mwake mwenyewe. Hata hivyo, Yehova anathamini muda, nguvu, na mali tunazotoa ili kutegemeza kazi anayotaka ifanywe.—2 Kor. 9:7.

BAKI KWENYE BARABARA YENYE NAFASI NDOGO

17. Kwa nini hupaswi kuvunjika moyo ikiwa unahisi kwamba unahitaji kurekebisha upya hatua zako?

17 Ili kubaki kwenye barabara yenye nafasi ndogo inayoongoza kwenye uzima, ni lazima sisi sote tufuate hatua za Yesu kwa ukaribu. (1 Pet. 2:21) Ukiona kwamba unahitaji kurekebisha upya hatua zako, usivunjike moyo. Kwa kweli, huenda hiyo ikawa ishara nzuri inayoonyesha kwamba unataka kufuata mwongozo wa Yehova. Kumbuka kwamba tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, Yehova hatarajii tuige mfano wa Yesu kikamilifu kwa sasa.

18. Ni lazima tufanye nini ili tufikie lengo letu?

18 Acheni sisi sote tukazie fikira wakati ujao na tuwe tayari kurekebisha njia yetu ya kufikiri, mtazamo wetu, na matendo yetu. (Met. 4:25; Luka 9:62) Na tuendelee kuwa wanyenyekevu, “[tuendelee] kushangilia, na kurekebishwa upya.” (2 Kor. 13:11) Ikiwa tutafanya hivyo, “Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja [nasi].” Na hatutafika tu tunakoelekea, bali pia tutafurahia safari yetu.

WIMBO 34 Kutembea kwa Utimilifu

^ fu. 5 Huenda isiwe rahisi kwa baadhi yetu kufanya mabadiliko katika njia yetu ya kufikiri, mtazamo wetu, na matendo yetu. Makala hii itazungumzia kwa nini tunahitaji kufanya mabadiliko na jinsi tunavyoweza kuendelea kudumisha shangwe yetu tunapofanya mabadiliko hayo.

^ fu. 76 MAELEZO YA PICHA: Ndugu kijana anaposimulia jambo lililotokea baada ya kufanya uamuzi mbaya, ndugu mwenye umri mkubwa (kulia) anasikiliza kwa utulivu ili kuona ikiwa anahitaji kutoa shauri fulani.