Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 48

Tazama Mbele Moja kwa Moja Kwenye Wakati Ujao

Tazama Mbele Moja kwa Moja Kwenye Wakati Ujao

“Macho yako yanapaswa kutazama mbele moja kwa moja, naam, yakaze macho yako moja kwa moja mbele yako.”​—MET. 4:25.

WIMBO 77 Nuru Katika Ulimwengu Wenye Giza

MUHTASARI *

1-2. Tunaweza kutumiaje ushauri tunaopata kwenye Methali 4:25? Toa mfano.

FIKIRIA visa vifuatavyo. Dada Mkristo mwenye umri mkubwa anatafakari mambo mazuri aliyofurahia wakati uliopita. Hata ingawa kwa sasa maisha yake yana changamoto, anaendelea kufanya yote anayoweza ili kumtumikia Yehova. (1 Kor. 15:58) Kila siku anajiwazia akiwa na wapendwa wake wakiishi pamoja katika ulimwengu mpya ulioahidiwa. Dada mwingine anakumbuka kwamba aliumizwa na mwamini mwenzake, lakini anaamua kutoweka kinyongo. (Kol. 3:13) Ndugu anakumbuka makosa yake ya wakati uliopita, lakini anakazia fikira kuendelea kuwa mwaminifu kwa Yehova.​—Zab. 51:10.

2 Wakristo hao watatu wana hali gani zinazofanana? Wote wanakumbuka mambo yaliyotukia wakati uliopita, lakini hawakazii fikira kupita kiasi mambo hayo. Badala yake, ‘wanatazama mbele moja kwa moja’ kwenye wakati ujao.​—Soma Methali 4:25.

3. Kwa nini tunahitaji “kutazama mbele moja kwa moja” kwenye wakati ujao?

3 Kwa nini ni muhimu “kutazama mbele moja kwa moja” kwenye wakati ujao? Kama vile tu ambavyo mtu hawezi kutembea kwenye mstari ulionyooka ikiwa anatazama nyuma mara kwa mara, hatuwezi kusonga mbele kwenye utumishi wa Yehova ikiwa tunakazia fikira tena na tena mambo ya wakati uliopita.—Luka 9:62.

4. Tutachunguza nini katika makala hii?

4 Katika makala hii, tutazungumzia mitego mitatu inayoweza kutufanya tukazie fikira kupita kiasi mambo yaliyopita. * Nayo ni: (1) kutamani maisha yetu ya zamani, (2) kuweka kinyongo, na (3) kuhisi hatia kupita kiasi. Katika kila hali, tutaona jinsi ambavyo kanuni za Biblia zinaweza kutusaidia tusikazie fikira “mambo ya nyuma,” bali tujinyooshe kuelekea “mambo yaliyo mbele.”​—Flp. 3:13.

MTEGO WA KUTAMANI MAISHA YETU YA ZAMANI

Ni nini kinachoweza kutuzuia kutazama mbele moja kwa moja kwenye wakati ujao? (Tazama fungu la 5, 9 na 13) *

5. Mhubiri 7:10 inatuonya kuhusu mtego gani?

5 Soma Mhubiri 7:10. Ona kwamba mstari huu hausemi kwamba ni vibaya kujiuliza: “Mbona siku za zamani zilikuwa nzuri?” Kumbukumbu nzuri ni zawadi kutoka kwa Yehova. Badala yake, mstari huo unasema: “Usiulize, ‘Mbona siku za zamani zilikuwa bora kuliko hizi?’” Kwa maneno mengine, mtego ni kulinganisha hali zetu za zamani na hali zetu za sasa, na kufikia mkataa kwamba sasa kila kitu ni kibaya. Mstari huo unasomeka hivi kwenye tafsiri nyingine: “Usiulize, ‘Kwa nini nyakati za kale zilikua bora kuliko za sasa?’ Huulizi hivyo kwa kutumia hekima.”

Waisraeli walifanya kosa gani baada ya kuondoka Misri? (Tazama fungu la 6)

6. Kwa nini si jambo la hekima kuendelea kufikiri kwamba maisha yetu yalikuwa mazuri zaidi wakati uliopita? Toa mfano.

6 Kwa nini si jambo la hekima kuendelea kufikiria kwamba maisha yetu yalikuwa bora zaidi wakati uliopita? Kutamani maisha yetu ya zamani kunaweza kutufanya tukumbuke tu mambo mazuri ya wakati uliopita. Au, kunaweza kutufanya tupuuze hali ngumu tulizokuwa tukipitia. Fikiria mfano wa Waisraeli wa kale. Baada ya kuondoka Misri, walisahau haraka sana jinsi maisha yalivyokuwa magumu nchini humo. Isitoshe, walikazia fikira chakula kizuri walichofurahia huko. Walisema hivi: “Tunakumbuka sana samaki wa bure tuliokuwa tukila nchini Misri, pamoja na matango, matikiti, vitunguu vya majani, vitunguu maji, na vitunguu saumu!” (Hes. 11:5) Lakini, je, ni kweli kwamba chakula walichokuwa wanakula kilikuwa cha “bure”? Hapana. Waisraeli walilipia gharama kubwa sana; wakati huo, walikuwa wakikandamizwa sana wakiwa watumwa nchini Misri. (Kut. 1:13, 14; 3:6-9) Licha ya hilo, baadaye walisahau kuhusu hali ngumu walizokuwa wamepitia na wakatamani mambo ya wakati uliopita. Walichagua kukazia fikira maisha yaliyopita ambayo walidhani yalikuwa mazuri, badala ya kukazia fikira mambo mazuri ambayo Yehova alikuwa tu ametoka kuwafanyia. Yehova hakupendezwa na mtazamo wao.​—Hes. 11:10.

7. Ni nini kilichomsaidia dada mmoja aepuke mtego wa kutamani maisha yake ya zamani?

7 Tunaweza kuepukaje kunaswa na mtego wa kutamani maisha yetu ya zamani? Fikiria mfano wa dada ambaye alianza kutumikia katika Betheli ya Brooklyn mwaka wa 1945. Miaka kadhaa baadaye, alifunga ndoa na Mwanabetheli mwenzake, nao waliendelea kutumikia hapo kwa miaka mingi. Hata hivyo, katika mwaka wa 1976, mume wake alianza kuugua. Dada huyo alisema kwamba mume wake alipotambua kuwa alikaribia kufa, alimpa ushauri mzuri ambao ungemsaidia kukabiliana na ujane. Mume wake alimwambia hivi: “Tumekuwa na ndoa yenye furaha. Wengi hawapati furaha kama hiyo katika ndoa.” Lakini pia alimsihi hivi: “Usiendelee kukazia fikira kupita kiasi mambo yaliyopita, ingawa utakuwa na kumbukumbu hizo. Utapona kadiri siku zinavyosonga. Usiwe mwenye uchungu na kujisikitikia. Shangilia kwamba umepata furaha na baraka hizo. . . . Kumbukumbu ni zawadi ambazo Mungu ametupatia.” Je, hukubali kwamba huo ulikuwa ushauri mzuri?

8. Dada yetu alinufaikaje kwa kutokazia fikira kupita kiasi mambo yaliyopita?

8 Dada yetu alifuata ushauri wa mume wake. Alimtumikia Yehova kwa uaminifu hadi alipokufa akiwa na umri wa miaka 92. Miaka michache kabla ya kifo chake, alisema hivi: “Ninapokumbuka miaka 63 ambayo nimemtumikia Yehova katika utumishi wa wakati wote, ninaweza kusema kwamba maisha yangu yamekuwa yenye kuridhisha.” Kwa nini? Alieleza hivi: “Jambo linalofanya maisha yawe yenye kuridhisha ni undugu wetu mzuri na tumaini la kuishi na ndugu na dada zetu katika Paradiso duniani, tukimtumikia milele Muumba wetu Mkuu, Mungu wa pekee wa kweli, Yehova.” * Huo ni mfano mzuri sana wa mtu aliyetazama mbele moja kwa moja kwenye wakati ujao!

MTEGO WA KUWEKA KINYONGO

9. Kama andiko la Mambo ya Walawi 19:18 linavyoonyesha, ni wakati gani ambapo huenda ikawa vigumu kumsamehe mtu aliyetukosea?

9 Soma Mambo ya Walawi 19:18. Mara nyingi ni vigumu kuweka kinyongo ikiwa mtu aliyetukosea ni mwabudu mwenzetu, rafiki wa karibu, au mtu wetu wa ukoo. Kwa mfano, dada fulani alishtakiwa kimakosa na mwabudu mwenzake kwamba alimwibia pesa. Baadaye, dada aliyekuwa amemshtaki mwenzake alimwomba msamaha, lakini dada aliyekuwa ameshtakiwa kimakosa alishindwa kuacha kufikiria jambo hilo. Je umewahi kuhisi hivyo? Hata kama hujawahi kukabiliana na hali iliyo sawa na hiyo, inaelekea wengi wetu tumewahi kumwekea mtu kinyongo na kuhisi kwamba hatuwezi kamwe kumsamehe yule aliyetukosea.

10. Ni nini kinachoweza kutusaidia tunapohisi tumemwekea mtu kinyongo?

10 Ni nini kinachoweza kutusaidia tunapohisi tumemwekea mtu kinyongo? Ni lazima tukumbuke kwamba Yehova anaona kila kitu. Anaona kila jambo tunalopitia, kutia ndani ukosefu wowote wa haki tunaotendewa. (Ebr. 4:13) Anaumia tunapoteseka. (Isa. 63:9) Na anaahidi kwamba mwishowe ataondoa madhara yoyote tunayopata kwa sababu ya kutendewa isivyo haki.​—Ufu. 21:3, 4.

11. Tunajinufaishaje sisi wenyewe tunapowasamehe wengine?

11 Pia, tungependa kukumbuka kwamba tunapowasamehe wengine tunajinufaisha sisi wenyewe. Hivyo ndivyo dada aliyekuwa ameshtakiwa kimakosa alivyokuja kutambua. Baada ya muda, dada huyo aliweza kusamehe. Alitambua kwamba tunapowasamehe wengine, Yehova anatusamehe pia. (Mt. 6:14) Hakupuuza au kupunguza uzito wa jambo ambalo mwamini mwenzake alikuwa amefanya, bali alichagua kusamehe. Matokeo ni kwamba dada yetu alikuwa na furaha zaidi na aliweza kukazia fikira utumishi wake kwa Yehova.

MTEGO WA KUHISI HATIA KUPITA KIASI

12. Andiko la 1 Yohana 3:19, 20 linatufundisha nini?

12 Soma 1 Yohana 3:19, 20. Sisi sote huhisi hatia nyakati fulani. Kwa mfano, baadhi ya watu huhisi hatia kwa sababu ya mambo waliyofanya kabla hawajajifunza kweli. Wengine wanahisi hatia kwa sababu ya makosa waliyofanya baada ya kubatizwa. Kuhisi hatia ni jambo la kawaida. (Rom. 3:23) Bila shaka, tungependa kufanya yaliyo sawa. Lakini “sisi sote hujikwaa mara nyingi.” (Yak. 3:2; Rom. 7:21-23) Ingawa hatufurahii kuhisi hatia, hisia hizo zinaweza kuwa na faida. Kwa nini? Kwa sababu hisia za hatia zinaweza kutuchochea turekebishe njia yetu na kuazimia kutorudia tena makosa yetu.​—Ebr. 12:12, 13.

13. Kwa nini tunahitaji kujilinda dhidi ya mtego wa kuhisi hatia kupita kiasi?

13 Kwa upande mwingine, tunaweza kuhisi hatia kupita kiasi, yaani, kuendelea kuhisi hatia hata baada ya kutubu na baada ya Yehova kutuonyesha kwamba ametusamehe. Kuhisi hatia kwa njia hiyo kunaweza kutuletea madhara. (Zab. 31:10; 38:3, 4) Jinsi gani? Fikiria mfano wa dada mmoja aliyepambana na hisia za hatia kutokana na dhambi alizofanya wakati uliopita. Anasema hivi: “Nilihisi kwamba sihitaji kujitoa kwa bidii zaidi katika utumishi wa Yehova kwa sababu inaelekea sitaokolewa.” Huenda wengi wetu tukahisi kama dada yetu alivyohisi. Ni muhimu sana tujilinde dhidi ya mtego wa kuhisi hatia kupita kiasi. Zaidi ya hayo, hebu fikiria jinsi Shetani atakavyofurahi ikiwa tutakata tamaa hata ingawa Yehova ametusamehe!​—Linganisha 2 Wakorintho 2:5-7, 11.

14. Tunawezaje kuwa na uhakika kwamba Yehova anataka kutusamehe?

14 Hata hivyo, huenda bado tukajiuliza, ‘Ninawezaje kuwa na uhakika kwamba Yehova amenisamehe?’ Ikiwa unajiuliza swali hilo, jambo hilo linaonyesha kwamba Yehova anaweza kukusamehe. Miaka mingi iliyopita, gazeti Mnara wa Mlinzi lilisema hivi: “Tunaweza kujikuta tukijikwaa na kuanguka mara nyingi juu ya tabia fulani mbaya ambayo [imekita sana kwenye] mtindo wetu wa maisha ya zamani kuliko tulivyokuwa tumetambua. . . . Usikate tamaa. Usikate kauli kwamba umetenda dhambi isiyoweza kusameheka. Hivyo ndivyo Shetani anavyotaka ufikiri. Jambo la kwamba una huzuni na [umejikasirikia] ni uthibitisho kwamba hujaenda mbali sana. Usichoke kumgeukia Mungu kwa unyenyekevu na kwa bidii, ukitafuta msamaha na usafishaji na msaada wake. Mwendee kama vile mtoto humwendea baba yake anapokuwa na matatizo, hata iwe ni mara ngapi juu ya udhaifu uleule, na kwa neema Yehova atakusaidia kwa sababu ya fadhili zake zisizostahiliwa.” *

15-16. Baadhi ya watu wamehisije walipotambua kwamba Yehova amewasamehe?

15 Watu wengi wa Yehova wamepata faraja kwa kutambua kwamba Yehova amewasamehe. Kwa mfano, ndugu mmoja alichochewa na simulizi lililochapishwa katika mfululizo wa makala, “Biblia Inabadili Maisha.” Katika makala hiyo, dada mmoja alisema kwamba kwa sababu ya makosa aliyofanya wakati uliopita, ilikuwa vigumu kwake kuamini kwamba Yehova angeweza kumpenda. Aliendelea kupambana na hisia hizo miaka mingi baada ya kubatizwa. Hata hivyo, baada ya kutafakari kuhusu fidia, alianza kuona mambo kwa njia tofauti. *

16 Simulizi hilo lilimsaidiaje ndugu huyo? Aliandika hivi: “Nilipokuwa kijana nilikuwa nikipambana na uraibu wa kutazama ponografia. Hivi karibuni, nilianza tena kutazama ponografia. Niliomba msaada kutoka kwa wazee Wakristo na nimefanya maendeleo katika kushinda tatizo langu. Wazee wamenisaidia niamini kwamba Mungu ananipenda na anataka kunisamehe. Hata hivyo, bado nyakati nyingine ninahisi sifai, kana kwamba Yehova hawezi kunipenda. Kusoma simulizi la dada huyo kumenisaidia sana. Sasa ninatambua kuwa ninapofikiri kwamba Mungu hawezi kunisamehe, ni kana kwamba ninasema dhabihu ya Mwana wake haitoshi kufunika dhambi zangu. Nimekata makala hiyo ili niweze kuisoma na kutafakari wakati wowote ninapohisi kwamba Yehova hanipendi.”

17. Mtume Paulo aliepukaje kunaswa na mtego wa kuhisi hatia kupita kiasi?

17 Masimulizi kama haya yanatukumbusha kuhusu mtume Paulo. Kabla ya kuwa Mkristo alifanya dhambi nyingi nzito. Paulo alikumbuka mambo aliyofanya awali, lakini hakuyakazia fikira kupita kiasi. (1 Tim. 1:12-15) Aliiona fidia kuwa zawadi ya kibinafsi kwa ajili yake. (Gal. 2:20) Hivyo, Paulo aliepuka mtego wa kuhisi hatia kupita kiasi na alianza kukazia fikira kumpa Yehova kilicho bora zaidi kuanzia wakati huo na kuendelea.

KAZIA FIKIRA WAKATI UJAO!

Acheni tuazimie kukazia fikira wakati ujao (Tazama fungu la 18 na 19) *

18. Tumejifunza nini katika makala hii?

18 Tumejifunza nini baada ya kuchunguza mitego iliyozungumziwa katika makala hii? (1) Kumbukumbu nzuri ni baraka kutoka kwa Yehova, lakini hata maisha yetu yawe yalikuwa mazuri kadiri gani wakati uliopita, wakati wetu ujao katika ulimwengu mpya utakuwa bora zaidi. (2) Wengine wanaweza kutuumiza, lakini tunapochagua kusamehe, tutaweza kusonga mbele. (3) Kuhisi hatia kupita kiasi kunaweza kutuzuia kumtumikia Yehova kwa shangwe. Hivyo, kama Paulo tunahitaji kuamini kwamba Yehova ametusamehe.

19. Tunajuaje kwamba katika ulimwengu mpya hatutasumbuliwa na hisia za majuto kuhusu mambo yaliyopita?

19 Tuna tarajio la kuishi milele. Katika ulimwengu mpya wa Mungu hatutasumbuliwa na hisia za majuto kuhusu wakati uliopita. Biblia inasema hivi kuhusu wakati ujao: “Mambo ya zamani hayataingia tena akilini.” (Isa. 65:17) Hebu fikiria: Baadhi yetu umri umesonga tukiwa katika utumishi wa Yehova, lakini katika ulimwengu mpya tutakuwa vijana tena. (Ayu. 33:25) Hivyo basi, acheni tuazimie kutokazia fikira kupita kiasi mambo yaliyopita. Badala yake, acheni tutazamie wakati ujao na kukazia fikira mambo mazuri yaliyo mbele yetu!

WIMBO 142 Kushikilia Tumaini Letu

^ fu. 5 Si vibaya kukumbuka mambo ya wakati uliopita. Lakini hatutaki kufikiria sana mambo yaliyopita hivi kwamba tushindwe kufurahia kikamili mambo ya wakati huu, au tusahau mambo yatakayotokea wakati ujao. Makala hii inazungumzia mitego mitatu inayoweza kutufanya tukazie fikira kupita kiasi mambo yaliyopita. Tutachunguza kanuni za Biblia na mifano ya kisasa ambayo inaweza kutusaidia tuepuke kunaswa katika mitego hiyo.

^ fu. 4 UFAFANUZI WA MANENO: Katika makala hii maneno “kukazia fikira kupita kiasi mambo yaliyopita” yanamaanisha kuendelea kutafakari kuhusu wakati wetu uliopita, yaani, kuuzungumzia tena na tena, kukumbuka sana maisha yaliyopita, au kufikiria kwamba maisha yalikuwa mazuri zaidi wakati huo kuliko sasa.

^ fu. 14 Tazama gazeti la Mnara wa Mlinzi, la Desemba 1, 1995, ukurasa wa 11.

^ fu. 59 MAELEZO YA PICHA: Kutamani maisha yetu ya zamani, kuweka kinyongo, na kuhisi hatia kupita kiasi ni kama mizigo mizito tunayokokota inayotuzuia tusiendelee kusonga mbele katika njia ya uzima.

^ fu. 66 MAELEZO YA PICHA: Baada ya kuacha kukokota hisia hizo zilizo kama mizigo mizito, tunakuwa na furaha, tunajihisi huru, na tunapata nguvu mpya. Kisha tutaweza kutazama mbele kwenye wakati ujao.