Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

“Yehova Ameendelea Kunikumbuka”

“Yehova Ameendelea Kunikumbuka”

NINAISHI Orealla, kijiji cha Wahindi Waamerika chenye watu karibu 2000, kilicho nchini Guyana, Amerika Kusini. Kijiji hicho kiko mbali sana na kinaweza kufikiwa tu kwa kutumia ndege ndogo, au boti.

Nilizaliwa mwaka wa 1983. Miaka ya mwanzoni ya maisha yangu nilikuwa mtoto mwenye afya, lakini nilipofikisha umri wa miaka kumi, nilianza kuhisi maumivu makali sana mwili mzima. Miaka miwili hivi baadaye, nilipoamka asubuhi moja, sikuweza kunyanyuka. Nilijaribu kunyanyua miguu yangu kwa uwezo wangu wote, lakini haikuwa na nguvu. Tangu siku hiyo, sijawahi kutembea tena. Ugonjwa wangu pia ulisababisha nisiendelee kukua. Leo, bado umbo langu ni kama la mtoto mdogo.

Mashahidi wawili wa Yehova walipofika nyumbani, sikuwa nimetoka nyumbani kwa miezi kadhaa. Kwa kawaida, wageni walipotembelea nyumbani nilijificha, lakini siku hiyo niliwaruhusu wanawake hao wazungumze nami. Walipokuwa wakizungumza kuhusu Paradiso, nilikumbuka jambo nililosikia nilipokuwa na umri wa miaka mitano hivi. Wakati huo, mmishonari aliyeitwa Jethro, aliyekuwa anaishi Suriname, alitembelea kijiji chetu mara moja kwa mwezi ili kujifunza Biblia pamoja na baba yangu. Jethro alinitendea kwa fadhili sana. Nilimpenda sana. Pia, babu na nyanya (bibi) yangu walienda pamoja nami kwenye baadhi ya mikutano ya Mashahidi iliyofanywa kijijini kwetu. Hivyo, Florence, mmoja kati ya wanawake walionitembelea, aliponiuliza ikiwa ningependa kujifunza mengi zaidi, nilijibu ndiyo.

Florence alirudi na Justus, mume wake, nao wakajifunza Biblia pamoja nami. Walipotambua kwamba sikujua kusoma, walinisaidia nijifunze kusoma. Baada ya muda, niliweza kusoma mwenyewe. Siku moja, wenzi hao wa ndoa waliniambia kwamba walikuwa wamepewa mgawo wa kwenda kutumikia nchini Suriname. Inasikitisha kwamba hakukuwa na mtu kijijini kwetu ambaye angeweza kuendelea kujifunza nami Biblia. Lakini ninafurahi kwamba Yehova aliendelea kunikumbuka.

Baada ya muda mfupi, painia aliyeitwa Floyd aliwasili kijijini kwetu, na alikutana nami alipokuwa akihubiri kutoka nyumba moja ya nyasi hadi nyingine. Aliponiambia kuhusu kujifunza Biblia, nilitabasamu. Akaniuliza: “Kwa nini unatabasamu?” Nilimwambia kwamba tayari nilikuwa nimemaliza kujifunza broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? na nilikuwa nimeanza kujifunza kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. * Nilimweleza kwa nini sikuwa ninaendelea kujifunza. Floyd alijifunza pamoja nami sehemu iliyobaki ya kitabu Ujuzi, lakini baadaye yeye pia alipewa mgawo wa kwenda kutumikia mahali pengine. Kwa mara nyingine tena, sikuwa na mwalimu wa Biblia.

Hata hivyo, mwaka wa 2004, mapainia wa pekee wawili, Granville na Joshua walipewa mgawo wa kuhubiri Orealla. Walihubiri kutoka nyumba moja ya nyasi hadi nyingine, nao wakanipata. Waliponiuliza ikiwa ningependa kujifunza, nilitabasamu. Niliomba wajifunze nami kitabu Ujuzi kuanzia mwanzo. Nilitaka kujua ikiwa wangenifundisha mambo yaleyale ambayo walimu wangu wa awali walinifundisha. Granville aliniambia kwamba mikutano ilikuwa ikifanywa kijijini hapo. Ingawa sikuwa nimetoka nyumbani kwa miaka kumi, nilitaka kuhudhuria. Hivyo, Granville alikuja nyumbani, akaniweka kwenye kiti cha magurudumu na kunisukuma hadi Jumba la Ufalme.

Baada ya muda, Granville alinitia moyo nijiandikishe kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Alisema hivi: “Wewe huwezi kutembea, lakini unaweza kuzungumza. Siku moja, utatoa hotuba ya watu wote. Bila shaka hilo litatukia.” Maneno yake yalinitia moyo na kunifanya nijiamini.

Nilianza kushiriki katika kazi ya kuhubiri na Granville. Lakini barabara nyingi kijijini zilikuwa za vumbi na zilikuwa na mashimo mengi, hivyo nisingeweza kutumia kiti cha magurudumu. Basi nilimwomba Granville anisukume kwenye toroli. Mpango huo ulifaa sana. Nilibatizwa Aprili 2005. Muda mfupi baada ya hapo, akina ndugu walinizoeza kushughulikia machapisho ya kutaniko na mfumo wa sauti katika Jumba la Ufalme.

Inasikitisha kwamba mwaka wa 2007, baba yangu alikufa katika aksidenti ya boti. Familia yetu ilihuzunika sana. Granville alisali kwa ajili yetu na kutufariji kupitia maandiko mbalimbali. Miaka miwili baadaye, tulishtushwa sana na msiba mwingine—Granville alikufa katika aksidenti ya boti.

Kutaniko letu dogo lililokuwa linaomboleza, liliachwa bila mzee na lilikuwa na mtumishi mmoja tu wa huduma. Kifo cha Granville kiliniumiza sana, alikuwa rafiki mpendwa. Alinisaidia kushughulikia mahitaji yangu ya kiroho na ya kimwili kwa uaminifu. Mkutano uliofuata baada ya kifo chake, nilikuwa na mgawo wa kusoma mafungu kwenye funzo la Mnara wa Mlinzi. Nilifanikiwa kusoma mafungu mawili ya kwanza, lakini baada ya hapo nilianza kulia na machozi yaliendelea kutiririka tu. Nililazimika kuondoka jukwaani.

Huzuni yangu ilianza kupungua akina ndugu kutoka kutaniko lingine walipokuja Orealla ili kutusaidia. Pia, ofisi ya tawi ilimtuma painia wa pekee anayeitwa Kojo. Nilifurahi sana mama yangu na ndugu yangu mdogo walipoanza kujifunza Biblia na kubatizwa. Kisha, mwezi wa Machi 2015, niliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa huduma. Baada ya muda, nilitoa hotuba yangu ya kwanza ya watu wote. Siku hiyo, nilitabasamu na kulia kwa machozi ya shukrani nilipokumbuka maneno ambayo Granville aliniambia miaka mingi iliyopita: “Siku moja, utatoa hotuba ya watu wote. Bila shaka hilo litatukia.”

Kupitia programu za JW Broadcasting® nimeona ndugu na dada ambao wana hali kama zangu. Licha ya matatizo ya afya waliyonayo, wanaweza kutimiza mambo mengi maishani na wana furaha. Kwa upande wangu, bado ninaweza kufanya baadhi ya mambo. Tamaa yangu ya kumpa Yehova nguvu zozote nilizo nazo, ilinichochea niwe painia wa kawaida. Na mwezi wa Septemba 2019, nilipokea habari nzuri sana ambazo sikutarajia! Mwezi huo niliwekwa rasmi kutumikia nikiwa mzee katika kutaniko letu lenye wahubiri 40 hivi.

Ninawashukuru sana ndugu na dada wapendwa ambao walijifunza nami na kunisaidia kutimiza huduma yangu. Zaidi ya yote, ninashukuru sana kwamba Yehova aliendelea kunikumbuka.

^ fu. 8 Vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini sasa havichapishwi tena.