Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 49

Tumaini la Ufufuo Ni Hakika!

Tumaini la Ufufuo Ni Hakika!

“Ninatumaini kwa Mungu . . . kwamba kutakuwa na ufufuo.”​—MDO. 24:15.

WIMBO 151 Ataita

MUHTASARI *

1-2. Waabudu wa kweli wana tumaini gani zuri?

TUMAINI ni sifa muhimu sana. Baadhi ya watu wanatumaini au kutarajia kwamba watakuwa na ndoa yenye furaha, watalea watoto wenye afya, au watapona kutokana na ugonjwa fulani mbaya. Tukiwa Wakristo huenda tunatamani kuwa na mambo hayo pia. Lakini tumaini tunalothamini zaidi linapita mambo hayo; linatia ndani wakati wetu ujao wa milele na pia wakati ujao wa wapendwa wetu waliokufa.

2 Mtume Paulo alisema hivi: “Nina tumaini kwa Mungu . . . kwamba kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Mdo. 24:15) Paulo hakuwa mtu wa kwanza kuzungumzia tumaini la ufufuo. Mzee wa ukoo Ayubu, alizungumza kuhusu tumaini hilo pia. Alikuwa na uhakika kwamba Mungu angemkumbuka na kumfufua ili aishi tena.—Ayu. 14:7-10, 12-15.

3. Andiko la 1 Wakorintho sura ya 15 linaweza kutusaidia jinsi gani?

3 “Kufufuliwa kwa wafu” ni sehemu ya “fundisho la msingi” la mafundisho yote ya Kikristo. (Ebr. 6:1, 2) Mazungumzo ya Paulo kuhusu ufufuo yameandikwa katika 1 Wakorintho sura ya 15. Ni lazima mambo aliyoandika yaliwaimarisha Wakristo wa karne ya kwanza. Na sura hiyo inaweza kutujenga na kuimarisha tumaini ambalo tumekuwa nalo kwa muda mrefu.

4. Msingi wa kuamini kwamba wapendwa wetu waliokufa watafufuliwa ni nini?

4 Ufufuo wa Yesu Kristo unatupatia msingi au uhakika wa kwamba kutakuwa na ufufuo wa wapendwa wetu waliokufa. Ufufuo huo ulikuwa sehemu ya “habari njema” ambayo Paulo aliwatangazia Wakorintho. (1 Kor. 15:1, 2) Isitoshe, alisema kwamba ikiwa Mkristo hakuamini kwamba kuna ufufuo, imani yake ingekuwa bure. (1 Kor. 15:17) Imani katika ufufuo wa Yesu ndio msingi wa tumaini letu la Kikristo.

5-6. Maneno yanayopatikana kwenye 1 Wakorintho 15:3, 4 yanamaanisha nini kwetu?

5 Mwanzoni mwa mazungumzo yake kuhusu ufufuo, Paulo alitaja mambo matatu ya kweli. Nayo ni (1) “Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu.” (2) “Alizikwa.” (3) “Alifufuliwa siku ya tatu kulingana na Maandiko.”—Soma 1 Wakorintho 15:3, 4.

6 Kufa kwa Yesu, kuzikwa, na kufufuliwa kwake kunamaanisha nini kwetu? Nabii Isaya alitabiri kwamba Masihi ‘angeondolewa katika nchi ya walio hai’ na ‘angepewa kaburi pamoja na waovu.’ Hata hivyo, mengi zaidi yalihusika. Isaya aliongeza kwamba Masihi ‘angebeba dhambi ya watu wengi.’ Yesu alifanya hivyo alipotoa uhai wake kuwa fidia. (Isa. 53:8, 9, 12; Mt. 20:28; Rom. 5:8) Hivyo kufa, kuzikwa, na kufufuliwa kwa Yesu kunatupatia msingi imara wa tumaini letu la kuwekwa huru kutokana na dhambi na kifo na kuungana tena na wapendwa wetu waliokufa.

USHAHIDI KUTOKA KWA WATU WENGI

7-8. Ni nini kinachowasaidia Wakristo kuwa na uhakika kwamba Yesu alifufuliwa?

7 Tumaini letu la ufufuo linategemea ufufuo wa Yesu, hivyo tunahitaji kusadiki kwamba Yesu alifufuliwa. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova alimfufua Yesu?

8 Kulikuwa na watu wengi waliomwona Yesu baada ya kufufuliwa nao walitoa ushahidi kwamba alikuwa amefufuliwa. (1 Kor. 15:5-7) Shahidi wa kwanza kutajwa katika orodha ya Paulo alikuwa mtume Petro (Kefa). Kikundi cha wanafunzi kilithibitisha kwamba Petro alimwona Yesu aliyefufuliwa. (Luka 24:33, 34) Pia, ‘wale mitume 12’ walimwona Yesu baada ya kufufuliwa. Kisha Kristo “aliwatokea ndugu zaidi ya 500 kwa wakati mmoja,” huenda ni huko Galilaya kwenye tukio lenye shangwe linalotajwa kwenye Mathayo 28:16-20. Pia, Yesu “alimtokea Yakobo,” ambaye inaelekea alikuwa ndugu nusu ya Yesu, na ambaye awali hakuamini kwamba Yesu alikuwa Masihi. (Yoh. 7:5) Baada ya kumwona Yesu aliyefufuliwa, Yakobo aliamini. Inapendeza kwamba karibu mwaka wa 55 W.K., Paulo alipoandika barua hiyo, watu wengi walioshuhudia ufufuo wa Yesu walikuwa hai, hivyo mtu yeyote ambaye alikuwa na shaka angeweza kuwauliza mashahidi hao wenye kutegemeka.

9. Kama tunavyosoma kwenye Matendo 9:3-5, Paulo angeweza kuongezeaje ushahidi kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa?

9 Baadaye, Yesu alimtokea Paulo mwenyewe. (1 Kor. 15:8) Paulo (Sauli) alikuwa njiani kuelekea Damasko aliposikia sauti ya Yesu aliyefufuliwa na kumwona Yesu katika utukufu wake wa mbinguni. (Soma Matendo 9:3-5.) Jambo ambalo Paulo alijionea liliongeza uthibitisho kwamba ufufuo wa Yesu haukuwa hadithi tu.—Mdo. 26:12-15.

10. Kusadiki kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa kutoka kwa wafu, kulimchochea Paulo kufanya nini?

10 Ushahidi wa Paulo ungewavutia sana baadhi ya watu kwa sababu pindi fulani aliwatesa Wakristo. Mara tu aliposadiki kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa, Paulo alifanya kazi kwa bidii ili kuwasadikisha wengine kuhusu ukweli huo. Alivumilia kupigwa, kufungwa gerezani, na kuvunjikiwa na meli alipokuwa akihubiri ukweli kwamba Yesu alikufa lakini alikuwa hai tena. (1 Kor. 15:9-11; 2 Kor. 11:23-27) Paulo alikuwa na uhakika kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa kutoka kwa wafu hivi kwamba alikuwa tayari kufa ili kuitetea imani yake. Je, ushahidi huo kutoka kwa Wakristo wa mapema haukusadikishi kwamba Yesu alifufuliwa kutoka kwa wafu? Na je, hauimarishi imani yako katika ufufuo?

PAULO ASAHIHISHA MAONI YA UWONGO

11. Huenda ni kwa nini baadhi ya watu huko Korintho walikuwa na maoni yasiyo sahihi kuhusu ufufuo?

11 Baadhi ya watu katika jiji la Kigiriki la Korintho walikuwa na maoni yasiyo sahihi kuhusu ufufuo, wengine hata walisema kwamba “hakuna ufufuo wa wafu.” Kwa nini? (1 Kor. 15:12) Katika jiji lingine la Kigiriki la Athene, wanafalsafa walidhihaki wazo la kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa. Mawazo kama hayo huenda yaliwaathiri baadhi ya watu huko Korintho. (Mdo. 17:18, 31, 32) Huenda wengine walifikiri ufufuo haukuwa halisi, kwamba kwa njia ya mfano ulimaanisha awali mtu alikuwa ‘mfu’ katika dhambi, lakini sasa amekuwa “hai” akiwa Mkristo. Haidhuru sababu yao, kukataa fundisho la ufufuo kulimaanisha imani yao ilikuwa ya bure. Ikiwa Mungu hakumfufua Yesu, fidia haikulipwa na watu wote walibaki katika dhambi. Hivyo, wale waliokataa fundisho la ufufuo hawakuwa na tumaini la kweli.—1 Kor. 15:13-19; Ebr. 9:12, 14.

12. Kulingana na 1 Petro 3:18, 22, ufufuo wa Yesu ulitofautianaje na ufufuo uliotukia awali?

12 Paulo alikuwa amejithibitishia kibinafsi kwamba ‘Kristo alikuwa amefufuliwa kutoka kwa wafu.’ Ufufuo huo ulikuwa bora kuliko ule uliokuwa umefanywa awali, kwa sababu wale waliofufuliwa walikuja kufa tena. Paulo alisema kwamba Yesu alikuwa “matunda ya kwanza ya wale ambao wamelala usingizi katika kifo.” Yesu alikuwa wa kwanza katika maana gani? Alikuwa mtu wa kwanza kufufuliwa akiwa kiumbe wa roho, na wa kwanza kati ya wanadamu kwenda mbinguni.—1 Kor. 15:20; Mdo. 26:23; soma 1 Petro 3:18, 22.

WALE AMBAO “WATAFANYWA KUWA HAI”

13. Paulo alionyesha tofauti gani kati ya Adamu na Yesu?

13 Kifo cha mtu mmoja kingewezaje kuwarudishia uhai mamilioni ya watu? Paulo anajibu swali hilo kwa hoja yenye kusadikisha. Anaonyesha tofauti kati ya kile ambacho Adamu aliwaletea wanadamu na kile ambacho kinawezekana kupitia Kristo. Paulo aliandika hivi kumhusu Adamu: “Kifo kilikuja kupitia mwanadamu.” Adamu alipotenda dhambi alisababisha msiba mkubwa kwake na kwa wazao wake. Bado tunaendelea kuteseka kwa sababu ya matokeo mabaya ya kutotii kwake. Matokeo tunayopata kutokana na Mungu kumfufua Mwana wake ni tofauti kabisa! “Ufufuo wa wafu pia unakuja kupitia mwanadamu,” Yesu. Paulo alitoa hoja hii: “Kwa maana kama vile katika Adamu wote wanakufa, vivyo hivyo pia katika Kristo wote watafanywa kuwa hai.”—1 Kor. 15:21, 22.

14. Je, Adamu atafufuliwa? Eleza.

14 Paulo alimaanisha nini aliposema “katika Adamu wote wanakufa”? Paulo alikuwa akizungumzia wazao wa Adamu, ambao wamerithi dhambi na kutokamilika kutoka kwa Adamu na kwa sababu hiyo wanakufa. (Rom. 5:12) Adamu hatakuwa miongoni mwa wale ambao “watafanywa kuwa hai.” Hatanufaika na fidia ya Kristo kwa sababu Adamu alikuwa mwanadamu mkamilifu, aliyeamua kumwasi Mungu kimakusudi. Kile kilichompata Adamu ni sawa na kile kitakachowapata wale ambao “Mwana wa binadamu” atawahukumu kuwa “mbuzi,” yaani, “watakatiliwa mbali milele.”—Mt. 25:31-33, 46; Ebr. 5:9.

Yesu alikuwa wa kwanza kufufuliwa kati ya wengi watakaofufuliwa kwenda mbinguni (Tazama fungu la 15 na 16) *

15. “Wote” ambao “watafanywa kuwa hai” wanatia ndani akina nani?

15 Ona kwamba Paulo alisema “katika Kristo wote watafanywa kuwa hai.” (1 Kor. 15:22) Paulo aliwaandikia barua hiyo Wakristo watiwa-mafuta huko Korintho, ambao wangefufuliwa ili wakaishi mbinguni. Wakristo hao walikuwa ‘wametakaswa katika muungano na Kristo Yesu na kuitwa kuwa watakatifu.’ Na Paulo aliwataja “wale ambao wamelala usingizi katika kifo wakiwa katika muungano na Kristo.” (1 Kor. 1:2; 15:18; 2 Kor. 5:17) Katika barua yake nyingine iliyoongozwa na roho, mtume Paulo aliandika kwamba wale ‘walioungana pamoja na Yesu katika mfano wa kifo chake wataunganishwa pamoja naye katika mfano wa ufufuo wake.’ (Rom. 6:3-5) Yesu alifufuliwa akiwa kiumbe wa roho na alienda mbinguni. Itakuwa vivyo hivyo kwa wote walio “katika muungano na Kristo,” yaani, Wakristo wote waliotiwa mafuta kwa roho.

16. Paulo alidokeza nini alipomwita Yesu “matunda ya kwanza”?

16 Paulo aliandika kwamba Kristo alifufuliwa akiwa “matunda ya kwanza ya wale ambao wamelala usingizi katika kifo.” Kumbuka kwamba wengine, kama vile Lazaro, walikuwa wamefufuliwa ili waishi duniani. Lakini Yesu alikuwa wa kwanza kufufuliwa kutoka kwa wafu akiwa kiumbe wa roho na kupata uzima wa milele. Angeweza kulinganishwa na matunda ya kwanza ya mavuno ambayo Waisraeli walimtolea Mungu. Zaidi ya hayo, kwa kumwita Yesu “matunda ya kwanza,” Paulo alikuwa akidokeza kwamba baada ya hapo kuna wengine ambao wangefufuliwa kutoka kwa wafu ili wakaishi mbinguni. Mitume na wengine walio “katika muungano pamoja na Kristo” wangemfuata Yesu. Hatimaye, wangepata ufufuo kama ule ambao Yesu alipata.

17. Wale walio “katika muungano pamoja na Kristo” watapokea lini thawabu yao ya kimbingu?

17 Paulo alipoandika barua yake kwa Wakorintho, ufufuo wa kwenda mbinguni kwa wale walio “katika muungano na Kristo” ulikuwa bado haujaanza. Lakini Paulo alionyesha kwamba ungetukia wakati ujao: “Kila mmoja kwa mpangilio wake unaofaa: Kristo aliye matunda ya kwanza, baadaye wale walio wa Kristo wakati wa kuwapo kwake.(1 Kor. 15:23; 1 The. 4:15, 16) Leo tunaishi katika kipindi hicho kilichotabiriwa cha “kuwapo” kwa Kristo. Naam, mitume na Wakristo wengine waliotiwa mafuta kwa roho ambao walikuwa wamekufa, walihitaji kusubiri kipindi hicho cha kuwapo kwa Kristo ili kupokea thawabu yao ya kimbingu na ‘kuunganishwa pamoja na Yesu katika mfano wa ufufuo wake.’

UNALO TUMAINI HAKIKA!

18. (a) Kwa nini tunaweza kufikia mkataa kwamba kutakuwa na ufufuo mwingine baada ya ule wa mbinguni? (b) Kama inavyoonyeshwa kwenye 1 Wakorintho 15:24-26, ni mambo gani yatakayotokea mbinguni?

18 Lakini vipi kuhusu Wakristo wote washikamanifu ambao hawana tumaini la kuishi mbinguni pamoja na Kristo? Wao pia wana tumaini la ufufuo. Biblia inasema kwamba Paulo na wengine ambao wanaenda mbinguni wanapata “ufufuo wa mapema kutoka kwa wafu.” (Flp. 3:11) Je, hilo halidokezi kwamba kuna ufufuo mwingine ambao ungefuata? Wazo hilo linapatana na maneno ambayo Ayubu alisema kuhusu wakati wake ujao. (Ayu. 14:15) “Wale walio wa Kristo wakati wa kuwapo kwake” watakuwa mbinguni pamoja na Yesu atakapokuwa akiangamiza serikali yote na mamlaka yote na nguvu zote. Hata “kifo” ambaye ni “adui wa mwisho” ataangamizwa. Kwa hakika, kifo tulichorithi hakitawaathiri tena wale wanaofufuliwa ili wakaishi mbinguni. Lakini vipi kuhusu wale ambao hawana tumaini la kwenda mbinguni?—Soma 1 Wakorintho 15:24-26.

19. Wale wasio na tumaini la kwenda mbinguni wanaweza kutarajia nini?

19 Wale wasio na tumaini la kwenda mbinguni wanaweza kutarajia nini? Wanaweza kupata tumaini kupitia maneno haya ya Paulo: “Nina tumaini . . . kwamba kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Mdo. 24:15) Ni wazi kwamba mtu asiye mwadilifu hawezi kwenda mbinguni, hivyo maneno hayo yanaonyesha kwamba wakati ujao kutakuwa na ufufuo duniani.

Kuamini ahadi ya ufufuo kunatusaidia kutazamia wakati ujao tukiwa na uhakika (Tazama fungu la 20) *

20. Tumaini lako limeimarishwa jinsi gani?

20 Bila shaka “kutakuwa na ufufuo!” Wale watakaofufuliwa dunia watakuwa na tarajio la kuishi hapahapa duniani milele. Unaweza kutumaini ahadi hiyo. Tumaini hilo linaweza kukupa faraja inapohusu wapendwa wako waliokufa. Wataweza kufufuliwa kutoka kwa wafu wakati Yesu na wenzake ‘watakapotawala wakiwa wafalme katika ile miaka 1,000.’ (Ufu. 20:6) Wewe pia unaweza kuwa na tumaini hilo hakika kwamba ikiwa utakufa kabla ya ile Miaka Elfu Moja kuanza, utafufuliwa. “Tumaini [hilo] halikatishi tamaa.” (Rom. 5:5) Linaweza kukuimarisha sasa na kuongeza shangwe yako ya kumtumikia Mungu. Lakini kuna mambo mengine tunayoweza kujifunza kutokana na 1 Wakorintho sura ya 15, kama makala inayofuata itakavyoonyesha.

WIMBO 147 Uzima wa Milele Umeahidiwa

^ fu. 5 Barua ya kwanza kwa Wakorintho sura ya 15, inakazia tumaini la ufufuo. Kwa nini fundisho hilo ni muhimu kwetu, na kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yesu alifufuliwa? Makala hii itajibu maswali hayo na maswali mengine muhimu kuhusu ufufuo.

^ fu. 56 MAELEZO YA PICHA: Yesu alikuwa mtu wa kwanza kwenda mbinguni. (Mdo. 1:9) Baadhi ya wanafunzi wake ambao wangeungana naye walitia ndani Tomasi, Yakobo, Lidia, Yohana, Maria, na Paulo.

^ fu. 58 MAELEZO YA PICHA: Ndugu amefiwa na mke wake mpendwa ambaye walimtumikia Yehova pamoja kwa miaka mingi. Anatumaini kwamba mke wake atafufuliwa, naye anaendelea kumtumikia Yehova kwa ushikamanifu.