Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 50

“Wafu Watafufuliwaje?”

“Wafu Watafufuliwaje?”

“Kifo, uko wapi ushindi wako? Kifo, uko wapi mchomo wako?”—1 KOR. 15:55.

WIMBO 141 Muujiza wa Uhai

MUHTASARI *

1-2. Kwa nini Wakristo wote wanapaswa kupendezwa na ufufuo wa kimbingu?

WATU wengi wanaomtumikia Yehova sasa wana tumaini la kuishi milele duniani. Hata hivyo, Wakristo watiwa-mafuta waliobaki, wana tumaini la kufufuliwa ili wakaishi mbinguni. Wakristo hao waliotiwa mafuta wanatazamia kwa hamu kujua jinsi maisha yao yatakavyokuwa wakati ujao, lakini vipi kuhusu wale walio na tumaini la kuishi duniani? Kama tutakavyoona, ufufuo wa kimbingu utawaletea pia baraka wale walio na tumaini la kuishi milele duniani. Hivyo, haidhuru tumaini letu ni la kimbingu au la kidunia, tunapaswa kupendezwa na ufufuo wa kimbingu.

2 Mungu aliwaongoza kwa roho baadhi ya wanafunzi wa Yesu katika karne ya kwanza waandikie kuhusu tumaini la kimbingu. Mtume Yohana alieleza hivi: “Sasa sisi ni watoto wa Mungu, lakini bado haijafunuliwa jinsi tutakavyokuwa. Tunajua kwamba atakapofunuliwa tutakuwa kama yeye.” (1 Yoh. 3:2) Hivyo, Wakristo watiwa-mafuta hawajui jinsi watakavyokuwa watakapofufuliwa wakiwa na miili ya kiroho. Hata hivyo, watamwona Yehova kihalisi watakapopokea thawabu yao. Biblia haifunui habari zote kuhusu ufufuo wa kimbingu, ingawa hivyo, mtume Paulo aliandika habari fulani kuhusu ufufuo huo. Wakristo watiwa-mafuta watakuwa pamoja na Kristo atakapokuwa ‘akiangamiza serikali yote na mamlaka yote na nguvu zote.’ Hilo linatia ndani ‘adui wa mwisho, kifo.’ Mwishowe, Yesu—pamoja na watawala wenzake—atajitiisha yeye mwenyewe pamoja na vitu vyote kwa Yehova. (1 Kor. 15:24-28) Huo utakuwa wakati mzuri kwelikweli! *

3. Kama andiko la 1 Wakorintho 15:30-32 linavyoonyesha, imani ya Paulo katika ufufuo ilimsaidia kufanya nini?

3 Imani ya Paulo katika ufufuo ilimsaidia avumilie majaribu mbalimbali. (Soma 1 Wakorintho 15:30-32.) Aliwaambia hivi Wakorintho: “Ninakabili kifo kila siku.” Pia, Paulo aliandika hivi: “Nimepigana na wanyama wa mwituni huko Efeso.” Huenda alikuwa akizungumzia jinsi alivyopigana kihalisi na wanyama kwenye uwanja huko Efeso. (2 Kor. 1:8; 4:10; 11:23) Au labda alikuwa akirejelea upinzani kutoka kwa Wayahudi na watu wengine waliokuwa kama “wanyama wa mwituni.” (Mdo. 19:26-34; 1 Kor. 16:9) Vyovyote vile, Paulo alikabiliana na hatari kubwa. Hata hivyo, aliendelea kuwa na mtazamo mzuri kuhusu wakati ujao.—2 Kor. 4:16-18.

Familia inayoishi kwenye eneo ambalo kazi yetu ya Kikristo imewekewa vizuizi inaendelea kufanya ibada huku wakiwa na imani thabiti kwamba Mungu amewaandalia mambo mema ya wakati ujao (Tazama fungu la 4)

4. Tumaini la ufufuo limewaimarishaje Wakristo leo? (Tazama picha kwenye jalada.)

4 Tunaishi katika nyakati zilizo hatari. Baadhi ya ndugu zetu wametendewa vitendo vya uhalifu. Wengine wanaishi maeneo yenye vita ambako hakuna usalama wa kutosha. Na bado wengine wanamtumikia Yehova kwenye nchi ambazo kazi ya kuhubiri imewekewa vizuizi au hata kupigwa marufuku, na wanafanya hivyo licha ya kwamba wanahatarisha maisha yao au uhuru wao. Licha ya hilo, ndugu na dada hao wote wanaendelea kumwabudu Yehova na kutuwekea sote kielelezo kizuri. Hawaogopi kwa sababu wanajua kwamba hata ikiwa watapoteza uhai wao wa sasa, Yehova anaahidi kuwapa jambo bora zaidi wakati ujao.

5. Ni mtazamo gani hatari unaoweza kudhoofisha imani yetu katika ufufuo?

5 Paulo aliwaonya ndugu zake kuhusu mtazamo huu hatari ambao baadhi ya watu walikuwa nao: “Ikiwa wafu hawatafufuliwa, ‘acheni tule na tunywe kwa maana kesho tutakufa.’” Ukweli ni kwamba mtazamo huo ulikuwepo hata kabla ya siku za Paulo. Huenda alikuwa akinukuu andiko la Isaya 22:13 ambalo linazungumzia mtazamo wa Waisraeli. Badala ya kumkaribia Mungu, walifuatia maisha ya starehe. Kwa ujumla, mtazamo wa Waisraeli hao ulikuwa “ponda raha kufa kwaja,” mtazamo ambao ni wa kawaida hata katika siku zetu. Hata hivyo, matokeo mabaya yaliyolipata taifa la Israeli yameandikwa kwenye Biblia.—2 Nya. 36:15-20.

6. Tumaini la ufufuo linapaswa kutuongoza jinsi gani tunapochagua marafiki?

6 Ni wazi, kujua ukweli kwamba Yehova anaweza kufufua wafu kunapaswa kuongoza jinsi tunavyochagua marafiki. Akina ndugu huko Korintho walihitaji kuepuka kushirikiana na wale ambao walikataa fundisho la ufufuo. Kuna somo kwetu leo: Matokeo hayawezi kuwa mazuri ikiwa tutachagua kushirikiana kwa ukawaida na wale ambao wanafikiria tu kuponda raha na hawafikirii maisha yao ya wakati ujao. Kushirikiana na watu kama hao kunaweza kupotosha mtazamo na tabia za Mkristo wa kweli. Isitoshe, kufanya hivyo kunaweza kumwongoza Mkristo huyo kwenye mtindo wa maisha ambao unatia ndani jambo ambalo Mungu anachukia, yaani, dhambi. Hivyo, Paulo alitoa himizo hili kwa uthabiti: “Amkeni kwa njia ya uadilifu na msiwe na mazoea ya kufanya dhambi.”—1 Kor. 15:33, 34.

WATAKUWA NA MWILI WA AINA GANI?

7. Kama andiko la 1 Wakorintho 15:35-38 linavyoonyesha, huenda baadhi ya watu waliuliza swali gani kuhusu ufufuo?

7 Soma 1 Wakorintho 15:35-38. Huenda mtu aliyetaka kupanda shaka kuhusu tumaini la ufufuo, angeuliza: “Wafu watafufuliwaje?” Itakuwa vyema tukichunguza jibu la Paulo kwa sababu watu wengi leo wana maoni yao binafsi kuhusu maisha baada ya kifo. Lakini Biblia inafundisha nini?

Kwa kutumia mfano wa mbegu na mmea, Paulo alifafanua kwamba Mungu anaweza kuwapatia mwili unaofaa wale wanaofufuliwa (Tazama fungu la 8)

8. Ni mfano gani unaoweza kutusaidia kuelewa ufufuo wa kimbingu?

8 Mtu anapokufa, mwili wake huoza. Lakini Yule aliyefanyiza ulimwengu ambao haukuwepo anaweza kumfufua mtu huyo, na kumpa mwili unaofaa. (Mwa. 1:1; 2:7) Paulo alitumia mfano kuonyesha kwamba Mungu hangehitaji kumrudishia mtu mwili uleule. Fikiria kuhusu “mbegu” ya mmea fulani. Mbegu ambayo imepandwa ardhini huchipuka na kuwa mmea mpya. Mmea huo mpya ni tofauti kabisa na mbegu ndogo iliyopandwa. Paulo alitumia ulinganisho huo kuonyesha kwamba Muumba wetu anaweza kutokeza “mwili kama anavyopenda.”

9. Andiko la 1 Wakorintho 15:39-41 linasema nini kuhusu tofauti za miili?

9 Soma 1 Wakorintho 15:39-41. Paulo alionyesha kwamba kuna uumbaji wa aina tofauti-tofauti. Kwa mfano, kuna miili tofauti-tofauti ya nyama kama vile ya ng’ombe, ndege na samaki. Alisema kwamba, angani tunaona tofauti kati ya jua na mwezi. Na alisema kwamba “nyota moja hutofautiana na nyota nyingine kwa utukufu.” Naam, hata kama hatuwezi kuona tofauti hizo kati ya nyota kwa macho yetu, kuna zile ambazo wanasayansi huziita nyota nyekundu zilizo kubwa mno, mbilikimo weupe, na nyota za njano, kama vile jua letu. Pia, Paulo alisema kwamba “kuna miili ya mbinguni na miili ya duniani.” Alimaanisha nini? Alimaanisha kwamba duniani tuna miili ya nyama, lakini mbinguni kuna miili ya roho, kama ile ambayo malaika wanayo.

10. Wale watakaofufuliwa kwenda mbinguni watakuwa na mwili wa aina gani?

10 Paulo aliendelea kusema hivi: “Ndivyo ilivyo kuhusu ufufuo wa wafu. Hupandwa katika uharibifu; hufufuliwa katika kutoweza kuharibika.” Bila shaka, mwanadamu anapokufa, mwili wake huoza nao unarudi kuwa mavumbi. (Mwa. 3:19) Basi, inawezekanaje kwamba mwili “[unafufuliwa] katika kutoweza kuharibika”? Paulo hakuwa akizungumza kuhusu wanadamu waliofufuliwa ili waishi duniani, kama vile wale waliofufuliwa na Eliya, Elisha, na Yesu. Paulo alikuwa akirejelea mtu aliyefufuliwa akiwa na mwili wa mbinguni, yaani, “mwili wa roho.”—1 Kor. 15:42-44.

11-12. Yesu alipitia badiliko gani alipofufuliwa, na Wakristo watiwa-mafuta wanapitiaje hali inayofanana na hiyo?

11 Yesu alipokuwa duniani, alikuwa na mwili wa nyama. Lakini alipofufuliwa, “akawa roho inayowapa watu uhai” na alirudi mbinguni. Vivyo hivyo, Wakristo waliotiwa mafuta watafufuliwa wakiwa na mwili unaoweza kuishi mbinguni. Paulo alieleza hivi: “Kama vile ambavyo tumeuchukua mfano wa yule aliyeumbwa kwa mavumbi; vivyo hivyo pia tutauchukua mfano wa yule wa mbinguni.”—1 Kor. 15:45-49.

12 Ni muhimu kukumbuka kwamba Yesu hakufufuliwa akiwa na mwili wa kibinadamu. Paulo alipokuwa akimalizia mazungumzo yake, alieleza sababu aliposema: “Nyama na damu haviwezi kuurithi Ufalme wa Mungu” mbinguni. (1 Kor. 15:50) Mitume na Wakristo wengine waliotiwa mafuta hangefufuliwa kwenda mbinguni wakiwa na miili inayoweza kuharibika ya nyama na damu. Wangeanza kufufuliwa lini? Paulo alisema kwamba ufufuo wao ungetukia baadaye; haungetukia mara tu baada ya wao kufa. Kufikia wakati ambapo Paulo aliandika 1 Wakorintho, tayari baadhi ya mitume kama vile mtume Yakobo, walikuwa “[wamelala] usingizi katika kifo.” (Mdo. 12:1, 2) Baadaye mitume wengine na Wakristo watiwa-mafuta wangelala “usingizi katika kifo.”—1 Kor. 15:6.

USHINDI DHIDI YA KIFO

13. Ni mambo gani ambayo yangetukia wakati wa kuwapo kwa Yesu?

13 Yesu na Paulo walizungumzia wakati ujao wa pekee katika historia—wakati wa kuwapo kwa Kristo. Katika kipindi hicho cha kuwapo kwa Kristo kungekuwa na vita, matetemeko ya ardhi, magonjwa hatari, na mambo mengine mabaya yanayotukia ulimwenguni. Tumeona unabii huo wa Biblia ukitimia tangu mwaka wa 1914. Bado kungekuwa na sehemu nyingine yenye kutokeza ya ishara hiyo. Yesu alisema kwamba habari njema ya Ufalme wa Mungu uliosimamishwa ingehubiriwa “katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote, na ndipo ule mwisho [ungekuja].” (Mt. 24:3, 7-14) Paulo alieleza kwamba wakati wa “kuwapo kwa Bwana” ungekuwa pia wakati wa kufufuliwa kwa Wakristo waliotiwa mafuta ambao walikuwa “wamelala usingizi katika kifo.”—1 The. 4:14-16; 1 Kor. 15:23.

14. Ni nini hutukia Wakristo watiwa-mafuta wanapokufa wakati wa kuwapo kwa Kristo?

14 Leo, Wakristo watiwa-mafuta wanapomaliza mwendo wao wa kidunia wanafufuliwa papo hapo kwenda mbinguni. Hilo linathibitishwa na maneno ya Paulo kwenye 1 Wakorintho 15:51, 52: “Hatutalala usingizi katika kifo sisi sote, bali sote tutabadilishwa, kwa muda mfupi, kufumba na kufumbua jicho, wakati wa tarumbeta ya mwisho.” Maneno hayo ya Paulo yanatimizwa sasa! Wakati wa ufufuo wao, ndugu hao wa Kristo watakuwa na shangwe kubwa; watakuwa “pamoja na Bwana sikuzote.”—1 The. 4:17.

Wale ambao wanabadilishwa, “kufumba na kufumbua jicho,” watashiriki pamoja na Yesu katika kuyavunjavunja mataifa (Tazama fungu la 15)

15. Ni kazi gani inayowasubiri wale ambao “kufumba na kufumbua jicho,” watabadilishwa?

15 Biblia inatueleza kuhusu kazi ambayo wale watakaobadilishwa, “kufumba na kufumbua jicho,” wataifanya huko mbinguni. Yesu aliwaambia hivi: “Yule atakayeshinda na kushika matendo yangu mpaka mwisho, nitampa mamlaka juu ya mataifa, kama vile nilivyopokea kutoka kwa Baba yangu, naye atawachunga watu kwa fimbo ya chuma hivi kwamba watavunjwa vipandevipande kama vyombo vya udongo.” (Ufu. 2:26, 27) Watamfuata Kamanda wao kutimiza kazi iliyo mbele yao, yaani, kuyachunga mataifa kwa fimbo ya chuma.—Ufu. 19:11-15.

16. Watu wengi watapataje ushindi dhidi ya kifo?

16 Ni wazi kwamba Wakristo watiwa-mafuta watakuwa washindi dhidi ya kifo. (1 Kor. 15:54-57) Ufufuo wao utawapa fursa ya kushiriki ushindi dhidi ya uovu ulioenea duniani kote wakati wa vita inayokuja ya Har–Magedoni. Mamilioni ya Wakristo wengine, wanaume kwa wanawake, ‘watatoka katika ile dhiki kuu’ na kuingia kwenye ulimwengu mpya. (Ufu. 7:14) Wale watakaookoka hapa duniani watashuhudia ushindi mwingine dhidi ya kifo, yaani, ufufuo wa mabilioni ya watu waliokufa zamani. Wazia shangwe itakayokuwapo wakati wa tukio hilo la ushindi! (Mdo. 24:15) Na wote ambao watathibitika kuwa washikamanifu kabisa kwa Yehova watakuwa washindi hata dhidi ya kifo walichorithi kutoka kwa Adamu. Nao wataweza kuishi milele.

17. Andiko la 1 Wakorintho 15:58, linatutia moyo tufanye nini sasa?

17 Kila Mkristo aliye hai leo anapaswa kuthamini sana maneno yenye kufariji kuhusu ufufuo ambayo Paulo aliwaandikia Wakorintho. Tuna kila sababu ya kuonyesha kwamba tunakubali himizo la Paulo la kuwa na mengi ya kufanya sasa “katika kazi ya Bwana.” (Soma 1 Wakorintho 15:58.) Ikiwa tutashiriki katika kazi hiyo kwa ushikamanifu na kwa bidii, tunaweza kutarajia wakati ujao wenye shangwe nyingi. Wakati huo ujao utakuwa mzuri ajabu kuliko kitu chochote tunachoweza kuwazia. Kwa hakika, tutajithibitishia kwamba kazi yetu haikuwa ya bure kuhusiana na Bwana.

WIMBO 140 Uzima wa Milele—Hatimaye!

^ fu. 5 Sehemu ya pili ya 1 Wakorintho sura ya 15 inazungumzia kuhusu ufufuo, hasa ule wa Wakristo watiwa-mafuta. Hata hivyo, yale ambayo Paulo aliandika yanawahusu pia kondoo wengine. Makala hii itaonyesha jinsi tumaini la ufufuo linavyopaswa kuathiri jinsi tunavyoishi sasa na kutupatia sababu ya kutazamia wakati ujao.

^ fu. 2 Makala ya “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika toleo hili inazungumzia maneno ya Paulo yanayopatikana kwenye 1 Wakorintho 15:29.