Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, maneno ya mtume Paulo yanayopatikana kwenye 1 Wakorintho 15:29 yanamaanisha kwamba baadhi ya Wakristo wa wakati huo walibatizwa kwa niaba ya wafu?

Hapana, Biblia wala vitabu vya historia havionyeshi kwamba jambo hilo lilitendeka.

Jinsi ambavyo mstari huo umetafsiriwa katika Biblia nyingi, umewafanya baadhi ya watu wafikiri kwamba katika siku za Paulo ubatizo wa maji ulifanywa kwa niaba ya watu waliokufa. Kwa mfano: “Kama hakuna ufufuo, je watu wale wanaobatizwa kwa ajili ya wafu wanatumainia kupata nini?”​—Biblia Habari Njema.

Hata hivyo, ona maelezo yafuatayo ya wasomi wawili wa Biblia. Dkt. Gregory Lockwood alisema wazo la kwamba ubatizo ulifanywa “kwa niaba ya watu ambao tayari wamekufa” linarejelea “aina ya ubatizo ambao kulingana na uchunguzi uliofanywa, haujawahi kutajwa kwenye vitabu vya historia au Biblia.” Vilevile, Profesa Godon D. Fee aliandika hivi: “Hakuna tukio lolote la awali la kihistoria au katika Biblia kuhusu ubatizo wa aina hiyo. Agano Jipya halitaji kabisa kuhusu jambo hilo; haitajwi popote kwamba ubatizo huo ulifanywa kwenye makanisa yoyote mengine, wala jamii yoyote ya Wakristo waothodoksi katika karne zilizofuata punde tu” baada ya mitume kufa.

Biblia inasema kwamba wafuasi wa Yesu walipaswa “[kufanya] wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, [wakiwabatiza] . . . , na kuwafundisha kushika mambo yote” aliyokuwa amewaamuru. (Mt. 28:19, 20) Kabla ya mtu kuwa mwanafunzi aliyebatizwa, alihitaji kujifunza, kumwamini, na kumtii Yehova na Mwana Wake. Mtu ambaye tayari alikuwa amekufa na kuzikwa kaburini hangeweza kufanya hivyo, wala Mkristo aliyehai hangeweza kufanya hivyo kwa niaba yake.​—Mhu. 9:5, 10; Yoh. 4:1; 1 Kor. 1:14-16.

Basi, Paulo alikuwa akimaanisha nini?

Baadhi ya Wakorintho walikuwa wakisema kwamba wafu hawatafufuliwa. (1 Kor. 15:12) Paulo alipinga maoni hayo. Jinsi gani? Alisema kwamba ‘alikabili kifo kila siku.’ Lakini licha ya kupitia hali zenye hatari, alikuwa na uhakika kwamba baada ya kifo angefufuliwa akiwa kiumbe wa roho mwenye nguvu, kama ilivyokuwa kwa Yesu.​—1 Kor. 15:30-32, 42-44.

Wakorintho walihitaji kuelewa kwamba kuwa Wakristo watiwa-mafuta kulimaanisha kwamba wangekabili majaribu kila siku na kufa kabla ya kuweza kufufuliwa. ‘Kubatizwa katika Kristo’ kulitia ndani ‘kubatizwa katika kifo chake.’ (Rom. 6:3) Ubatizo wao wa mfano ungewaongoza kwenye njia ya maisha ambayo mwishowe wangekufa kihalisi na kufufuliwa kwenda mbinguni.

Baada ya zaidi ya miaka miwili tangu Yesu alipobatizwa katika maji, aliwaambia hivi mitume wake wawili: “Ubatizo ninaobatizwa mtabatizwa.” (Marko 10:38, 39) Pindi hiyo Yesu hakuwa akibatizwa kwenye maji. Alimaanisha kwamba maisha yake ya utimilifu yangeongoza kwenye kifo chake halisi. Paulo aliandika kwamba Wakristo watiwa-mafuta ‘wangeteseka pamoja ili waweze pia kutukuzwa pamoja.’ (Rom. 8:16, 17; 2 Kor. 4:17) Hivyo, wao pia wangekufa ili wafufuliwe na kwenda kuishi mbinguni.

Kwa hiyo, maneno ya Paulo yanaweza kutafsiriwa hivi kwa usahihi: “Kama sivyo, watafanya nini wale wanaobatizwa kwa kusudi la kuwa wafu? Ikiwa wafu hawatafufuliwa kamwe, kwa nini basi wanabatizwa kwa kusudi la kuwa hivyo?”