Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Methali 24:16 inasema: “Mwadilifu anaweza kuanguka mara saba, lakini atainuka tena.” Je, andiko hilo linarejelea mtu ambaye anaanguka katika dhambi tena na tena, lakini anasamehewa na Mungu?

Kwa kweli, mstari huo haumaanishi hivyo. Badala yake, unarejelea mtu ambaye anaanguka katika maana ya kwamba anakabili matatizo au changamoto tena na tena, na ambaye anainuka tena katika maana ya kwamba anayashinda matatizo hayo.

Acheni tuchunguze muktadha wa andiko hilo unaosema hivi: “Usivizie kwa uovu karibu na makao ya mtu mwadilifu; usiharibu mahali pake pa kupumzikia. Kwa maana mwadilifu anaweza kuanguka mara saba, lakini atainuka tena, lakini waovu watakwazwa na msiba. Adui yako akianguka, usishangilie, na akijikwaa, usiruhusu moyo wako uwe na shangwe.”​—Met. 24:15-17.

Baadhi ya watu wanafikiri kwamba mstari wa 16 unazungumzia mtu ambaye anaanguka katika dhambi, lakini anarudisha uhusiano wake mzuri pamoja na Mungu. Makasisi wawili Waingereza waliandika kwamba “wahubiri, wa zamani na wa sasa, wamelitumia sana andiko hilo” kwa njia hiyo. Makasisi hao waliongezea kusema kuwa maoni hayo yanamaanisha kwamba “mwanamume mwema anaweza kuanguka katika . . . dhambi nzito, lakini hapotezi kamwe upendo wake kwa Mungu, na anainuka tena kwa kutubu kila mara anapoanguka.” Maoni kama hayo yanaweza kumvutia mtu ambaye hataki kupambana ili asifanye dhambi. Anaweza kufikiri kwamba hata ikiwa atafanya dhambi tena na tena, sikuzote Mungu atamsamehe.

Lakini kihalisi mstari wa 16 haumaanishi hivyo.

Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “kuanguka” na “akianguka” kwenye mstari wa 16 na 17 linaweza kutumiwa kwa njia mbalimbali. Linaweza kumaanisha kuanguka kihalisi​—kwa mfano, ng’ombe dume kuanguka barabarani, mtu kuanguka kutoka kwenye paa, au kijiwe kuanguka chini. (Kum. 22:4, 8; Amo. 9:9) Neno hilo pia linaweza kutumiwa kwa njia ya mfano, kama ifuatavyo: “Yehova huongoza hatua za mtu njia ya mtu huyo inapompendeza Yeye. Hata akianguka, hataangushwa chini kabisa, kwa maana Yehova anaushika mkono wake na kumtegemeza.”​—Zab. 37:23, 24; Met. 11:5; 13:17; 17:20.

Hata hivyo, ona jambo ambalo Profesa Edward H. Plumptre anasema: “Neno la Kiebrania linalotafsiriwa [“kuanguka”] halitumiwi kamwe kumaanisha kuanguka katika dhambi.” Hivyo, msomi mwingine anaufafanua mstari huo wa 16 kwa njia hii: “Ingekuwa ubatili na kazi ya bure kuwatendea watu wa Mungu kwa njia mbaya, kwa sababu wao huokoka​—lakini sivyo ilivyo kwa watu waovu!”

Naam, badala ya kuzungumzia “kuanguka” katika maana ya kimaadili, yaani, kuanguka katika dhambi, Methali 24:16 inarejelea kupatwa na matatizo au hali ngumu zinazoweza kutokea tena na tena. Katika mfumo huu mwovu wa mambo, mtu mwadilifu anaweza kukabili matatizo ya kiafya au matatizo mengine. Hata anaweza kukabili mateso makali kutoka kwa serikali. Lakini anaweza kutumaini kwamba Mungu atamtegemeza na atamsaidia kukabiliana na hali hiyo, naye atafanikiwa. Jiulize hivi: ‘Je, sijajionea mara kwa mara jinsi ambavyo mambo huwaendea vyema watumishi wa Mungu?’ Kwa nini? Tunahakikishiwa kwamba “Yehova huwategemeza wote wanaoanguka na kuwainua juu wote walioinama chini.”​—Zab. 41:1-3; 145:14-19.

“Mtu mwadilifu” hafurahi wengine wanapopata matatizo. Badala yake, anafurahi kujua kwamba “mambo yatawaendea vyema wale wanaomwogopa Mungu wa kweli kwa sababu wanamwogopa.”​—Mhu. 8:11-13; Ayu. 31:3-6; Zab. 27:5, 6.