Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 52

Jinsi Unavyoweza Kushinda Hisia za Kuvunjika Moyo

Jinsi Unavyoweza Kushinda Hisia za Kuvunjika Moyo

“Mtupie Yehova mzigo wako, naye atakutegemeza.” —ZAB. 55:22.

WIMBO 33 Mtupie Yehova Mzigo Wako

MUHTASARI *

1. Kuvunjika moyo kunaweza kutuathirije?

KILA siku tunapata matatizo na kushughulika nayo kadiri tunavyoweza. Lakini je, hukubali kwamba tunaweza kushughulikia matatizo yetu vizuri zaidi wakati hatujavunjika moyo? Hivyo tunapaswa kuona hisia za kuvunjika moyo kama mwizi anayeweza kutunyang’anya uhakika wetu, ujasiri wetu, na shangwe yetu. Methali 24:10 na maelezo ya chini yanasema: “Ukivunjika moyo nyakati za taabu, nguvu zako zitakuwa chache.” Naam, kuvunjika moyo kunaweza kumaliza nguvu tunazohitaji ili tushinde matatizo tunayokabiliana nayo maishani kwa mafanikio.

2. Ni mambo gani yanayoweza kutufanya tuvunjike moyo, na tutachunguza nini katika makala hii?

2 Kuna mambo mengi yanayoweza kutuvunja moyo​—yanaweza kutokana na hali zetu sisi wenyewe, au mambo yanayotuzunguka. Huenda hali hizo zikatia ndani makosa yetu wenyewe, udhaifu wetu, na matatizo ya afya. Pia, zinaweza kutia ndani kutopata mgawo tunaotamani katika utumishi wa Yehova, au eneo letu la kuhubiri linapoonekana kuwa halina matokeo. Katika makala hii, tutachunguza mambo tunayoweza kufanya ili kukabiliana na hisia za kuvunjika moyo.

TUNAPOKABILIANA NA UDHAIFU NA MAKOSA YETU

3. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuwa na maoni yaliyosawazika kuhusu makosa yetu?

3 Ni rahisi kwetu kusitawisha maoni yasiyo na usawaziko kuhusu udhaifu fulani tulio nao na makosa yetu. Hivyo, huenda tukahisi kwamba kwa sababu ya mapungufu yetu, Yehova hatatukaribisha kwenye ulimwengu wake mpya. Mtazamo kama huo unaweza kuwa hatari sana. Tunapaswa kuyaonaje makosa yetu? Biblia inafunua kwamba wanadamu wote “wamefanya dhambi” isipokuwa Yesu Kristo. (Rom. 3:23) Mtungaji wa Biblia hatafuti makosa, wala hatarajii ukamilifu kutoka kwetu. Badala yake, yeye ni Baba mwenye upendo anayetaka kutusaidia. Pia yeye ni mwenye subira. Anaona jitihada ambazo tunafanya ili kupambana na udhaifu wetu mbalimbali na kushinda maoni yasiyo na usawaziko ambayo tunayo kujihusu, naye yuko tayari kutusaidia.​—Rom. 7:18, 19.

Yehova anajua mambo mazuri tuliyofanya wakati uliopita na pia mambo mazuri tunayofanya sasa (Tazama fungu la 5) *

4-5. Kulingana na 1 Yohana 3:19, 20, kwa nini dada zetu wawili hawakukatishwa tamaa na hisia za kuvunjika moyo?

4 Fikiria mfano wa Deborah na Maria. * Alipokuwa mtoto, mara nyingi Deborah alitendewa kwa njia isiyo na upendo na hilo lilimfanya awe na maoni yasiyofaa kujihusu. Alipongezwa mara chache sana. Hivyo, akasitawisha maoni mabaya kujihusu. Alipofanya makosa madogo-madogo, alijihisi hafai kitu. Maria alikuwa na tatizo kama hilo pia. Hivyo alipambana na hisia za kujiona kuwa mtu asiyefaa kitu. Hata baada ya kupata kweli, alihisi hakustahili kulibeba jina la Mungu!

5 Licha ya hayo, dada hao wawili hawakuacha kumtumikia Yehova. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba walimtupia Yehova mizigo yao kupitia sala za kutoka moyoni. (Zab. 55:22) Mwishowe walikubali kwamba Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo, anajua jinsi hali tulizopitia maishani na maoni yasiyofaa tuliyo nayo kujihusu yanavyoweza kutuathiri. Lakini pia anaona mambo mazuri yaliyo moyoni mwetu​—sifa ambazo huenda sisi wenyewe hatuzioni.​—Soma 1 Yohana 3:19, 20.

6. Huenda mtu akahisije ikiwa atarudia kosa ambalo aliwahi kufanya awali?

6 Huenda mtu anayepambana ili kushinda tabia fulani mbaya iliyokita mizizi akajikuta akirudia kosa hilo na kuvunjika moyo. Bila shaka, ni kawaida kuhisi hatia kwa kadiri fulani tunapofanya dhambi. (2 Kor. 7:10) Hata hivyo, hatupaswi kuhisi hatia kupita kiasi na kujihukumu vikali na kufikiri hivi: ‘Mimi sifai kitu. Yehova hawezi kunisamehe kamwe.’ Mtazamo huo usiofaa hauna msingi katika kweli na unaweza kufanya tuache kumtumikia Yehova. Kumbuka jambo tulilosoma kwenye Methali 24:10​—nguvu zetu zitakuwa chache tunapovunjika moyo. Badala yake, ‘nyoosha mambo’ kati yako na Yehova kwa kumwendea katika sala na kumwomba rehema yake. (Isa. 1:18) Yehova anapoona kwamba umetubu kikweli na unajitahidi kubadilika, atakusamehe. Pia, waone wazee wa kutaniko. Kwa subira, watakusaidia urudie tena hali nzuri ya kiroho.​—Yak. 5:14, 15.

7. Kwa nini hatupaswi kuvunjika moyo ikiwa ni vigumu kwetu kufanya yaliyo sawa?

7 Jean-Luc, mzee wa kutaniko kutoka nchini Ufaransa, huwaambia hivi wale wanaopambana na udhaifu fulani: “Mtu mwadilifu machoni pa Yehova, si yule ambaye hakosei kamwe, bali ni mtu anayejutia makosa yake na sikuzote hutubu.” (Rom. 7:21-25) Hivyo, usijihukumu vikali ikiwa unapambana na udhaifu fulani. Kumbuka kwamba hatuwezi kuwa na msimamo wa uadilifu mbele za Mungu kwa jitihada zetu wenyewe. Sote tunahitaji fadhili zisizostahiliwa za Mungu kupitia dhabihu ya fidia.​—Efe. 1:7; 1 Yoh. 4:10.

8. Tunapovunjika moyo, tunaweza kupata msaada kutoka kwa nani?

8 Tunaweza kuwaendea ndugu na dada zetu ambao ni familia yetu ya kiroho ili tutiwe moyo! Wanaweza kutusikiliza tunapohitaji mtu wa kuzungumza naye na kutufariji kwa maneno yanayoweza kutuchangamsha moyo. (Met. 12:25; 1 The. 5:14) Joy, dada kutoka nchini Nigeria ambaye amepambana na hisia za kuvunjika moyo anasema hivi: “Ningekuwa wapi bila ndugu na dada zangu? Ndugu na dada zangu ni uthibitisho kwamba Yehova anajibu sala zangu. Hata nimejifunza kutoka kwao jinsi ya kuwatia moyo wengine ambao wamevunjika moyo.” Hata hivyo, tunahitaji kukumbuka kwamba si nyakati zote ndugu na dada zetu watajua ni wakati gani tunahitaji kitia-moyo. Hivyo, huenda tukahitaji kuchukua hatua ya kwanza kwa kumfikia Mkristo mkomavu na kumweleza kwamba tunahitaji msaada.

TUNAPOPAMBANA NA MATATIZO YA AFYA

9. Andiko la Zaburi 41:3 na 94:19, linatutia moyo jinsi gani?

9 Mwombe Yehova msaada. Tunapokuwa wagonjwa na hasa ikiwa tunapambana na ugonjwa wa kudumu, huenda ikawa vigumu kwetu kuwa na maoni yanayofaa kuhusu hali yetu. Ingawa Yehova hatuponyi kimuujiza kwa sasa, anatufariji na anaweza kutupatia nguvu tunazohitaji ili kuvumilia. (Soma Zaburi 41:3; 94:19.) Kwa mfano, huenda akawachochea Wakristo wenzetu watusaidie tunapohitaji msaada wa kufanya kazi fulani za nyumbani au kufanya ununuzi. Anaweza kuwachochea ndugu zetu wasali pamoja nasi. Au anaweza kutukumbusha mawazo yenye kufariji yanayopatikana katika Neno lake, kama vile tumaini zuri la uhai mkamilifu usio na magonjwa wala maumivu katika ulimwengu mpya unaokuja.​—Rom. 15:4.

10. Kwa nini Isang hakuendelea kubaki na hisia za kuvunjika moyo baada ya kupata aksidenti?

10 Isang, anayeishi nchini Nigeria, alipata aksidenti iliyosababisha apooze. Daktari wake alimwambia kwamba hatatembea tena kamwe. Isang anasema hivi: “Nilivunjika moyo na kupondeka roho.” Lakini je, aliendelea kuwa na hisia hizo? Hapana! Ni nini kilichomsaidia? Isang anaeleza hivi: “Mimi na mke wangu hatujaacha kamwe kusali kwa Yehova na kujifunza Neno lake. Pia, tuliazimia kuhesabu baraka zetu, kutia ndani tumaini letu la uzima katika ulimwengu mpya wa Mungu.”

Hata wale ambao wana matatizo ya afya wanaweza kupata matokeo mazuri na shangwe wanaposhiriki katika huduma (Tazama fungu la 11 hadi 13)

11. Cindy alipataje shangwe alipokuwa mgonjwa sana?

11 Cindy, dada anayeishi nchini Mexico, aligunduliwa kuwa ana ugonjwa uliohatarisha maisha yake. Alikabilianaje na hali hiyo? Alipokuwa akipata matibabu, alijiwekea lengo la kutoa ushahidi kila siku. Aliandika hivi: “Kwa kufanya hivyo, niliweza kukazia fikira mambo mengine badala ya upasuaji, maumivu, au jinsi nilivyohisi vibaya sana. Niliamua kufanya hivi: Nilipokuwa na mazungumzo pamoja na madaktari au wauguzi ningewauliza kuhusu familia zao. Kisha ningewauliza kwa nini walichagua kufanya kazi hiyo ngumu? Baada ya hapo, ilikuwa rahisi kujua ni habari zipi ambazo huenda zingegusa mioyo yao. Baadhi yao walisema kwamba halikuwa jambo la kawaida kwa mgonjwa kuwauliza, ‘Unaendeleaje?’ Na wengi wao walinishukuru kwa kuwaonyesha kwamba ninawajali. Baadhi yao hata walinipa anwani au namba zao za simu. Hivyo, katika kipindi hiki kigumu maishani mwangu, Yehova amenipa shangwe kubwa sana ya moyoni ambayo imenishangaza hata mimi!”​—Met. 15:15.

12-13. Baadhi ya ndugu na dada ambao ni wagonjwa au wazee-wazee wamewezaje kushiriki katika huduma, na wamepata matokeo gani?

12 Huenda wagonjwa au wazee-wazee wakavunjika moyo kwa sababu hawawezi kufanya mengi katika huduma. Licha ya hilo, wengi wao wameweza kutoa ushahidi mzuri. Nchini Marekani, Dada anayeitwa Laurel alilazimika kulala ndani ya mashine ya chuma iliyomsaidia kupumua kwa miaka 37! Laurel alikabiliana na kansa, upasuaji mbalimbali mkubwa, na magonjwa ya kudumu ya ngozi. Lakini hata changamoto hizo kubwa hazikumnyamazisha. Aliwatolea ushahidi wauguzi na wahudumu wengine wa afya ambao walifika nyumbani kwake. Matokeo yakawaje? Aliwasaidia angalau watu 17 kupata ujuzi sahihi wa Biblia! *

13 Richard, mzee wa kutaniko kutoka nchini Ufaransa, ana pendekezo zuri kwa wale ambao hawawezi kutoka nyumbani au walio kwenye makao ya kuwatunza waliozeeka. Anasema hivi: “Ninawapendekezea kwamba waweke machapisho mahali ambapo watu wanaweza kuyaona. Watu wanapopita wanaweza kuvutiwa na kuuliza maswali. Mazungumzo hayo yanaweza kuwatia moyo ndugu na dada zetu ambao hawawezi tena kuhubiri nyumba kwa nyumba.” Wale ambao hawawezi kutoka nyumbani wanaweza pia kushiriki katika huduma kwa kuandika barua na kuhubiri kwa njia ya simu.

TUSIPOPATA PENDELEO TUNALOTAMANI

14. Mfalme Daudi alituwekea mfano gani wa pekee?

14 Kwa sababu ya umri, afya, au hali nyingine, huenda tusiweze kupata mgawo au pendeleo fulani kutanikoni au kwenye mzunguko. Ikiwa tunapitia hali kama hiyo, tunaweza kujifunza kutokana na mfano wa Mfalme Daudi. Alipoambiwa kwamba hakuwa amechaguliwa kujenga hekalu la Mungu​—jambo ambalo Daudi alitamani sana kufanya—​alimuunga mkono kabisa yule ambaye Mungu alimchagua kutimiza mgawo huo. Daudi hata alichangia kwa ukarimu ili kufanikisha mradi huo. Huo ni mfano mzuri sana wa kuiga!​—2 Sam. 7:12, 13; 1 Nya. 29:1, 3-5.

15. Hugues alishindaje hisia za kuvunjika moyo?

15 Kwa sababu ya matatizo ya afya, Hugues, ndugu kutoka nchini Ufaransa, aliacha kutumikia akiwa mzee wa kutaniko, na hangeweza kufanya hata kazi ndogo-ndogo za nyumbani. Anaandika hivi: “Mwanzoni nilijiona sifai na nilivunjika moyo sana. Lakini baada ya muda, niliona umuhimu wa kuikubali hali yangu, na nikaanza kupata shangwe kwa kumtumikia Yehova kulingana na hali yangu ya sasa. Nimeazimia kutokufa moyo. Kama Gideoni na wale wanaume mia tatu waliokuwa pamoja naye​—ambao walikuwa wamechoka—​nitaendelea kupambana!”​—Amu. 8:4.

16. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa malaika?

16 Malaika waaminifu ni mfano mzuri. Wakati wa utawala wa Mfalme Ahabu, Yehova aliwaomba malaika watoe mapendekezo ya jinsi ya kumdanganya mfalme huyo mwovu. Malaika kadhaa walitoa mapendekezo, lakini Mungu alimchagua malaika mmoja na kumwambia kwamba pendekezo lake litafanikiwa. (1 Fal. 22:19-22) Je, malaika wengine walivunjika moyo, labda wakifikiri hivi: ‘Kwa nini nilijisumbua?’ Hatuna sababu ya kuamini hivyo. Malaika wana unyenyekevu wa kweli na wanataka heshima zote zimwendee Yehova.​—Amu. 13:16-18; Ufu. 19:10.

17. Tunapaswa kufanya nini ikiwa tunahisi tumeshuka moyo kwa sababu hatujapata pendeleo fulani la utumishi tunalotamani?

17 Kumbuka pendeleo tulilo nalo la kubeba jina la Mungu na kuutangaza Ufalme wake. Tunaweza kupata mgawo fulani au kuupoteza, lakini si migawo yetu inayotufanya tuwe wenye thamani machoni pa Mungu. Tunapokuwa wenye kiasi na wanyenyekevu ndipo tunapokuwa wenye thamani kwelikweli machoni pa Yehova na kwa ndugu na dada zetu. Hivyo, msihi Yehova akusaidie ili uendelee kuwa na sifa ya unyenyekevu na kiasi. Tafakari kuhusu mifano mingi mizuri iliyoandikwa katika Neno lake, ya watu walioonyesha sifa ya unyenyekevu na kiasi. Kwa hiari, watumikie ndugu na dada zako kwa njia yoyote unayoweza.​—Zab. 138:6; 1 Pet. 5:5.

TUNAPOKUWA KATIKA ENEO LINALOONEKANA KUWA HALINA MATOKEO MAZURI

18-19. Unaweza kupataje shangwe katika huduma yako hata ikiwa eneo lenu linaonekana kuwa halina matokeo mazuri?

18 Je, nyakati fulani umewahi kuvunjika moyo kwa sababu eneo lenu linaonekana kuwa halina matokeo mazuri au kwa sababu ni watu wachache wanaopatikana nyumbani? Katika hali kama hiyo, tunaweza kufanya nini ili kudumisha au kuongeza shangwe yetu? Baadhi ya mapendekezo yameorodheshwa katika sanduku “ Njia za Kuboresha Huduma Yako.” Pia, ni muhimu kuwa na mtazamo unaofaa kuhusu huduma. Hilo linahusisha nini?

19 Kazia fikira kutangaza jina la Mungu na Ufalme wake. Yesu alisema waziwazi kwamba ni watu wachache watakaoipata barabara inayoongoza kwenye uzima. (Mt. 7:13, 14) Tunapokuwa katika huduma tuna pendeleo la kufanya kazi pamoja na Yehova, Yesu, na malaika. (Mt. 28:19, 20; 1 Kor 3:9; Ufu. 14:6, 7) Yehova anawavuta kwake wale wanaostahili. (Yoh. 6:44) Hivyo ikiwa mtu haitikii vizuri ujumbe wetu kwa sasa, huenda akasikiliza wakati ujao tutakapomtembelea.

20. Andiko la Yeremia 20:8, 9 linatufundisha nini kuhusu jinsi ya kupambana na hisia za kuvunjika moyo?

20 Tunaweza kujifunza mambo mengi kutoka kwa nabii Yeremia. Alipewa mgawo kwenye eneo gumu sana. Watu walimtukana na kumdhihaki “siku nzima.” (Soma Yeremia 20:8, 9.) Pindi fulani alivunjika moyo sana hivi kwamba alitaka kukata tamaa. Lakini hakufanya hivyo. Kwa nini? “Neno la Yehova” lilikuwa kama moto unaowaka ndani ya Yeremia, naye hangeweza kulizuia ndani yake! Hivyo ndivyo ilivyo kwetu pia tunapolijaza Neno la Mungu kwenye akili na mioyo yetu. Hiyo ni sababu nyingine inayotufanya tusome na kutafakari Biblia kila siku. Matokeo ni kwamba shangwe yetu itaendelea kuongezeka, na huenda tukawa na matokeo mazuri zaidi katika huduma yetu.​—Yer. 15:16.

21. Tunaweza kushindaje pambano dhidi ya hisia za kuvunjika moyo, haidhuru chanzo chake?

21 Deborah, dada aliyetajwa awali, anasema hivi: “Hisia za kuvunjika moyo zinaweza kuwa silaha yenye nguvu ambayo Shetani huitumia.” Lakini Yehova Mungu ana nguvu nyingi kuliko Shetani na silaha zake zote. Hivyo unapovunjika moyo kwa sababu yoyote ile, toa dua kwa Yehova ukimwomba msaada wake. Atakusaidia kukabiliana na hisia za kuvunjika moyo zinazotokana na udhaifu fulani ulio nao na makosa uliyofanya. Atakutegemeza unapokuwa mgonjwa. Atakusaidia udumishe maoni yaliyosawazika kuhusu migawo ya utumishi. Naye atakusaidia uwe na maoni yanayofaa kuhusu huduma yako. Zaidi ya yote, mmiminie Baba yako wa mbinguni mahangaiko yako. Kwa msaada wake, utaweza kushinda pambano dhidi ya hisia za kuvunjika moyo.

WIMBO 41 Tafadhali Sikiliza Sala Yangu

^ fu. 5 Pindi fulani sisi sote huvunjika moyo. Katika makala hii, tutazungumzia mambo hususa tunayoweza kufanya tunapovunjika moyo. Kama tutakavyoona, kwa msaada wa Yehova tunaweza kushinda hisia za kuvunjika moyo.

^ fu. 4 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 12 Unaweza kusoma simulizi la maisha la Laurel Nisbet kwenye toleo la Amkeni!, Januari 22, 1993.

^ fu. 69 MAELEZO YA PICHA: Dada Mkristo alivunjika moyo kwa muda fulani, lakini anatafakari kuhusu utumishi aliofanya wakati uliopita na kusali kwa Yehova. Ana uhakika kwamba Yehova anakumbuka yale aliyofanya wakati uliopita na anayofanya sasa.