Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jitoe kwa Moyo Wako Wote Kwenye Mgawo Wako!

Jitoe kwa Moyo Wako Wote Kwenye Mgawo Wako!

UNAHISIJE unapopokea barua yenye kutia moyo kutoka kwa rafiki yako mpendwa? Mwanafunzi Mkristo Timotheo alipokea barua kama hiyo kutoka kwa mtume Paulo, ambayo sasa inajulikana kama barua ya pili kwa Timotheo. Bila shaka, Timotheo alitamani kuketi kwenye eneo tulivu ili aweze kusoma kile ambacho rafiki yake mpendwa alitaka kumweleza. Huenda Timotheo alikuwa akifikiri hivi: ‘Paulo anaendeleaje? Je, ana ushauri wowote ambao angependa kunipa kuhusu jinsi ya kushughulikia migawo yangu? Je, barua hii inaweza kunisaidia nifanikiwe katika huduma yangu ya Kikristo na niwasaidie wengine?’ Kama tutakavyoona, Timotheo alipata majibu ya maswali hayo na mambo mengine katika barua hiyo yenye thamani. Lakini kwa sasa, acheni tukazie fikira mambo machache muhimu yanayopatikana katika barua hiyo yatakayotusaidia.

“NINAENDELEA KUVUMILIA MAMBO YOTE”

Timotheo alipoanza kusoma maneno ya mwanzoni ya barua hiyo, angeweza kutambua mara moja uhusiano wa karibu uliokuwepo kati yake na Paulo. Paulo alimwita Timotheo kwa hisia “mtoto mpendwa.” (2 Tim. 1:2) Ingawa huenda Timotheo alikuwa na umri wa miaka thelathini hivi alipopokea barua hiyo karibu mwaka wa 65 W.K., tayari alikuwa mzee Mkristo mwenye uzoefu. Alikuwa ameshirikiana na Paulo kwa zaidi ya miaka kumi na alikuwa amejifunza mambo mengi.

Ni lazima Timotheo alitiwa moyo sana kujua kwamba Paulo alikuwa akivumilia majaribu kwa uaminifu. Paulo alikuwa mfungwa huko Roma na angeuawa baada ya muda mfupi. (2 Tim. 1:15, 16; 4:6-8) Timotheo angeweza kuona ujasiri wa Paulo kupitia maneno haya: “Ninaendelea kuvumilia mambo yote.” (2 Tim. 2:8-13) Kama Timotheo sisi pia tunaweza kuimarishwa na uvumilivu wa Paulo.

“ICHOCHEE KAMA MOTO ILE ZAWADI”

Paulo alimhimiza Timotheo auone mgawo wake katika utumishi wa Mungu kuwa ni wenye thamani sana. Paulo alimwambia Timotheo ‘aichochee kama moto zawadi ya Mungu iliyokuwa ndani yake.’ (2 Tim. 1:6) Paulo alitumia neno la Kigiriki khaʹri·sma linalotafsiriwa kuwa “zawadi.” Kimsingi neno hilo la Kigiriki linarejelea zawadi ya bure na isiyostahiliwa, kitu ambacho mtu anakipata au kupewa bila kufanyia kazi. Timotheo alipokea zawadi hiyo alipochaguliwa kulitumikia kutaniko kwa njia ya pekee.​—1 Tim. 4:14.

Timotheo alihitaji kufanya nini na zawadi hiyo? Alipokuwa akisoma maneno, “uichochee kama moto,” huenda alikumbuka ukweli huu kwamba nyakati nyingine moto unaotumika nyumbani huishia kuwa makaa yanayowaka moto. Makaa hayo yalihitaji kuchochewa ili kutoa miale ya moto na joto zaidi. Kamusi moja inasema kwamba kitenzi cha Kigiriki ambacho Paulo alitumia (a·na·zo·py·reʹo) kinamaanisha “kuwasha upya moto, kuuchochea, kuupepea moto,” na hivyo kwa njia ya mfano kilimaanisha “kusisimkia kazi fulani.” Hivyo Paulo alikuwa akimshauri hivi Timotheo: ‘Jitoe kwa moyo wako wote kwenye mgawo wako!’ Tunaweza kuona kwamba leo pia tunahitaji kufanya vivyo hivyo, yaani, kujitahidi kwa bidii kwenye utumishi wetu.

“LINDA AMANA HII NZURI”

Alipoendelea kusoma barua hiyo kutoka kwa rafiki yake mpendwa, Timotheo alikutana na maneno mengine ambayo yangemsaidia kuwa na mafanikio katika huduma yake. Paulo aliandika hivi: “Linda amana hii nzuri kupitia roho takatifu inayokaa ndani yetu.” (2 Tim. 1:14) Amana hiyo ilikuwa nini? Timotheo alikuwa amekabidhiwa nini? Katika mstari uliotangulia, Paulo alirejelea “maneno yenye manufaa,” yaani, kweli inayopatikana kwenye Maandiko. (2 Tim. 1:13) Akiwa mhudumu Mkristo, Timotheo alipaswa kuihubiri ile kweli ndani na nje ya kutaniko. (2 Tim. 4:1-5) Pia, Timotheo alikuwa amewekwa rasmi kuwa mzee ili kulichunga kundi la Mungu. (1 Pet. 5:2) Timotheo angeweza kulinda amana aliyopewa, yaani, kweli aliyopaswa kufundisha—kwa kutegemea roho takatifu ya Yehova na Neno Lake.​—2 Tim. 3:14-17.

Leo, sisi pia tumekabidhiwa kweli ambayo tunashiriki na wengine katika huduma ya Kikristo. (Mt. 28:19, 20) Tunaweza kuendelea kuithamini amana hii ya pekee kwa kuendelea kudumu katika sala na kusitawisha zoea zuri la kujifunza Neno la Mungu. (Rom. 12:11, 12; 1 Tim. 4:13, 15, 16) Pia, huenda tukawa na mgawo mwingine wa kutumikia tukiwa wazee waliowekwa rasmi au kutumikia katika utumishi wa wakati wote. Amana kama hiyo inapaswa kutusaidia tuwe wanyenyekevu na kutambua kwamba tunapaswa kumtegemea Mungu. Hivyo, tunaweza kulinda amana yetu kwa kuithamini na kumtegemea Yehova atusaidie kuitunza.

“MAMBO HAYO WAKABIDHI WANAUME WAAMINIFU”

Migawo ambayo Timotheo alipokea haikumhusu yeye peke yake. Wengine walihusika pia. Hiyo ndiyo sababu Paulo alimhimiza Timotheo hivi: “Mambo uliyosikia kutoka kwangu . . . uwakabidhi wanaume waaminifu, ambao watastahili vya kutosha kuwafundisha wengine.” (2 Tim. 2:2) Naam, Timotheo alihitaji kujifunza na kisha kushiriki mambo aliyojifunza na ndugu zake Wakristo. Ni muhimu kwamba waangalizi wote kwenye makutaniko ya Kikristo leo, wajitahidi kufanya vivyo hivyo. Mwangalizi mzuri si mtu mwenye wivu, anayeficha ujuzi alio nao kuhusu kazi fulani. Badala yake, anawafundisha wengine ili waweze kufanya kazi hiyo. Haogopi kwamba watajua mengi zaidi au kufanya kazi hiyo kwa uwezo mkubwa zaidi kuliko yeye. Hivyo, mwangalizi huyo hatawafundisha tu mambo ya msingi ya kazi hiyo. Anataka wale anaowazoeza wasitawishe uwezo mzuri wa kufanya maamuzi na wawe na utambuzi, yaani, wakue kiroho. Kwa njia hiyo, wanaume hao waaminifu ambao amewafundisha watathibitika kuwa wenye faida kubwa zaidi kwa kutaniko.

Hapana shaka kwamba Timotheo aliithamini sana barua hiyo yenye kuchochea aliyoipokea kutoka kwa Paulo. Tunaweza kumwazia akipitia mara kwa mara ushauri huo wenye thamani na kutafakari kuhusu jinsi anavyoweza kuutumia kwa njia bora katika migawo yake.

Sisi pia, tungependa kutumia ushauri huo. Jinsi gani? Tunaweza kujitahidi kuichochea kama moto zawadi yetu, kulinda amana yetu, na kuwakabidhi wengine ujuzi na uzoefu tulio nao. Kwa njia hiyo, tutaweza ‘kutimiza kikamili huduma yetu’ kama Paulo alivyomwambia Timotheo.​—2 Tim. 4:5.