Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 2

Mambo Tunayojifunza Kutoka kwa “Mwanafunzi Ambaye Yesu Alimpenda”

Mambo Tunayojifunza Kutoka kwa “Mwanafunzi Ambaye Yesu Alimpenda”

“Na tuendelee kupendana, kwa sababu upendo unatoka kwa Mungu.”—1 YOH. 4:7.

WIMBO 105 “Mungu Ni Upendo”

MUHTASARI *

1. Upendo wa Mungu unakufanya uhisije?

MTUME YOHANA aliandika, “Mungu ni upendo.” (1 Yoh. 4:8) Maneno hayo rahisi yanatukumbusha ukweli huu wa msingi: Mungu, aliye Chanzo cha uhai, ndiye pia Chanzo cha upendo. Yehova anatupenda! Upendo wake hutufanya tuhisi tukiwa salama, wenye furaha, na tukiwa tumeridhika.

2. Kulingana na Mathayo 22:37-40, ni amri gani mbili zilizo kuu zaidi, na kwa nini huenda ikawa vigumu kwetu kutii amri ya pili?

2 Kwa Wakristo, kuonyesha upendo si jambo la hiari. Ni amri tuliyopewa. (Soma Mathayo 22:37-40.) Tunapomjua Yehova vizuri, huenda ikawa rahisi kwetu kutii ile amri ya kwanza. Hiyo ni kwa sababu Yehova ni mkamilifu; anatutendea kwa ufikirio na upole. Lakini huenda ikawa vigumu kwetu kutii amri ya pili. Kwa nini? Kwa sababu ndugu na dada zetu, ambao ni miongoni mwa majirani wetu wa karibu zaidi, si wakamilifu. Nyakati fulani huenda wakasema au kutenda kwa njia inayotufanya tuhisi kwamba hawatujali na hawatupendi. Yehova alijua kwamba tungekabili changamoto hiyo, hivyo, aliwaongoza baadhi ya waandikaji wa Biblia waandike ushauri hususa kuhusu sababu za kuonyeshana upendo, na jinsi ya kufanya hivyo. Mmoja wa waandikaji hao ni Yohana.—1 Yoh. 3:11, 12.

3. Yohana alikazia jambo gani?

3 Katika vitabu alivyoandika, Yohana anakazia kwamba ni lazima Wakristo waonyeshe upendo. Isitoshe, katika simulizi lake kuhusu maisha ya Yesu, Yohana anatumia maneno ya Kigiriki yanayotafsiriwa kuwa “upendo” na ‘-penda’ mara nyingi zaidi kuliko wale waandishi wengine watatu wa Injili kwa ujumla. Yohana alikuwa na umri wa miaka 100 hivi alipoandika Injili ya Yohana na barua zake tatu. Vitabu hivyo vilivyoongozwa na roho ya Mungu vinafunua kwamba mambo yote ambayo Mkristo anafanya ni lazima yachochewe na upendo. (1 Yoh. 4:10, 11) Hata hivyo, ilichukua muda kwa Yohana kujifunza somo hilo.

4. Je, Yohana aliwaonyesha wengine upendo nyakati zote?

4 Yohana alipokuwa kijana, hakuonyesha upendo nyakati zote. Kwa mfano, pindi moja Yesu na wanafunzi wake walikuwa wakisafiri kwenda Yerusalemu kupitia Samaria. Watu wa kijiji fulani cha Samaria walikataa kuwaonyesha ukarimu. Yohana alitendaje? Alimwomba Yesu ikiwa wangeweza kuagiza moto kutoka mbinguni na kuwaangamiza wakazi wote wa kijiji hicho! (Luka 9:52-56) Pindi nyingine, Yohana alishindwa kuwaonyesha upendo mitume wenzake. Inaonekana kwamba yeye na Yakobo, ndugu yake, walimwomba mama yao azungumze na Yesu ili awape nafasi za pekee kando yake katika Ufalme. Mitume wengine walipojua jambo ambalo Yakobo na Yohana walikuwa wamefanya, walikasirika sana! (Mt. 20:20, 21, 24) Hata hivyo, Yesu alimpenda Yohana licha ya mapungufu hayo yote.—Yoh. 21:7.

5. Tutachunguza nini katika makala hii?

5 Katika makala hii, tutachunguza mfano wa Yohana na baadhi ya mambo aliyoandika kuhusu upendo. Tunapofanya hivyo, tutajifunza jinsi tunavyoweza kuwaonyesha upendo ndugu na dada zetu. Pia, tutajifunza kuhusu njia muhimu ambayo kichwa cha familia anaweza kuonyesha kwamba anaipenda familia yake.

UPENDO UNAONYESHWA KWA MATENDO

Yehova alionyesha upendo wake kwetu kwa kumtuma Mwana wake duniani ili afe kwa ajili yetu (Tazama fungu la 6 na 7)

6. Yehova amefunuaje upendo wake kwetu?

6 Mara nyingi tunafikiri kwamba upendo ni hisia inayotoka moyoni inayoonyeshwa kwa maneno ya fadhili. Lakini ili upendo uwe halisi, ni lazima pia uonyeshwe kwa matendo. (Linganisha Yakobo 2:17, 26.) Kwa mfano, Yehova anatupenda. (1 Yoh. 4:19) Na anaonyesha upendo wake kupitia maneno mazuri yaliyoandikwa kwenye Biblia. (Zab. 25:10; Rom. 8:38, 39) Hata hivyo, hatusadiki tu kwamba Mungu anatupenda kwa sababu ya yale anayosema, bali pia kwa sababu ya yale anayotenda. Yohana aliandika hivi: “Hivi ndivyo upendo wa Mungu ulivyofunuliwa kwetu, kwamba Mungu alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee ulimwenguni ili tupate uzima kupitia yeye.” (1 Yoh. 4:9) Yehova aliruhusu mwana wake mpendwa ateseke na kufa kwa ajili yetu. (Yoh. 3:16) Je, tunaweza kuwa na shaka yoyote kwamba kwa kweli Yehova anatupenda?

7. Yesu alifanya nini kuthibitisha upendo wake kwetu?

7 Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake kwamba alikuwa anawapenda. (Yoh. 13:1; 15:15) Alithibitisha kina cha upendo wake kwao na kwetu pia kupitia mambo aliyosema na pia mambo aliyotenda. Yesu alisema “hakuna mtu aliye na upendo mkuu kuliko huu, kwamba mtu atoe uhai wake kwa ajili ya rafiki zake.” (Yoh. 15:13) Tunachochewa kufanya nini tunapofikiria kuhusu mambo ambayo Yehova na Yesu wamefanya kwa ajili yetu?

8. Andiko la 1 Yohana 3:18 linasema tunapaswa kufanya nini?

8 Tunaonyesha kwamba tunampenda Yehova na Yesu kwa kuwatii. (Yoh. 14:15; 1 Yoh. 5:3) Na Yesu alituamuru kihususa kwamba tupendane. (Yoh. 13:34, 35) Ni lazima tuonyeshe kwamba tunawapenda ndugu na dada zetu si kwa maneno tu, bali pia tuonyeshe upendo huo kwa matendo. (Soma 1 Yohana 3:18.) Tunaweza kufanya mambo gani hususa ili kuonyesha kwamba tunawapenda?

WAPENDE NDUGU NA DADA ZAKO

9. Upendo ulimchochea Yohana afanye nini?

9 Yohana angeweza kuamua kubaki na baba yake na kupata pesa kwa kufanya kazi kwenye biashara ya familia ya kuvua. Lakini badala ya kufanya hivyo, alitumia maisha yake yote yaliyobaki kuwasaidia wengine wajifunze ukweli kumhusu Yehova na Yesu. Maisha ambayo Yohana alichagua hayakuwa rahisi. Aliteswa, na karibu na mwishoni mwa karne ya kwanza alipokuwa amezeeka, alipelekwa uhamishoni. (Mdo. 3:1; 4:1-3; 5:18; Ufu. 1:9) Hata alipokuwa amefungwa kwa sababu ya kuhubiri kuhusu Yesu, Yohana alionyesha kwamba alikuwa akiwafikiria wengine. Kwa mfano, alipokuwa kwenye kisiwa cha Patmo, aliandika kitabu cha Ufunuo na kukituma kwa makutaniko ili yajue mambo ‘yaliyopaswa kutukia hivi karibuni.’ (Ufu. 1:1) Kisha, inaelekea baada ya kuachiwa huru kutoka Patmo, Yohana aliandika kitabu chake cha Injili kuhusu maisha na huduma ya Yesu. Pia, aliandika barua tatu ili kuwatia moyo na kuwaimarisha ndugu na dada zake. Unaweza kuigaje maisha ya kujidhabihu ya Yohana?

10. Unaweza kuonyeshaje kwamba unawapenda watu?

10 Unaweza kuonyesha kwamba unawapenda watu kupitia mambo unayochagua kufanya maishani mwako. Ulimwengu wa Shetani ungependa utumie muda na nguvu zako zote kwa ajili yako mwenyewe, ukijaribu kutafuta pesa ili kujitengenezea jina. Badala ya kufanya hivyo, wahubiri wa Ufalme waliojidhabihu ulimwenguni pote wanatumia muda wao mwingi kadiri wawezavyo ili waweze kuhubiri habari njema na kuwasaidia watu wamkaribie Yehova. Baadhi yao hata wanaweza kuhubiri na kufundisha wakiwa watumishi wa wakati wote.

Tunaonyesha kwamba tunawapenda ndugu na dada zetu na familia zetu kupitia yale tunayowafanyia (Tazama fungu la 11 na 17) *

11. Wahubiri wengi waaminifu wameonyeshaje kwamba wanampenda Yehova na ndugu na dada zao?

11 Wakristo wengi washikamanifu wanalazimika kufanya kazi ya kimwili ya wakati wote ili waweze kujitegemeza na kuandalia familia zao. Hata hivyo, wahubiri hao waaminifu hulitegemeza tengenezo la Mungu kwa njia yoyote wanayoweza. Kwa mfano, baadhi wanaweza kutoa msaada wakati wa msiba, wengine wanaweza kufanya kazi kwenye mradi wa ujenzi, na sote tuna fursa ya kutoa michango kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote. Wanafanya mambo hayo kwa sababu wanampenda Mungu na wanadamu wenzao. Kila juma, tunaonyesha kwamba tunawapenda ndugu na dada zetu kwa kuhudhuria na kushiriki kwenye mikutano ya kutaniko. Ingawa huenda tukawa tumechoka, bado tunahudhuria mikutano hiyo. Ingawa huenda tuna wasiwasi, bado tunatoa maelezo. Na ingawa sote tuna matatizo ya kibinafsi, tunawatia moyo wengine kabla au baada ya mkutano. (Ebr. 10:24, 25) Tunathamini sana kazi inayofanywa na wahubiri wenzetu!

12. Yohana aliwaonyesha upendo ndugu na dada zake kwa njia gani nyingine?

12 Yohana hakuonyesha kwamba anawapenda ndugu na dada zake kwa kuwapongeza tu, bali pia kwa kuwashauri. Kwa mfano, katika barua zake, Yohana aliwapongeza ndugu na dada zake kwa imani yao na matendo yao mazuri, lakini aliwapa pia shauri la moja kwa moja kuhusu dhambi. (1 Yoh. 1:8–2:1, 13, 14) Vivyo hivyo, tunahitaji kuwapongeza ndugu na dada zetu kwa mambo mazuri wanayofanya. Lakini ikiwa ndugu au dada fulani anasitawisha mtazamo au zoea fulani baya, tunaweza kumwonyesha upendo kwa kumwambia kwa busara jambo analohitaji kusikia. Inahitaji ujasiri ili kumpa rafiki yetu shauri, lakini Biblia inasema kwamba marafiki wa kweli huonyana au kurekebishana.—Met. 27:17.

13. Tunapaswa kuepuka kufanya nini?

13 Nyakati nyingine tunaonyesha kwamba tunawapenda ndugu na dada zetu kupitia mambo ambayo hatufanyi. Kwa mfano, hatukwaziki haraka kwa sababu ya mambo wanayosema. Fikiria jambo lililotokea karibu na mwishoni mwa maisha ya Yesu hapa duniani. Aliwaambia wanafunzi wake kwamba ili kupata uzima walihitaji kula mwili wake na kunywa damu yake. (Yoh. 6:53-57) Maneno hayo yalikuwa yenye kushtua sana hivi kwamba wanafunzi wake wengi walimwacha—lakini marafiki zake wa kweli kutia ndani Yohana, hawakumwacha. Waliendelea kushikamana naye. Hawakuelewa kile ambacho Yesu alisema, na inaelekea walishangazwa na maneno yake. Hata hivyo, marafiki washikamanifu wa Yesu hawakufikiri kwamba mambo aliyosema hayakuwa sahihi na kukwazwa nayo. Badala yake walimtumaini, wakijua kwamba alisema kweli. (Yoh. 6:60, 66-69) Ni jambo la muhimu sana kwamba tusikwazike haraka kwa sababu ya mambo ambayo rafiki zetu watasema! Badala yake, tunawapa fursa watueleze walichomaanisha.—Met. 18:13; Mhu. 7:9.

14. Kwa nini haturuhusu kamwe chuki isitawi mioyoni mwetu?

14 Pia, Yohana alituhimiza tusiwachukie ndugu au dada zetu. Ikiwa hatutatii shauri hilo, Shetani anaweza kutushawishi. (1 Yoh. 2:11; 3:15) Hilo liliwapata baadhi ya watu mwishoni mwa karne ya kwanza W.K. Shetani alikuwa akifanya yote ambayo angeweza ili kuchochea chuki na kuwagawa watu wa Mungu. Kufikia wakati ambapo Yohana alikuwa akiandika barua zake, watu walioonyesha roho kama ya Shetani walikuwa sehemu ya kutaniko. Kwa mfano, Diotrefe alikuwa akisababisha migawanyiko mikubwa kutanikoni. (3 Yoh. 9, 10) Hakuwa akiwaheshimu wazee waliosafiri waliotumwa na baraza lililoongoza. Hata alijaribu kuwatupa nje ya kutaniko wale waliowakaribisha watu ambao hakuwapenda. Hilo lilikuwa jambo baya sana! Bado Shetani anajaribu sana kusababisha migawanyiko ili kuwashinda watu wa Mungu leo. Tusiruhusu kamwe chuki itugawe.

IPENDE FAMILIA YAKO

Yesu alimwomba Yohana amtunze mama yake kimwili na kiroho. Leo, ni lazima vichwa vya familia washughulikie mahitaji ya familia zao (Tazama fungu la 15 na 16)

15. Ni lazima kichwa cha familia akumbuke nini?

15 Njia moja muhimu ambayo kichwa cha familia anaweza kuonyesha kwamba anaipenda familia yake ni kwa kuiandalia mahitaji ya kimwili. (1 Tim. 5:8) Hata hivyo, ni lazima akumbuke kwamba vitu vya kimwili haviwezi kutosheleza mahitaji ya kiroho ya familia yake. (Mt. 5:3) Ona mfano ambao Yesu aliwawekea vichwa vya familia. Kulingana na Injili ya Yohana, Yesu alipokuwa akifa kwenye mti wa mateso, bado alikuwa akiifikiria familia yake. Yohana alikuwa amesimama na Maria, mama wa Yesu, mahali ambapo Yesu alikuwa akiuawa. Licha ya kuwa na maumivu makali, Yesu alifanya mipango ili Yohana amtunze Maria. (Yoh. 19:26, 27) Yesu alikuwa na ndugu wa kimwili ambao bila shaka wangemwandalia Maria mahitaji yake ya kimwili, lakini inaonekana kufikia wakati huo hakuna hata mmoja kati yao aliyekuwa mwanafunzi wa Yesu. Hivyo, Yesu alitaka kuhakikisha kwamba Maria angetuzwa kimwili na pia kiroho.

16. Yohana alikuwa na majukumu gani?

16 Yohana alikuwa na majukumu mengi. Akiwa mmoja wa mitume, aliongoza katika kazi ya kuhubiri. Huenda pia alikuwa ameoa, hivyo huenda alihitaji kupanga ratiba iliyosawazika ili kuiandalia familia yake mahitaji ya kimwili na vilevile kuiandalia mahitaji ya kiroho. (1 Kor. 9:5) Vichwa vya familia leo wanajifunza nini?

17. Kwa nini ni muhimu kwa kichwa cha familia kuhakikisha anaiandalia familia yake mahitaji ya kiroho?

17 Huenda ndugu ambaye ni kichwa cha familia akawa na majukumu mengi mazito. Kwa mfano, anapokuwa katika kazi yake ya kimwili ni lazima aifanye kwa bidii kazi hiyo ili aliletee sifa jina la Yehova. (Efe. 6:5, 6; Tito 2:9, 10) Na huenda ana majukumu kutanikoni, kama vile uchungaji na kuongoza katika kazi ya kuhubiri. Wakati huohuo, ni muhimu ajifunze Biblia kwa ukawaida na mke na watoto wake. Watathamini sana jitihada zake za kuwasaidia wawe na afya kimwili, kihisia, na kiroho.—Efe. 5:28, 29; 6:4.

“KAENI KATIKA UPENDO WANGU”

18. Yohana alikuwa na uhakika gani?

18 Yohana aliishi miaka mingi na kujionea mambo mengi. Alipitia changamoto za aina nyingi ambazo zingeweza kudhoofisha imani yake. Lakini siku zote alifanya yote aliyoweza ili kutii amri za Yesu, kutia ndani amri ya kuwapenda ndugu na dada zake. Na kwa sababu hiyo, Yohana alikuwa na uhakika kwamba Yehova na Yesu walimpenda na kwamba wangempa nguvu za kushinda jaribu lolote. (Yoh. 14:15-17; 15:9, 10; 1 Yoh. 4:16) Hakuna jambo lolote ambalo Shetani au mfumo wake ungeweza kufanya ambalo lingemzuia Yohana kuonyesha upendo wake kwa maneno na matendo.

19. Andiko la 1 Yohana 4:7 linatutia moyo tufanye nini, na kwa nini?

19 Kama Yohana, sisi pia tunaishi katika ulimwengu unaotawaliwa na Shetani, mungu mwenye chuki wa mfumo huu. (1 Yoh. 3:1, 10) Ingawa anataka tuache kuwapenda ndugu na dada zetu, hawezi kufanya hilo liwezekane, isipokuwa sisi wenyewe tumruhusu. Acheni tuazimie kuwapenda ndugu na dada zetu, na tuonyeshe upendo huo kupitia yale tunayosema na kutenda. Tunapoonyesha upendo huo, tutakuwa na shangwe ya kuwa sehemu ya familia ya Yehova, na tutakuwa na maisha yenye furaha kwelikweli.—Soma 1 Yohana 4:7.

WIMBO 88 Nijulishe Njia Zako

^ fu. 5 Inaaminika kwamba mtume Yohana ndiye aliyekuwa “mwanafunzi ambaye Yesu alimpenda.” (Yoh. 21:7) Hivyo, hata ingawa alikuwa kijana, ni lazima alikuwa na sifa nyingi zenye kuvutia. Miaka mingi baadaye, Yehova alimtumia kuandika mambo mengi kuhusu upendo. Makala hii itazungumzia baadhi ya mambo aliyoandika na tutachunguza mambo tunayoweza kujifunza kutokana na mfano wake.

^ fu. 59 MAELEZO YA PICHA: Kichwa cha familia mwenye bidii anashiriki katika kazi ya kutoa misaada, anaunga mkono kazi ya ulimwenguni pote kwa kutoa michango, na amewakaribisha wengine wajiunge naye pamoja na mke na watoto wake katika ibada ya familia.