Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 5

“Kichwa cha Kila Mwanaume Ni Kristo”

“Kichwa cha Kila Mwanaume Ni Kristo”

“Kichwa cha kila mwanaume ni Kristo.”​—1 KO. 11:3.

WIMBO 12 Mungu Mkuu, Yehova

KIFUPI CHA HABARI *

1. Wanaume fulani wanatendea bibi na watoto wao kulingana na nini?

UNAWAZA kuwa “kichwa” cha familia maana yake nini? Wanaume fulani wanatendea bibi na watoto wao kulingana na desturi za kwao, ao kulingana na namna mambo ilikuwa inapitika mu familia yao. Yanita, dada mwenye kuishi Ulaya, anasema hivi: “Kwenye ninaishi, watu wanaamini kabisa kama wanamuke ni wa hali ya chini kuliko wanaume na wanapaswa kuonwa kuwa watumishi.” Na ndugu mwenye anaitwa Luke, mwenye anaishi mu inchi ya Amerika, anasema hivi: “Baba fulani wanaambia watoto wao wanaume kama mwanamuke ni wa kuangalia tu na macho, haiko wa kusikiliza, juu hakuwake na mawazo ya maana.” Lakini, haiko vile njo Yehova anapenda wanaume watendee wanamuke. (Linganisha na Marko 7:13.) Sasa, nini njo inaweza kusaidia mwanaume akuwe kichwa muzuri wa familia?

2. Kichwa cha familia anapaswa kujua nini, na juu ya nini?

2 Ili kuwa kichwa muzuri wa familia, mwanaume anapaswa kwanza kuelewa mambo yenye Yehova anapenda afanye. Anapaswa pia kujua juu ya nini Yehova alianzisha mupango wa ukichwa, na mambo yenye anapaswa kufanya ili kufuata mufano wa Yehova na Yesu. Juu ya nini inaomba mwanaume ajue ile mambo? Juu Yehova amepatia kichwa cha familia mamlaka fulani, na anapenda aitumikishe muzuri.​—Lu. 12:48b.

UKICHWA, MAANA YAKE NINI?

3. 1 Wakorinto 11:3 inatufundisha nini juu ya ukichwa?

3 Soma 1 Wakorinto 11:3. Ile andiko inazungumuzia namna Yehova amepanga familia yake mbinguni na ku dunia. Ukichwa unatia ndani mambo mbili ya maana: mamlaka na kutoa hesabu. Juu Yehova ni “kichwa,” iko na mamlaka yote. Kupitia mupango wa ukichwa, amepatia wengine mamlaka fulani. Lakini, watatoa hesabu juu ya namna wanatumia mamlaka yao. (Ro. 14:10; Efe. 3:14, 15) Yehova amepatia Yesu mamlaka juu ya kutaniko. Lakini, Yesu anapaswa kutoa hesabu kwa Yehova juu ya namna anatutendea. (1 Ko. 15:27) Yehova amepatia pia bwana mamlaka juu ya bibi na watoto wake. Lakini, bwana anapaswa kutoa hesabu kwa Yehova na Yesu juu ya namna anatendea familia yake.​—1 Pe. 3:7.

4. Yehova na Yesu wako na mamlaka ya kufanya nini?

4 Juu Yehova njo Kichwa cha familia yake, mbinguni na ku dunia, iko na mamlaka ya kuwekea watoto wake wote sheria juu ya namna wanapaswa kujiendesha. Na iko na haki ya kuhakikisha kama wanafuata zile sheria. (Isa. 33:22) Juu Yesu njo kichwa cha kutaniko, iko pia na haki ya kuwekea kutaniko sheria na kuhakikisha kama kutaniko linafuata zile sheria.​—Gal. 6:2; Kol. 1:18-20.

5. Kichwa cha familia iko na mamlaka gani, na mamlaka yake iko na mipaka gani?

5 Kama vile Yehova na Yesu, kichwa cha familia iko na mamlaka ya kukamata maamuzi kwa ajili ya familia yake. (Ro. 7:2; Efe. 6:4) Lakini, mamlaka yake iko na mipaka. Kwa mufano, sheria zenye anaweka zinapaswa kutegemea kanuni za Neno la Mungu. (Mez. 3:5, 6) Na kichwa cha familia hana mamlaka ya kuwekea sheria watu wenye hawako mu familia yake. (Ro. 14:4) Pia, wakati watoto wake wanakomaa na kutoka ku nyumba, wanaendelea kumuheshimia, lakini hana tena mamlaka juu yao.​—Mt. 19:5.

JUU YA NINI YEHOVA ALIANZISHA MUPANGO WA UKICHWA?

6. Juu ya nini Yehova alianzisha mupango wa ukichwa?

6 Yehova alianzisha mupango wa ukichwa juu anapenda familia yake. Ule mupango ni zawadi. Ukichwa unasaidia mu familia ya Yehova mukuwe amani na utaratibu. (1 Ko. 14:33, 40) Kama hakungekuwa ukichwa, ni kusema, kama hakungekuwa wenye kusimamia mambo, mu familia ya Yehova mungekuwa muvurugo na hamungekuwa furaha. Kwa mufano, hakuna mwenye angejua ni nani anapaswa kukamata maamuzi ya mwisho na mwenye anapaswa kuhakikisha kama ile maamuzi inatimizwa.

7. Kulingana na Waefeso 5:25, 28, Yehova alipenda wanaume wakuwe wanatawala wanamuke?

7 Kama ni muzuri wanaume wakuwe na mamlaka katika familia, juu ya nini wanamuke wengi wanaona kama bwana zao wanawatendea mubaya na kuwatawala? Ni juu, kuliko kufuata kanuni zenye Yehova ameweka kwa ajili ya familia, wanaume wengi wanafuata desturi za kwao. Pia, wanaweza kutendea bibi zao mubaya ili kutimiza tamaa zao wenyewe. Kwa mufano, bwana anaweza kutawala bibi yake ili ajione kuwa mutu wa maana ao ili kuonyesha wengine kama yeye ni “mwanaume kabisa.” Anaweza kuwaza hivi: ‘Siwezi kulazimisha bibi yangu anipende, lakini naweza kufanya aniogope.’ Na anaweza kutumia ile woga ili kumutawala. * Wanaume wenye kuwa na ile mawazo na wenye kutendea bibi zao vile hawapatie bibi zao heshima yenye wanastahili, na ile ni kinyume na mapenzi ya Yehova.​—Soma Waefeso 5:25, 28.

NI NINI INAWEZA KUSAIDIA MWANAUME AKUWE KICHWA MUZURI WA FAMILIA?

8. Ni nini inaweza kusaidia mwanaume akuwe kichwa muzuri wa familia?

8 Kuiga namna Yehova na Yesu wanatumia mamlaka yao inaweza kusaidia mwanaume akuwe kichwa muzuri wa familia. Yehova na Yesu wanaonyeshaka sifa mingi. Lakini, tufikirie tu sifa mbili na tuone namna kichwa cha familia anaweza kuonyesha bibi yake na watoto wake zile sifa.

9. Namna gani Yehova anaonyeshaka unyenyekevu?

9 Unyenyekevu. Yehova iko na hekima kuliko mutu mwingine yeyote. Lakini, anasikilizaka mawazo ya watumishi wake. (Mwa. 18:23, 24, 32) Alipatia wale wenye kuwa chini ya mamlaka yake nafasi ya kutoa mapendekezo yao. (1 Fa. 22:19-22) Yehova ni mukamilifu, lakini kwa sasa, hatazamie tufanye mambo kwa ukamilifu. Tofauti na ile, anasaidiaka wanadamu wenye hawakamilike wenye wanamutumikia. (Zb. 113:6, 7) Biblia hata inamuita Yehova kuwa “musaidizi.” (Zb. 27:9; Ebr. 13:6) Mufalme Daudi alitambua kama ni unyenyekevu wa Yehova tu njo ulimuwezesha kutimiza mambo yote yenye alifanya.​—2 Sa. 22:36.

10. Namna gani Yesu alionyesha unyenyekevu?

10 Fikiria mufano wa Yesu. Hata kama alikuwa Bwana na Mwalimu wa wanafunzi wake, aliwanawisha miguu. Ni sababu gani moja yenye ilifanya Yehova aandikishe ile habari mu Biblia? Alifanya vile ili kutolea kila mutu mufano wa kufuata, hata vichwa vya familia. Yesu mwenyewe alisema hivi: “Niliwawekea ninyi mufano, ili kama vile niliwafanyia ninyi, ninyi pia mufanye vilevile.” (Yoh. 13:12-17) Hata kama alikuwa na mamlaka, Yesu hakuwaza kama wengine njo wanapaswa kumutumikia. Lakini, yeye njo alitumikia wengine.​—Mt. 20:28.

Kichwa cha familia anaweza kuonyesha unyenyekevu na upendo kwa kufanya kazi za ku nyumba na kutimiza mahitaji ya kiroho ya familia yake (Ona fungu la 11, 13)

11. Namna Yehova na Yesu wanaonyesha unyenyekevu inaweza kufundisha nini kichwa cha familia?

11 Mambo yenye tunajifunza. Kichwa cha familia anaweza kuonyesha unyenyekevu mu njia za mingi. Kwa mufano, hatazamie bibi na watoto wake wafanye mambo kwa ukamilifu. Anasikilizaka mawazo ya watu wa familia yake, hata kama haipatane na yake. Marley, mwenye anaishi mu inchi ya Amerika, anasema hivi: “Wakati fulani, miye na bwana yangu tunakuwaka na mawazo tofauti. Lakini, ninajua kama anaona mawazo yangu kuwa ya maana na ananiheshimia kwa sababu ananiulizaka mawazo yangu na anaifikiriaka mbele akamate uamuzi.” Zaidi ya ile, bwana munyenyekevu iko tayari kufanya kazi za ku nyumba, hata kama fasi kwenye anaishi watu wanaona kama zile kazi ni za mwanamuke. Haiko mwepesi kufanya vile. Juu ya nini? Dada mwenye kuitwa Rachel anasema hivi: “Kwetu, kama mwanaume anasaidia bibi yake kusafisha masahani ao kusafisha nyumba, majirani na watu wa jamaa wanawazaka kama haiko ‘mwanaume kabisa.’ Na wanawazaka kama bibi yake alishamutawala.” Kama fasi kwenye unaishi watu wako na ile mawazo, ukumbuke kama Yesu alinawishaka wanafunzi wake miguu, hata kama watu wengi waliona kuwa ile ni kazi ya mutumwa. Kichwa muzuri wa familia hatafutake kujionyesha kama yeye njo “mwanaume kabisa,” anatafutaka njo kufurahisha bibi na watoto wake. Zaidi ya unyenyekevu, kichwa muzuri wa familia iko na lazima ya sifa gani ingine?

12. Upendo unachochea Yehova na Yesu kufanya nini?

12 Upendo. Kila kitu chenye Yehova anafanya, anakifanya kwa sababu anatupenda. (1 Yo. 4:7, 8) Kwa upendo, anatutimizia mahitaji yetu ya kiroho kwa kutupatia Neno lake Biblia, na tengenezo lake. Anatutimizia pia mahitaji yetu ya kihisia, ni kusema anafanya tujisikie kuwa salama kwa kutuhakikishia kama anatupenda. Halafu mahitaji yetu ya kimwili? Yehova “anatupatia kwa wingi vitu vyote vyenye tunafurahia.” (1 Ti. 6:17) Wakati tunakosea, anaturekebisha, lakini haache kutupenda. Kwa sababu Yehova anatupenda, alitoa bei ya ukombozi kwa ajili yetu. Yesu pia alionyesha kama anatupenda kwa kukubali kufa kwa ajili yetu. (Yoh. 3:16; 15:13) Hakuna kitu kinaweza kufanya Yehova na Yesu waache kupenda wale wenye kuwa washikamanifu kwao.​—Yoh. 13:1; Ro. 8:35, 38, 39.

13. Juu ya nini ni jambo la maana kichwa cha familia aonyeshe familia yake upendo? (Ona pia kisanduku “ Kama Umetoka Tu Kuoa, Namna Gani Unaweza Kufanya Bibi Yako Akuheshimie?”)

13 Mambo yenye tunajifunza. Kila kitu chenye kichwa cha familia anafanya, anapaswa kukifanya kwa sababu ya upendo. Juu ya nini ni jambo la maana afanye vile? Mutume Yohana anajibia hivi: “Mutu mwenye hamupendi ndugu [ao familia] yake, mwenye anaona, hawezi kumupenda Mungu mwenye hajaonaka.” (1 Yo. 4:11, 20) Mwanaume mwenye anapenda familia yake na mwenye anapenda kufuata mufano wa Yehova na Yesu, anapaswa kutimizia familia yake mahitaji ya kiroho, ya kihisia, na ya kimwili. (1 Ti. 5:8) Anapaswa kufundisha watoto wake na kuwarekebisha. Anapaswa pia kuendelea kujifunza namna ya kukamata maamuzi yenye inamutukuza Yehova na yenye italetea familia yake faida. Tuzungumuzie basi ile mambo yenye kichwa cha familia anapaswa kufanya na tuone namna anaweza kufuata mufano wa Yehova na Yesu.

MAMBO YENYE KICHWA CHA FAMILIA ANAPASWA KUFANYA

14. Namna gani kichwa cha familia anaweza kutimiza mahitaji ya kiroho ya familia yake?

14 Kutimiza mahitaji ya kiroho ya familia yake. Yesu alifuata mufano wa Baba yake. Njo maana, alitimiza mahitaji ya kiroho ya wafuasi wake. (Mt. 5:3, 6; Mk. 6:34) Vilevile, jambo la maana sana lenye kichwa cha familia anapaswa kuhangaikia ni kutimiza mahitaji ya kiroho ya familia yake. (Kum. 6:6-9) Anafanya vile kwa kukamata mipango ili yeye na familia yake wakuwe wanasoma na kujifunza Neno la Mungu, kuhuzuria mikutano, kuhubiri habari njema, na kuendelea kuwa na urafiki muzuri pamoja na Yehova.

15. Kichwa cha familia anaweza kufanya nini ili watu wa familia yake wajisikie kuwa wanapendwa?

15 Kufanya watu wa familia yake wajisikie kuwa wanapendwa. Yehova aliambia Yesu mbele ya watu wengine kama anamupenda. (Mt. 3:17) Yesu naye alionyesha kama anapenda wafuasi wake, kupitia mambo yenye alifanya na kusema. Wafuasi wake pia walimuambia kama wanamupenda. (Yoh. 15:9, 12, 13; 21:16) Kichwa cha familia anaweza kuonyesha kama anapenda bibi na watoto wake kupitia mambo yenye anafanya, kwa mufano kwa kujifunza nao Biblia. Anapaswa pia kuwaambia kama anawapenda na kama anawaona kuwa wa maana. Na wakati inafaa, anapaswa kuwapongeza mbele ya watu wengine.​—Mez. 31:28, 29.

Ili kumufurahisha Yehova, kichwa cha familia anapaswa kutimiza mahitaji ya kimwili ya familia yake (Ona fungu la 16)

16. Kichwa cha familia anapaswa kufanya nini ingine, na namna gani anaweza kuonyesha usawaziko?

16 Kutimiza mahitaji ya kimwili ya familia yake. Yehova alipatia Waisraeli mambo yenye walikuwa nayo lazima hata wakati alikuwa anawapatia malipizi kwa sababu ya kukosa kutii. (Kum. 2:7; 29:5) Sisi pia, anatupatia mambo yenye tuko nayo lazima leo. (Mt. 6:31-33; 7:11) Vilevile, Yesu alikulisha wale wenye walikuwa wanamufuata. (Mt. 14:17-20) Aliponyesha pia magonjwa yao. (Mt. 4:24) Ili kumufurahisha Yehova, kichwa cha familia anapaswa kutimiza mahitaji ya kimwili ya familia yake. Lakini, anapaswa kuwa na usawaziko. Hapaswe kuruhusu kazi yenye anafanya ili kutimiza mahitaji ya kimwili ya familia yake imukamate wakati mingi sana, mupaka ashindwe kutimiza muzuri mahitaji ya kiroho ya familia yake na kufanya watu wa familia yake wajisikie kuwa wanapendwa.

17. Namna gani Yehova na Yesu wanatufundishaka na kuturekebisha?

17 Kufundisha watu wa familia yake. Yehova anatufundishaka na kuturekebisha ili kutusaidia. (Ebr. 12:7-9) Kama Baba yake, Yesu anafundishaka kwa upendo wale wenye kuwa chini ya mamlaka yake. (Yoh. 15:14, 15) Anawatoleaka mashauri mazito lakini kwa upole. (Mt. 20:24-28) Anaelewa kama tuko wanadamu wenye hawakamilike, kwa hiyo tuko na muelekeo wa kufanya makosa.​—Mt. 26:41.

18. Kichwa muzuri wa familia anakumbuka nini?

18 Kichwa cha familia mwenye anafuata mufano wa Yehova na Yesu anakumbuka kama bibi na watoto wake hawakamilike. Kwa hiyo, ‘hawakasirikie kwa uchungu.’ (Kol. 3:19) Kuliko kufanya vile, anatumikisha kanuni yenye iko mu Wagalatia 6:1 na anajikaza kuwarekebisha “kwa roho ya upole,” bila kusahau kama yeye pia hakamilike. Kama Yesu, anatambua kama mufano wake njo njia ya muzuri ya kuwafundisha.​—1 Pe. 2:21.

19-20. Namna gani kichwa cha familia anaweza kufuata mufano wa Yehova na Yesu wakati anakamata maamuzi?

19 Kukamata maamuzi yenye italetea familia yake faida. Yehova anakamataka maamuzi yenye italetea wengine faida. Kwa mufano, aliamua kutuumba na kuumba vitu vingine, haiko kwa faida yake mwenyewe lakini ili sisi pia tufurahie maisha. Hakuna mutu mwenye alimukaza atoe Mwana wake ili akufe kwa ajili ya zambi zetu. Aliamua kufanya vile ili kutusaidia. Yesu pia alikuwa anakamata maamuzi yenye ingesaidia wengine. (Ro. 15:3) Kwa mufano, wakati fulani, hata kama alikuwa na lazima ya kupumuzika, aliamua kufundisha kikundi cha watu wengi.​—Mk. 6:31-34.

20 Kichwa muzuri wa familia anajua kama jambo la nguvu lenye anapaswa kufanya ni kukamata maamuzi ya muzuri kwa ajili ya familia yake. Na anakamata ile daraka kwa uzito. Anaepuka kukamata maamuzi bila kufikiri ao kukamata maamuzi yenye inategemea namna iko anajisikia ile wakati. Kuliko kufanya vile, anaacha Yehova amufundishe namna ya kukamata maamuzi ya muzuri. * (Mez. 2:6, 7) Ile itamusaidia akuwe anakamata maamuzi yenye italetea wengine faida, kuliko kujiletea yeye mwenyewe faida.​—Flp. 2:4.

21. Habari yenye inafuata itajibia maulizo gani?

21 Yehova amepatia kichwa cha familia daraka nzito. Na kichwa cha familia atatoa hesabu juu ya namna anatimiza ile daraka. Lakini, kama bwana anajikaza kufuata mufano wa Yehova na Yesu, atakuwa kichwa muzuri wa familia. Na kama bibi anafanya mambo yenye Maandiko inamuomba, ndoa itakuwa na furaha. Namna gani bibi anapaswa kuona ukichwa? Na bibi anapambanaka na matatizo gani? Habari yenye inafuata itajibia ile maulizo.

WIMBO 16 Msifuni Yah kwa Mwana Wake Mtiwa Mafuta

^ fu. 5 Wakati mwanaume anaoa, anakuwa kichwa cha familia. Mu hii habari, tutazungumuzia maana ya ukichwa, juu ya nini Yehova alianzisha mupango wa ukichwa, na mambo yenye wanaume wanaweza kujifunza kupitia mufano wa Yehova na Yesu. Mu habari ya pili, tutaona mambo yenye bibi na bwana wanaweza kujifunza kupitia mufano wa Yesu na mifano ingine yenye inazungumuziwa mu Biblia. Na mu habari ya tatu, tutazungumuzia ukichwa mu kutaniko.

^ fu. 7 Wazo la kwamba ni sawa mwanaume kutendea mubaya bibi yake, na hata kumutendea mubaya kimwili limeonyeshwa wakati fulani katika filme, teatre, na vitabu vya kuchekesha. Ile imefanya watu wawaze kama haiko mubaya mwanaume kutawala bibi yake.

^ fu. 20 Ili kupata habari zaidi juu ya namna ya kukamata maamuzi ya muzuri, ona habari “Fanya Maamuzi Ambayo Yanamletea Mungu Heshima,” yenye ilitolewa mu Munara wa Mulinzi wa tarehe 15, Mwezi wa 4, 2011, uku. 13-17.