Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Sababu tu ya Tabasamu!

Kwa Sababu tu ya Tabasamu!

WANAWAKE wawili vijana walikuwa wakitembea pamoja kwenye eneo la biashara katika jiji la Baguio, nchini Ufilipino. Walikiona kigari cha mahubiri ya hadharani, lakini hawakukisogelea. Helen, dada aliyekuwa amesimama kando ya kigari hicho, aliwaonyesha tabasamu kubwa. Wanawake hao waliendelea na safari yao, lakini walipendezwa na tabasamu yenye uchangamfu ya Helen.

Baadaye, wanawake hao walipokuwa wakirudi nyumbani wakiwa kwenye basi, waliona ubao mkubwa wenye ishara ya jw.org kwenye Jumba la Ufalme. Walikumbuka kwamba yalikuwa maandishi yaleyale yaliyokuwa kwenye kigari cha mahubiri ya hadharani. Wakashuka kwenye basi na kuangalia ratiba ya mikutano ya makutaniko mbalimbali yaliyoorodheshwa kwenye lango la Jumba la Ufalme.

Wanawake hao wawili walihudhuria mojawapo ya mikutano iliyofuata. Na ni nani waliyemwona walipoingia ndani ya Jumba la Ufalme? Helen! Walitambua mara moja kwamba yeye ndiye aliyewaonyesha tabasamu kubwa siku ile. Helen anasema, “Waliponifuata, nilipata wasiwasi kidogo. Nilifikiri labda nimefanya jambo fulani baya.” Lakini wanawake hao walimwambia Helen kilichokuwa kimetukia.

Wanawake hao vijana walifurahia mkutano na ushirika; walijihisi wakiwa nyumbani. Walipowaona wengine wakifanya usafi wa jumba baada ya mkutano, waliomba ikiwa wao pia wangeweza kusaidia. Mmoja kati ya wanawake hao aliondoka nchini, lakini mwingine alianza kuhudhuria mikutano na kujifunza Biblia—kwa sababu tu ya tabasamu!