Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Mtume Paulo alimaanisha nini aliposema: “Kupitia sheria nilikufa kuielekea sheria”?—Gal. 2:19.

Paulo aliandika hivi: “Kupitia sheria nilikufa kuielekea sheria, ili niwe hai kumwelekea Mungu.”—Gal. 2:19.

Jambo ambalo Paulo aliandika lilipatana na wazo kuu ambalo alikuwa akiwasilisha kwa makutaniko yaliyokuwa kwenye mkoa wa Galatia huko Roma. Baadhi ya Wakristo huko walikuwa wakishawishiwa na walimu wa uwongo. Wanaume hao walikuwa wakifundisha kwamba ili mtu apate wokovu alihitaji kushika Sheria ya Musa, hasa tohara. Lakini Paulo alijua kwamba Mungu hakuhitaji tena waabudu wake watahiriwe. Kwa usadikisho wenye nguvu, alipinga mafundisho ya uwongo na kuimarisha imani ya akina ndugu katika dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo.—Gal. 2:4; 5:2.

Biblia inasema wazi kwamba mtu anapokufa, hajui jambo lolote au hawezi kuathiriwa na kitu chochote kinachomzunguka. (Mhu. 9:5) Paulo aliposema: “Nilikufa kuielekea sheria,” alimaanisha kwamba Sheria ya Musa haikuwa tena na mamlaka yoyote juu yake. Badala yake, Paulo alikuwa na uhakika kwamba kwa kuwa na imani katika dhabihu ya fidia, alikuwa “hai kumwelekea Mungu.”

Badiliko katika hali ya Paulo lilikuja “kupitia sheria.” Jinsi gani? Alikuwa ametoka tu kueleza kwamba “mtu hutangazwa kuwa mwadilifu, si kupitia matendo ya sheria, bali kupitia tu imani katika Yesu Kristo.” (Gal. 2:16) Sheria ilikuwa imetimiza jambo muhimu sana. Paulo aliwaambia hivi Wagalatia: “Iliongezwa ili kufanya makosa yawe wazi, mpaka ufike ule uzao ambao ulikuwa umepewa ahadi.” (Gal. 3:19) Naam, Sheria iliweka wazi kwamba wanadamu wasio wakamilifu na watenda dhambi hawangeweza kuishika kikamili Sheria na kwamba walihitaji dhabihu kamilifu ambayo haingehitaji kutolewa tena. Hivyo, Sheria iliwaongoza watu kwa “ule uzao,” yaani, Kristo. Kwa kumwamini Yesu Kristo, mtu angeweza kutangazwa na Mungu kuwa mwadilifu. (Gal. 3:24) Paulo alifikia mkataa huo kwa sababu kupitia Sheria alikuja kumkubali na kumwamini Yesu. Hivyo, Paulo akawa ‘amekufa kuielekea sheria’ na kuwa “hai kumwelekea Mungu.” Sheria haikuwa na mamlaka tena juu yake, lakini Mungu alikuwa nayo.

Paulo alieleza wazo kama hilo katika barua yake kwa Waroma. Alisema hivi: “Ndugu zangu, ninyi pia mlifanywa wafu kuhusiana na Sheria kupitia mwili wa Kristo . . . Tumewekwa huru kutoka katika Sheria, kwa sababu tumekufa kwa kile ambacho kilituzuia.” (Rom. 7:4, 6) Andiko hilo na pia Wagalatia 2:19, yanafunua kwamba Paulo hakuwa akizungumzia kuhusu kifo kinachotokana na kuhukumiwa dhambi chini ya Sheria. Badala yake, alikuwa kihususa akizungumza kuhusu kuwekwa huru. Sheria haikuwa na mamlaka juu yake na wengine walio kama yeye. Waliwekwa huru kupitia imani katika fidia ya Kristo.