Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 30

Thamini Sehemu Yako Katika Familia ya Yehova

Thamini Sehemu Yako Katika Familia ya Yehova

“Ulimfanya awe mdogo kidogo kuliko malaika, nawe ukamvika taji la utukufu na fahari.”—ZAB. 8:5, maelezo ya chini.

WIMBO 123 Kutii Utaratibu wa Kitheokrasi kwa Ushikamanifu

MUHTASARI *

1. Huenda tukajiuliza swali gani tunapotafakari kuhusu vitu vyote ambavyo Yehova ameumba?

TUNAPOTAFAKARI kuhusu ulimwengu wote ambao Yehova aliumba, huenda tukahisi kama mtunga zaburi Daudi, aliyesali hivi: “Ninapoziona mbingu zako, kazi za vidole vyako, mwezi na nyota ambazo umetayarisha, mwanadamu anayeweza kufa ni nini hivi kwamba unamweka akilini, na mwana wa mtu hivi kwamba unamtunza?” (Zab. 8:3, 4) Kama Daudi, huenda tukahisi sisi ni wadogo sana tunapojilinganisha na ulimwengu, na hivyo tukastaajabishwa na wazo la kwamba Yehova hata anatuweka akilini. Hata hivyo, kama tutakavyoona, Yehova hakutambua tu uwepo wa wanadamu wa kwanza Adamu na Hawa, bali pia aliwafanya kuwa sehemu ya familia yake.

2. Kusudi la Yehova kwa watoto wake wa kwanza wa kidunia lilikuwa nini?

2 Adamu na Hawa walikuwa watoto wa kwanza wa Yehova wa kidunia, na Yehova alikuwa Baba yao wa mbinguni aliyewapenda. Aliwapa wenzi hao wa ndoa kazi ya kufanya. Mungu aliwaambia hivi: “Zaeni, muwe wengi, muijaze dunia na kuitiisha.” (Mwa. 1:28) Alitaka wazae watoto na kuitunza vizuri dunia. Ikiwa wangetii na kuunga mkono kusudi la Yehova kwa ajili yao, Adamu na Hawa na wazao wao, wangeendelea kuwa washiriki wa familia ya Mungu milele.

3. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Adamu na Hawa walipewa sehemu yenye kuheshimika katika familia ya Yehova?

3 Adamu na Hawa walikuwa na sehemu yenye kuheshimika katika familia ya Yehova. Kama Zaburi 8:5 na maelezo ya chini yanavyoonyesha, alipokuwa akizungumzia uumbaji wa Yehova wa mwanadamu, Daudi alisema hivi: “Ulimfanya awe mdogo kidogo kuliko malaika, nawe ukamvika taji la utukufu na fahari.” Ni kweli kwamba wanadamu hawakupewa nguvu, akili, na uwezo sawa na malaika. (Zab. 103:20) Hata hivyo, mwanadamu ni “mdogo kidogo” tu kuliko viumbe hao wenye nguvu wa kiroho. Hebu wazia hilo! Kwa kweli, Yehova aliwapa wazazi wetu wa kwanza mwanzo mzuri.

4. Adamu na Hawa walipatwa na nini kwa sababu ya kutomtii Yehova, na tutachunguza nini katika makala hii?

 4 Inasikitisha kwamba Adamu na Hawa walipoteza sehemu yao katika familia ya Yehova. Hilo limesababisha matokeo mabaya sana kwa wazao wao, kama tutakavyoona katika makala hii. Lakini kusudi la Yehova halijabadilika. Anataka wanadamu watiifu wawe watoto wake milele. Kwanza, acheni tuchunguze jinsi ambavyo Yehova ametuonyesha heshima. Kisha, tutachunguza mambo tunayoweza kufanya sasa ili kuonyesha kwamba tunataka kuwa sehemu ya familia ya Mungu. Mwishowe, tutachunguza baraka ambazo watoto wa Yehova walio duniani watafurahia milele.

YEHOVA AMEWAONYESHAJE HESHIMA WANADAMU?

Yehova ametuonyesha heshima katika njia zipi? (Tazama fungu la 5 hadi 11) *

5. Tunaweza kumwonyeshaje Mungu kuwa tunathamini kwamba alituumba kwa mfano wake?

5 Yehova ametuonyesha heshima kwa kutuumba kwa mfano wake. (Mwa. 1:26, 27) Kwa sababu tuliumbwa kwa mfano wa Mungu, tunaweza kusitawisha na kuonyesha sifa zake nyingi nzuri kama vile upendo, huruma, ushikamanifu, na uadilifu. (Zab. 86:15; 145:17) Tunapositawisha sifa hizo, tunamtukuza Yehova na kuthibitisha kwamba tunathamini yote aliyotufanyia. (1 Pet. 1:14-16) Tunapotenda kwa njia inayompendeza Baba yetu wa mbinguni, tunakuwa na furaha na wenye kuridhika. Na alipotuumba kwa mfano wake, Yehova alitupatia uwezo wa kuwa aina ya watu ambao anawataka katika familia yake.

6. Yehova aliwaonyeshaje heshima wanadamu alipoiandaa dunia?

6 Yehova alituandalia makao ya pekee. Muda mrefu kabla ya kumuumba mwanadamu wa kwanza, Yehova aliandaa dunia kwa ajili ya wanadamu. (Ayu. 38:4-6; Yer. 10:12) Kwa sababu Yehova ni mwenye ufikirio na mkarimu, alituandalia vitu vingi vizuri ili tuvifurahie. (Zab. 104:14, 15, 24) Pindi fulani, alitafakari kuhusu kazi yake ya uumbaji na ‘akaona kuwa vitu alivyoumba ni vyema.’ (Mwa. 1:10, 12, 31) Aliwaonyesha heshima wanadamu kwa kuwapa “mamlaka juu” ya kazi zake zote maridadi duniani. (Zab. 8:6) Kusudi la Mungu ni kwamba wanadamu wakamilifu wafurahie kutunza kazi hizo maridadi milele. Je, unamshukuru Yehova kwa ukawaida kwa ajili ya ahadi hiyo nzuri sana?

7. Andiko la Yoshua 24:15 linaonyeshaje kwamba mwanadamu ana uhuru wa kuchagua?

7 Yehova ametupatia zawadi ya uhuru wa kuchagua. Tunaweza kuchagua mambo tunayotaka kufanya maishani. (Soma Yoshua 24:15.) Mungu wetu mwenye upendo anashangilia tunapochagua kumtumikia. (Zab. 84:11; Met. 27:11) Tunaweza kutumia vizuri uhuru wetu wa kuchagua katika njia nyingine nyingi. Kwa mfano, fikiria kielelezo kilichowekwa na Yesu.

8. Taja njia moja ambayo Yesu alitumia uhuru wake wa kuchagua.

8 Tunaweza kufuata mfano wa Yesu kwa kuchagua kutanguliza mapendezi ya wengine. Pindi moja, Yesu na mitume wake walipokuwa wamechoka sana, walienda kwenye eneo lililotulia ili waweze kupumzika. Hata hivyo, hawakufaulu kupumzika. Umati wa watu uliwafuata na walikuwa na hamu ya kufundishwa na Yesu. Lakini Yesu hakukasirika. Badala yake, aliwahurumia watu hao. Hivyo Yesu akafanya nini? “Akaanza kuwafundisha mambo mengi.” (Marko 6:30-34) Tunapomwiga Yesu kwa kudhabihu muda na nguvu zetu ili kuwasaidia wengine, tunamtukuza Baba yetu wa mbinguni. (Mt. 5:14-16) Pia, tunamwonyesha Yehova kwamba tunataka kuwa sehemu ya familia yake.

9. Wazazi wanapaswa kuweka akilini jambo gani?

9 Yehova amewapa wanadamu uwezo wa kupata watoto na pia wajibu wa kuwafundisha wampende na kumtumikia yeye. Ikiwa wewe ni mzazi, je, unathamini zawadi hiyo ya pekee? Ingawa malaika wamebarikiwa sana na Yehova, hawajapewa pendeleo hilo. Wakiwa na hilo akilini, wale wanaolea watoto wanapaswa kuthamini pendeleo walilo nalo la kuwatunza. Wazazi wamepewa amana, wajibu mtakatifu wa kuwalea watoto wao katika “nidhamu na maagizo ya Yehova.” (Efe. 6:4; Kum. 6:5-7; Zab. 127:3) Ili kuwasaidia wazazi, tengenezo la Mungu limeandaa vifaa vingi vinavyotegemea Biblia, kama vile machapisho, video, muziki, na habari mtandaoni. Ni wazi kwamba Baba yetu wa mbinguni na Mwana wake wanawathamini watoto wetu. (Luka 18:15-17) Wazazi wanapomtegemea Yehova na kufanya yote wanayoweza ili kuwatunza watoto wao wenye thamani, Yehova anafurahi. Na wazazi hao wanawasaidia watoto wao kuwa na tumaini la kuwa sehemu ya familia ya Yehova milele!

10-11. Yehova amefanya jambo gani liwezekane kupitia dhabihu ya fidia?

10 Yehova alimtoa Mwana wake anayempenda zaidi ili tuweze kuwa washiriki wa familia Yake tena. Kama ilivyotajwa kwenye  fungu la 4, Adamu na Hawa walipotenda dhambi hawangeweza tena kuwa washiriki wa familia ya Yehova, na watoto wao pia. (Rom. 5:12) Adamu na Hawa waliamua kimakusudi kutomtii Mungu, hivyo walistahili kuondolewa kwenye familia ya Yehova. Lakini namna gani wazao wao? Kwa upendo, Yehova aliandaa mpango ili wale wanaostahili kati ya wazao wa Adamu, waweze kufanywa kuwa wana katika familia yake. Alifanya hivyo kupitia dhabihu ya Mwana wake mzaliwa pekee, Yesu Kristo. (Yoh. 3:16; Rom. 5:19) Kwa sababu ya dhabihu ya Yesu, wanadamu watimilifu 144,000 wanafanywa kuwa wana wa Mungu.—Rom. 8:15-17; Ufu. 14:1.

11 Kwa kuongezea, mamilioni ya wanadamu wengine waaminifu wanafanya mapenzi ya Yehova kwa utiifu. Wana tumaini la kuwa washiriki kamili katika familia ya Mungu baada ya jaribu la mwisho, yaani, mwishoni mwa ile Miaka Elfu Moja. (Zab. 25:14; Rom. 8:20, 21) Wakiwa na tumaini hilo akilini, hata sasa wanamwita “Baba,” Yehova, Muumba wao. (Mt. 6:9) Pia, wale watakaofufuliwa watapata fursa ya kujifunza kuhusu mambo ambayo Yehova anatarajia wafanye. Wale watakaokubali kutii mwongozo wake, mwishowe watakuwa washiriki wa familia yake pia.

12. Tutajibu swali gani sasa?

12 Kama tulivyoona, tayari Yehova amefanya mambo mengi ili kuwaonyesha heshima wanadamu. Amewafanya Wakristo watiwa-mafuta kuwa wana, na wale wa “umati mkubwa” amewapa tumaini la kuwa wana kamili katika ulimwengu mpya. (Ufu. 7:9) Tunaweza kufanya nini sasa ili kumwonyesha Yehova kwamba tunataka kuwa sehemu ya familia yake milele?

MWONYESHE YEHOVA KWAMBA UNATAKA KUWA SEHEMU YA FAMILIA YAKE

13. Tunaweza kufanya nini ili tuwe sehemu ya familia ya Mungu? (Marko 12:30)

13 Onyesha upendo wako kwa Yehova kwa kumtumikia kwa moyo wako wote. (Soma Marko 12:30.) Kati ya mambo yote ambayo kwa fadhili Mungu ametupatia, zawadi kubwa zaidi aliyotupatia ni uwezo wa kumwabudu. Tunamwonyesha Yehova kwamba tunampenda kwa ‘kushika amri zake.’ (1 Yoh. 5:3) Akizungumza kwa niaba ya Baba yake, Yesu alituamuru tufanye wanafunzi na kuwabatiza. (Mt. 28:19) Pia, alituamuru tupendane. (Yoh. 13:35) Yehova atawakaribisha wale wanaomtii wawe sehemu ya familia yake ya waabudu wake wa ulimwenguni pote.—Zab. 15:1, 2.

14. Tunaweza kuwaonyeshaje wengine upendo? (Mathayo 9:36-38; Waroma 12:10)

14 Wapende wengine. Upendo ni sifa muhimu zaidi ya Yehova. (1 Yoh. 4:8) Yehova alituonyesha upendo hata kabla ya sisi kumjua. (1 Yoh. 4:9, 10) Tunamwiga tunapowaonyesha wengine upendo. (Efe. 5:1) Mojawapo ya njia bora kabisa tunayoweza kuonyesha kwamba tunawapenda watu, ni kwa kuwasaidia wajifunze kumhusu Yehova muda ungali upo. (Soma Mathayo 9:36-38.) Kwa kufanya hivyo, tunawapa fursa ya kuwa na tumaini la kuwa washiriki wa familia ya Mungu. Baada ya mtu kubatizwa, ni lazima tuendelee kumpenda na kumheshimu. (1 Yoh. 4:20, 21) Hilo linahusisha nini? Kwanza, tutamwamini na kutotilia shaka nia yake. Kwa mfano, ikiwa hatuelewi kwa nini amefanya jambo fulani, hatutafikiria haraka kwamba amefanya hivyo akichochewa na ubinafsi au nia mbaya. Badala yake, tutamwonyesha heshima ndugu yetu, tukimwona kuwa bora kuliko sisi.—Soma Waroma 12:10; Flp. 2:3.

15. Tunapaswa kuwaonyesha nani rehema na fadhili?

15 Waonyeshe watu wote rehema na fadhili. Ikiwa tunataka kuwa miongoni mwa wale watakaoweza kustahili kumwita Yehova, Baba yao milele, ni lazima tutumie Neno la Mungu maishani mwetu. Kwa mfano, Yesu alifundisha kwamba tunapaswa kuwaonyesha watu wote rehema na fadhili, hata maadui wetu. (Luka 6:32-36) Huenda nyakati nyingine tukaona ni vigumu kwetu kufanya hivyo. Ikiwa ndivyo, ni lazima tujifunze kufikiri na kutenda kama Yesu. Tunapofanya yote tunayoweza ili kumtii Yehova na kumwiga Yesu, tunamwonyesha Baba yetu wa mbinguni kwamba tunataka kuwa sehemu ya familia yake milele.

16. Tunaweza kuilindaje sifa nzuri ya familia ya Yehova?

16 Linda sifa nzuri ya familia ya Yehova. Katika familia halisi, ni kawaida kwa mvulana mdogo kumwiga ndugu yake mkubwa. Ikiwa ndugu mkubwa anatumia kanuni za Biblia maishani mwake, atamwekea mfano mzuri ndugu yake mdogo. Ikiwa ndugu mkubwa anafanya mambo mabaya, huenda ndugu yake mdogo akafuata mfano wake mbaya. Ndivyo ilivyo pia katika familia ya Yehova. Ikiwa Mkristo ambaye awali alikuwa mwaminifu anakuwa mwasi-imani au kujiingiza katika maadili yaliyopotoka, huenda wengine wakashawishiwa kujiunga naye katika kufanya mambo mabaya. Wale wanaofanya hivyo, wanaharibu sifa nzuri ya familia ya waabudu wa Yehova. (1 The. 4:3-8) Ni lazima tuepuke kufuata mifano mibaya na kutoruhusu jambo lolote liharibu uhusiano wetu mzuri pamoja na Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo.

17. Tunapaswa kuepuka mtazamo gani, na kwa nini?

17 Mtumaini Yehova badala ya vitu vya kimwili. Yehova anaahidi kwamba atatuandalia chakula, mavazi, na malazi ikiwa tutatafuta Ufalme kwanza na kuishi kulingana na viwango vyake vya uadilifu. (Zab. 55:22; Mt. 6:33) Tukiwa na hilo akilini, tunaepuka mtazamo wa kwamba vitu vya kimwili katika ulimwengu huu, vitatupatia usalama na furaha ya kudumu. Tunajua kwamba njia pekee inayoweza kutupatia amani ya kweli ya akili ni kufanya mapenzi ya Yehova. (Flp. 4:6, 7) Hata kama tunaweza kununua vitu vingi, ni lazima tufikirie ikiwa kwa kweli tuna muda na nguvu za kutumia na kuvitunza vitu hivyo. Je, tunaweza kuanza kupenda kupita kiasi vitu tulivyo navyo? Ni lazima tukumbuke kwamba Mungu ametupatia kazi ya kufanya tukiwa washiriki wa familia yake. Hilo linamaanisha kwamba hatupaswi kujiruhusu tukengeushwe. Bila shaka, hatutaki kuwa kama yule mwanaume kijana ambaye alikataa fursa ya kumtumikia Yehova, na pia tumaini la kufanywa kuwa mmoja kati ya wana wake—kwa sababu tu alipenda sana vitu vyake vichache vya kimwili!—Marko 10:17-22.

WATOTO WA YEHOVA WATAFURAHIA NINI MILELE?

18. Wanadamu watiifu watafurahia milele pendeleo gani lenye kuheshimika zaidi na baraka zipi?

18 Wanadamu watiifu watafurahia pendeleo lenye kuheshimika zaidi, yaani, kumpenda na kumwabudu Yehova milele! Wale walio na tumaini la kuishi duniani watafurahia pia kuitunza sayari hii maridadi ambayo Yehova aliibuni kikamilifu iwe makao yao. Hivi karibuni, dunia na viumbe wote waliopo watafanywa kuwa maridadi tena chini ya utawala wa Ufalme. Yesu atarekebisha hali zilizotokana na uamuzi wa Adamu na Hawa wa kuiacha familia ya Mungu. Yehova atafufua mamilioni ya watu na kuwapa fursa ya kuishi milele wakiwa na afya kamilifu katika dunia iliyogeuzwa na kuwa paradiso. (Luka 23:42, 43) Sehemu ya kidunia ya familia ya waabudu wa Yehova itakapofikia ukamilifu, kila mmoja ataonyesha “utukufu na fahari” ambayo Daudi aliandika kuihusu.—Zab. 8:5.

19. Tunapaswa kukumbuka nini?

19 Ikiwa wewe ni sehemu ya “umati mkubwa,” una tumaini la pekee. Kumbuka kwamba Mungu anakupenda na anataka uwe mshiriki wa familia yake. Hivyo, fanya yote unayoweza ili kumpendeza yeye. Kila siku kazia akilini na moyoni mwako ahadi za Mungu. Thamini pendeleo lako la kumwabudu Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo, na uthamini tumaini la kumsifu yeye milele!

WIMBO 107 Mungu Kielelezo cha Upendo

^ fu. 5 Ili familia iwe na furaha, ni lazima kila mshiriki ajue mambo anayotarajiwa kufanya na ni lazima ashirikiane vizuri na wengine katika familia. Kwa upendo, baba anaiongoza familia, mama anamuunga mkono, na watoto wanawatii wazazi wao. Ndivyo ilivyo na familia ya Yehova. Mungu wetu ana kusudi zuri kwa ajili yetu, na ikiwa tutaunga mkono kusudi hilo, tutakuwa sehemu ya familia ya waabudu wake milele.

^ fu. 55 MAELEZO YA PICHA: Kwa kuwa wamefanywa kwa mfano wa Mungu, wenzi hao wa ndoa wanaweza kuonyeshana upendo na huruma na pia kuwaonyesha wana wao. Wenzi hao wa ndoa wanampenda Yehova. Zawadi ya kupata watoto inawapa fursa ya kuwalea wana wao ili wampende na kumtumikia Yehova. Wazazi hao wanatumia video kuwaelezea watoto wao kwa nini Yehova alimtoa Yesu awe fidia. Pia, wanawafundisha kwamba katika paradiso inayokuja tutaitunza dunia na wanyama milele.