Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 36

Thamini Nguvu za Vijana

Thamini Nguvu za Vijana

“Utukufu wa vijana ni nguvu zao.”​—MET. 20:29.

WIMBO 88 Nijulishe Njia Zako

MUHTASARI *

1. Tunaweza kujiwekea lengo gani zuri kadiri umri wetu unavyosonga?

 KADIRI umri wetu unavyosonga, huenda tukahofu kwamba hatutaweza kutumiwa na Yehova kama tulipokuwa vijana. Ingawa huenda ni kweli kwamba hatuna nguvu zilezile tulizokuwa nazo awali, tunaweza kutumia hekima na uzoefu ambao tumejipatia ili kuwasaidia vijana watumie kikamili uwezo wao, na kukubali majukumu zaidi katika tengenezo la Yehova. Mzee wa kutaniko wa miaka alieleza hivi: “Nilipoanza kuhisi kwamba siwezi kutimiza mengi kwa sababu ya umri wangu kusonga, nilishukuru kwamba kulikuwa na ndugu vijana waliostahili ambao wangeweza kuendeleza kazi.”

2. Tutazungumzia nini katika makala hii?

2 Makala iliyotangulia ilizungumzia jinsi vijana wanavyoweza kunufaika wanapokuwa karibu na ndugu na dada wenye umri mkubwa. Katika makala hii, tutaona jinsi sifa kama vile unyenyekevu, kiasi, kuwa wenye shukrani, na ukarimu zinavyoweza kuwasaidia wenye umri mkubwa kufanya kazi pamoja na vijana, na hivyo kuliletea baraka kutaniko zima.

UWE MNYENYEKEVU

3. Kulingana na Wafilipi 2:3, 4, unyenyekevu ni nini, na unaweza kumsaidiaje Mkristo?

3 Ni lazima ndugu na dada wenye umri mkubwa wawe wanyenyekevu ikiwa wanataka kuwasaidia vijana. Mtu mnyenyekevu huwaona wengine kuwa bora kuliko yeye. (Soma Wafilipi 2:3, 4.) Wakristo wenye umri mkubwa wanaoonyesha sifa ya unyenyekevu wanatambua kwamba mara nyingi kuna zaidi ya njia moja ya Kimaandiko na yenye matokeo ya kutimiza mgawo fulani. Hivyo, wana maoni yaliyosawazika kuhusu jinsi walivyofanya mambo wakati uliopita. (Mhu. 7:10) Ingawa wana uzoefu mwingi wenye thamani, ambao wanaweza kushiriki na vijana, wanatambua kwamba “tamasha ya ulimwengu huu inabadilika” na kwamba huenda wakalazimika kuzoea njia mpya za kufanya mambo.​—1 Kor. 7:31.

Kwa ukarimu, wale wenye umri mkubwa wanashiriki uzoefu wao pamoja na wengine (Tazama fungu la 4 na 5) *

4. Waangalizi wa mzunguko wanaonyeshaje mtazamo kama ule wa Walawi?

4 Ndugu na dada wenye umri mkubwa ambao ni wanyenyekevu, wanatambua kwamba kadiri umri wao unavyosonga, hawawezi kufanya mengi kama walivyofanya wakati uliopita. Kwa mfano, fikiria waangalizi wetu wa mzunguko. Wanapofikia umri wa miaka 70, wanaombwa wafanye migawo tofauti. Hilo linaweza kuwa changamoto kwao. Walithamini sana pendeleo la kuwatumikia ndugu na dada zao. Walipenda mgawo wao, na tamaa yao ya kutumiwa kwa njia hiyo bado ipo moyoni mwao. Hata hivyo, wanatambua kwamba vijana wanahitajika ili kuendeleza kazi. Hivyo, wanaonyesha mtazamo kama ule wa Walawi katika Israeli la kale, ambao walipofikisha umri wa miaka 50, hawakuendelea na utumishi wao katika hema la ibada. Shangwe ya Walawi hao wenye umri mkubwa haikutegemea pendeleo hususa. Walitimiza kikamili mapendeleo waliyoweza kuwa nayo, wakifanya yote wawezayo kuwasaidia vijana. (Hes. 8:25, 26) Leo, ingawa waangalizi wa mzunguko wa zamani hawatumikii tena makutaniko mengi, wanathibitika kuwa baraka kwa kutaniko ambalo wanatumikia.

5. Unaweza kujifunza nini kutokana na mfano uliowekwa na Dan na Katie?

5 Fikiria mfano wa Dan, ambaye alitumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko kwa miaka 23. Dan alipofikisha umri wa miaka 70, yeye na Katie, mke wake, walipewa mgawo wa upainia wa pekee. Wanaonaje mgawo wao mpya? Dan anasema kwamba sasa yeye ni mwenye shughuli nyingi sana! Anashughulikia majukumu yake ya kutanikoni, anawasaidia akina ndugu wastahili kuwa watumishi wa huduma, na anawazoeza wengine katika mahubiri ya miji mikubwa na kwenye magereza. Enyi ndugu na dada wenye umri mkubwa, iwe mko katika utumishi wa wakati wote au la, mnaweza kufanya mengi ili kuwasaidia wengine. Jinsi gani? Jifunze kuzoea hali zako mpya, jiwekee malengo mapya, na ukazie fikira mambo unayoweza kufanya, badala ya yale usiyoweza kufanya.

UWE MWENYE KIASI

6. Kwa nini ni jambo la hekima kuwa mwenye kiasi? Toa mfano.

6 Mtu mwenye kiasi anatambua mipaka yake. (Met. 11:2) Sifa ya kiasi inamsaidia kuwa na matarajio yaliyosawazika kuhusu mambo anayoweza kufanya. Matokeo ni kwamba ataendelea kuwa mwenye furaha na kufanya kazi kwa bidii. Tunaweza kumlinganisha mtu mwenye kiasi na mtu anayeendesha gari kwenye kilima. Dereva anahitaji kubadili gia ya gari na kuweka gia ndogo ili aendelee kuendesha kwenye mwinuko. Ni kweli kwamba huenda gari likasonga taratibu zaidi, lakini litaendelea kusonga mbele. Vivyo hivyo, mtu mwenye kiasi anajua wakati anapohitaji “kubadili gia” ili aendelee kutenda na kuwa mwenye bidii katika utumishi wa Yehova.—Flp. 4:5.

7. Barzilai alionyeshaje sifa ya kiasi?

7 Fikiria mfano wa Barzilai aliyekuwa na umri wa miaka 80 Mfalme Daudi alipomwomba akaishi kwenye makao ya mfalme. Barzilai, ambaye alikuwa na sifa ya kiasi, alikataa mwaliko huo. Kwa kuwa alitambua mipaka ya umri wake, Barzilai alipendekeza Kimhamu aliyekuwa na umri mdogo zaidi achukue nafasi yake. (2 Sam. 19:35-37) Kama Barzilai, ndugu wenye umri mkubwa wanafurahi kuwapa wanaume vijana fursa za kutumikia.

Mfalme Daudi alikubaliana na uamuzi wa Mungu kwamba mwana wake angejenga hekalu (Tazama fungu la 8)

8. Mfalme Daudi alionyeshaje sifa ya kiasi ilipohusu ujenzi wa hekalu?

8 Mfalme Daudi pia alikuwa mfano mzuri sana wa mtu mwenye kiasi. Kwa moyo wake wote, alitaka kumjengea Yehova nyumba. Lakini Yehova alipomwambia kwamba pendeleo hilo angepewa kijana Sulemani, Daudi alikubali uamuzi wa Yehova na kuunga mkono mradi huo kwa moyo wake wote. (1 Nya. 17:4; 22:5) Daudi hakuhisi kwamba yeye ndiye angefaa zaidi kwa ajili ya mgawo huo kwa sababu Sulemani alikuwa “mchanga na hana uzoefu.” (1 Nya. 29:1) Daudi alijua kwamba kufanikiwa kwa mradi huo wa ujenzi kulitegemea baraka za Yehova, na si umri au uzoefu wa wale wanaoongoza. Kama Daudi, wale wenye umri mkubwa leo wanaendelea kufanya kazi kwa bidii, hata wakati migawo yao inapobadilika. Na wanajua kwamba Yehova atawabariki vijana wanaofanya kazi ambazo awali wao walifanya.

9. Mshiriki fulani wa Halmashauri ya Tawi alionyeshaje sifa ya kiasi?

9 Mfano wa siku zetu wa mtu mwenye sifa ya kiasi ni ndugu anayeitwa Shigeo. Mwaka wa 1976, alipokuwa na umri wa miaka 30, Shigeo aliwekwa rasmi kuwa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi. Mwaka wa 2004, alikuwa mratibu wa Halmashauri ya Tawi. Baadaye, alitambua kwamba hana nguvu alizokuwa nazo zamani na kwamba angechukua muda mrefu zaidi kukamilisha kazi zake. Alisali na kutafakari kuhusu faida za kuwa na ndugu mwenye umri mdogo kuliko yeye, ambaye angepokea majukumu yake. Ingawa kwa sasa si mratibu wa Halmashauri ya Tawi, Shigeo bado anaendelea kushirikiana vizuri na washiriki wenzake wa Halmashauri ya Tawi. Kama tulivyoona katika mfano wa Barzilai, Mfalme Daudi, na Shigeo, mtu mnyenyekevu na mwenye kiasi hatakazia fikira kwamba vijana hawana uzoefu, bali atakazia fikira uwezo walio nao. Hatawaona kuwa washindani, bali kuwa wafanyakazi wenzi.​—Met. 20:29.

UWE MWENYE SHUKRANI

10. Ndugu na dada wenye umri mkubwa wana mtazamo gani kuelekea vijana kutanikoni?

10 Ndugu na dada wenye umri mkubwa wanawaona vijana kuwa zawadi kutoka kwa Yehova, na wanaonyesha shukrani kwa mambo yote ambayo vijana wanafanya. Kadiri nguvu zao zinavyopungua, wenye umri mkubwa wanashukuru kwamba wale walio na nguvu za ujana, wako tayari na wana uwezo wa kubeba majukumu yao na kulitumikia kutaniko.

11. Andiko la Ruthu 4:13-16 linaonyeshaje baraka ambazo wenye umri mkubwa wanapata wanaposhukuru na kukubali msaada unaotoka kwa vijana?

11 Naomi ni mfano mzuri sana wa mtu anayetajwa katika Biblia ambaye alishukuru sana kwa msaada aliopata kutoka kwa kijana. Mwanzoni, Naomi alimhimiza Ruthu, binti mkwe wake aliyekuwa mjane, arudi kwa watu wake. Hata hivyo, Ruthu aliposisitiza kwamba ataandamana na Naomi kurudi Bethlehemu, alikubali utegemezo wa Ruthu aliyekuwa mshikamanifu. (Rut. 1:7, 8, 18) Na kufanya hivyo kulikuja kuwa baraka kwa wanawake hao wote wawili! (Soma Ruthu 4:13-16.) Unyenyekevu utawachochea ndugu na dada wenye umri mkubwa kuiga mfano wa Naomi.

12. Mtume Paulo alionyeshaje kwamba alikuwa mtu mwenye shukrani?

12 Mtume Paulo alishukuru kwa msaada aliopata. Kwa mfano, aliwashukuru Wakristo huko Filipi kwa zawadi ambazo walimtumia. (Flp. 4:16) Alishukuru kwa msaada aliopata kutoka kwa Timotheo. (Flp. 2:19-22) Na Paulo alimshukuru Mungu kwa sababu ya wale waliokuja kumtia moyo alipokuwa akisafirishwa kwenda Roma akiwa mfungwa. (Mdo. 28:15) Paulo alikuwa mtu mwenye nguvu aliyesafiri maelfu ya kilomita ili kuhubiri na kuyaimarisha makutaniko. Hata hivyo, alikuwa mnyenyekevu na alikubali msaada kutoka kwa ndugu na dada zake.

13. Ndugu na dada wenye umri mkubwa wanaweza kuonyeshaje kwamba wanashukuru msaada ambao vijana huwapatia?

13 Enyi ndugu na dada wenye umri mkubwa, mnaweza kuonyesha kwa njia mbalimbali kwamba mnashukuru msaada wa vijana kutanikoni. Ikiwa wanataka kukupatia usafiri, kwenda kukufanyia ununuzi, au kukusaidia kufanya mambo mengine muhimu, kubali na uwashukuru kwa msaada wao. Uone msaada huo kuwa wonyesho wa upendo wa Yehova. Huenda ukashangazwa na urafiki wa karibu ambao utasitawisha na wale wanaokusaidia. Sikuzote onyesha kwamba unapendezwa na ukuzi wa kiroho wa marafiki hao wapya vijana, na uwaambie jinsi unavyofurahi kuona vijana wakijitoa ili kufanya mengi zaidi kutanikoni. Na uwe tayari kutumia muda pamoja nao kuwasimulia mambo uliyopitia maishani. Unapofanya hivyo, ‘utajionyesha kuwa mwenye shukrani’ kwa Yehova, kwa ajili ya vijana ambao amewavuta kutanikoni.​—Kol. 3:15; Yoh. 6:44; 1 The. 5:18.

UWE MKARIMU

14. Mfalme Daudi alionyeshaje ukarimu?

14 Mfalme Daudi alionyesha sifa nyingine muhimu ambayo wale wenye umri mkubwa wanahitaji kuionyesha, yaani, ukarimu. Alitoa mchango mkubwa kutoka katika mali zake mwenyewe ili kuunga mkono ujenzi wa hekalu. (1 Nya. 22:11-16; 29:3, 4) Alifanya hivyo hata ingawa sifa za kujenga mradi huo zingeenda kwa Sulemani, mwana wake. Ikiwa hatuna tena nguvu za kushiriki katika miradi ya ujenzi ya kitheokrasi, tunaweza kuendelea kuunga mkono miradi hiyo kwa kutoa michango kadiri hali zetu zinavyoruhusu. Na tunaweza kuwasaidia vijana wanufaike kutokana na uzoefu ambao tumepata kwa miaka mingi.

15. Mtume Paulo alimpatia Timotheo zawadi gani zenye thamani?

15 Fikiria kuhusu mfano wa ukarimu aliotuwekea mtume Paulo. Alimwalika Timotheo ajiunge naye katika kazi ya umishonari, na kwa ukarimu alimfundisha kijana huyo mbinu za kuhubiri na kufundisha alizotumia. (Mdo. 16:1-3) Mazoezi ambayo Paulo alitoa, yalimsaidia Timotheo awe na matokeo mazuri alipoeneza habari njema. (1 Kor. 4:17) Naye Timotheo, alitumia mbinu alizojifunza kutoka kwa Paulo kuwazoeza wengine.

16. Kwa nini Shigeo aliwazoeza wengine?

16 Leo, ndugu na dada wenye umri mkubwa hawaogopi kwamba hawatahitajika tena ikiwa watawazoeza vijana kufanya kazi ambazo walikuwa wanafanya kutanikoni. Kwa mfano, kwa miaka mingi Shigeo aliyetajwa awali, alikuwa akiwazoeza washiriki wenzake wa Halmashauri ya Tawi waliokuwa na umri mdogo kuliko yeye. Alifanya hivyo ili kuendeleza masilahi ya Ufalme kwenye nchi ambayo alikuwa akitumikia. Matokeo ni kwamba wakati ulipofika, ndugu aliyezoezwa vizuri aliweza kupatikana ili kuchukua nafasi yake na kuwa mratibu wa Halmashauri ya Tawi. Shigeo anaendelea kushiriki pamoja na ndugu vijana uzoefu wake wa zaidi ya miaka 45 kwenye Halmashauri ya Tawi. Ndugu kama hao ni baraka kubwa kwa watu wa Mungu!

17. Kulingana na andiko la Luka 6:38, wale wenye umri mkubwa wanaweza kuwapa nini wengine?

17 Ninyi ndugu na dada wenye umri mkubwa ni uthibitisho ulio wazi kwamba kumtumikia Yehova kwa imani na utimilifu ndiyo njia bora ya maisha. Kupitia mfano wenu, mnaonyesha kwamba jitihada za kujifunza kanuni za Biblia na kuzitumia maishani si za bure. Kwa sababu ya uzoefu wenu, mnajua jinsi mambo yalivyofanywa wakati uliopita, lakini pia mnaona uhitaji wa kufanya mabadiliko kulingana na hali za sasa. Ninyi ndugu na dada wenye umri mkubwa ambao mmebatizwa hivi karibuni, mna mambo mengi pia ya kushiriki na wengine; mnaweza kuwasimulia kuhusu shangwe ya kumjua Yehova wakati huu maishani mwenu. Vijana watathamini kusikia kuhusu mambo mliojionea na kujifunza maishani. Ikiwa mtakuwa na “mazoea ya kuwapa watu” vitu kutoka kwenye ghala lenu la uzoefu, Yehova atawabariki sana.—Soma Luka 6:38.

18. Ndugu na dada wenye umri mkubwa na vijana,wanaweza kusaidiana jinsi gani?

18 Kadiri ninyi ndugu na dada wapendwa wenye umri mkubwa mnavyokuwa na uhusiano wa karibu zaidi na vijana, ndivyo mtakavyoweza kutegemezana zaidi. (Rom. 1:12) Kila mmoja ana kitu fulani chenye thamani ambacho mwingine hana. Wenye umri mkubwa wana hekima na uzoefu ambao wameupata kwa miaka mingi. Vijana wana nishati na nguvu. Vijana na wenye umri mkubwa wanapofanya kazi pamoja wakiwa marafiki, wanamletea sifa Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo, nao ni baraka kwa wote kutanikoni.

WIMBO 90 Tianeni Moyo

^ fu. 5 Makutaniko yetu yamebarikiwa kuwa na ndugu na dada wengi vijana ambao wanajitahidi kuliunga mkono tengenezo la Yehova. Ndugu na dada wenye umri mkubwa kutanikoni, haidhuru utamaduni na malezi yao, wanaweza kuwasaidia vijana watumie nguvu zao kikamili katika utumishi wa Yehova.

^ fu. 55 MAELEZO YA PICHA: Mwangalizi wa mzunguko alipofika umri wa miaka 70, yeye na mke wake walipata mgawo mpya. Uzoefu wao wa miaka mingi unawawezesha kuwazoeza wengine kwenye kutaniko wanalotumikia sasa.