MAKALA YA 38

Imarisha Upendo Wako kwa Familia Yako ya Kiroho

Imarisha Upendo Wako kwa Familia Yako ya Kiroho

“Ninapanda kwenda kwa Baba yangu na Baba yenu.”​—YOH. 20:17.

WIMBO 3 Tumaini, Nguvu, na Uhakika Wetu

MUHTASARI a

1. Wanadamu waaminifu wanaweza kuwa na uhusiano gani pamoja na Yehova?

 FAMILIA ya waabudu wa Yehova inatia ndani Yesu, ambaye ni “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote,” na malaika wengi sana. (Kol. 1:15; Zab. 103:20) Yesu alipokuwa duniani, alionyesha kwamba wanadamu waaminifu wanaweza kumwona Yehova kuwa Baba yao. Alipokuwa akizungumza na wanafunzi wake, Yesu alimrejelea Yehova akimwita, “Baba yangu na Baba yenu.” (Yoh. 20:17) Na tunapojiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa, tunakuwa sehemu ya familia yenye upendo ya ndugu na dada zetu.​—Marko 10:29, 30.

2. Tutachunguza nini katika makala hii?

2 Baadhi ya watu wanaona ni vigumu kumwona Yehova kuwa Baba mwenye upendo. Huenda wengine hawajui jinsi ya kuwaonyesha upendo ndugu na dada zao. Katika makala hii, tutachunguza jinsi Yesu anavyotusaidia tumwone Yehova kuwa Baba mwenye upendo, ambaye tunaweza kumkaribia. Pia, tutajifunza njia ambazo tunaweza kuiga jinsi Yehova anavyowatendea ndugu na dada zetu.

YEHOVA ANATAKA UMKARIBIE

3. Sala ya kielelezo inatusaidiaje kumkaribia zaidi Yehova?

3 Yehova ni Baba mwenye upendo. Yesu anataka tumwone Yehova kama yeye anavyomwona, yaani, kama mzazi mwenye upendo na wororo ambaye ni rahisi kumfikia, na si kama mtu anayetumia mamlaka yake kwa ukali bila fadhili. Hilo linaonekana wazi kupitia mambo ambayo Yesu aliwafundisha wanafunzi wake wasali kuhusu. Alianza sala yake ya kielelezo kwa maneno: “Baba yetu.” (Mt. 6:9) Yesu angeweza kutuambia tumwite Yehova, “Mweza yote,” “Muumba,” au “Mfalme wa milele”—vyeo ambavyo vinafaa na ni vya Kimaandiko. (Mwa. 49:25; Isa. 40:28; 1 Tim. 1:17) Hata hivyo, Yesu alitumia neno linaloonyesha uhusiano wa karibu, “Baba.”

4. Tunajuaje kwamba Yehova anataka tumkaribie?

4 Je, unaona vigumu kumwona Yehova kuwa Baba mwenye upendo? Baadhi yetu tunahisi hivyo. Ikiwa baba yetu hakututendea kwa fadhili tulipokuwa tukikua, huenda tukaona vigumu hata kumwazia mzazi mwenye upendo. Inafariji sana kujua kwamba Yehova anaelewa kabisa hisia zetu! Anataka kuwa karibu nasi. Hiyo ndiyo sababu Neno lake linatuhimiza hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yak. 4:8) Yehova anatupenda, naye anasema kwamba atakuwa Baba bora zaidi ambaye tunaweza kuwa naye.

5. Kulingana na Luka 10:22, Yesu anaweza kutusaidiaje kumkaribia zaidi Yehova?

5 Yesu anaweza kutusaidia tumkaribie Yehova. Yesu anamjua Yehova vizuri sana na anaiga sifa Zake kwa ukamilifu sana hivi kwamba alisema: “Yeyote ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” (Yoh. 14:9) Kama ndugu yetu mkubwa, Yesu anatufundisha jinsi ya kumheshimu na kumtii Baba yetu, jinsi ya kuepuka kumchukiza, na jinsi ya kupata kibali Chake. Lakini maisha ya Yesu hapa duniani yanafunua hasa jinsi Yehova alivyo mwenye fadhili na upendo. (Soma Luka 10:22.) Acheni tuchunguze mifano kadhaa.

Akiwa Baba mwenye upendo, Yehova alimwimarisha Mwana wake kupitia malaika (Tazama fungu la 6) c

6. Yehova alisikiliza sala za Yesu jinsi gani?

6 Yehova huwasikiliza watoto wake. Fikiria jinsi Yehova alivyomsikiliza Mwana wake mzaliwa wa kwanza. Bila shaka, Yehova alisikiliza sala nyingi zilizotolewa na Mwana wake alipokuwa duniani. (Luka 5:16) Alimsikiliza Yesu akisali kuhusu maamuzi mbalimbali muhimu, kama vile alipochagua mitume wake 12. (Luka 6:12, 13) Pia, Yehova alisikiliza sala ya Yesu alipokuwa akitaabika. Muda mfupi kabla ya kusalitiwa, Yesu alisali kwa bidii kwa Baba yake kuhusu jaribu gumu alilokuwa karibu kukabili. Yehova hakusikiliza tu sala ya Yesu, bali pia alimtuma malaika ili amwimarishe Mwana Wake mpendwa.​—Luka 22:41-44.

7. Unahisije kujua kwamba Yehova husikiliza sala za watu wake?

7 Leo, Yehova anaendelea kusikiliza sala za watumishi wake, naye huwajibu kwa wakati unaofaa na kwa njia bora kabisa. (Zab. 116:1, 2) Fikiria jinsi dada mmoja kutoka India alivyojionea jambo hilo yeye mwenyewe. Alikuwa akikabiliana na tatizo kubwa la kihisia, naye alisali kwa Yehova kwa bidii kuhusu jambo hilo. Anasema hivi: “Programu ya JW Broadcasting® ya Mei 2019, kuhusu jinsi ya kukabiliana na mahangaiko na wasiwasi ilikuwa jambo nililohitaji. Ilikuwa jibu la sala zangu.”

8. Yehova alimwonyesha Yesu upendo kwa njia zipi?

8 Yehova anatupenda na kutujali, kama tu alivyompenda Yesu na kumjali wakati wa huduma yake yenye changamoto hapa duniani. (Yoh. 5:20) Alimwandalia Yesu mahitaji yake yote ya kiroho, kihisia, na kimwili. Na Yehova hakusita kumweleza Mwana wake kwamba anampenda na kumkubali. (Mt. 3:16, 17) Kwa sababu sikuzote angeweza kumtegemea Baba yake wa mbinguni mwenye upendo, Yesu hakuhisi kamwe akiwa peke yake.​—Yoh. 8:16.

9. Tuna uthibitisho gani kwamba Yehova anatupenda?

9 Kama Yesu, sisi sote tumejionea upendo wa Yehova kwa njia nyingi mbalimbali. Hebu fikiria: Yehova ametuvuta kwake na kutupatia familia ya kiroho yenye upendo na umoja ili tuwe na furaha na tutunzwe kihisia. (Yoh. 6:44) Pia, Yehova anatuandalia chakula cha kiroho cha kutosha chenye kujenga. Na hata anatusaidia kupata mahitaji yetu ya kimwili. (Mt. 6:31, 32) Tunapotafakari upendo wa Yehova kwetu, upendo wetu kwake unaimarika.

ITENDEE FAMILIA YAKO YA KIROHO KAMA YEHOVA ANAVYOITENDEA

10. Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Yehova anavyowatendea ndugu na dada zetu?

10 Yehova anawapenda ndugu na dada zetu. Lakini huenda isiwe rahisi kwetu kuhisi na kuwaonyesha upendo sikuzote washiriki wa familia yetu ya kiroho. Isitoshe, tunatoka kwenye tamaduni na malezi tofauti. Na sote tunafanya makosa ambayo yanaweza kuwaudhi na kuwavunja moyo wengine. Hata hivyo, bado tunaweza kuchangia upendo katika familia yetu ya kiroho. Jinsi gani? Kwa kumwiga Baba yetu katika kuwaonyesha upendo ndugu na dada zetu. (Efe. 5:1, 2; 1 Yoh. 4:19) Acheni tuone mambo tunayoweza kujifunza kutoka kwa Yehova.

11. Yesu alionyeshaje “huruma nyororo” ya Yehova?

11 Yehova huonyesha “huruma nyororo.” (Luka 1:78) Mtu mwenye huruma anajali anapoona kwamba watu wanateseka; anatafuta njia za kuwasaidia na kuwafariji. Yesu aliwaonyesha watu jinsi ambavyo Yehova anawajali kupitia njia ambayo aliwatendea. (Yoh. 5:19) Pindi moja alipouona umati, Yesu “akausikitikia, kwa sababu walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mt. 9:36) Huruma ya Yesu ilikuwa zaidi ya hisia nyororo tu. Aliponya wagonjwa na kuwapa burudisho wale waliokuwa ‘wanataabika na kulemewa na mizigo.’​—Mt. 11:28-30; 14:14.

Mwige Yehova kwa kuwa mwenye upendo na mkarimu kwa ndugu na dada zako (Tazama fungu la 12 hadi 14) d

12. Toa mfano wa jinsi tunavyoweza kuonyesha huruma.

12 Ili tuwaonyeshe huruma ndugu na dada zetu, tunahitaji kufikiria changamoto wanazokabili. Kwa mfano, huenda dada fulani ana tatizo kubwa la afya. Halalamiki kuhusu tatizo lake, lakini inaelekea atathamini kupata msaada fulani hususa. Anaiandaliaje familia yake mahitaji ya kimwili? Je, tunaweza kumsaidia kuandaa mlo au kusafisha nyumba yake? Huenda ndugu amepoteza kazi yake. Je, zawadi ya kiasi fulani cha pesa, ambayo labda inatolewa bila yeye kujua imetoka kwa nani, inaweza kumsaidia kujikimu hadi atakapopata kazi nyingine?

13-14. Tunaweza kuonyeshaje ukarimu kama Yehova?

13 Yehova ni mkarimu. (Mt. 5:45) Hatupaswi kusubiri hadi ndugu na dada zetu waombe msaada ili tuwaonyeshe huruma. Kama Yehova, tunaweza kuchukua hatua ya kwanza. Anafanya jua liwake kila siku bila hata sisi kumwomba! Na joto la jua linamnufaisha kila mtu, hata wale wasio na shukrani. Je, hukubali kwamba kwa kutuandalia mahitaji yetu, Yehova anatuonyesha kwamba anatupenda? Kwa kweli, tunampenda sana Yehova kwa fadhili na ukarimu wake!

14 Ndugu na dada zetu wengi wanamwiga Baba yetu wa mbinguni kwa kuchukua hatua ya kwanza kuwaonyesha wengine ukarimu. Kwa mfano, mwaka 2013, Kimbunga Haiyan kilisababisha madhara makubwa sana nchini Ufilipino. Ndugu na dada wengi walipoteza nyumba na mali zao. Lakini familia yao ya kiroho ya ulimwenguni pote iliandaa msaada haraka. Wengi walichangia pesa au kushiriki katika mradi mkubwa wa ujenzi, ambao ulisaidia kurekebisha au kujenga upya karibu nyumba 750 kwa kipindi kisichozidi mwaka mmoja! Wakati wa janga la COVID-19, Mashahidi walifanya jitihada kubwa ili kuwategemeza ndugu na dada zao. Tunapochukua hatua haraka ya kuisaidia familia yetu ya kiroho, tunawaonyesha kwamba tunawapenda.

15-16. Kulingana na Luka 6:36, ni kwa njia gani muhimu tunaweza kumwiga Baba yetu wa mbinguni?

15 Yehova ni mwenye rehema na mwenye kusamehe. (Soma Luka 6:36.) Kila siku tunajionea rehema ya Baba yetu wa mbinguni. (Zab. 103:10-14) Wafuasi wa Yesu hawakuwa wakamilifu, hata hivyo, aliwaonyesha rehema na kuwasamehe. Hata alikuwa tayari kudhabihu uhai wake ili dhambi zetu zisamehewe. (1 Yoh. 2:1, 2) Je, unavutiwa zaidi na Yehova na Yesu kwa sababu wao ni wenye rehema na wenye kusamehe?

16 Tunaimarisha kifungo cha upendo kwa familia yetu ya kiroho ‘tunaposameheana kwa hiari.’ (Efe. 4:32) Bila shaka, nyakati nyingine inaweza kuwa vigumu sana kuwasamehe wengine, hivyo tunahitaji kufanyia kazi jambo hilo. Dada mmoja alihisi kwamba makala yenye kichwa “Msameheane kwa Hiari” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi ilimsaidia kufanya hivyo. b Anasema hivi: “Kujifunza makala hiyo kumenifanya niwe na mtazamo tofauti na unaofaa kuhusu jambo hilo. Lilieleza kwamba kuwa tayari kuwasamehe wengine hakumaanishi kwamba ni lazima ukubali mwenendo wao mbaya au kupuuza madhara ya mwenendo huo. Lakini kusamehe kunamaanisha kuondoa kabisa kinyongo moyoni unapokosewa na kudumisha amani yako mwenyewe.” Tunapowasamehe kwa hiari ndugu na dada zetu, tunaonyesha kwamba tunawapenda na kwamba tunamwiga Yehova, Baba yetu.

THAMINI SEHEMU YAKO KATIKA FAMILIA YETU YA KIROHO

Vijana kwa wazee wamewaonyesha upendo ndugu na dada zao (Tazama fungu la 17) e

17. Kulingana na Mathayo 5:16, tunaweza kumwonyesha heshima Baba yetu wa mbinguni jinsi gani?

17 Ni pendeleo kubwa kuwa sehemu ya familia ya kimataifa yenye upendo. Tunataka watu wengi kadiri iwezekanavyo wajiunge nasi kumwabudu Mungu wetu. Tukiwa na hilo akilini, tunapaswa kuwa waangalifu ili tusifanye jambo lolote linaloweza kuharibu sifa ya Baba yetu wa mbinguni au watu wa Yehova. Tunajitahidi kujiendesha kwa njia ambayo itawavutia watu wakubali habari njema.​—Soma Mathayo 5:16.

18. Ni jambo gani linaloweza kutusaidia kutoa ushahidi bila woga?

18 Nyakati nyingine, huenda baadhi ya watu wakatudharau au hata kututesa kwa sababu tunamtii Baba yetu wa mbinguni. Namna gani ikiwa tunahisi wasiwasi tunapozungumza na wengine kuhusu imani yetu? Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova na Mwana wake watatusaidia. Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake kwamba hawakuhitaji kuhangaika kuhusu jinsi ya kusema au kile watakachosema. Kwa nini? Yesu alisema hivi: “Mtapewa jambo la kusema katika saa hiyo; kwa maana si ninyi tu mnaosema, bali ni roho ya Baba yenu inayosema kupitia ninyi.”​—Mt. 10:19, 20.

19. Toa mfano wa mtu aliyehubiri kwa ujasiri.

19 Fikiria mfano wa Robert. Muda fulani uliopita alipokuwa mwanafunzi mpya wa Biblia na ujuzi wake wa Biblia ukiwa mdogo, alifikishwa mbele ya mahakama ya kijeshi nchini Afrika Kusini. Kwa ujasiri aliieleza mahakama kwamba hakutaka kuunga mkono upande wowote kwa sababu aliwapenda ndugu zake Wakristo. Alithamini sehemu yake katika familia yetu ya kiroho! Ghafla hakimu akamuuliza hivi: “Ndugu zako ni nani?” Robert hakuwa ametarajia swali hilo, lakini haraka alikumbuka andiko la siku hiyo. Lilikuwa Mathayo 12:50 linalosema: “Yeyote anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni, huyo ndiye ndugu yangu, dada yangu, na mama yangu.” Ingawa Robert alikuwa mwanafunzi mpya wa Biblia, roho ya Yehova ilimsaidia kujibu swali hilo na maswali mengine kadhaa ambayo hakutarajia. Ni lazima Yehova alimwonea fahari Robert! Na Yehova anatuonea fahari pia tunapomtegemea ili kutoa ushahidi kwa ujasiri katika hali ngumu.

20. Tunapaswa kuazimia kufanya nini? (Yohana 17:11, 15)

20 Acheni tuendelee kuthamini baraka tuliyo nayo ya kuwa sehemu ya familia ya kiroho yenye upendo. Tuna Baba bora kuliko wote na pia ndugu na dada wengi wanaotupenda. Hatupaswi kamwe kuchukulia mambo hayo kivivi hivi. Shetani na wafuasi wake wenye chuki wanajaribu kutufanya tutilie shaka upendo wa Baba yetu wa mbinguni na kujaribu kuvuruga umoja tunaofurahia. Hata hivyo, Yesu alisali kwa ajili yetu, akimwomba Baba yetu atulinde ili familia yetu iendelee kuwa na umoja. (Soma Yohana 17:11, 15.) Yehova anajibu sala hiyo. Kama Yesu, kamwe tusitilie shaka upendo na utegemezo wa Baba yetu wa mbinguni. Na tuazimie kuendelea kuimarisha upendo wetu kwa familia yetu ya kiroho.

WIMBO 99 Ndugu Makumi ya Elfu

a Tunafurahia pendeleo la pekee la kuwa sehemu ya familia ya ndugu na dada wanaotupenda. Sisi sote tungependa kuimarisha kifungo cha upendo kilichopo miongoni mwetu. Tunaweza kufanyaje hivyo? Ni kwa kuiga jinsi Baba yetu mwenye upendo anavyotutendea na kwa kufuata mfano wa Yesu na wa ndugu na dada zetu.

b Tazama gazeti la Mnara wa Mlinzi la Novemba 15, 2012, ukurasa wa 26-30.

c MAELEZO YA PICHA: Yehova alimtuma malaika ili akamwimarishe Yesu katika bustani ya Gethsemane.

d MAELEZO YA PICHA: Wakati wa janga la COVID-19, wengi walifanya kazi ya kutayarisha na kugawanya chakula.

e MAELEZO YA PICHA: Mama anamsaidia binti yake anayeandika barua ya kumtia moyo ndugu aliye gerezani.