Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 40

Kutubu Kikweli Maana Yake Nini?

Kutubu Kikweli Maana Yake Nini?

“Nilikuja kuita . . . watenda-zambi ili watubu.”​—LU. 5:32.

WIMBO 36 Tulinde Moyo Wetu

KIFUPI YA HABARI *

1-2. Kulikuwa tofauti gani kati ya Ahabu na Manase, na tutazungumuzia maulizo gani?

 TUZUNGUMUZIE wafalme wawili wenye waliishi zamani. Mumoja, alitawala makabila kumi ya Ufalme wa Israeli; na mwingine alitawala makabila mbili ya Ufalme wa Yuda. Hata kama waliishi wakati tofauti, kuko mambo mingi yenye walifanya yenye inafanana. Wale wafalme wote wawili walimuasi Yehova na walichochea watu kutenda zambi. Wote wawili waliabudu miungu ya uongo na walikuwa wauaji. Lakini, kulikuwa pia tofauti fulani kati ya wale wanaume wawili. Mumoja aliendelea na maisha yake ya mubaya mupaka wakati alikufa, lakini ule mwingine, alitubu na alisamehewa juu ya matendo maovu yenye alifanya. Tuko tunazungumuzia nani?

2 Tuko tunazungumuzia Ahabu, Mufalme wa Israeli, na Manase, Mufalme wa Yuda. Tofauti zenye zilikuwa kati ya wale wanaume wawili, zinaweza kutufundisha mambo mingi juu ya jambo moja ya maana sana: kutubu. (Mdo. 17:30; Ro. 3:23) Kutubu maana yake nini, na namna gani mutu anaweza kuonyesha kama anatubu kikweli? Tunapaswa kujua ile, juu tunapenda Yehova atusamehe wakati tunafanya zambi. Juu ya kupata jibu ya ile maulizo, tutachunguza maisha ya wale wafalme wawili na tutaona ni mambo gani tunaweza kujifunza kupitia mufano wao. Kisha pale, tutachunguza mambo Yesu alifundisha kuhusu kutubu.

MUFANO WA MUFALME AHABU UNAWEZA KUTUFUNDISHA NINI?

3. Ahabu alikuwa Mufalme wa namna gani?

3 Ahabu alikuwa Mufalme wa saba wa Ufalme wa makabila kumi ya Israeli. Alioa Yezebeli, binti ya Mufalme wa Sidoni, taifa tajiri lenye lilikuwa kaskazini. Juu Ahabu alimuoa Yezebeli, taifa la Israeli lilikuwa sasa na nafasi za mingi za kupata makuta. Lakini ile ndoa ilifanya pia taifa ya Israeli imukosee Yehova tena sana. Yezebeli alikuwa muabudu wa Baali, na ni yeye alimutia moyo Ahabu achochee dini ya mubaya sana, yenye ilitia ndani ukahaba na hata kutoa watoto kama zabihu. Hakuna nabii wa Yehova mwenye alijisikia salama wakati Yezebeli alikuwa malkia. Yezebeli aliua manabii wengi. (1 Fa. 18:13) Ahabu yeye mwenyewe “alikuwa muovu mbele ya macho ya Yehova kuliko wale wote wenye walimutangulia.” (1 Fa. 16:30) Ile haionyeshe kama Yehova hakukuwa anaona mambo yenye Yezebeli na Ahabu walikuwa wanafanya. Aliijua muzuri. Lakini Yehova alionyesha rehema, na akamutuma nabii Eliya ili kutia moyo watu wabadilike na wamutumikie yeye. Lakini Ahabu na Yezebeli walikatala kusikiliza.

4. Ni hukumu gani ilitolewa juu ya Ahabu, na alitenda namna gani?

4 Ku mwisho ya yote, wakati wa kutenda wa Yehova ukafika. Alimutuma Eliya ili atangaze hukumu juu ya Ahabu na Yezebeli. Familia yao yote ingeuawa. Maneno ya Eliya ilimuhuzunisha sana Ahabu! Lakini jambo ya kushangaza, Ahabu mwenye alikuwa na kiburi sana ‘akajinyenyekeza.’​—1 Fa. 21:19-29.

Mufalme Ahabu alitia mu gereza nabii wa Mungu. Ile ilionyesha kama hakutubu kikweli (Ona fungu ya 5-6) *

5-6. Ni nini inaonyesha kabisa kama Ahabu hakutubu kikweli?

5 Hata kama Ahabu alijinyenyekeza mu ile wakati, mwenendo wenye alionyesha kisha pale, ulionyesha kama hakutubu kikweli. Hakutosha ibada ya Baali mu Ufalme wake. Na hakuchochea watu wamuabudu Yehova. Na mambo ingine yenye Ahabu alifanya inahakikisha kama hakutubu kikweli.

6 Kisha, Ahabu alimuambia Yehoshafati Mufalme wa Yuda, waende pamoja ili kupigana na Wasiria. Yehoshafati alikuwa Mufalme muzuri mwenye alimutumainia Yehova. Na alimuambia Ahabu, wamuulize kwanza nabii wa Yehova mambo yenye walipaswa kufanya mbele waende ku vita. Mara moja, Ahabu hakuitika ile wazo. Akasema: “Kungali mutu mumoja mwenye kupitia yeye tunaweza kumuuliza Yehova; lakini ninamuchukia, kwa maana hatabiri hata kidogo mambo ya muzuri juu yangu, ya mubaya tu.” Hata vile, walienda kumuona nabii Mikaya. Ahabu alisema kweli, nabii wa Mungu alitabiri mambo ya mubaya kumuhusu! Kuliko kutubu na kutafuta musamaha wa Yehova, muovu Ahabu alimutupa nabii wa Yehova mu gereza. (1 Fa. 22:7-9, 23, 27) Hata kama Ahabu alimutia Mikaya mu gereza, ile haikufanya unabii usitimie. Ku vita yenye ilifuata, Ahabu aliuawa.​—1 Fa. 22:34-38.

7. Kisha kifo ya Ahabu, nabii wa Yehova alisema nini kumuhusu?

7 Kisha kifo ya Ahabu, Yehova alionyesha namna alikuwa anamuona ule mwanaume. Wakati Mufalme muzuri Yehoshafati alirudia salama ku nyumba, Yehova alimutumia nabii Yehu amuambie kama alifanya mubaya kumusaidia Ahabu. Nabii wa Yehova alisema hivi: “Je, waovu ndio unapaswa kusaidia, na je, wale wenye wanamuchukia Yehova ndio unapaswa kupenda?” (2 Ny. 19:1, 2) Waza kidogo: Kama Ahabu alitubu kikweli, nabii wa Yehova hangesema kama Ahabu alikuwa muovu na kama alimuchukia Yehova. Inaonekana wazi kama, hata kama Ahabu alionyesha kabisa kama anahuzunika, hakutubu kikweli.

8. Mufano wa Ahabu, unaweza kutufundisha nini kuhusu kutubu?

8 Mufano wa Ahabu, unaweza kutufundisha mambo gani? Wakati Eliya alimuambia Ahabu kama familia yake itapatwa na malipizi, mara moja Ahabu alijinyenyekeza. Na ile ilikuwa jambo ya muzuri yenye alifanya. Lakini kisha, matendo yake ilionyesha kama hakutubu kikweli. Kutubu, inatia ndani mambo mingi, zaidi ya kuhuzunikia mambo yenye tulifanya. Tuzungumuzie mufano ingine yenye itatusaidia kuelewa maana ya kutubu kikweli.

MUFANO WA MUFALME MANASE UNAWEZA KUTUFUNDISHA NINI?

9. Manase alikuwa Mufalme wa namna gani?

9 Kisha miaka 200 hivi, Manase akakuwa Mufalme wa Yuda. Zambi zake pengine zilikuwa za mubaya sana kuliko zenye Ahabu alifanya. Biblia inasema hivi: “Alifanya kwa kiasi kikubwa mambo ya mubaya mbele ya macho ya Yehova, ili kumukasirisha.” (2 Ny. 33:1-9) Manase alisimamisha mazabahu kwa ajili ya miungu ya uongo, na hata alitengeneza sanamu ya kuchongwa ya muti mutakatifu mu hekalu ya Yehova. Inawezekana ile muti mutakatifu ilikuwa alama ya ibada ya ngono! Alifanya uchawi, alitumia uaguzi, na alifanya ulozi. Alimwanga pia “damu nyingi sana yenye haina kosa.” Aliua watu wengi na hata alipitisha “wana wake mwenyewe katika moto,” ili kutolea miungu ya uongo zabihu.​—2 Fa. 21:6, 7, 10, 11, 16.

10. Namna gani Yehova alimupatia Manase malipizi, naye alitenda namna gani?

10 Sawa vile Ahabu, Manase alikatala kusikiliza mashauri yenye Yehova alimupatia kupitia manabii wake. Kisha, “Yehova akaleta wakubwa wa jeshi la mufalme wa Ashuru ili wawashambulie, na wakamukamata Manase kwa kulabu na kumufunga kwa pingu mbili za shaba na kumupeleka Babiloni.” Wakati alikuwa mu gereza kule Babiloni, inaonekana kama Manase alifikiri kwa uangalifu kuhusu mambo yenye alikuwa amefanya. “Akaendelea kujinyenyekeza sana mbele ya Mungu wa mababu zake.” Alifanya hata zaidi. Ni kusema “alimuomba Yehova Mungu wake rehema.” Kwa hiyo, Manase “aliendelea kusali kwake Yeye.” Ule mwanaume muovu, alikuwa anabadilika. Alianza kumuona Yehova sawa “Mungu wake,” na alisali sana kwake.​—2 Ny. 33:10-13.

Mufalme Manase aliondoa ibada ya uongo. Ile inaonyesha kama alitubu kikweli (Ona fungu ya 11) *

11. Kulingana na 2 Mambo ya Nyakati 33:15, 16, Manase alionyesha namna gani kama alitubu kikweli?

11 Kisha, Yehova alijibia sala za Manase. Aliona namna ule mwanaume alibadilisha moyo wake, sawa vile sala zake zilionyesha. Njo maana Yehova alisikiliza Manase wakati alimuomba amusamehe na alimuruhusu akuwe tena Mufalme. Manase alifanya yake yote ili kuonyesha kabisa kama alitubu kikweli. Alifanya jambo yenye Ahabu hakufanyaka. Alibadilisha tabia yake. Alipinga ibada ya uongo na akachochea ibada ya kweli. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 33:15, 16.) Manase alikuwa kabisa na lazima ya uhodari na imani ili kufanya vile, juu mbele atubu, alikuwa mufano mubaya kwa familia yake, kwa watu wake wenye vyeo, na kwa watu wengi kwa miaka mingi. Wakati Manase alikuwa muzee, alijikaza kutosha mambo fulani ya mubaya yenye alikuwa amefanya. Pengine, alikuwa mufano muzuri kwa mujukuu wake Yosia, mwenye alifikia kuwa Mufalme muzuri sana.​—2 Fa. 22:1, 2.

12. Mufano wa Manase unaweza kutufundisha nini kuhusu kutubu?

12 Mufano wa Manase unaweza kutufundisha nini? Alijinyenyekeza, na alifanya hata zaidi. Alisali, na kumuomba Yehova amuhurumie. Na alibadilisha tabia yake. Alijikaza sana ili kurekebisha mambo yote ya mubaya yenye alikuwa amefanya. Alifanya yake yote ili kumuabudu Yehova na alisaidia wengine wafanye vile. Mufano wa Manase, unapatia hata wale wenye walifanya zambi nzito, tumaini. Mambo yenye ilimupata Manase, inaonyesha kama Yehova Mungu ni ‘mwema na iko tayari kusamehe.’ (Zb. 86:5) Yehova anasamehe wale wenye wanatubu kikweli.

13. Leta mufano wenye unaweza kutusaidia kuelewa jambo fulani ya maana sana kuhusu kutubu.

13 Manase alifanya mambo mingi zaidi ya kuhuzunikia zambi zake. Ile inatufundisha jambo ya maana sana kuhusu kutubu. Kwa mufano: Unaenda fasi kwenye wanauzishiaka keki na unaomba keki. Lakini kuliko wakupatie keki, ule mwenye anauzishaka mule anakupatia liyai. Utafurahi? Hapana! Utatosheka juu ule mutu mwenye kuuzisha anakuambia kama liyai ni kitu ya maana sana yenye inasaidiaka kufanya nayo keki? Jibu ni hapana! Vilevile, Yehova anaomba watenda-zambi watubu kikweli. Kama mutenda-zambi anahuzunika juu ya zambi yenye alifanya, ni muzuri. Kujisikia vile ni jambo ya maana sana, lakini haiko ile tu njo inaonyesha kama mutu anatubu kikweli. Ni mambo gani ingine mutenda-zambi anapaswa kufanya? Tunajifunza mambo mingi yenye kutia moyo kupitia mufano wenye Yesu alizungumuzia.

NAMNA YA KUJUA KAMA MUTU ANATUBU KIKWELI

Kisha mwana mupotevu kurudiwa na akili, alifanya safari ya murefu ili kurudia kwao (Ona fungu ya 14-15) *

14. Mu mufano wa Yesu, mwana mupotevu alianza kufanya nini ili kuonyesha kama anatubu kikweli?

14 Yesu alitoa mufano wenye kutia moyo kuhusu mwana mupotevu, wenye kuwa mu Luka 15:11-32. Kijana moja mudogo alimuasi baba yake, na akatoka kwao na akasafiri “kuenda inchi ya mbali.” Kule aliishi maisha ya upotovu. Wakati maisha yake ilikuwa mubaya sana, alianza kufikiria uamuzi wake wa mubaya. Alifikia kutambua kama zamani, maisha yake ilikuwa muzuri zaidi wakati alikuwa ku nyumba ya baba yake. Yesu alisema kama ule kijana mudogo “alirudiwa na fahamu.” Aliamua kurudia ku nyumba yao, na kumuomba baba yake amusamehe. Ilikuwa jambo ya maana sana kwa ule mwana kutambua kama alikuwa amekamata maamuzi mingi ya mubaya. Kufanya vile kulitosha? Hapana. Alipaswa kubadilisha tabia yake!

15. Namna gani mwana mupotevu alionyesha kabisa kama alitubu kikweli?

15 Mwana mupotevu alionyesha kabisa kama alitubu kikweli juu ya mambo yenye alifanya. Alifanya safari ya murefu mupaka kwao. Kisha wakati alizungumuza na baba yake, alisema hivi: “Nimetenda zambi juu ya mbingu na juu yako. Sistahili tena kuitwa mwana wako.” (Lu. 15:21) Juu alitubu kikweli, ile inaonyesha kabisa kama alikuwa anapenda kutengeneza urafiki wake pamoja na Yehova. Alitambua pia kama, matendo yake ilimuumiza baba yake. Na alikuwa tayari kufanya mabadiliko, ili kukubaliwa tena na baba yake; alikuwa hata tayari kutendewa kama mumoja wa wafanyakazi wa baba yake! (Lu. 15:19) Hii mufano, haiko tu yenye kutia moyo, lakini ni mufano yenye inaweza kusaidia sana wazee. Inaweza kuwasaidia wakati wanapenda kujua kama, mutu mwenye alifanya zambi nzito, anatubu kabisa kikweli.

16. Juu ya nini ni nguvu kwa wazee kujua kama mutu anatubu kabisa kikweli?

16 Haiko mwepesi kwa wazee kujua kama, mutu mwenye alifanya zambi nzito, anatubu kikweli kabisa. Juu ya nini? Juu wazee hawawezi kusoma mioyo. Njo maana wanapaswa kujikaza kutafuta mambo yenye inaonyesha kama ndugu yao alijifunza kabisa kuchukia mambo yenye alifanya. Mu hali fulani, pengine mutu anaweza kufanya zambi nzito, na wazee wenye wanamusaidia, pengine hawako hakika kabisa kama anatubu kikweli.

17. (a) Ni mufano gani wenye kuonyesha kama tendo moja ya kuhuzunika juu ya zambi yenye mutu alifanya haionyeshe kama anatubu kikweli? (b) Kama vile inaonyeshwa mu 2 Wakorinto 7:11, mutu mwenye anatubu kikweli anatazamiwa kufanya nini?

17 Fikiria hii mufano. Ndugu mumoja anafanya uzinifu kwa miaka mingi. Kuliko kutafuta musaada, anaficha mwenendo wake mubaya na haambie bibi yake, marafiki wake, na hata wazee. Kisha, wazee wanafikia kujua mambo yenye alifanya. Wakati wazee wanamuambia kama wako na ushuhuda wenye kuonyesha kama alifanya uzinifu, anakubali mambo yenye alifanya na pengine anaonyesha kama anahuzunika sana. Lakini, ile inaonyesha kabisa kama anatubu kikweli? Hapana. Juu wazee waweze kumusaidia, watahakikisha kama ule mutenda-zambi, anafanya mabadiliko zaidi ya kuhuzunikia zambi yake. Ule mutu hakufanya zambi mara moja tu juu alikamata uamuzi wa mubaya, lakini, alifanya vile mara mingi. Tena ule mutenda-zambi hakutubu kwa kujipendea lakini ni juu mutu fulani alivumbua zambi yake na akaiambia wazee. Kwa hiyo, wazee wako na lazima ya ushuhuda, wenye kuonyesha kama ule mutenda-zambi amebadilisha namna yake ya kufikiri, ya kujisikia na ya kutenda. (Soma 2 Wakorinto 7:11.) Na ile inaweza kukamata wakati mingi juu afanye mabadiliko; pengine anaweza kutengwa na kutaniko ya Kikristo, mupaka wakati anaonyesha kama anatubu kikweli.​—1 Ko. 5:11-13; 6:9, 10.

18. Namna gani mutu mwenye ametengwa anaweza kuonyesha kama anatubu kikweli, na ile itakuwa na matokeo gani?

18 Ili kuonyesha kama anatubu kikweli, mutu mwenye alitengwa, anapaswa kukusanyika kwa ukawaida na kufuata mashauri ya wazee kuhusu kusali na kuwa na programu ya muzuri ya funzo ya Biblia. Anapaswa pia kuepuka hali zenye zilifanya aangukie mu zambi. Kama anajikaza kutengeneza uhusiano wake pamoja na Yehova, anaweza kuwa hakika kama Yehova atamusamehe kabisa, na kama wazee watamusaidia arudishwe mu kutaniko. Wakati wazee wako wanajaribu kujua kama mutu alitubu kikweli ao hapana, wanajua kama kila hali iko tofauti na ingine. Njo maana wanachunguza kila hali kwa uangalifu sana, na wanaepuka kukamata uamuzi haraka-haraka.

19. Namna gani mutu anaweza kuonyesha kama anatubu kikweli? (Ezekieli 33:14-16)

19 Sawa vile tuliona, mutenda-zambi anaonyesha kama anatubu kikweli, hapana tu kwa kusema kama anahuzunikia zambi yenye alifanya. Lakini anapaswa pia kubadilisha namna yake ya kufikiri na kufanya mambo yenye kuonyesha kabisa kama anatubu kikweli. Na anapaswa kuacha tabia yake ya mubaya na kutii kanuni za Yehova. (Soma Ezekieli 33:14-16.) Jambo ya maana sana yenye mutenda-zambi anapaswa kufanya ni kurudisha uhusiano wake wa muzuri pamoja na Yehova.

SAIDIA MUTENDA-ZAMBI ATUBU

20-21. Namna gani tunaweza kusaidia mutu mwenye alifanya zambi nzito?

20 Yesu alifasiria sehemu fulani ya maana sana ya utumishi wake, wakati alisema: “Nilikuja kuita . . . watenda-zambi ili watubu.” (Lu. 5:32) Na siye tunapaswa kumuiga Yesu juu ya ile jambo. Kwa mufano unafikia kusikia kama, rafiki yako wa karibu sana alifanya zambi nzito. Unapaswa kufanya nini?

21 Tutakuwa tumefanya kosa sana kama tunafichika zambi ya rafiki yetu. Kufanya vile ni kujichokesha tu bure, juu Yehova iko anaona. (Mez. 5:21, 22; 28:13) Unaweza kusaidia rafiki yako wakati unamuambia kuwa wazee wanapenda kumusaidia. Kama rafiki yako anakatala kuenda kutubu kwa wazee, weye uende kuwaambia ile zambi. Kufanya vile ni kumusaidia kabisa rafiki yako, juu uhusiano wake na Yehova uko mu hatari!

22. Tutaona nini mu habari yenye kufuata?

22 Tuseme nini kama mutenda-zambi alifanya zambi nzito na kama aliifanya kwa muda murefu, na wazee wanaamua kama anapaswa kutengwa? Ile inaonyesha kama hawakumutendea kwa huruma? Mu habari yenye kufuata, tutaona huruma ya Yehova mu namna yenye iko anatendea watenda-zambi na namna tunaweza kumuiga.

WIMBO 103 Yehova Ametupatia Wachungaji

^ Kutubu kikweli haiko tu kusema kama tunahuzunika juu tulifanya zambi fulani. Kupitia mufano wa Mufalme Ahabu, Mufalme Manase, na mwana mupotevu mwenye Yesu alizungumuzia, hii habari itatusaidia kuelewa maana ya kutubu kikweli. Tena, itaonyesha ni mambo gani wazee wanapaswa kufikiria sana ili kuamua kama ndugu ao dada fulani mwenye alifanya zambi, anatubu kikweli.

^ MAFASIRIO YA PICHA: Kwa hasira, Mufalme Ahabu anaamuru walinzi wake wamutie nabii wa Yehova Mikaya mu gereza.

^ MAFASIRIO YA PICHA: Mufalme Manase iko anaongoza kazi ya kuharibu sanamu zenye yeye aliwekaka mu hekalu.

^ MAFASIRIO YA PICHA: Mwana mupotevu, iko mwenye kuchoka juu alifanya safari ya murefu, lakini iko mwenye furaha juu anaona kwao, kwa umbali.