Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 43

Usife Moyo!

Usife Moyo!

“Tusife moyo katika kufanya mema.”​—GAL. 6:9.

WIMBO 68 Kupanda Mbegu ya Ufalme

MUHTASARI *

1. Kwa nini tuna shangwe na tunajivunia nini?

 TUNA shangwe na tunajivunia kuwa Mashahidi wa Yehova! Tunabeba jina la Mungu na kuishi kupatana na jina hilo kwa kushiriki katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Tunashangilia tunapomsaidia mtu aliye na “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima” kuwa mwamini. (Mdo. 13:48) Tunahisi kama Yesu, ‘aliyekuwa na shangwe kubwa kupitia roho takatifu’ wanafunzi wake waliporudi kutoka kwenye kampeni ya kuhubiri iliyofanikiwa.​—Luka 10:1, 17, 21.

2. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunaichukulia huduma yetu kwa uzito?

2 Tunaichukulia kwa uzito huduma yetu. Mtume Paulo alimhimiza hivi Timotheo: “Jiangalie daima wewe mwenyewe na kufundisha kwako.” Paulo aliongeza hivi: “Ukifanya hivyo utajiokoa wewe mwenyewe na wale wanaokusikiliza pia.” (1 Tim. 4:16) Hivyo, maisha ya watu yako hatarini. Tunajiangalia daima sisi wenyewe kwa sababu sisi ni raia wa Ufalme wa Mungu. Sikuzote tunataka kutenda kwa njia inayomletea sifa Yehova na inayopatana na habari njema tunazohubiri. (Flp. 1:27) Tunaonyesha kwamba ‘tunaangalia kufundisha kwetu’ kwa kujitayarisha vizuri kwa ajili ya huduma na kuomba baraka za Yehova kabla ya kuwahubiria wengine.

3. Huenda watu wakaitikiaje wanaposikia ujumbe wa Ufalme? Toa mfano.

3 Ingawa hivyo, hata tunapofanya yote tunayoweza, huenda watu katika eneo letu wasipendezwe na ujumbe wa Ufalme. Fikiria kisa cha Ndugu Georg Lindal, aliyehubiri peke yake eneo lote la nchi ya Iceland, kuanzia mwaka wa 1929 hadi 1947. Aliwaachia watu maelfu ya machapisho, lakini hakuna hata mmoja aliyekubali kweli. Aliandika hivi: “Yaonekana watu kadhaa wameamua kukataa kweli, lakini walio wengi hawajali hata kidogo.” Hata baada ya wamishonari waliozoezwa katika shule ya Gileadi kuwasili na kupanua kazi, miaka mingine tisa ilipita kabla ya baadhi ya wenyeji wa Iceland kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. *

4. Huenda tukahisije watu wasipoitikia vizuri habari njema?

4 Tunavunjika moyo watu wasipoitikia vizuri habari njema. Huenda tukahisi kama mtume Paulo, ambaye alikuwa na “huzuni kubwa na maumivu yasiyoisha” kwa sababu Wayahudi kwa ujumla walikataa kumkubali Yesu kuwa Masihi aliyeahidiwa. (Rom. 9:1-3) Vipi ikiwa licha ya jitihada zako zote kwa ajili ya mwanafunzi wa Biblia na kusali kwa ajili yake, anashindwa kufanya maendeleo na unahitaji kusitisha funzo? Au vipi ikiwa wewe binafsi hujawahi kumsaidia mtu afikie hatua ya ubatizo? Je, unapaswa kuhisi hatia, labda ukifikiri kwamba Yehova hajabariki huduma yako? Katika makala hii, tutajibu maswali mawili: (1) Ni nini kinachofanya huduma yetu ifanikiwe? (2) Tunapaswa kuwa na matarajio gani halisi?

NI NINI KINACHOFANYA HUDUMA YETU IFANIKIWE?

5. Kwa nini huenda tusipate matokeo tunayotarajia katika kazi yetu kwa Yehova?

5 Biblia inasema hivi kuhusu mtu anayefanya mapenzi ya Mungu: “Kila jambo analofanya litafanikiwa.” (Zab. 1:3) Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba katika kila jambo tunalofanya kwa ajili ya Yehova, tutapata matokeo kama tulivyotarajia. Maisha ya mwanadamu “yamejaa taabu” kwa sababu ya kutokamilika kwetu na kwa wengine pia. (Ayu. 14:1) Zaidi ya hayo, wapinzani wetu huenda wakafanikiwa kwa muda mfupi kuingilia jitihada zetu za kutimiza huduma kwa njia yetu ya kawaida. (1 Kor. 16:9; 1 The. 2:18) Hivyo, Yehova anapimaje mafanikio yetu? Fikiria baadhi ya kanuni za Biblia zinazotusaidia kujibu swali hilo.

Yehova anathamini jitihada zetu, iwe tunawahubiria watu ana kwa ana, kupitia barua, au kupitia simu (Tazama fungu la 6)

6. Yehova anapimaje mafanikio ya kazi yetu kwa ajili yake?

6 Yehova hutazama jitihada na uvumilivu wetu. Machoni pa Yehova, kazi yetu inafanikiwa tunapoifanya kwa bidii na upendo, haidhuru wengine wanaitikiaje. Paulo aliandika hivi: “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuhudumu na kuendelea kuwahudumia watakatifu.” (Ebr. 6:10) Yehova anakumbuka jitihada na upendo wetu, hata ikiwa jitihada hizo hazitakuwa na matokeo mazuri. Hivyo, maneno haya ambayo Paulo aliwaambia Wakorintho yanakuhusu pia: “Kazi yenu si ya bure kuhusiana na Bwana,” haidhuru kazi hiyo ilileta matokeo uliyotarajia au la.​—1 Kor. 15:58.

7. Tunaweza kujifunza nini kutokana na njia ambayo mtume Paulo alifafanua huduma yake?

7 Mtume Paulo alikuwa mmishonari mwenye bidii, aliyeanzisha makutaniko mapya katika majiji mengi. Hata hivyo, wakati alipohisi alihitaji kutetea kustahili kwake akiwa mhudumu wa Kristo, hakukazia idadi ya watu aliokuwa amewasaidia kuwa waamini. Badala yake, akikataa madai ya wale waliotafuta kujikweza juu yake, Paulo aliandika hivi: “Nimefanya kazi nyingi zaidi.” (2 Kor. 11:23) Kama Paulo, kumbuka kwamba jambo muhimu zaidi kwa Yehova ni jitihada na uvumilivu wetu.

8. Tunapaswa kukumbuka nini kuhusu huduma yetu?

8 Huduma yetu inamfurahisha Yehova. Yesu aliwatuma wanafunzi wake 70 wakahubiri ujumbe wa Ufalme, na walipomaliza kampeni hiyo ‘walirudi wakiwa na shangwe.’ Shangwe yao ilitokana na nini? Walisema hivi: “Hata tunawatiisha roho waovu kwa kutumia jina lako.” Hata hivyo, Yesu alirekebisha njia yao ya kufikiri alipowaambia hivi: “Msishangilie kwa sababu mnawatiisha roho waovu, bali shangilieni kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni.” (Luka 10:17-20) Yesu alijua kwamba hawatapata matokeo mazuri kama hayo sikuzote katika huduma yao. Isitoshe, hatujui ni watu wangapi kati ya wale ambao mwanzoni waliwasikiliza wanafunzi wa Yesu, walikuja kuwa waamini. Wanafunzi hao walihitaji kupata shangwe, si tu katika mambo waliyotimiza, bali jambo la muhimu hata zaidi, kwa kujua kwamba Yehova alikuwa akifurahishwa na bidii yao.

9. Kulingana na Wagalatia 6:7-9, tutapata nini ikiwa tutavumilia katika huduma yetu?

9 Ikiwa tutavumilia katika huduma yetu, tutapata uzima wa milele. Tunapopanda kwa moyo wote mbegu za kweli ya Ufalme na kuzitunza, ‘tunapanda pia kwa roho,’ kwa kuruhusu roho takatifu ya Mungu itende kwa uhuru maishani mwetu. Maadamu ‘hatufi moyo’ au ‘kuchoka,’ Yehova anaahidi kwamba tutavuna uzima wa milele, haidhuru tumemsaidia mwanafunzi mpya ajiweke wakfu kwa Mungu au la.​—Soma Wagalatia 6:7-9.

TUNAPASWA KUWA NA MATARAJIO GANI HALISI?

10. Ni nini kinachoamua itikio la watu katika huduma yetu?

10 Kihalisi, itikio tunalopata linategemea hali ya moyoni ya wasikilizaji wetu. Yesu alieleza kweli hiyo katika mfano wake wa mpandaji aliyepanda mbegu katika aina tofauti za udongo, ambapo ni moja tu ilizaa matunda. (Luka 8:5-8) Yesu alisema kwamba aina tofauti za udongo zinawakilisha watu ambao mioyo yao huitikia kwa njia tofauti wanapolisikia “neno la Mungu.” (Luka 8:11-15) Kama mpandaji huyo, hatuwezi kudhibiti matokeo ya kazi yetu, kwa kuwa yanategemea hali ya moyoni ya wasikilizaji wetu. Wajibu wetu ni kuendelea kupanda mbegu nzuri ya ujumbe wa Ufalme. Kama mtume Paulo alivyosema, “kila mtu atapokea thawabu yake kulingana na kazi yake mwenyewe,” na si kulingana na matokeo ya kazi yake.​—1 Kor. 3:8.

Ingawa Noa alihubiri kwa uaminifu kwa miaka mingi, hakuna watu wengine waliojiunga naye katika safina isipokuwa watu wake wa karibu wa familia. Hata hivyo, Noa alifanikiwa kumtii Mungu! (Tazama fungu la 11)

11. Kwa nini Noa alikuwa “mhubiri wa uadilifu” aliyefanikiwa? (Tazama picha kwenye jalada.)

11 Watumishi wa Yehova wa mapema waliwahubiria watu ambao hawakuwasikiliza. Kwa mfano, inaelekea Noa alikuwa “mhubiri wa uadilifu” kwa miaka 40 au 50 hivi. (2 Pet. 2:5) Bila shaka, alitumaini kwamba watu wengine wangeitikia vizuri ujumbe aliohubiri, lakini Yehova hakumpa ishara yoyote kuonyesha ingekuwa hivyo. Badala yake, Mungu alimwambia hivi Noa alipomwagiza ajenge safina: “Nawe lazima uingie ndani ya safina, wewe, wanao, mke wako, na wake wa wanao.” (Mwa. 6:18) Na kulingana na vipimo na ukubwa wa safina ambayo Mungu alimwambia ajenge, huenda Noa alitambua kwamba si watu wengi ambao wangemsikiliza. (Mwa. 6:15) Kama tu ilivyotukia, hakuna hata mtu mmoja kutoka katika ulimwengu huo wenye jeuri aliyeitikia vizuri ujumbe ambao Noa alihubiri. (Mwa. 7:7) Je, Yehova aliona kwamba Noa alikuwa ameshindwa kuitimiza kazi? La hasha! Machoni pa Yehova, Noa alikuwa mhubiri mwenye mafanikio kwa sababu alifanya kwa uaminifu jambo ambalo Yehova alimwambia afanye.​—Mwa. 6:22.

12. Nabii Yeremia alipataje shangwe katika huduma yake licha ya watu kutosikiliza na kukabili upinzani?

12 Kwa miaka mingi, nabii Yeremia pia aliwahubiria watu ambao hawakumsikiliza na waliompinga. Alivunjika moyo sana kwa sababu ya ‘kutukanwa na kudhihakiwa’ na wapinzani hivi kwamba alifikiria kuacha mgawo wake. (Yer. 20:8, 9) Lakini Yeremia hakufa moyo! Ni nini kilichomsaidia kushinda mawazo yake yasiyofaa na kupata shangwe katika huduma yake? Alikazia mambo mawili muhimu. Kwanza, ujumbe wa Mungu ambao Yeremia aliwapelekea watu ungewapatia “wakati ujao na tumaini.” (Yer. 29:11) Pili, Yehova alimchagua Yeremia aitwe kwa jina lake ili awatangazie watu ujumbe Wake. (Yer. 15:16) Sisi pia tunawapelekea watu wa ulimwengu huu wenye kukatisha tamaa ujumbe wa tumaini, na tunalibeba jina la Yehova tukiwa Mashahidi wake. Tunapokazia fikira mambo hayo mawili muhimu, tunaweza kupata shangwe haidhuru watu wanaitikia vizuri au la.

13. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Yesu katika andiko la Marko 4:26-29?

13 Ukuzi wa kiroho unatokea hatua kwa hatua. Yesu alifundisha kweli hiyo katika mfano wake wa mpandaji anayelala. (Soma Marko 4:26-29.) Matokeo ya jitihada za mpandaji huyo yalikuja hatua kwa hatua na kwa sehemu kubwa yalikuwa nje ya uwezo wake. Huenda wewe pia kwa kipindi fulani cha wakati usione matokeo katika kazi yako ya kufanya wanafunzi, kwa sababu ukuzi hufanyika polepole na hatua kwa hatua. Kama tu ambavyo mkulima hawezi kuilazimisha mimea yake ikue kwa kasi anayotamani, sisi pia hatuwezi kuwalazimisha wanafunzi wetu wa Biblia wafanye maendeleo ya kiroho kwa kasi tunayotaka. Hivyo, usivunjike au kufa moyo ikiwa wanafanya maendeleo polepole, tofauti na ulivyotarajia. Kama kazi ya kilimo ilivyo, kazi ya kufanya wanafunzi inahitaji subira.​—Yak. 5:7, 8.

14. Ni mfano gani unaoonyesha kwamba huenda tukapata matokeo katika huduma yetu hatua kwa hatua?

14 Katika baadhi ya maeneo, huenda ikachukua muda mrefu kabla ya matokeo ya huduma yetu kuonekana. Fikiria kisa cha Gladys na Ruby Allen, dada wawili wa kimwili ambao mwaka wa 1959 walipewa mgawo wa upainia wa kawaida katika mji fulani kwenye jimbo la Quebec, Kanada. * Kwa sababu ya kushinikizwa na jamii na ushawishi wa kanisa Katoliki, watu hawakukubali kusikiliza ujumbe wa Ufalme. Gladys anakumbuka hivi: “Tulienda nyumba kwa nyumba kwa saa nane kila siku kwa miaka miwili na hakuna hata mtu mmoja aliyefungua mlango wake! Watu walifika tu mlangoni na kushusha pazia. Lakini hatukukata tamaa.” Baada ya muda, mtazamo wa watu ulibadilika na eneo likawa lenye matokeo zaidi. Sasa kuna makutaniko matatu katika mji huo.​—Isa. 60:22.

15. Andiko la 1 Wakorintho 3:6, 7 linatufundisha nini kuhusu kazi ya kufanya wanafunzi?

15 Kazi ya kufanya wanafunzi inahitaji jitihada za pamoja. Imesemwa kwamba inahitaji kutaniko zima ili kumsaidia mtu afikie hatua ya ubatizo. (Soma 1 Wakorintho 3:6, 7.) Mhubiri fulani anamwachia trakti au gazeti mtu anayependezwa. Kisha ndugu huyo anatambua kwamba ratiba yake haitamruhusu kumrudia mtu huyo ili kuendeleza upendezi, hivyo anamwomba mhubiri mwingine akamfanyie ziara mtu huyo. Mhubiri huyo anafaulu kuanzisha funzo la Biblia. Kisha, anawaalika ndugu na dada kadhaa waandamane naye kwenye funzo hilo la Biblia katika pindi tofauti-tofauti, na kila mmoja anamtia moyo mwanafunzi kwa njia tofauti. Kila ndugu au dada ambaye mwanafunzi huyo anakutana naye, atasaidia kutia maji kwenye mbegu hiyo ya kweli. Kwa njia hiyo, kama Yesu alivyosema, mpandaji na mvunaji wanaweza kushangilia pamoja katika mavuno ya kiroho.​—Yoh. 4:35-38.

16. Kwa nini unaweza kupata shangwe katika huduma yako hata ikiwa afya yako si nzuri au huna nguvu za kutosha?

16 Namna gani ikiwa huwezi kutimiza mengi katika kazi ya kuhubiri na kufundisha habari njema kwa sababu afya yako si nzuri au huna nguvu za kutosha? Bado unaweza kupata shangwe katika kazi ya mavuno. Fikiria kisa cha Mfalme Daudi pindi yeye na wanaume wake walipokomboa familia na mali zao kutoka kwa Waamaleki waliowashambulia. Wanaume 200 kati yao walikuwa wamechoka sana hivi kwamba wasingeweza kupigana, hivyo walibaki nyuma ili kulinda mizigo. Baada ya kushinda pambano, Daudi aliamuru kwamba nyara zigawanywe kwa usawa miongoni mwao wote. (1 Sam. 30:21-25) Ndivyo ilivyo na kazi yetu ya ulimwenguni pote ya kufanya wanafunzi. Kila anayefanya yote anayoweza, atashiriki shangwe ileile pamoja na wengine kwa kila mtu mpya anayekombolewa na kusaidiwa kuanza kutembea katika barabara ya uzima.

17. Tunapaswa kumshukuru Yehova kwa ajili ya nini?

17 Tunamshukuru Yehova kwa mtazamo wake wenye upendo kuelekea utumishi wetu kwake. Anajua kwamba hatuwezi kuongoza matokeo ya jitihada zetu. Hata hivyo, anaona bidii na nia yetu nzuri, naye atatuthawabisha. Pia, anatufundisha jinsi ya kupata shangwe katika yale tunayoweza kutimiza kwenye kazi hii kubwa ya mavuno. (Yoh. 14:12) Tunaweza kuwa na hakika kwamba tutapata kibali cha Yehova maadamu hatufi moyo!

WIMBO 67 “Lihubiri Neno”

^ fu. 5 Tunafurahia watu wanapoitikia vizuri habari njema, na tunavunjika moyo wanaposhindwa kufanya hivyo. Vipi ikiwa mwanafunzi wa Biblia unayemsaidia hafanyi maendeleo? Au vipi ikiwa wewe binafsi hujawahi kumsaidia mtu yeyote afikie hatua ya ubatizo? Je, ufikie mkataa kwamba umeshindwa kutimiza kazi ya kufanya wanafunzi? Katika makala hii, tutaona kwa nini tunaweza kufanikiwa katika huduma yetu na kupata shangwe licha ya itikio tunalopata.

^ fu. 3 Tazama Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 2005, ukurasa wa 205 hadi 211.

^ fu. 14 Tazama simulizi la maisha la Gladys Allen lenye kichwa “Siwezi Kubadili Kitu Ng’o!” kwenye gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 2002.