Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Jitihada Yangu ya Kutafuta Maisha Yenye Kujaa Kusudi

Jitihada Yangu ya Kutafuta Maisha Yenye Kujaa Kusudi

NILIPOKUWA nikisafiri kwa mashua katikati ya Bahari ya Mediterania, nilishtuka kugundua kwamba mashua yangu iliyozeeka ilikuwa ikivuja sana na kuingiza lita nyingi sana za maji. Kisha kukawa na dhoruba. Nikaogopa, na kwa mara ya kwanza baada ya miaka mingi, nikasali. Ilikuwaje nikajipata katika hali hiyo? Acheni nianzie mwanzoni.

Nilipokuwa na umri wa miaka 7, familia yetu iliishi nchini Brazili

Nilizaliwa nchini Uholanzi mwaka wa 1948. Mwaka uliofuata, familia yetu ilihamia jijini São Paulo, Brazili. Wazazi wangu walikuwa na bidii ya kwenda kanisani, na tukiwa familia tulisoma Biblia kwa ukawaida baada ya mlo wa jioni. Mwaka wa 1959 tulihama tena, lakini wakati huu, tulihamia Marekani kwenye jimbo la Massachusetts.

Baba alifanya kazi kwa bidii ili kuitunza familia yetu yenye watu nane. Alifanya kazi akiwa muuza bidhaa aliyesafiri, mfanyakazi kwenye ujenzi wa barabara, na mwakilishi wa mauzo wa shirika moja la ndege la kimataifa. Wote katika familia tulifurahi sana alipopata kazi kwenye shirika la ndege kwa sababu shirika hilo lilituwezesha kusafiri maeneo mbalimbali.

Wakati nilipokuwa shule ya sekondari, mara kwa mara nilijiuliza, ‘Nitafanya nini maishani nitakapokua?’ Baadhi ya rafiki zangu walichagua kwenda chuo kikuu, na wengine walienda jeshini. Lakini mimi sikutaka kwenda jeshini kwa sababu sikuwahi kupenda mabishano, sembuse kwenda kupigana! Niliamua kwenda chuo kikuu ili kuepuka kwenda jeshini. Hata hivyo, moyoni mwangu nilitamani kuwasaidia wengine, nikifikiri kwamba kufanya hivyo kungenifanya niwe na kusudi la kweli maishani mwangu.

MAISHA YA CHUONI

Kwa miaka mingi, nilitafuta kusudi la maisha

Nikiwa chuoni, nilivutiwa na somo la anthropolojia, kwa kuwa nilikuwa na udadisi kuhusu chanzo cha uhai. Tulifundishwa nadharia ya mageuzi na tulitarajiwa tuikubali kuwa jambo hakika. Lakini kwangu, baadhi ya ufafanuzi haukupatana na akili na ulihitaji mtu aamini bila kuwa na uthibitisho, jambo ambalo ni kinyume na mbinu ya kisayansi.

Katika vipindi nilivyohudhuria, hatukufundishwa viwango vya juu vya maadili. Badala yake, walikazia zaidi jinsi ya kufanikiwa kwa gharama yoyote ile. Nilifurahia niliposhirikiana na watu kwenye tafrija na kutumia dawa za kulevya, lakini furaha hiyo haikudumu. Nilijiuliza, ‘Je, kwa kweli haya ndiyo maisha yenye kusudi?’

Wakati huo, nilihamia katika jiji la Boston na kujiunga na chuo kikuu huko. Ili kulipia gharama za masomo, nilifanya kazi wakati wa likizo ambapo nilikutana na Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza. Mfanyakazi mwenzangu alinieleza kuhusu unabii wa “nyakati saba” unaopatikana katika Danieli sura ya 4, na kunieleza kwamba tulikuwa tunaishi wakati wa mwisho. (Dan. 4:13-17) Haraka nikatambua kwamba ikiwa nitaendelea kuwa na mazungumzo hayo na kuyachukulia kwa uzito, ningehitaji kubadili njia yangu ya maisha. Hivyo, nilimwepuka mfanyakazi huyo kadiri nilivyoweza.

Nikiwa chuoni, nilijifunza masomo ambayo yangeniandaa kuwa mjitoleaji huko Amerika ya Kusini. Nilifikiri kwamba kutoa misaada ya kijamii kungenipa kusudi maishani. Lakini shaka nilizokuwa nazo kuhusu jinsi ya kupata kusudi maishani zilizidi kuongezeka. Nikiwa nimevunjika moyo, niliacha masomo ya chuo mwishoni mwa muhula.

JITIHADA YANGU YA KUTAFUTA MAISHA YENYE KUSUDI YAENDELEA KATIKA NCHI ZA MBALI

Mwezi wa Mei 1970, nilihamia Amsterdam, Uholanzi, ili kufanya kazi katika shirika la ndege lilelile ambalo baba yangu alifanya kazi. Kwa sababu ya kazi hiyo, niliweza kusafiri sehemu mbalimbali, nilitembelea nchi za Afrika, Amerika, Ulaya, na Mashariki ya Mbali. Baada ya muda mfupi, nilitambua kwamba haidhuru nchi niliyotembelea, zote zilikabili matatizo makubwa na ilionekana hakuna aliyekuwa na suluhisho la matatizo hayo. Tamaa yangu ya kutimiza jambo fulani muhimu iliporudi tena, niliamua kurudi Marekani na kuendelea na masomo kwenye chuo kikuu kilekile cha Boston.

Hata hivyo, muda mfupi baada ya kurudi chuoni nilitambua kwamba bado nilikuwa sipati majibu ya maswali yangu kuhusu uhai. Nikiwa sijui la kufanya, niliamua kumwomba ushauri profesa wangu wa anthropolojia. Alinishangaza aliponijibu hivi: “Kwa nini uendelee na masomo? Kwa nini usiache sasa hivi?” Hakuhitaji kurudia ushauri huo. Niliacha chuo na sikurudi tena.

Bado maisha yalikosa kusudi, hivyo nikaamua kujihusisha zaidi na kile kilichojulikana kuwa kizazi cha flower-power, kilichohamasisha amani na upendo. Mimi pamoja na baadhi ya marafiki wangu tulisafiri kutoka Marekani hadi Acapulco, Mexico, kwa kuomba lifti kutoka kwa watu mbalimbali. Tuliishi pamoja na wale waliofahamika kama hippies, ambao walionekana wanaishi maisha yasiyo na matatizo au mahangaiko. Lakini muda mfupi baada ya kuishi nao, niligundua kwamba njia yao ya maisha haikuwa na kusudi na haikuleta furaha ya kudumu. Badala yake, niliona kwamba wengi wao hawakuwa wanyoofu na washikamanifu.

JITIHADA YANGU YAENDELEA KWENYE MASHUA

Pamoja na rafiki yangu, tulitafuta kisiwa kilicho kama paradiso

Wakati huo, nilianza kufikiria tena ndoto yangu ya utotoni. Nilitamani kuendesha mashua baharini, lakini si kama baharia, bali kama nahodha. Njia pekee ambayo ningeweza kufanya hivyo ni kwa kuwa na mashua yenye tanga niliyomiliki mwenyewe. Kwa kuwa rafiki yangu aliyeitwa Tom, alikuwa na tamaa kama yangu, tuliamua kusafiri pamoja kwa mashua kuizunguka dunia. Nilitaka kutafuta kisiwa cha kitropiki kilicho kama paradiso ambako ningekuwa mbali na mifumo ya kijamii na sheria zake.

Mimi na Tom tulisafiri kwenda Arenys de Mar, karibu na jiji la Barcelona, Hispania. Huko tulinunua mashua yenye tanga iliyokuwa na urefu wa mita 9.4, iliyoitwa Llygra. Tulianza kuifanyia marekebisho ili ihimili safari za baharini. Kwa kuwa hatukuwa na haraka ya kufika mwisho wa safari yetu, tulitoa injini na tukatumia nafasi iliyobaki kuweka maji ya kunywa ya ziada. Ili kuiendesha mashua hiyo kwenye bandari ndogo, tulikuwa na makasia mawili yenye urefu wa mita 5. Hatimaye, tukaanza safari yetu kuelekea kwenye visiwa vya Shelisheli katika Bahari ya Hindi. Lengo letu lilikuwa ni kusafiri kando ya pwani ya Afrika Magharibi na kupita Rasi ya Tumaini Jema, Afrika Kusini. Tulitumia kifaa cha kupima pembe (sextant) ili tuchore ramani ya kutuongoza, kwa kutumia nyota, chati za nyota, na vitabu. Nilishangazwa na jinsi tulivyoweza kutambua kwa usahihi mahali tulipokuwa.

Baada ya muda mfupi, tulitambua kwamba mashua hiyo ya mbao ilikuwa haifai kusafiri baharini. Iliingiza maji kiasi cha lita 22 kwa saa! Kama nilivyotaja mwanzoni, wakati wa dhoruba niliogopa na nilisali kwa mara ya kwanza baada ya miaka mingi na kumwahidi Mungu kwamba ikiwa nitaokoka nitajitahidi kumjua. Dhoruba ilitulia, na pindi hii nilitimiza ahadi yangu.

Nilianza kusoma Biblia tulipokuwa baharini. Wazia ilivyopendeza kuwa katikati ya Bahari ya Mediterania, ukizungukwa na samaki wanaoruka, pomboo, na kutazama upeo wa bahari usio na mwisho. Usiku, nilivutiwa sana na kundi la nyota la Kilimia na nikasadikishwa zaidi kwamba kuna Mungu anayependezwa na wanadamu.

Baada ya majuma kadhaa baharini, tuliwasili kwenye bandari ya Alicante, Hispania, ambapo tulijaribu kuuza mashua yetu ili tupate nzuri zaidi. Haishangazi kwamba haikuwa rahisi kupata mtu ambaye angenunua mashua yetu iliyozeeka, isiyo na injini, na inayovuja! Kwa upande mwingine, huo ulikuwa wakati mzuri sana wa kusoma Biblia yangu.

Kadiri nilivyoisoma Biblia, ndivyo nilivyoanza kuiona kuwa kitabu kinachoweza kutusaidia kufanikiwa maishani. Nilipendezwa na lugha iliyo wazi ya Biblia kuhusu kuishi maisha yaliyo safi kiadili na nikajiuliza kwa nini watu wengi—kutia ndani mimi mwenyewe—wanajiona kuwa Wakristo lakini bado wanapuuza yale ambayo Biblia inasema.

Niliazimia kuchukua hatua muhimu ili kusafisha maisha yangu, hivyo nikaacha kutumia dawa za kulevya. Nilifikiri kwamba lazima kuwe na watu walioishi kulingana na viwango vya juu vya maadili vya Biblia, na nilitaka kukutana nao. Kwa mara ya pili, nilisali, nikimwomba Mungu anisaidie kuwapata.

JITIHADA ZA KUTAFUTA DINI YA KWELI

Kwangu, njia iliyopatana na akili ilikuwa kuchunguza dini moja baada ya nyingine hadi nitakapoipata ya kweli. Nilipokuwa nikipita kwenye mitaa ya jiji la Alicante, niliona majengo mengi ya kidini. Lakini kwa sababu majengo mengi yalikuwa na sanamu, ilikuwa rahisi kwangu kuyaondoa kwenye orodha.

Jumapili moja mchana, nilikuwa kwenye kilima kinachotazama bandari, nikisoma Yakobo 2:1-5, andiko linaloonya dhidi ya kuwaonyesha upendeleo matajiri. Nilipokuwa nikirudi kwenye mashua, niliona jengo lililoonekana kama mahali pa ibada, na kwenye mwingilio wake kulikuwa na ishara, “Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova.”

Nilijiambia, ‘Ninapaswa kuwajaribu watu hawa. Acha nione watakavyonipokea.’ Hivyo, nikaingia Jumba la Ufalme bila viatu, nikiwa na ndevu, na kuvaa suruali ya jinzi iliyochanika-chanika. Mkaribishaji alinielekeza kwenye kiti kilichokuwa karibu na dada mwenye umri mkubwa ambaye kwa fadhili alinisaidia kupata mistari ya Biblia iliyotajwa na msemaji. Baada ya mkutano, nilishangazwa na fadhili niliyoonyeshwa na wale waliokuja kunisalimu. Mwanamume mmoja alinialika nyumbani kwake kwa ajili ya mazungumzo, lakini kwa sababu sikuwa nimemaliza kusoma Biblia, nilimwambia, “Nitakwambia nitakapokuwa tayari.” Wakati huo, nilianza kuhudhuria mikutano yote.

Majuma kadhaa baadaye, nilimtembelea mwanamume huyo nyumbani kwake, naye alinijibu maswali yangu ya Biblia. Juma moja baadaye, alinipatia mfuko uliojaa nguo nzuri sana. Aliniambia kwamba mwenye nguo hizo alikuwa gerezani kwa sababu ya kutii amri ya Biblia ya kupendana na kutojifunza vita tena. (Isa. 2:4; Yoh. 13:34, 35) Sasa nilikuwa na uhakika kwamba nimepata kile nilichokuwa ninatafuta—watu wanaoishi kulingana na lugha iliyo wazi ya Biblia kuhusu maadili! Lengo langu halikuwa tena kutafuta kisiwa kilicho kama paradiso, bali kujifunza Biblia kwa kina. Hivyo, nikarudi Uholanzi.

NATAFUTA KAZI

Nilisafiri kwa siku nne nikiomba lifti kwa watu mbalimbali ili kufika kwenye jiji la Groningen, Uholanzi. Huko nilihitaji kupata kazi ili kujitegemeza. Kwenye karakana moja ya useremala nilipoomba kazi, fomu niliyojaza ilihitaji niandike dini yangu. Niliandika, “Mashahidi wa Yehova.” Mmiliki wa karakana hiyo alipoona hilo, mwonekano wa uso wake ulibadilika. Akasema, “Nitakupigia.” Lakini hakufanya hivyo.

Katika karakana nyingine ya useremala, nilimuuliza mmiliki ikiwa alihitaji msaada. Aliniomba vyeti vya diploma na barua za kumbukumbu. Nilimweleza kwamba nilikuwa nimefanya kazi ya kurekebisha mashua ya mbao. Nilishangaa aliposema, “Unaweza kuanza kazi mchana huu lakini kwa sharti moja. Sitaki usababishe tatizo lolote katika karakana yangu kwa sababu mimi ni Shahidi wa Yehova na ninaishi kulingana na kanuni za Biblia.” Nilimtazama kwa mshangao na kumjibu, “Mimi pia!” Bila shaka, kwa sababu ya nywele na ndevu zangu ndefu, aliniambia hivi, “Basi, nitajifunza Biblia pamoja nawe!” Nilikubali kwa shangwe mwaliko huo. Sasa ilikuwa wazi kwangu kwa nini yule mmiliki mwingine hakunipigia. Yehova alikuwa akijibu sala zangu. (Zab. 37:4) Nilifanya kazi katika karakana ya ndugu huyo kwa mwaka mmoja. Katika kipindi hicho, alijifunza Biblia pamoja nami, kisha nikabatizwa Januari 1974.

HATIMAYE, NAPATA MAISHA YALIYOJAA KUSUDI!

Mwezi mmoja baadaye, nilianza kazi mpya​—utumishi wa upainia—ambayo imenipatia uradhi mwingi. Mwezi uliofuata, nilihamia Amsterdam ili kuunga mkono kikundi cha Kihispania kilichokuwa kimeanzishwa. Ilikuwa shangwe kubwa sana kuongoza mafunzo ya Biblia katika Kihispania na Kireno! Mwezi wa Mei 1975, nilipata pendeleo la kutumikia nikiwa painia wa pekee.

Siku moja, Ineke, dada painia wa pekee, alikuja kwenye mkutano wetu wa Kihispania ili kumtambulisha mwanafunzi wake wa Biblia kutoka Bolivia. Mimi na Ineke tuliamua kufahamiana vizuri zaidi kupitia barua, jambo ambalo ndani ya muda mfupi lilifunua kwamba tulikuwa na malengo yanayofanana. Tulifunga ndoa mwaka wa 1976 na kuendelea kutumikia tukiwa mapainia wa pekee hadi mwaka wa 1982 tulipoalikwa kuhudhuria darasa la 73 la Gileadi. Tulishangaa na kufurahi sana tulipopewa mgawo wa kwenda Afrika Mashariki, ambapo tulitumikia kwa miaka 5 jijini Mombasa, Kenya! Mwaka wa 1987, tulipewa mgawo wa kwenda Tanzania, ambako marufuku ya kazi yetu ilikuwa imeondolewa. Tulitumikia nchini humo kwa miaka 26 kabla ya kurudi tena nchini Kenya.

Kuwasaidia watu Afrika Mashariki wajifunze kweli za Biblia kumenipatia mimi na mke wangu shangwe nyingi sana

Kuwasaidia watu wenye uthamini wajifunze kweli za Biblia kumetupatia kusudi la kweli maishani. Kwa mfano, mwanafunzi wangu wa kwanza wa Biblia huko Mombasa ni mwanamume niliyekutana naye nilipokuwa nafanya mahubiri ya hadharani. Nilipompatia magazeti mawili, akasema, “Nitakapoyamaliza, nifanye nini?” Juma lililofuata tulianza kujifunza Biblia kwa kutumia kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, kilichokuwa kimetolewa karibuni katika Kiswahili. Alibatizwa mwaka mmoja baadaye na kuwa painia wa kawaida. Tangu wakati huo, yeye na mke wake wamewasaidia karibu watu 100 wajiweke wakfu na kubatizwa.

Mimi na Ineke tumejionea jinsi Yehova huwabariki watumishi wake kwa kuwapatia maisha yaliyojaa kusudi

Nilipotambua kwa mara ya kwanza kusudi la maisha, nilihisi kama yule mfanyabiashara anayesafiri aliyegundua lulu ya pekee na hakutaka kuipoteza. (Mt. 13:45, 46) Nilitaka kutumia maisha yangu kuwasaidia wengine wapate kusudi la kweli maishani. Pamoja na mke wangu mpendwa, tumejionea wenyewe jinsi Yehova anavyowabariki watu wake kwa kuwapatia maisha yaliyojaa kusudi.