Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI JUU YA MAISHA YA WATU

Nilikuwa Natafuta Kusudi ya Maisha

Nilikuwa Natafuta Kusudi ya Maisha

WAKATI tulifika katikati ya Bahari ya Mediterania, nilivumbula kama mashua yangu ilikuwa na tundu, na ile ilifanya maji mingi ianze kuingia mu mashua. Kisha pale, kulitokea upepo. Niliogopa na nikasali kwa mara ya kwanza mu maisha yangu. Nini njo ilinifikishaka mu ile hali? Muache niwaelezee.

Wakati nilikuwa na miaka saba, miye na familia yangu tulikuwa naishi Brazili

Nilizaliwa Pays-Bas mu 1948. Mwaka yenye ilifuata, familia yangu ilihamia São Paulo, mu Brazili. Wazazi wangu walipenda sana kanisa, na siye wote mu familia tulikuwa tunasoma Biblia kwa ukawaida kisha chakula ya mangaribi. Mu 1959 tulihamia mu inchi ya Amerika, na tukaikala mu Massachusetts.

Baba alikuwa natumika sana juu ya kuhangaikia familia yetu ya watu munane. Alitumika kazi mbalimbali; alikuwa mufanyabiashara, alitumika mu kazi ya kujenga mabarabara, na alitumika mu kompanyi ya avion ya kuenda fasi yote mu dunia. Tulifurahi sana wakati baba alipata kazi mu ile kompanyi, juu ile ilitupatia nafasi ya kutembea sana.

Wakati nilikuwa ku segondere, mara mingi nilikuwa najiuliza, ‘Nitafanyaka nini wakati nitakuwa mutu mukubwa?’ Wamoja kati ya marafiki wangu walichagua kuenda ku université, wengine walienda mu kazi ya kiaskari. Lakini miye, sikupenda hata kidogo kazi ya kiaskari juu sikukuwa napenda kusumbuana, na kupigana. Kwa hiyo niliamua kuenda ku université. Lakini ile nilikuwa napenda sana ni kusaidia watu. Nilikuwa nawaza kama ile ingefanya nikuwe na maisha yenye kuwa na kusudi.

WAKATI NILIKUWA KU UNIVERSITÉ

Nilitafuta kusudi ya maisha kwa miaka mingi

Ku université, nilikuwa napenda sana masomo ya antropolojia, juu nilikuwa napenda sana kujua namna uzima ulianza. Walimu wetu walitufundisha mageuzi na walipenda tuiamini. Lakini mafasirio ingine haikueleweka na iliomba tu niiamini sawa vile kipofu.

Mu masomo yetu, hatukufundishwa kanuni za juu za mwenendo. Ile tulikuwa naambiwa kila wakati, ni kufanya kila kitu yenye tunaweza juu tuweze masomo. Nilifurahia kutumia dawa za kulewesha, na kuenda ku karamu mbalimbali ili kujifurahisha pamoja na marafiki. Lakini niliona kama ile haikuniletea furaha ya kuendelea. Nilijiuliza hivi: ‘Hii njo kusudi ya maisha kweli?’

Kisha, nilihamia mu muji wa Boston na nikajiandikisha ku université moja kule. Nilikuwa natumika wakati wa mapumuziko juu nipate makuta ya kulipa ku masomo. Na ni ile wakati njo nilikutana na Shahidi moja wa Yehova kwa mara ya kwanza. Mufanyakazi mwenzangu aliniambia kuhusu unabii wa “nyakati saba” wenye kuwa mu Danieli sura ya 4, na akanifasiria kama tulikuwa naishi mu siku za mwisho. (Da. 4:13-17) Palepale nilitambua kama, nikiendelesha mazungumuzo ya Biblia pamoja naye, na kuamini mambo yenye nilikuwa najifunza, ile ingefanya nibadilishe njia yangu ya maisha. Kwa hiyo, nilianza kufanya yangu yote juu nimuepuke.

Mambo nilikuwa nasoma ku université ingenitayarisha juu nikuwe mujitoleaji mu kazi fulani mu Amerika ya Kusini. Niliwaza kama, juu nipate kusudi ya maisha, iliomba nikuwe nasaidia watu fulani wenye kuwa na lazima ya musaada. Lakini nilifikia kuona kama, hata ile haikunisaidia kupata kusudi ya maisha. Nilivunjika moyo na kisha miezi sita nikaacha masomo.

NAENDA MU INCHI ZA MBALI ILI KUTAFUTA KUSUDI YA MAISHA

Mwezi wa 5, 1970 nilihamia Amsterdam, mu Pays-Bas, juu ya kutumika mu kompanyi ya avion yenye baba yangu alikuwa anatumika amo. Ile kazi ilinisaidia nikuwe natembea sana. Nilitembelea inchi za mu Afrika, Amerika ya kaskazini na ya kusini, Ulaya, na Asia. Lakini niliona kama mu kila inchi yenye nilitembelea, watu wote walikuwa tu na magumu ya nguvu na hakuna mwenye alionekana kama iko na uwezo ya kuimaliza. Juu nilikuwa napenda kabisa kufanya jambo fulani ya maana mu maisha yangu, niliamua kurudia mu inchi ya Amerika na nilijiandikisha tena ku ileile université ya Boston.

Lakini, hata kama nilianza masomo tena, niliona kama haikunisaidia kupata majibu ku maulizo yenye nilikuwa najiuliza kuhusu maisha. Juu sikujua nifanye nini, niliomba mashauri mwalimu wangu wa antropolojia. Nilishangaa wakati aliniambia hivi: “Uko najisumbua juu ya nini? Si uache tu masomo?” Niliona kama mashauri yenye alinipatia ilikuwa ya muzuri. Kwa hiyo, niliacha masomo lote.

Juu nilikuwa bado siyapata kusudi ya maisha yangu, niliamua kujiunga na kikundi ya watu wenye hawakufuata-fuata watu juu ya desturi zao na walionekana sawa vile wanapenda kusaidia watu wote wakuwe na amani na wapendane. Miye na marafiki wangu fulani, tulitoka mu Inchi ya Amerika na tukaenda Acapulco, mu Mexico. Tulianza kuishi na watu wenye namna yao ya kuishi ilikuwa tofauti na ya watu wengine, na walionekana sawa vile hawana mahangaiko ao shida mu maisha yao. Lakini wakati tulianza kuishi nao, nilitambua kama namna yao ya kuishi haikukuwa na kusudi na haikuleta furaha ya kuendelea. Wengi kati yao hawakukuwa wanyoofu na washikamanifu.

NATUMIA MASHUA ILI KUENDELEA KUTAFUTA KUSUDI YA MAISHA

Miye na rafiki yangu, wakati nilikuwa natafuta kisiwa ya muzuri

Ile wakati, nilianza kuwaza tena juu ya muradi wenye nilikuwa nao wakati nilikuwaka mutoto. Nilikuwa napenda kufanya safari mu bahari, na nilipenda nikuwe kapiteni, hapana mutumishi wa mashua. Juu niweze kufanya vile, iliomba tu nikuwe na mashua yangu. Rafiki yangu Tom naye alikuwa na mawazo ya vile, kwa hiyo, tuliamua kutembea mu dunia yote kwa kutumia mashua. Nilipenda kutafuta kisiwa ya muzuri yenye kuwa na kifukutu, mwenye ningeweza kuikala bila kusumbuliwa na sheria mingi-mingi.

Miye na Tom tulienda Arenys de Mar, karibu na Barcelona, mu Espagne. Kule, tuliuza mashua ya metre 9,4 yenye kuitwa Llygra. Tulianza kuitengeneza muzuri, juu tusafiri muzuri mu bahari. Vile hatukukuwa mu haraka ya kufika kwenye tulikuwa tunaenda, tulitosha motere na tukatumia ile fasi juu ya kuweka amo maji mingi ya kunywa. Kwa hiyo, juu ya kutembeza mashua yetu ili tufike ku bandari mbalimbali, tuliuza makasia mbili za metre 5. Ku mwisho, tulianza safari yetu ya kuenda Seychelle, mu Bahari ya India. Tulikuwa na mupango ya kupita pembeni ya pwani ya mangaribi ya Afrika, na kuzunguka Cap de Bonne Esperance, mu Afrika ya Kusini. Tulikuwa naangalia nyota, tulitumia karte, vitabu na vifaa fulani juu vitusaidie kujua njia. Nilishangaa kuona vile hatukupotea.

Lakini, tulitambua bila kukawia kama ile mashua yetu ya zamani ya mbao haikufaa kabisa kwa ajili ya safari mu bahari. Ilikuwa naingiza litre 22 hivi ya maji kila saa! Sawa vile nilisema ku mwanzo, wakati ya upepo, niliogopaka na nikasali kwa mara ya kanza mu maisha yangu. Nilikuwa namuambia Mungu kama tukiokoka, nitajikaza kumujua. Upepo ulitulia, na kisha nilianza kutimiza ahadi yangu.

Nilianza kusoma Biblia na tuko mu bahari. Wazia vile ilifurahisha wakati nilikuwa mu mashua, katikati ya Bahari ya Mediterania, niko naangalia aina mbalimbali za samaki, na sione kwenye bahari inaishia. Wakati ya usiku, nilikuwa nafurahia sana kuangalia nyota mingi, na ile ilifanya nikuwe hakika kabisa kama kuko Mungu mwenye anahangaikiaka wanadamu.

Kisha kufanya majuma fulani mu bahari, tulifika ku bandari ya Alicante, mu Espagne. Ni kule njo tuliuzisha mashua yetu juu tuuze ingine ya muzuri zaidi. Haikukuwa mwepesi kupata mutu wa kuiuza juu ilikuwa mashua ya zamani, haikukuwa na motere, na ilikuwa naingiza maji! Lakini, niliona kama ile ilikuwa wakati ya muzuri zaidi kwangu kusoma Biblia.

Kadiri nilikuwa nasoma Biblia, ni vile nilianza kuelewa kama ni kitabu yenye kuwa na mashauri ya muzuri, yenye inaweza kutusaidia ili tukuwe na furaha. Nilifurahi kuona vile Biblia inafasiria waziwazi namna ya kuwa na mwenendo safi mu maisha, na nilianza kujiuliza juu ya nini watu wengi, kutia ndani na miye, tunajiona kuwa Wakristo, lakini hatufuate mambo yenye Biblia inasema.

Niliamua kukamata maamuzi ya maana juu nikuwe na mwenendo ya muzuri. Kwa hiyo, niliacha kutumia dawa za kulewesha. Niliwaza kama kunapaswa kuwa watu wenye kuishi kulingana na kanuni za juu za mwenendo, zenye kuwa mu Biblia, na nilipenda kuonana nao. Nilisali kwa mara ya pili mu maisha yangu; nilimuomba Mungu anisaidie niwaone.

NATAFUTA DINI YA KWELI

Juu nipate dini ya kweli, nilianza kuchunguza kila dini. Wakati nilikuwa natembea mu barabara za Alicante, niliona majengo mingi ya dini. Lakini juu ku majengo ya mingi kulikuwa sanamu, nilitambua kama haikukuwa dini ya kweli.

Siku moja ya Yenga kisha midi, nilikuwa ku mulima na niko naona bandari kwa mbali; nilikuwa nasoma Yakobo 2:1-5, yenye inasema kama ni mubaya kupendelea watu juu ni matajiri. Wakati nilikuwa narudia fasi kwenye kulikuwa mashua yetu, niliona jengo fulani yenye ilionekana sawa vile munafanyiwaka mikutano ya kidini. Juu ya mulango ya ile jengo kulikuwa naandikwa: “Jumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova.”

Nilijiambia hivi, ‘Napaswa kujaribu hawa watu. Acha nione vile watanipokelea.’ Kwa hiyo niliingia mu ile Jumba ya Ufalme bila kuvala viato, nilikuwa na ndevu mingi, na pantalon yangu ilikuwa ya kutoboka-toboka. Mukaribishaji alinipatia fasi karibu na mwanamuke fulani mwenye kuzeeka, mwenye alikuwa nanisaidia kupata maandiko yenye musemaji alikuwa nazungumuzia. Kisha mukutano, nilishangaa kuona vile wote wenye walikuja kunisalimia, walinitendea mu njia ya muzuri. Mwanaume moja alinialika kwake juu ya kuzungumuza na miye, lakini juu nilikuwa siyamaliza kusoma Biblia, nilimuambia hivi: “Siku nitakuwa tayari, nitakuambia.” Kuanzia pale, nilianza kuhuzuria mikutano yote.

Kisha majuma fulani, nilienda kumuona ule mwanaume kwake, na alijibia maulizo yenye nilikuwa nayo juu ya Biblia. Kisha juma moja, alinipatia sakoshe yenye ilikuwa nayala manguo ya muzuri sana. Aliniambia kama mwenye ile manguo alikuwa mu gereza, juu alitii amri yenye kuwa mu Biblia ya kupendana na kuepuka kujifunza vita tena. (Isa. 2:4; Yoh. 13:34, 35) Ni pale sasa njo nilihakikisha kama nilipata kile nilikuwaka natafuta, ni kusema, watu wenye kutumikisha mashauri yenye kuwa mu Biblia, ya kuwa na mwenendo safi! Sikuendelea tena na muradi yangu ya kutafuta kisiwa ya muzuri, lakini niliamua kuanza kujifunza Biblia kwa undani. Kwa hiyo, nilirudia Pays-Bas.

NATAFUTA KAZI

Nilifanya siku ine juu nifike mu muji wa Groningen, mu Pays-Bas. Iliomba nipate kazi ya kunisaidia kutimiza mahitaji yangu. Nilienda kutafuta kazi ku atelier moja ya useremala; kisha nilipewa makaratasi ya kujaza, na ku moja kati ya ile makaratasi, iliomba nionyesha kama niko wa dini gani. Niliandika hivi: “Mashahidi wa Yehova.” Wakati mwenye ile atelier aliisoma, niliona sura yake inabadilika. Kisha akasema hivi: “Nitakuita.” Lakini hakuniitaka.

Niliamua kuenda ku atelier ingine ya useremala. Kisha nikauliza mwenye nayo kama alikuwa na lazima ya musaada. Aliniomba nionyeshe diplome yangu na mabarua yenye kuonyesha kazi yenye nilikuwa nafanya. Nikamuambia kama nilitengenezaka mashua moja ya mbao yenye ilikuwaka ilishachoka. Nilishangaa wakati aliniambia hivi: “Utaanza kutumika leo kisha midi. Lakini, usiniharibishie kazi yangu, juu niko Shahidi wa Yehova na ninaishi kulingana na kanuni za Biblia.” Nilishangaa sana kisha nikamuambia hivi: “Na miye niko Shahidi wa Yehova!” Lakini juu nilikuwa na nywele murefu na ndevu ya mingi, alitambua kama siko Shahidi, kisha akaniambia hivi: “Sawa, nitaanza kujifunza Biblia na weye!” Niliitikia ile kwa furaha. Pale njo nilielewa waziwazi juu ya nini ule wa atelier ya kwanza hakuniitaka tena. Yehova alikuwa ananitimizia tamaa ya moyo wangu. (Zb. 37:4) Nilitumika mu atelier ya ule ndugu kwa mwaka moja. Mu ile kipindi alijifunza Biblia pamoja na miye, kisha nilibatizwa Mwezi wa 1, 1974.

KU MWISHO, NILIPATA KUSUDI YA MAISHA!

Kisha mwezi moja, nilianza kazi ingine; kazi ya upainia. Ile kazi ilinifurahisha sana. Mwezi yenye ilifuata, nilienda Amsterdam juu ya kutegemeza kikundi ya luga ya Kihispania, yenye ilikuwa imeanzishwa. Nilifurahi sana kuongoza mafunzo ya Biblia mu luga ya Kihispania na ya Kireno (Portugais)! Mwezi wa 5, 1975, nilipata pendeleo ya kuwa painia wa pekee.

Siku moja, Catharina, dada moja mwenye alikuwa painia wa pekee, alikuja ku mukutano yetu ya luga ya Kihispania juu ya kutuonyesha mwanafunzi wake wa Biblia wa mu inchi ya Bolivia. Miye na Catharina tuliamua kuanza kuandikiana barua juu tujuane muzuri, na ile ilifanya tuone kama siye wote tulikuwa na miradi moja. Tulioana mu 1976 na tukaendelea kuwa mapainia wa pekee mupaka 1982; na ni mu ile mwaka njo tulialikwa ku masomo ya Gileadi ya 73. Tulifurahi na kushangaa sana wakati tulitumwa mu Afrika ya Mashariki. Tulifanya miaka tano na tuko natumikia Mombasa, mu Kenya! Mu 1987, tulitumwa Tanzania, mwenye kazi ya kuhubiri ilikuwa haikatazwe tena. Tulifanya kule miaka 26 mbele ya kurudia Kenya.

Miye na bibi yangu tumepata furaha mingi kwa kusaidia watu wajifunze kweli za Biblia mu Afrika ya Mashariki

Kusaidia wapole wajifunze kweli ya Biblia, kulitusaidia tukuwe na maisha yenye kuwa na kusudi. Kwa mufano, mwanafunzi wangu wa kwanza wa Biblia mu Mombasa, ni mwanaume mwenye nilipataka wakati nilikuwa nahubiri mahali pa watu wengi. Kisha kumupatia magazeti mbili, alisema hivi: “Kama minamaliza kuisoma, nitafanya nini tena?” Juma yenye ilifuata, tulianza kujifunza naye mu kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, yenye ilikuwa imetoka tu kutolewa mu Swahili. Kisha mwaka moja, alibatizwa na akakuwa painia wa kawaida. Kuanzia pale, yeye na bibi yake walishasaidia watu karibu 100 kujitoa kwa Yehova na kubatizwa.

Miye na Catharina tumejionea namna Yehova anabariki watumishi wake kwa kuwasaidia kupata maisha yenye kuwa na kusudi

Wakati nilielewa kwa mara ya kwanza kusudi ya maisha, nilijisikia sawa ule mufanyabiashara mwenye kusafiri, mwenye alipata lulu ya pekee, na hakupenda kuipoteza. (Mt. 13:45, 46) Mu maisha yangu nilipenda kusaidia watu wapate kusudi ya maisha. Miye na bibi yangu mupendwa, tumejionea kabisa namna Yehova anabariki watu kwa kuwasaidia wapate maisha yenye kuwa na kusudi.