Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 48

“Munapaswa Kuwa Watakatifu”

“Munapaswa Kuwa Watakatifu”

“Mukuwe watakatifu katika mwenendo wenu wote.”​1 PE. 1:15.

WIMBO 34 Nitatembea kwa Uaminifu-Mushikamanifu

KIFUPI YA HABARI *

1. Ni shauri gani yenye mutume Petro alipatia waamini wenzake, na juu ya nini inaweza kuonekana kama haiwezekane kutumikisha ile shauri?

 IKUWE tuko na tumaini ya kuishi mbinguni ao ku dunia, tunaweza kupata faida kwa kuchunguza mambo yenye mutume Petro aliambia Wakristo watiwa-mafuta wa karne ya kwanza. Petro aliandika hivi: “Kama ule Mutakatifu mwenye aliwaita ninyi, ninyi wenyewe pia mukuwe watakatifu katika mwenendo wenu wote, kwa maana imeandikwa: ‘Munapaswa kuwa watakatifu, kwa sababu mimi ni mutakatifu.’” (1 Pe. 1:15, 16) Kupitia hii maneno tunajifunza kama, Yehova ni mufano muzuri zaidi wa utakatifu. Tunaweza na tunapaswa kuwa watakatifu mu mwenendo wetu. Juu hatukamilike ile inaweza kuonekana kama haiwezekane. Petro alifanya makosa ya mingi, lakini mufano wake unaonyesha kama tunaweza “kuwa watakatifu.”

2. Tutazungumuzia maulizo gani mu hii habari?

2 Mu hii habari tutazungumuzia hii maulizo: Utakatifu njo nini? Biblia inatufundisha nini kuhusu utakatifu wa Yehova? Namna gani tunaweza kuwa watakatifu katika mwenendo wetu? Na kuko uhusiano gani kati ya utakatifu na urafiki wetu pamoja na Yehova?

UTAKATIFU NJO NINI?

3. Watu wengi wanakuwaka na mawazo gani kuhusu maana ya utakatifu, na ni wapi tunaweza kupata maana ya kweli?

3 Watu wengi wanawaza kama mutu mutakatifu ni mwenye hachekake-chekake, mwenye anavalaka nguo za dini na mutu mwenye ukiona tu sura yake inaonyesha kama hapendake tu mizaha. Lakini ile haiko kweli. Yehova mwenye ni mutakatifu, anazungumuziwa kama “Mungu mwenye furaha.” (1 Ti. 1:11) Wale wenye wanamuabudu wanaitwa kuwa “wenye furaha.” (Zb. 144:15) Yesu alihukumu wale wenye kuvala nguo yenye kuwa tofauti na za wengine na kufanya mambo ya muzuri juu tu waonekane na watu. (Mt. 6:1; Mk. 12:38) Tukiwa Wakristo wa kweli, tunajua maana ya utakatifu, juu ya mambo yenye tumejifunza mu Biblia. Tuko hakika kama Mungu wetu mutakatifu na mwenye upendo hawezi kutuambia tufanye jambo yenye hatuwezi kufanya. Kwa hiyo, wakati Yehova anatuambia hivi: “Munapaswa kuwa watakatifu,” tuko hakika kama inawezekana kuwa watakatifu. Kusema kweli, mbele tukuwe watakatifu katika mwenendo wetu, tunapaswa kuelewa kwanza maana ya utakatifu.

4. Maneno “takatifu” na “mutakatifu” inamaanisha nini?

4 Utakatifu njo nini? Mu Biblia maneno “utakatifu” na “mutakatifu” inatumiwa ili kuonyesha utakatifu mu mambo ya mwenendo na utakatifu mu mambo ya ibada. Ile maneno mbili inaleta pia wazo ya kutiwa pembeni ili kumutumikia Mungu. Mu maneno ingine tunaweza kuonwa kuwa watakatifu kama tuko na mwenendo safi ikiwa tunamutumikia Yehova vile inaomba na kama tuko na urafiki wa kipekee pamoja naye. Tunashangaa kujua kama hata ikiwa hatukamilike na hata kama Yehova ni mukamilifu kabisa anapenda tukuwe marafiki wake.

“MUTAKATIFU, MUTAKATIFU, MUTAKATIFU NI YEHOVA”

5. Malaika waaminifu wanaweza kutufundisha nini kumuhusu Yehova?

5 Yehova ni mutakatifu na safi mu mambo yote. Ile njo mambo yenye maserafi ao malaika wenye walikuwa karibu na kiti ya Ufalme ya Yehova walisema. Wamoja kati yao walisema hivi: “Mutakatifu, mutakatifu, mutakatifu ni Yehova wa majeshi.” (Isa. 6:3) Juu wakuwe na urafiki wa karibu pamoja na Mungu wao mutakatifu, malaika wanapaswa kuwa watakatifu na ni vile wanakuwaka. Njo maana fasi mbalimbali kwenye malaika walileta ujumbe ku dunia, ile fasi ilionwa kuwa takatifu. Ni ile njo ilifikia Musa wakati alikuwa karibu na ule muti mudogo wa miiba wenye ulikuwa unawaka moto.​—Kut. 3:2-5; Yos. 5:15.

Maneno “Utakatifu ni wa Yehova” ilikuwa kwenye bamba yenye kungaa ya zahabu kwenye kilemba ya kuhani mukubwa (Ona fungu ya 6-7)

6-7. (a) Kulingana na Kutoka 15:1, 11, Musa alifasiria namna gani utakatifu wa Mungu? (b) Ni mambo gani ilikumbusha Waisraeli kama Mungu ni mutakatifu? (Ona picha kwenye jalada.)

6 Kisha Musa kuongoza Waisraeli kupitia bahari nyekundu, aliwafasiria waziwazi kama Mungu wao, Yehova ni mutakatifu. (Soma Kutoka 15:1, 11.) Waabudu wa miungu ya Misri hawakukuwa na mwenendo safi, ilikuwa pia vile kwa waabudu wa miungu ya Kanaani. Ibada yao ilitia ndani kutolea miungu yao watoto kama zabihu na kufanya matendo ya uasherati ya mubaya sana. (Law. 18:3, 4, 21-24; Kum. 18:9, 10) Lakini, Yehova hangeweza kuwaambia waabudu wake wafanye jambo fulani yenye ingewashushia heshima, juu Yeye ni mutakatifu kabisa. Ili kuwakumbusha Waisraeli ile jambo, kulikuwa bamba yenye kungaa ya zahabu kwenye kilemba ya kuhani mukubwa. Ku ile bamba kulikuwa maneno “Utakatifu ni wa Yehova.”​—Kut. 28:36-38.

7 Ujumbe wenye ulikuwa ku ile bamba ungehakikishia kila mutu mwenye anaiona kuwa Yehova ni mutakatifu kabisa. Lakini, tuseme nini juu ya Mwisraeli mwenye hangeweza kuona ile bamba juu hangeweza kumukaribia kuhani mukubwa? Ni kusema hangeweza kupata ule ujumbe wa maana sana? Hapana! Kila Mwisraeli alisikia ule ujumbe wakati sheria ilisomwa mbele ya wanaume, wanamuke na watoto. (Kum. 31:9-12) Kama ungekuwa pale ungesikia maneno: “Mimi ni Yehova Mungu wenu, na munapaswa . . . kuwa watakatifu, kwa sababu mimi ni mutakatifu.” “Munapaswa kuwa watakatifu mbele yangu, kwa sababu mimi, Yehova, niko mutakatifu.”​—Law. 11:44, 45; 20:7, 26.

8. Tunajifunza nini mu Mambo ya Walawi 19:2 na mu 1 Petro 1:14-16?

8 Tufikirie maneno fulani yenye kuwa mu Mambo ya Walawi 19:2 yenye ilisomwa mbele ya Waisraeli wote. Yehova aliambia Musa hivi: “Sema na kutaniko lote la Waisraeli na uwaambie, ‘Munapaswa kuwa watakatifu, kwa sababu mimi, Yehova Mungu wenu, ni mutakatifu.’” Inawezekana Petro alitaja maneno fulani ya mu ile andiko wakati aliambia Wakristo ‘wakuwe watakatifu.’ (Soma 1 Petro 1:14-16.) Kusema kweli, hatuko chini ya Sheria ya Musa, lakini mambo yenye Petro aliandika inahakikisha mambo yenye tunajifunza mu Mambo ya Walawi 19:2, yenye inasema kama Yehova ni mutakatifu na wale wenye wanamupenda wanapaswa kujikaza kuwa watakatifu. Ile kabisa ni kweli, ikuwe tuko na tumaini ya kuishi mbinguni ao hapa ku dunia mu paradiso.​—1 Pe. 1:4; 2 Pe. 3:13.

“MUKUWE WATAKATIFU KATIKA . . . MWENENDO WENU WOTE”

9. Namna gani tunaweza kufaidika kwa kuchunguza Mambo ya Walawi sura ya 19?

9 Juu tunapenda kumufurahisha Mungu wetu mutakatifu, tunapenda kujifunza namna tunaweza kuwa watakatifu. Yehova anatutolea mashauri fulani juu tujue namna ya kufanya vile. Tunaweza kupata ile mashauri mu Mambo ya Walawi sura ya 19. Mutu moja mwenye elimu, mwenye kuitwa Marcus Kalisch, aliandika hivi: “Hii sura ya pekee, pengine njo sura yenye kueleweka zaidi, ya maana zaidi ya kitabu ya Mambo ya Walawi na njo sura ya maana zaidi kati ya vitabu tano vya kwanza vya Biblia.” Wakati tutakuwa tunaona zile somo mbalimbali, tusisahau kama maneno “Munapaswa kuwa watakatifu” iko mu mustari wa 2. Tuzungumuzie sasa mistari fulani ya mu hii sura yenye inatufundisha njia mbalimbali zenye zinaweza kutusaidia kuwa watakatifu mu maisha yetu ya kila siku.

Amri kuhusu wazazi yenye kuwa mu Mambo ya Walawi 19:3 inapaswa kuchochea Wakristo kufikiria nini? (Ona fungu ya 10-12) *

10-11. Mambo ya Walawi 19:3 inasema tunapaswa kufanya nini, na juu ya nini ni jambo ya maana kufanya vile?

10 Kisha kusema kama Waisraeli walipaswa kuwa watakatifu, Yehova aliongezea hivi: “Kila mumoja wenu anapaswa kumuheshimia mama yake na baba yake . . . Mimi ni Yehova Mungu wenu.”​—Law. 19:2, 3.

11 Ni wazi kuwa tunapaswa kukamata kwa uzito amri ya kuheshimia wazazi wetu. Tukumbuke mambo yenye Yesu alisema wakati mwanaume moja alimuuliza hivi: “Ni mambo gani mema yenye ninapaswa kufanya ili nipate uzima wa milele?” Sehemu ya jibu ya Yesu iliomba ule mwanaume aheshimie baba yake na mama yake. (Mt. 19:16-19) Yesu alihukumu hata mafarisayo na masadukayo juu walifanya yao yote ili wasihangaikie wazazi wao. Njo maana mu ile njia ‘walifanya neno la Mungu kuwa kitu cha bure.’ (Mt. 15:3-6) “Neno la Mungu” inatia ndani amri ya tano kati ya zile amri Kumi yenye tunasoma mu Mambo ya Walawi 19:3. (Kut. 20:12) Tena, tusisahau kama muongozo yenye kupatikana mu Mambo ya Walawi 19:3, ni kusema, kuheshimia mama na baba inakuya tu kisha maneno “Munapaswa kuwa watakatifu, kwa sababu mimi, Yehova Mungu wenu, ni mutakatifu.”

12. Kulingana na shauri yenye kuwa mu Mambo ya Walawi 19:3, tunaweza kujiuliza ulizo gani?

12 Wakati tunafikiria amri yenye Yehova alitupatia ya kuheshimia wazazi wetu, pengine tunaweza kujiuliza hivi, ‘Ninaheshimiaka wazazi wangu?’ Kama unawaza kuwa zamani ungepaswa kufanya zaidi ni wakati sasa wa kuamua kufanya mabadiliko. Hauwezi kubadilisha mambo ya zamani, lakini sasa unaweza kufanya yako yote ili kupitisha wakati mingi pamoja na wazazi wako na ili kuwasaidia zaidi. Pengine unaweza kufanya vile kwa kupanga programu ya kupitisha wakati nao. Ao pengine unaweza kuwasaidia kwa kuwauzia vitu vyenye wako navyo lazima ao kwa kuwasaidia waendelee kumukaribia Yehova na kuendelea kumutumikia. Ao tena unaweza kuwatia moyo na kuwafariji zaidi. Kama unafanya vile, unatii amri yenye kuwa mu Mambo ya Walawi 19:3.

13. (a) Ni mashauri gani ingine yenye tunapata mu Mambo ya Walawi 19:3? (b) Leo, namna gani tunaweza kuiga mufano wa Yesu wenye kuwa mu Luka 4:16-18?

13 Mambo ya Walawi 19:3 inatufundisha jambo ingine kuhusu kuwa watakatifu. Inazungumuzia kushika Sabato. Wakristo hawako chini ya Sheria ya Musa, njo maana hatushikake Sabato. Lakini tunaweza kujifunza mambo mingi kupitia namna Waisraeli walishika Sabato na namna walipata faida kwa kufanya vile. Sabato ilikuwa wakati wa kupumuzika, ni kusema, wa kutofanya kazi, lakini wakati wa kukazia uangalifu mambo ya kiroho. * Njo maana siku ya Sabato Yesu alikuwa anaenda mu sinagogi mu muji kwenye alikomalia na alisoma Neno ya Mungu. (Kut. 31:12-15; Soma Luka 4:16-18.) Amri ya Mungu yenye kuwa mu Mambo ya Walawi 19:3 ya “kushika Sabato [zake]” inapaswa kutuchochea kukamata wakati mu maisha yetu ya kila siku ili kumuabudu Mungu. Unawaza kama kuko mabadiliko fulani yenye unapaswa kufanya ili kutii ile amri? Kila mara kama unakamata wakati wa kukazia uangalifu mambo ya kiroho utakomalisha urafiki wako pamoja na Yehova, na ile ni jambo ya maana sana ili kuwa mutakatifu.

UTIE NGUVU URAFIKI WAKO PAMOJA NA YEHOVA

14. Ni kweli gani ya maana yenye inarudiliwa mara mingi mu Mambo ya Walawi sura ya 19?

14 Mambo ya Walawi sura ya 19 inarudilia mara mingi kweli ya maana yenye inaweza kutusaidia tubakie watakatifu. Mustari wa 4 unamalizia na maneno: “Mimi ni Yehova Mungu wenu.” Ile maneno inapatikana mara 16 mu hii sura. Ile inatukumbusha amri ya kwanza: “Mimi ni Yehova Mungu wako . . . Haupaswe kuwa na miungu mingine isipokuwa mimi.” (Kut. 20:2, 3) Kila Mukristo mwenye anapenda kuwa mutakatifu, anapaswa kuwa hakika kama hakuna jambo fulani ao mutu yeyote mwenye kuwa wa maana sana kuliko urafiki wake pamoja na Yehova. Na juu tuko Mashahidi wa Yehova, tunafanya yetu yote ili kuepuka kila tendo yenye inaweza kuchafua jina takatifu ya Mungu.​—Law. 19:12; Isa. 57:15.

15. Mistari yenye kupatikana mu Mambo ya Walawi sura ya 19, yenye inahusu zabihu, inapaswa kutuchochea kufanya nini?

15 Waisraeli walionyesha kama walikubali Yehova kuwa Mungu wao kwa kutii amri zake. Mambo ya Walawi 18:4 inasema hivi: “Munapaswa kutimiza maamuzi yangu ya hukumu, na munapaswa kushika amri zangu na kuzifuata. Mimi ni Yehova Mungu wenu.” Sura ya 19 inatia ndani “amri” fulani za Waisraeli. Kwa mufano, mistari ya 5-8, 21, 22 inataja zabihu za wanyama. Waisraeli walipaswa kutoa zile zabihu mu njia yenye haingepaswa ‘kuchafua kitu kitakatifu cha Yehova.’ Kusoma ile mistari kunapaswa kutuchochea kumupendeza na kumutolea Yehova zabihu ya sifa sawa vile Waebrania 13:15 inatutia moyo kufanya.

16. Ni jambo gani yenye inaweza kutukumbusha tofauti yenye kuwa kati ya wale wenye kumutumikia Mungu na wale wenye hawamutumikie?

16 Ili kuwa watakatifu tunapaswa kuishi mu namna yenye watu wataona kama tuko tofauti na wale wenye hawamutumikie Mungu. Inaweza kuwa nguvu kufanya vile. Wakati fulani, wanafunzi wenzetu, wafanyakazi wenzetu ao watu wa familia yetu wenye hawamutumikie Yehova na watu wengine wanaweza kutuzuia kumuabudu mu njia yenye anapenda tumuabudu. Kama wanafanya vile, ni lazima tukamate uamuzi fulani. Nini njo inaweza kutusaidia tukamate uamuzi wa muzuri? Fikiria kanuni fulani ya muzuri yenye kuwa mu Mambo ya Walawi 19:19, yenye sehemu moja yake inasema hivi: “Haupaswe kuvaa nguo yenye ilitengenezwa na nyuzi za aina mbili zenye kuchanganywa pamoja.” Ile amri ilisaidia Waisraeli kuwa tofauti na mataifa yenye iliwazunguka. Leo, vile hatuko chini ya Sheria ya Musa, haiko mubaya kwa Mukristo kuvala nguo zenye zilifanywa na coton na polyester. Lakini tunakatala kuwa sawa vile watu wenye imani yao na mambo yenye wanafanya haipatane kabisa na mambo Biblia inafundisha, hata kama wale watu ni wanafunzi wenzetu, wafanyakazi wenzetu ao watu wa familia yetu. Kusema kweli, tunapenda watu wa familia yetu na tunapenda pia watu wengine, lakini maamuzi yenye tunakamata mu maisha njo itaonyesha kama tutamutii Yehova hata kama ile inafanya tukuwe tofauti na watu wenye kutuzunguka. Tukumbuke kama kuwa ngambo ya Mungu ni sehemu ya utakatifu. Na ile ni jambo ya maana kama tunapenda kuwa watakatifu.​—2 Ko. 6:14-16; 1 Pe. 4:3, 4.

Ni somo gani Waisraeli walipaswa kujifunza mu Mambo ya Walawi 19:23-25, na ni somo gani unajifunza mu ile mistari? (Ona fungu ya 17-18) *

17-18. Ni somo gani ya maana yenye tunaweza kujifunza mu Mambo ya Walawi 19:23-25?

17 Maneno “Mimi ni Yehova Mungu wako” ilipaswa kusaidia Waisraeli kuona urafiki wao pamoja na Yehova kuwa jambo ya maana sana mu maisha yao. Namna gani? Mambo ya Walawi 19:23-25 inaonyesha njia moja. (Soma.) Fikiria mambo ile maneno ilimaanisha kwa Waisraeli, wakati tu waliingia mu Inchi ya Ahadi. Kama mwanaume fulani alipanda miti kwa ajili ya chakula, hangepaswa kula matunda ya ile miti kwa miaka tatu. Ku mwaka wa ine matunda ya ile miti ilitiwa pembeni ili kutumiwa katika patakatifu pa Mungu. Ni ku mwaka wa tano njo mwenye alipanda ile miti angeweza kula matunda yake. Ile amri ilipaswa kusaidia Waisraeli kuelewa kama hawakupaswa kutia faida zao pa nafasi ya kwanza. Yehova alipenda watumainie kama angewahangaikia na alipenda watie ibada yake pa nafasi ya kwanza mu maisha yao. Angehakikisha kama walikuwa na chakula ya kutosha. Na Mungu aliwatia moyo kutoa zawadi katika patakatifu, ni kusema, fasi kwenye walimuabudu.

18 Amri yenye kuwa mu Mambo ya Walawi 19:23-25 inatukumbusha maneno ya Yesu ya mu Mahubiri ya Kwenye Mulima. Alisema hivi: ‘Muache kuhangaika . . . juu ya kile mutakula ao kile mutakunywa.’ Yesu aliendelea kusema hivi: “Baba yenu wa mbinguni anajua muko na lazima ya vitu hivi vyote.” Mungu atatupatia mambo yenye tuko nayo lazima sawa vile tu anakulisha ndege. (Mt. 6:25, 26, 32) Tunatumainia kama Yehova atatuhangaikia. Na tunatoa “zawadi za rehema” ili kusaidia wale wenye kuwa na lazima ya musaada, bila kuambia wengine. Tuko pia na furaha ya kutoa yote yenye tuko nayo ili kusaidia garama za kutaniko. Yehova anaona ukarimu wetu wakati tunategemeza ibada yake na atatulipa. (Mt. 6:2-4) Wakati tuko wakarimu tunaonyesha kama tunaelewa somo zenye kuwa mu Mambo ya Walawi 19:23-25.

19. Ni faida gani umepata kwa kuchunguza sehemu fulani ya kitabu ya Mambo ya Walawi?

19 Tumechunguza tu mistari fulani ya Mambo ya Walawi sura ya 19, na imetusaidia kuelewa namna tunaweza kuwa kama Mungu wetu mutakatifu. Wakati tunamuiga, ile inaonyesha kama tuko tunajikaza ‘kuwa watakatifu katika mwenendo wetu wote.’ (1 Pe. 1:15) Watu wengi wenye hawamutumikie Yehova wamejionea na macho yao mwenendo muzuri wa watu wa Yehova. Kwa hiyo, ile imechochea watu fulani wamutukuze Yehova. (1 Pe. 2:12) Lakini kuko mambo mingi yenye tunaweza kujifunza mu Mambo ya Walawi sura ya 19. Habari yenye kufuata itazungumuzia mistari ingine ya mu ile sura na itatusaidia kuelewa njia zingine zenye tunaweza “kuwa watakatifu,” sawa vile Petro alisema.

WIMBO 80 Uonje na Uone Vile Yehova Ni Mwema

^ Tunamupenda Yehova sana na tunapenda kumufurahisha. Yehova ni mutakatifu na anatazamia waabudu wake wakuwe pia watakatifu. Je, ile inawezekana kabisa kwa wanadamu wenye hawakamilike? Ndiyo, inawezekana. Tunaweza kujifunza namna ya kuwa watakatifu mu mambo yote yenye tunafanya wakati tunachunguza mambo yenye mutume Petro aliambia Wakristo na mambo yenye Yehova aliamuru taifa ya Israeli kufanya.

^ Ili kupata habari zaidi juu ya Sabato na kujifunza somo fulani kuhusu Sabato, ona habari “Kuko Wakati wa Kufanya Kazi na Wakati wa Kupumuzika” yenye kuwa mu Munara wa Mulinzi wa Mwezi wa 12, 2019.

^ MAFASIRIO YA PICHA: Mutoto moja mwanaume mwenye kukomala anapitisha wakati na wazazi wake, analeta bibi yake na mutoto wake ili wawatembelee, na anazungumuza nao kila mara.

^ MAFASIRIO YA PICHA: Mwisraeli moja mwenye ni mulimaji anachunguza matunda yenye kuwa ku miti yenye alipanda.