Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wewe Ni Mfanyakazi Mwenzi Mzuri?

Je, Wewe Ni Mfanyakazi Mwenzi Mzuri?

“NILIKUWA kando yake nikiwa mfanyakazi stadi. . . . Nilishangilia mbele zake wakati wote.” (Met. 8:30) Hivyo ndivyo Biblia inavyofafanua jinsi Mwana wa Mungu alivyofanya kazi na Baba yake kwa miaka mingi kabla ya kuja duniani. Ona pia kwamba mstari huo unatuambia jinsi ambavyo Yesu alihisi akiwa mfanyakazi mwenzi wa Mungu; ‘alishangilia’ mbele Zake.

Yesu alijifunza sifa ambazo baadaye zilimfanya awe mfano mzuri wa mfanyakazi mwenzi kwa wale ambao alishirikiana nao duniani. Tunaweza kunufaikaje kutokana na mfano wa Yesu? Kwa kuchunguza kwa ukaribu mfano wake, tunaweza kutambua kanuni tatu ambazo zinaweza kutusaidia kuwa wafanyakazi wenzi wazuri. Kanuni hizo zitatusaidia kuendeleza roho ya umoja na ushirikiano.

Kwa kuzingatia mfano wa Yehova na Yesu, uwe tayari kushiriki uzoefu na ujuzi wako pamoja na wafanyakazi wenzako

KANUNI YA 1: “KUONYESHANA HESHIMA”

Kwa unyenyekevu, mfanyakazi mwenzi mzuri anawathamini wafanyakazi wenzake, naye hajaribu kujionyesha. Yesu alijifunza mtazamo huo wa unyenyekevu kutoka kwa Baba yake. Ingawa Yehova peke yake ndiye anayestahili kuitwa Muumba, alikazia uangalifu jukumu ambalo Mwana wake na mfanyakazi mwenzi, alitimiza. Hilo linaonekana kupitia maneno haya ambayo Mungu alisema: “Na tufanye mtu kwa mfano wetu.” (Mwa. 1:26) Yehova aliposema maneno hayo, Yesu alitambua kwamba Yehova ni mnyenyekevu.​—Zab. 18:35.

Alipokuwa duniani, Yesu alionyesha unyenyekevu kama huo. Aliposifiwa kwa mambo aliyotimiza, alimpa sifa Yule anayestahili. (Marko 10:17, 18; Yoh. 7:15, 16) Yesu alijitahidi kudumisha amani pamoja na wanafunzi wake na aliwaona kuwa rafiki, bali si watumwa. (Yoh. 15:15) Hata aliosha miguu yao ili kuwafundisha unyenyekevu. (Yoh. 13:5, 12-14) Itakuwa vema ikiwa sisi pia tutawathamini wafanyakazi wenzetu badala ya kutanguliza mapendezi yetu ya kibinafsi. Tunaweza kutimiza mengi ikiwa ‘tutawaonyesha heshima’ wengine, badala ya kujaribu kujitafutia sifa.​—Rom. 12:10.

Mtu mnyenyekevu anatambua kwamba “mambo hufanikiwa kupitia washauri wengi.” (Met. 15:22) Licha ya uzoefu au uwezo wetu, tunapaswa kukumbuka kwamba hakuna mtu anayejua kila kitu. Hata Yesu alikiri kwamba kuna mambo ambayo hakujua. (Mt. 24:36) Alitaka pia kujua mambo ambayo wanafunzi wake ambao hawakuwa wakamilifu walijua au walifikiri. (Mt. 16:13-16) Ndiyo sababu wafanyakazi wake wenzi walikuwa huru kuwa karibu naye! Vivyo hivyo, tunapokuwa wanyenyekevu na kutambua kwamba hatujui mambo yote na kusikiliza maoni ya wengine, tunaendeleza amani na wengine, na kwa pamoja ‘mambo yanafanikiwa.’

Ni muhimu hasa kwa wazee wa kutaniko kuiga unyenyekevu wa Yesu wanapofanya kazi pamoja. Wanapaswa kukumbuka kwamba roho takatifu inaweza kutenda kwa mzee yeyote katika baraza. Ikiwa kwenye mikutano yao wazee watajitahidi kudumisha hali ambayo kila mmoja anakuwa huru kutoa maoni yake, kwa pamoja watafanya maamuzi ambayo yatalinufaisha kutaniko lote.

KANUNI YA 2: “USAWAZIKO WENU NA UJULIKANE”

Mfanyakazi mwenzi mzuri anashughulika na wafanyakazi wenzake kwa usawaziko. Anabadilikana na hashikilii maoni yake. Bila shaka, Yesu alikuwa na fursa nyingi za kujionea usawaziko wa Baba yake. Kwa mfano, Yehova alimtuma awakomboe wanadamu kutokana na hukumu ya kifo ambayo walikuwa wanastahili.​—Yoh. 3:16.

Yesu alikuwa tayari kubadili maoni yake hali ilipolazimu au ilipofaa kufanya hivyo. Kumbuka jinsi alivyomsaidia mwanamke Mfoinike, hata ingawa alikuwa ametumwa katika nyumba ya Israeli. (Mt. 15:22-28) Pia, alikuwa mwenye usawaziko kuhusu mambo aliyotarajia kutoka kwa wanafunzi wake. Baada ya Petro, rafiki yake wa karibu, kumkana hadharani, Yesu alikuwa tayari kumsamehe. Baadaye, alimkabidhi Petro majukumu mazito. (Luka 22:32; Yoh. 21:17; Mdo. 2:14; 8:14-17; 10:44, 45) Mfano wa Yesu unatuonyesha wazi kwamba tunapaswa kuacha ‘usawaziko wetu ujulikane kwa watu wote,’ kwa kuwa tayari kubadili maoni yetu.​—Flp. 4:5.

Kuwa na usawaziko kutatuchochea pia kubadilika kulingana na hali ili kufanya kazi kwa upatano na watu wa namna zote. Yesu aliwatendea kwa njia nzuri sana watu waliomzunguka hivi kwamba adui zake wenye wivu walimshutumu kwamba alikuwa “rafiki ya wakusanya kodi na watenda dhambi,” ambao walikubali ujumbe wake. (Mt. 11:19) Kama Yesu, je, sisi pia tunaweza kushirikiana vizuri na wengine? Louis, ndugu ambaye ametumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko na Mwanabetheli na kufanya kazi na watu wa malezi tofauti-tofauti, anasema hivi: “Nimejaribu kulinganisha kila kikundi ambacho nimefanya nacho kazi na ukuta uliojengwa kwa mawe ambayo hayajakatwa. Unaporekebisha vizuri mpangilio wa mawe hayo, unaweza kujenga ukuta ulionyooka. Mimi pia nimejitahidi kufanya marekebisho ili niweze kuchangia kutokeza ukuta ulionyooka.” Hiyo ni roho nzuri sana!

Mfanyakazi mwenzi mzuri hajaribu kuwadhibiti wafanyakazi wenzake kwa kutowapa habari wanazohitaji

Ni wakati gani ambao tunaweza kuonyesha roho ya ushirikiano katika kutaniko letu? Tuna fursa ya kufanya hivyo tunapokuwa na kikundi chetu cha utumishi. Tunaweza kuhubiri pamoja na wahubiri ambao wana majukumu ya kifamilia tofauti na yetu au wenye umri tofauti na sisi. Je, tunaweza kujitahidi kuwa na usawaziko kwa kuzingatia hali yao au kubadili njia yetu ya kuhubiri ili wafurahie zaidi utumishi?

KANUNI YA 3: UWE “TAYARI KUSHIRIKI VITU NA WENGINE”

Mfanyakazi mwenzi mzuri yuko “tayari kushiriki vitu na wengine.” (1 Tim. 6:18) Alipokuwa akifanya kazi kando ya Baba yake, lazima Yesu alitambua kwamba Baba yake hakuwa akimficha mambo. Yehova “alipozitayarisha mbingu,” Yesu ‘alikuwepo’ na angeweza kujifunza kutoka kwake. (Met. 8:27) Baadaye, kwa furaha Yesu pia alishiriki na wanafunzi wake ‘mambo aliyokuwa amesikia’ kutoka kwa Baba yake. (Yoh. 15:15) Tukiwa na mfano huo akilini, sisi pia tunapaswa kuwa tayari kushiriki ujuzi na uzoefu wetu pamoja na wafanyakazi wenzetu. Bila shaka, mfanyakazi mwenzi mzuri hajaribu kuwadhibiti wafanyakazi wenzake kwa kutowapa habari zinazoweza kuwasaidia au wanazohitaji kujua. Anafurahi kushiriki na wengine mambo mazuri ambayo amejifunza.

Pia, tunaweza kuwatia moyo wafanyakazi wenzetu. Tunafurahi ikiwa mtu fulani anatambua jitihada zetu, na kutushukuru kutoka moyoni. Yesu alitumia wakati kuwaambia wafanyakazi wenzake sifa zao nzuri. (Linganisha Mathayo 25:19-23; Luka 10:17-20.) Hata aliwaambia kwamba wangefanya “kazi kubwa kuliko” zake. (Yoh. 14:12) Usiku kabla ya kifo chake, aliwapongeza mitume wake waaminifu kwa kusema: “Ninyi ndio mmeshikamana nami katika majaribu yangu.” (Luka 22:28) Ni lazima maneno hayo yaliwagusa moyo na kuwachochea kutenda! Ikiwa sisi pia tutawapongeza wafanyakazi wenzetu, bila shaka watakuwa wenye furaha zaidi na kufanya kazi kwa bidii zaidi.

UNAWEZA KUWA MFANYAKAZI MWENZI MZURI

Ndugu anayeitwa Kayode, anasema hivi: “Mfanyakazi mwenzi mzuri si lazima awe mkamilifu, lakini anafanya wengine wafurahi na kurahisisha kazi.” Je, wewe ni mfanyakazi mwenzi wa aina hiyo? Kwa nini usiwaulize baadhi ya Wakristo wenzako maoni yao kukuhusu? Ikiwa wanafurahia kufanya kazi pamoja nawe, kama wanafunzi wa Yesu walivyofurahia kufanya kazi pamoja naye, basi kama mtume Paulo unaweza kusema hivi: “Sisi ni wafanyakazi wenzenu kwa ajili ya shangwe yenu.”—2 Kor. 1:24.