Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 50

Sikilizeni Sauti ya Mchungaji Mwema

Sikilizeni Sauti ya Mchungaji Mwema

“Wataisikiliza sauti yangu.”​—YOH. 10:16.

WIMBO 3 Tumaini, Nguvu, na Uhakika Wetu

MUHTASARI *

1. Ni sababu gani ambayo huenda ilimfanya Yesu awalinganishe wafuasi wake na kondoo?

 YESU alilinganisha uhusiano kati yake na wafuasi wake na uhusiano wa karibu kati ya mchungaji na kondoo wake. (Yoh. 10:14) Ulinganisho huo unafaa. Kondoo wanamjua mchungaji wao, nao huitikia sauti yake. Mtalii mmoja alijionea jambo hilo. Anasema hivi: “Tulitaka kuwapiga picha kondoo fulani na tukajaribu kuwaita waje karibu. Lakini hawakutufuata kwa sababu hawakujua sauti yetu. Kisha mvulana mdogo mchungaji akaja; na mara tu alipowaita wakamfuata.”

2-3. (a) Wafuasi wa Yesu wanaonyeshaje kwamba wanaisikiliza sauti yake? (b) Tutachunguza nini katika makala hii na ile inayofuata?

2 Jambo ambalo mtalii huyo alijionea linatukumbusha maneno ambayo Yesu alisema kuhusu kondoo wake, yaani, wanafunzi wake. Alisema hivi: “Wataisikiliza sauti yangu.” (Yoh. 10:16) Lakini Yesu yuko mbinguni. Tunawezaje kumsikiliza? Njia kuu tunayoonyesha kwamba tunasikiliza sauti ya Bwana wetu, ni kwa kutumia mafundisho yake maishani.​—Mt. 7:24, 25.

3 Katika makala hii na ile inayofuata, tutachunguza baadhi ya mafundisho ya Yesu. Kama tutakavyoona, Yesu alitufundisha kwamba tunapaswa kuacha kufanya mambo fulani na kuna mambo ambayo tunapaswa kufanya. Tutachunguza kwanza mambo mawili hususa ambayo mchungaji mwema anatuagiza tuache kufanya.

“ACHENI KUHANGAIKA KWA WASIWASI”

4. Kulingana na Luka 12:29, ni nini kinachoweza kutufanya ‘tuhangaike kwa wasiwasi’?

4 Soma Luka 12:29. Yesu aliwahimiza wafuasi wake ‘waache kuhangaika kwa wasiwasi’ kuhusu mahitaji yao ya kimwili. Tunajua kwamba sikuzote shauri la Yesu ni lenye hekima na linafaa. Tungependa kulitumia, lakini nyakati nyingine huenda ikawa vigumu kufanya hivyo. Kwa nini?

5. Kwa nini huenda baadhi ya watu wakawa na mahangaiko kwa sababu ya mahitaji yao ya kimwili?

 5 Huenda wengine wakawa na mahangaiko kuhusu mahitaji yao ya kimwili, yaani, chakula, mavazi, na makao. Huenda wanaishi katika nchi iliyo maskini kiuchumi. Huenda ikawa vigumu kwao kupata pesa za kutosha ili kuitunza familia yao. Au huenda mtu anayeiandalia riziki familia amekufa, na kuiacha familia bila pesa za kupata mahitaji. Huenda janga la COVID-19 limesababisha watu wapoteze kazi na kipato. (Mhu. 9:11) Ikiwa tumepatwa na mojawapo ya hali au changamoto hizo tunaweza kufuataje mwongozo wa Yesu wa kuacha kuhangaika?

Badala ya kuzamishwa na mahangaiko kuhusu vitu vya kimwili, imarisha uhakika wako katika Yehova (Tazama fungu la 6 hadi 8) *

6. Fafanua jambo lililompata mtume Petro pindi fulani.

6 Pindi moja, mtume Petro na mitume wengine walikuwa kwenye mashua katika Bahari ya Galilaya wakati wa dhoruba walipomwona Yesu akitembea juu ya maji. Petro alisema hivi: “Bwana, ikiwa ni wewe, niamuru nije kwako nikitembea juu ya maji.” Yesu alipomwambia “njoo,” Petro alitoka kwenye mashua “akatembea juu ya maji kumwelekea Yesu.” Ona kilichotokea baada ya hapo. “Alipoitazama ile dhoruba ya upepo akaogopa. Alipoanza kuzama, akapaza sauti: ‘Bwana, niokoe!’” Yesu alinyoosha mkono wake na kumwokoa. Kumbuka kwamba Petro angefaulu kutembea juu ya maji ikiwa tu angeendelea kumtazama Yesu. Lakini Petro alipoitazama ile dhoruba, alilemewa na woga na shaka, naye akaanza kuzama.​—Mt. 14:24-31.

7. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Petro?

7 Tunaweza kujifunza kutokana na mfano wa Petro. Petro alipotoka kwenye mashua na kukanyaga bahari, hakutarajia kwamba angekengeushwa na kuanza kuzama. Alitaka kuendelea kutembea juu ya maji hadi atakapomfikia Bwana wake. Hata hivyo, alishindwa kuendelea kukazia fikira lengo hilo. Ni kweli kwamba sisi hatutembei juu ya maji, lakini tunakabili majaribu ya imani. Tukiacha kumkazia fikira Yehova na ahadi zake, tutaanza kuzama kiroho. Hata tukabili dhoruba gani ya mfano maishani, tunapaswa kuendelea kumkazia fikira Yehova na uwezo wake wa kutusaidia. Tunaweza kufanyaje hivyo?

8. Ni nini kinachoweza kutusaidia tusihangaike kupita kiasi kuhusu mahitaji yetu ya kimwili?

8 Badala ya kuhangaishwa na matatizo yetu, tunapaswa kumtumaini Yehova. Kumbuka kwamba Yehova, Baba yetu mwenye upendo, anaahidi kuwa atatuandalia mahitaji ya kimwili ikiwa tutatanguliza mambo ya kiroho. (Mt. 6:32, 33) Sikuzote ametimiza ahadi hiyo. (Kum. 8:4, 15, 16; Zab. 37:25) Ikiwa Yehova anawaandalia ndege na maua, kwa hakika hatupaswi kuwa na mahangaiko kuhusu chakula au mavazi! (Mt. 6:26-30; Flp. 4:6, 7) Kama vile upendo unavyowachochea wazazi wanaojali kuwaandalia watoto wao mahitaji ya kimwili, upendo unamchochea Baba yetu wa mbinguni kuwaandalia mahitaji ya kimwili watu wake. Naam, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatutunza!

9. Tunaweza kujifunza nini kutokana na kisa cha wenzi fulani wa ndoa?

9 Fikiria mfano unaoonyesha jinsi Yehova anavyoweza kutuandalia mahitaji ya kimwili. Wenzi fulani wa ndoa ambao ni watumishi wa wakati wote, waliendesha gari lao lililozeeka kwa mwendo wa saa moja ili kuwachukua akina dada waliokuwa wakiishi kwenye kambi ya wakimbizi na kuwapeleka kwenye mkutano. Ndugu alieleza hivi: “Baada ya mkutano tuliwaalika dada hao kwa ajili ya mlo, lakini tuligundua kwamba hatukuwa na kitu chochote cha kuwaandalia.” Wenzi hao wangefanya nini? Ndugu aliendelea kusema hivi: “Tulipofika nyumbani tulikuta mifuko miwili mikubwa iliyojaa chakula mbele ya mlango wetu. Hatukujua ni nani aliyekuwa ameiweka hapo. Yehova alitutunza.” Baada ya muda kupita, gari la wenzi hao liliharibika. Walilihitaji kwa ajili ya utumishi wao; hata hivyo, hawakuwa na pesa za kulirekebisha. Fundi wa magari alipokuwa akilikagua gari hilo kwenye karakana, mwanamume fulani alikuja na kuuliza: “Gari hili ni la nani?” Ndugu huyo alisema ni lake na linahitaji kurekebishwa. Mwanamume huyo akajibu: “Usijali. Mke wangu anahitaji aina hii ya gari lenye rangi kama hii. Utaliuza kwa bei gani?” Ndugu huyo aliliuza gari hilo na akapata pesa za kutosha kununua gari lingine. Ndugu huyo anamalizia kwa kusema hivi: “Siwezi kuelezea jinsi tulivyofurahi sana siku hiyo. Tulijua kwamba jambo hilo halikujitokeza lenyewe. Ni mkono wa Yehova.”

10. Andiko la Zaburi 37:5 linatutiaje moyo tuache kuwa na mahangaiko kuhusu mahitaji yetu ya kimwili?

10 Tunaposikiliza sauti ya mchungaji mwema na kuacha kuhangaika isivyo lazima kuhusu mahitaji ya kimwili, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatuandalia mahitaji yetu. (Soma Zaburi 37:5; 1 Pet. 5:7) Fikiria hali zilizotajwa katika  fungu la 5. Huenda kufikia sasa, Yehova amemtumia kichwa cha familia au mwajiri kutusaidia kupata mahitaji yetu ya kila siku. Ikiwa kichwa cha familia hawezi tena kutuandalia au tukipoteza kazi, Yehova atatutunza kwa njia nyingine. Tuna uhakika kabisa kwamba atatuandalia mahitaji yetu. Acheni sasa tuchunguze jambo lingine ambalo mchungaji mwema anatuhimiza tuache kufanya.

“ACHENI KUHUKUMU”

Tunaweza kuacha kuwahukumu wengine ikiwa tutakazia fikira sifa zao nzuri (Tazama fungu la 11, 14 hadi 16) *

11. Kulingana na Mathayo 7:1, 2, Yesu alisema tuache kufanya nini, na kwa nini hilo linaweza kuwa changamoto?

11 Soma Mathayo 7:1, 2. Yesu alijua kwamba wale waliokuwa wanamsikiliza hawakuwa wakamilifu na walikuwa na mwelekeo wa kuwachambua wengine. Ona kwamba alisema: “Acheni kuhukumu.” Huenda tukajitahidi sana kutowahukumu waabudu wenzetu. Hata hivyo, sisi sote si wakamilifu. Ikiwa nyakati nyingine tunajikuta tukiwachambua wengine, tunapaswa kufanya nini? Msikilize Yesu, na ujitahidi kuacha kuhukumu.

12-13. Kutafakari maoni ya Yehova kumwelekea Mfalme Daudi kunaweza kutusaidiaje tuache kuwahukumu wengine?

12 Tunaweza kunufaika kutokana na mfano wa Yehova. Yeye hukazia fikira sifa nzuri za watu. Tunaona jambo hilo kupitia jinsi alivyoshughulika na Mfalme Daudi, mwanamume aliyefanya makosa mazito. Kwa mfano, alifanya uzinzi na Bath-sheba, na hata akapanga mume wake auawe. (2 Sam. 11:2-4, 14, 15, 24) Matokeo ni kwamba Daudi alijiumiza yeye mwenyewe na pia familia yake, kutia ndani wake zake. (2 Sam. 12:10, 11) Pindi nyingine, Daudi hakumtumaini kikamili Yehova, alipoagiza jeshi la Israeli lihesabiwe kinyume na maagizo ya Yehova. Huenda alichochewa na kiburi na alitumaini ukubwa wa jeshi lake. Matokeo yalikuwa nini? Waisraeli 70,000 hivi walikufa kutokana na ugonjwa hatari!​—2 Sam. 24:1-4, 10-15.

13 Ikiwa ungekuwa unaishi Israeli wakati huo, ungemwonaje Daudi? Je, ungemhukumu kwamba hastahili rehema ya Yehova? Yehova hakufanya hivyo. Alikazia fikira maisha ya uaminifu ya Daudi na toba yake ya kutoka moyoni. Matokeo ni kwamba, Yehova alimsamehe Daudi dhambi hizo nzito. Yehova alijua kwamba Daudi alimpenda sana na alitaka kufanya yaliyo sawa. Tunashukuru kwamba Mungu wetu anakazia fikira sifa zetu nzuri.​—1 Fal. 9:4; 1 Nya. 29:10, 17.

14. Ni mtazamo gani ambao umewasaidia Wakristo waache kuwahukumu wengine?

14 Yehova anatambua kwamba sisi si wakamilifu, hivyo sisi pia tunapaswa kukazia fikira sifa nzuri za wengine. Kwa kawaida, ni rahisi kuona kasoro za wengine na kuanza kuwachambua. Hata hivyo, Mkristo mkomavu anaona kasoro hizo, lakini anawatendea wengine kwa njia nzuri. Huenda jiwe la almasi likawa na mikwaruzo, lakini mtu mwenye utambuzi haangalii tu mwonekano wa nje, bali anaona thamani yake litakapokuwa limekatwa na kung’arishwa. Kama Yehova na Yesu, hatuangalii kasoro za wengine, bali tunakazia fikira sifa nzuri za watu.

15. Kufikiria hali za watu kunaweza kutusaidiaje tuepuke kuwahukumu vikali?

15 Zaidi ya kukazia fikira sifa nzuri za wengine, ni nini kinachoweza kutusaidia tuepuke kuwahukumu vikali wengine? Jaribu kuwazia hali yao ya maisha. Fikiria mfano huu. Siku moja hekaluni, Yesu alimwona mjane maskini akitumbukiza sarafu mbili zenye thamani ndogo kwenye sanduku la hazina. Hakuuliza: “Kwa nini hakutumbukiza mchango mkubwa zaidi?” Badala ya kukazia fikira kiasi ambacho mjane huyo alitoa, Yesu alifikiria nia na hali ya mwanamke huyo na alimsifu kwa kufanya yote aliyoweza.​—Luka 21:1-4.

16. Unaweza kujifunza nini kutoka kwa Veronica?

16 Jambo ambalo dada anayeitwa Veronica alijionea, linaonyesha umuhimu wa kufikiria hali za wengine. Katika kutaniko lao kulikuwa na dada asiye na mwenzi wa ndoa na mwana wake. Veronica anasema hivi: “Nilihisi kwamba hawakuhudhuria mikutano na kushiriki huduma kwa ukawaida. Hivyo, nilikuwa na maoni yasiyofaa kuwaelekea. Lakini siku moja nilihubiri pamoja na dada huyo. Alinielezea kwamba alikabili hali ngumu kwa sababu mwanaye alikuwa na tatizo la akili. Alikuwa akijitahidi kadiri alivyoweza ili kuiandalia familia yake mahitaji ya kimwili na ya kiroho. Nyakati nyingine, kwa sababu ya ugonjwa wa mwana wake, alilazimika kuhudhuria mikutano katika kutaniko lingine.” Veronica anamalizia kwa kusema hivi: “Sikuwahi kutambua kwamba alikuwa akikabili hali ngumu sana. Sasa ninampenda na kumheshimu sana dada huyo kwa sababu ya jitihada zake zote za kumtumikia Yehova.”

17. Andiko la Yakobo 2:8 linatuamuru tufanye nini, na tunaweza kufanyaje hivyo?

17 Tunapaswa kufanya nini tukitambua kwamba tumemhukumu mwamini mwenzetu? Ni lazima tukumbuke kuwa tunapaswa kuwapenda ndugu zetu. (Soma Yakobo 2:8.) Pia, tunapaswa kusali kutoka moyoni kwa Yehova, tukimsihi atusaidie tuache kuhukumu. Tunaweza kutenda kupatana na sala zetu kwa kuchukua hatua ya kwanza kuzungumza na mtu ambaye tumekuwa tukimchambua. Kufanya hivyo kutatusaidia tumfahamu vizuri. Tunaweza kufanya mpango wa kuhubiri pamoja naye au kumkaribisha kwa ajili ya chakula. Kadiri tunavyomfahamu vizuri zaidi ndugu yetu, ndivyo tutakavyojitahidi kufuata mfano wa Yehova na Yesu wa kukazia fikira sifa zake nzuri. Kwa kufanya hivyo, tunaonyesha kwamba tunasikiliza amri ya mchungaji mwema ya kuacha kuhukumu wengine.

18. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunasikiliza sauti ya mchungaji mwema?

18 Kama tu kondoo halisi wanavyosikiliza sauti ya mchungaji wao, wafuasi wa Yesu wanasikiliza sauti yake. Tukijitahidi kuacha kuwa na mahangaiko kuhusu mahitaji yetu ya kimwili na kuacha kuwahukumu wengine, Yehova na Yesu watabariki jitihada zetu. Iwe sisi ni sehemu ya “kundi dogo” au “kondoo wengine,” acheni tuendelee kusikiliza na kutii sauti ya mchungaji mwema. (Luka 12:32; Yoh. 10:11, 14, 16) Katika makala inayofuata, tutachunguza mambo mawili ambayo Yesu aliwaambia wafuasi wake wanapaswa kufanya.

WIMBO 101 Kufanya Kazi Pamoja kwa Umoja

^ fu. 5 Yesu aliposema kwamba kondoo wake wangesikiliza sauti yake, alimaanisha kwamba wanafunzi wake wangesikiliza mafundisho yake na kuyatumia katika maisha yao. Katika makala hii, tutachunguza mafundisho mawili muhimu ya Yesu, ambayo ni kuacha kuwa na mahangaiko kuhusu vitu vya kimwili na kuacha kuwahukumu wengine. Tutazungumzia jinsi tunavyoweza kutumia shauri lake.

^ fu. 51 MAELEZO YA PICHA: Ndugu amepoteza kazi, hana pesa za kuitunza familia, na analazimika kuhamia nyumba nyingine. Asipokuwa mwangalifu anaweza kuwa na mahangaiko mengi sana na kupunguza bidii yake katika utumishi wa Mungu.

^ fu. 53 MAELEZO YA PICHA: Ndugu anafika mkutanoni akiwa amechelewa. Lakini sifa zake nzuri zinaonekana kupitia kutoa ushahidi isivyo rasmi, kumsaidia Mkristo mwenye umri mkubwa, na kutunza Jumba la Ufalme.