Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, umesoma kwa makini matoleo ya Mnara wa Mlinzi ya mwaka huu? Ona ikiwa unaweza kujibu maswali yafuatayo:

Andiko la Yakobo 5:11 linatoa uhakikisho gani linaposema Yehova “ni mwenye upendo mwororo sana” na “mwenye rehema”?

Tunajua kwamba Yehova ni mwenye rehema, na hivyo anatusamehe makosa yetu. Andiko la Yakobo 5:11 linatuhakikishia kwamba yuko tayari kutusaidia kwa upendo. Tunapaswa kumwiga.​—w21.01, uku. 21.

Kwa nini Yehova alianzisha mpango wa ukichwa?

Alianzisha mpango wa ukichwa kwa sababu ya upendo. Mpango huo unawezesha familia yake yenye ushikamanifu iwe na amani na utaratibu. Kila mshiriki wa familia anayefuata mpango huo anafahamu yule aliye na jukumu la kufanya uamuzi wa mwisho na kuhakikisha kwamba unatekelezwa.​—w21.02, uku. 3.

Kwa nini Wakristo wanapaswa kuwa waangalifu inapohusu kutumia programu za kielektroni za kutuma ujumbe mfupi?

Mtu akiamua kutumia programu hizo anapaswa kuchagua kwa makini watu ambao atashirikiana nao. Ni vigumu kufanya hivyo inapohusu vikundi vikubwa vya kutumiana ujumbe mfupi. (1 Tim. 5:13) Pia, kuna hatari ya kueneza habari ambazo hazijathibitishwa na kuutumia undugu wetu kwa makusudi ya kibiashara.​—w21.03, uku. 31.

Ni sababu gani zilizofanya Mungu amruhusu Yesu ateseke na kufa?

Kwanza, Yesu alipotundikwa kwenye mti wa mateso, ingewezekana kwa Wayahudi kuwekwa huru kutokana na laana. (Gal. 3:10, 13) Pili, Yehova alikuwa akimzoeza Yesu kwa ajili ya jukumu lake la baadaye akiwa Kuhani Mkuu. Na tatu, ushikamanifu wa Yesu hadi kifo ulithibitisha kwamba wanadamu wanaweza kuwa waaminifu licha ya kujaribiwa vikali. (Ayu. 1:9-11)​—w21.04, uku. 16-17.

Unaweza kufanya nini ikiwa watu hawapatikani katika huduma?

Jitahidi kuwatafuta wakati ambao kuna uwezekano mkubwa wa kuwapata nyumbani. Jaribu kuhubiri kwenye eneo tofauti. Na unaweza kujaribu kutumia mbinu tofauti, kama vile kuandika barua.​—w21.05, uku. 15-16.

Mtume Paulo alimaanisha nini aliposema: “Kupitia sheria nilikufa kuielekea sheria”? (Gal. 2:19)

Sheria ya Musa iliweka wazi kwamba wanadamu si wakamilifu na iliwaongoza Waisraeli kwa Kristo. (Gal. 3:19, 24) Hivyo, Paulo alimkubali Kristo. Kwa kufanya hivyo, Paulo ‘alikufa kuielekea sheria’; hakuwa tena chini ya Sheria.​—w21.06, uku. 31.

Yehova ametuwekeaje kielelezo cha kuonyesha uvumilivu?

Yehova amevumilia kuchafuliwa kwa jina lake, kupingwa kwa enzi yake kuu, kuasi kwa baadhi ya watoto wake, uwongo wenye kuendelea wa Shetani, kuteseka kwa watumishi wake, kutenganishwa na marafiki wake waliokufa, wanadamu waovu wanaowakandamiza wanadamu wenzao, na kuharibiwa kwa uumbaji wake.—w21.07, uku. 9-12.

Yosefu alituwekea mfano gani bora wa kuwa na subira?

Alivumilia kutendewa isivyo haki na ndugu zake. Na baadaye akashtakiwa kwa uwongo na kufungwa gerezani huko Misri kwa miaka mingi.​—w21.08, uku. 12.

Andiko la Hagai 2:6-9, 20-22 linatabiri kuhusu mtikisiko gani wa mfano?

Mataifa hayakubali ujumbe wa Ufalme unaohubiriwa, lakini watu wengi wamevutwa kwenye kweli. Hivi karibuni mataifa yatatikiswa mara ya mwisho yatakapoharibiwa.​—w21.09, uku. 15-19.

Kwa nini hatupaswi kufa moyo kuhusu huduma yetu?

Yehova anaona jitihada zetu, na anafurahi. Ikiwa hatutakufa moyo au kuacha, tutapata uzima wa milele.​—w21.10, uku. 25-26.

Andiko la Mambo ya Walawi sura ya 19 linaweza kutusaidiaje kufuata shauri hili: “Iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote”? (1 Pet. 1:15)

Inawezekana kwamba mstari huo umenukuliwa kutoka kwenye Mambo ya Walawi 19:2. Sura ya 19 ina mifano mingi ya jinsi tunavyoweza kutumia andiko la 1 Petro 1:15 katika maisha yetu ya kila siku.​—w21.12, uku. 3-4.