Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 2

Ujifunze Kupitia Ndugu Moja Mudogo wa Yesu

Ujifunze Kupitia Ndugu Moja Mudogo wa Yesu

“Yakobo, mutumwa wa Mungu na wa Bwana Yesu Kristo.”​—YAK. 1:1.

WIMBO 88 Unijulishe Njia Zako

KIFUPI YA HABARI *

1. Familia ya Yakobo ilikuwa ya namna gani?

YAKOBO, ndugu ya Yesu, alikomalishwa mu familia yenye ilikuwa nguvu kiroho. * Wazazi wake, Yosefu na Maria, walimupenda Yehova sana na walifanya yao yote ili kumutumikia. Yakobo alikuwa na baraka ingine. Ndugu yake mukubwa alifikia kuwa Masiya. Yakobo alikuwa na pendeleo ya muzuri kabisa ya kuwa mu ile familia!

Wakati alikuwa anakomala pamoja na ndugu yake mukubwa Yesu, Yakobo alifikia kumujua muzuri sana (Ona fungu ya 2)

2. Ni sababu gani zilipaswa kufanya Yakobo amuheshimie sana ndugu yake mukubwa?

2 Yakobo alikuwa na sababu mingi ya kumuheshimia ndugu yake mukubwa. (Mt. 13:55) Kwa mufano, Yesu alijua Maandiko muzuri sana, na siku moja, wakati alikuwa na miaka 12, alishangazaka sana wazee wenye kusoma sana, kule Yerusalemu. (Lu. 2:46, 47) Inawezekana Yakobo alitumika pamoja na Yesu mu kazi ya useremala. Kama ni vile, angemujua muzuri sana ndugu yake. Nathan Knorr alikuwa anazoea kusema hivi: “Unajuaka mutu muzuri wakati uko unatumika naye.” * Na inawezekana Yakobo aliona kama ‘Yesu aliendelea kuwa na hekima zaidi na kukomaa kimwili na kuendelea kukubaliwa na Mungu na wanadamu.’ (Lu. 2:52) Kwa hiyo, tunaweza kusema kama Yakobo alipaswa kuwa kati ya watu wa kwanza wenye walifikia kuwa wanafunzi wa Yesu. Lakini, haiko njo vile mambo ilikuwa.

3. Yakobo alitenda namna gani wakati Yesu alikuwa angali hapa ku dunia?

3 Wakati Yesu alikuwa hapa ku dunia, Yakobo hakufikiaka kuwa mwanafunzi wake. (Yoh. 7:3-5) Inawezekana Yakobo alikuwa kati ya watu wa jamaa ya Yesu wenye waliwaza kama Yesu alikuwa “amepoteza akili.” (Mk. 3:21) Na hakuna ushuhuda wowote wenye unaonyesha kama Yakobo alikuwaka pamoja na mama yake Maria wakati Yesu aliuawa ku muti wa mateso.​—Yoh. 19:25-27.

4. Ni somo gani tutazungumuzia?

4 Kisha wakati fulani, Yakobo alifikia kuonyesha imani katika Yesu na kuwa mushiriki mwenye kuheshimiwa sana mu kutaniko ya Kikristo. Mu hii habari, tutazungumuzia somo mbili zenye tunaweza kujifunza kupitia Yakobo: (1) juu ya nini tunapaswa kubakia wanyenyekevu na (2) namna gani tunaweza kuwa walimu wazuri.

UENDELEE KUWA MUNYENYEKEVU KAMA YAKOBO

Wakati Yesu alimutokea, Yakobo alikubali kwa unyenyekevu kama Yesu alikuwa Masiya na kisha pale Yakobo alifikia kuwa mwanafunzi muaminifu wa Kristo (Ona fungu ya 5-7)

5. Yakobo alitenda namna gani wakati Yesu alifufuliwa na kisha akamutokea?

5 Ni wakati gani Yakobo alifikia kuwa mufuasi muaminifu wa Yesu? Wakati Yesu alifufuliwa kutoka kwa wafu, “alimutokea Yakobo, na kisha mitume wote.” (1 Ko. 15:7) Kisha kuonana na Yesu, Yakobo akafikia kuwa mwanafunzi wake. Alikuwa pale wakati mitume walikuwa wanachunga roho takatifu yenye Yesu aliahidi kama wangepokea, wakati walikuwa mu chumba fulani ya juu kule Yerusalemu. (Mdo. 1:13, 14) Kisha, Yakobo alitumika kwa furaha kama mushiriki wa Baraza Yenye Kuongoza ya karne ya kwanza. (Mdo. 15:6, 13-22; Gal. 2:9) Na wakati fulani mbele ya 62 K.K.Y., aliongozwa na roho takatifu ya Yehova ili kuandikia Wakristo watiwa-mafuta barua. Ile barua iko ya maana sana kwetu hata leo, ikuwe tuko na tumaini ya kuenda kuishi mbinguni ao hapa ku dunia. (Yak. 1:1) Kulingana na mwanahistoria Josephus, mwenye aliishi mu karne ya kwanza, Yakobo aliuawa kwa amri ya Kuhani moja Mukubwa Muyahudi mwenye aliitwa Anania Kijana. Yakobo alibakia muaminifu kwa Yehova mupaka ku mwisho wa maisha yake hapa ku dunia.

6. Ni mu njia gani Yakobo alikuwa tofauti kabisa na viongozi wa dini wa wakati wake?

6Yakobo alikuwa munyenyekevu. Juu ya nini tunasema vile? Fikiria namna Yakobo alitenda tofauti na namna viongozi wengi wa dini walitenda. Wakati Yakobo aliona uhakikisho wa kweli wenye kuonyesha kama Yesu njo Mwana wa Mungu, alikubali kabisa ile jambo kwa unyenyekevu wote. Lakini wakubwa wa makuhani wenye walikuwa Yerusalemu hawakufanya vile. Kwa mufano, hawangeweza kubisha kama Yesu alimufufua Lazaro kutoka kwa wafu. Kuliko kukubali kama Yesu njo alikuwa mwakilishi wa Yehova, wao walijaribu kumuua Yesu na Lazaro. (Yoh. 11:53; 12:9-11) Wakati fulani kisha Yesu kufufuliwa kutoka kwa wafu, walikamata mupango fulani ili kujaribu kuficha watu ile jambo. (Mt. 28:11-15) Kiburi ya wale viongozi wa dini njo ilifanya wamukatale Masiya.

7. Juu ya nini tunapaswa kuepuka kiburi?

7Somo: Epuka kiburi, lakini ukuwe tayari kukubali kufundishwa na Yehova. Sawa vile ugonjwa unaweza kufanya ikuwe nguvu kwa moyo wa mutu fulani kutumika muzuri, kiburi nayo pia inaweza kufanya ikuwe nguvu kwetu kutii muongozo wa Yehova. Wafarisayo waliacha moyo wao ukuwe mugumu sana. Njo maana walikatala kabisa kutambua uhakikisho wenye kuwa wazi wenye kuonyesha kama Yesu alikuwa na roho ya Mungu na kama alikuwa Mwana wa Mungu. (Yoh. 12:37-40) Ile kiburi yao ilikuwa mubaya sana sababu iliwazuia kupata uzima wa milele. (Mt. 23:13, 33) Njo maana ni jambo ya lazima sana kuacha Neno ya Mungu na roho yake ifinyange utu wetu na ichochee namna yetu ya kuwaza na maamuzi yenye tunakamata! (Yak. 3:17) Juu Yakobo alikuwa munyenyekevu, alikuwa tayari kufundishwa na Yehova. Na sawa vile tutaona, ni juu alikuwa munyenyekevu njo maana alifikia kuwa mwalimu muzuri sana.

UKUWE MWALIMU MUZURI KAMA YAKOBO

8. Nini njo itatusaidia kuwa walimu wazuri?

8 Yakobo hakusoma masomo mingi ya ulimwengu yenye kuvutia. Viongozi wa dini wa wakati wake walimuona kama vile waliona mutume Petro na Yohana, ni kusema, kama “watu wenye hawana elimu na watu wa kawaida.” (Mdo. 4:13) Lakini Yakobo alijifunza kuwa mwalimu muzuri, kama vile inaonyeshwa wakati tunasoma kitabu yenye kuwa na jina yake. Kama Yakobo, tunaweza kuwa hatukusoma masomo mingi ya ulimwengu. Hata vile, kwa musaada wa roho ya Yehova na mazoezi mbalimbali yenye tengenezo yake inatutolea, siye pia tunaweza kuwa walimu wazuri. Tuzungumuzie basi mufano wenye Yakobo alituachia akiwa mwalimu na tuone somo fulani zenye tunaweza kujifunza.

9. Namna gani unaweza kufasiria njia ya Yakobo ya kufundisha?

9Yakobo hakutumia maneno ya nguvu ao mafasirio yenye haieleweke. Ile ilisaidia wasikilizaji wake wajue mambo yenye walipaswa kufanya na namna walipaswa kuifanya. Kwa mufano, mu njia ya mwepesi Yakobo alifundisha kama Wakristo wanapaswa kuwa tayari kuteseka bila kuweka kinyongo. Aliandika hivi: “Tunaona wale wenye wamevumilia kuwa wenye furaha. Mumesikia juu ya uvumilivu wa Yobu na mumeona matokeo yenye Yehova alileta, kwamba Yehova ni mwenye upendo mwingi sana na mwenye rehema.” (Yak. 5:11) Kumbuka kama mambo yenye Yakobo alikuwa anafundisha ndugu zake ilitegemea Maandiko. Alitumia Neno ya Mungu ili kusaidia wasikilizaji wake waone kama siku zote Yehova anabariki wale wenye kuwa washikamanifu kwake, kama Yobu. Yakobo alifundisha ile somo wakati alitumia maneno ya mwepesi na yenye kuwa wazi. Mu ile njia, hakupenda watu wamukazie yeye uangalifu, lakini wakazie Yehova uangalifu.

10. Ni mu njia gani moja yenye tunaweza kumuiga Yakobo wakati tuko nafundisha?

10Somo: Tumia habari ya mwepesi, na utumie Neno ya Mungu ili kufundisha. Wakati tuko nafundisha wengine, kusudi yetu haipaswe kuwa kuwaonyesha namna tunajua mambo mingi, lakini tunapaswa kuwaonyesha namna Yehova anajua mambo mingi na namna anawahangaikia. (Ro. 11:33) Tunaweza kufikia kufanya vile kwa kuacha kila mara mambo yenye tunasema itegemee Maandiko. Kwa mufano, kuliko kuambia wanafunzi wetu wa Biblia mambo yenye tungefanya ku fasi yao, tunapaswa kuwasaidia kufikiri kuhusu mifano ya Biblia na kuwasaidia waelewe mawazo ya Yehova na namna anajisikia. Kisha watatumikisha mambo yenye wanajifunza juu wanapenda kumufurahisha Yehova, hapana siye.

11. Ni magumu gani Wakristo fulani walikutana nayo mu wakati wa Yakobo, na ni shauri gani aliwapatia? (Yakobo 5:13-15)

11Yakobo aliona mambo vile ilikuwa. Mu barua yake, ni wazi kama Yakobo alijua magumu yenye waamini wenzake walikutana nayo, na aliwatolea muongozo juu ya namna ya kupambana nayo. Kwa mufano, Wakristo fulani hawakutumikisha ile shauri palepale. (Yak. 1:22) Wengine walipendelea matajiri. (Yak. 2:1-3) Tena, ilikuwa nguvu kwa wengine kuzuia kutumia mubaya ulimi wao. (Yak. 3:8-10) Wale Wakristo walikuwa na magumu ya nguvu sana, lakini Yakobo aliamini kama wangebadilika. Alitoa shauri yake mu njia ya muzuri lakini pia mu njia ya moja kwa moja, na alitia moyo wale wenye walikuwa na magumu kiroho watafute musaada ingine kwa wazee.​—Soma Yakobo 5:13-15.

12. Namna gani tunaweza kuendelea kuwa na maoni yenye kufaa wakati tuko tunasaidia wanafunzi wetu wa Biblia?

12Somo: Ona mambo vile iko, lakini pia uendelee kuwa na maoni yenye kufaa juu ya wengine. Inaweza kuwa nguvu kwa watu wengi wenye tunajifunzaka nao Biblia kutumikisha mashauri yenye kuwa ndani yake. (Yak. 4:1-4) Inaweza kuchukua wakati fulani juu waache tabia zao za mubaya na kuwa na sifa za Kikristo. Juu ya kuiga Yakobo, tunapaswa kuwa na uhodari wa kuambia wanafunzi wetu ni wapi wanapaswa kufanya mabadiliko. Tuko pia na lazima ya kuwa na maoni yenye kufaa, kutumainia kama Yehova atavuta watu wanyenyekevu kwake na atawapatia nguvu ya kufanya mabadiliko mu maisha yao.​—Yak. 4:10.

13. Kama vile inaonyeshwa mu andiko ya Yakobo 3:2 na maelezo ya chini, Yakobo alijua nini?

13Yakobo aliendelea kuwa na maoni ya muzuri juu yake mwenyewe. Yakobo hakuwaza kama alikuwa wa maana zaidi kuliko Wakristo wengine juu alikuwa ndugu ya Yesu ao juu ya mapendeleo ya utumishi yenye alikuwa nayo. Aliita Wakristo wengine kuwa “ndugu zangu wapendwa.” (Yak. 1:16, 19; 2:5) Hakuonyesha kama alikuwa mukamilifu. Lakini, alijitia pia ndani wakati alisema hii maneno yenye kufuata: “Sisi wote tunafanya makosa mara nyingi.”​—Soma Yakobo 3:2 na maelezo ya chini.

14. Juu ya nini tunapaswa kuwa tayari kukubali makosa yetu?

14Somo: Usisahau kama siye wote tuko watenda-zambi. Hatupaswe kuwaza kama tunapita wale wenye tunafundishaka. Juu ya nini tunasema vile? Kama tunafanya mwanafunzi wetu awaze kama hatufanyake makosa, anaweza kuwaza kama hawezi kutimiza kabisa mambo yenye Mungu anatuomba kufanya. Lakini, kama tunamuambia waziwazi kama haikuwake pia mwepesi kwetu kufuata kanuni za Maandiko na kama tunamufasiria namna Yehova alitusaidia kushinda magumu yetu, ile itasaidia mwanafunzi wetu aone kama yeye pia anaweza kumutumikia Yehova.

Mifano yenye Yakobo alitumia ilikuwa mwepesi, wazi, na yenye kufaa (Ona fungu ya 15-16) *

15. Yakobo alitumia mifano ya namna gani? (Yakobo 3:2-6, 10-12)

15Yakobo alitumia mifano yenye kugusa moyo. Bila shaka roho takatifu ilimusaidia, lakini inaonekana pia kama alijifunza mambo mingi kuhusu namna ya kufundisha kwa kuchunguza mifano yenye ndugu yake mukubwa Yesu alitumia. Mifano yenye Yakobo alitumia mu barua yake iko mwepesi na somo iko wazi.​—Soma Yakobo 3:2-6, 10-12.

16. Juu ya nini tunapaswa kutumia mifano yenye kufaa?

16Somo: Tumia mifano yenye kufaa. Wakati uko natumia mifano yenye kufaa, ile inasaidia wasikilizaji wako wasisikie tu mufano lakini pia wakuwe na wazo fulani mu akili yao juu ya mambo yenye unawafundisha. Ile mufano inasaidia wasikilizaji wako wakumbuke kweli za maana zenye kuwa mu Biblia. Yesu alikuwa fundi wa kutumia mifano yenye kufaa, na ndugu yake Yakobo alifuata mufano wake. Tuzungumuzie basi moja kati ya mifano ya Yakobo na tuone juu ya nini ni yenye kufaa sana.

17. Juu ya nini mufano wenye kuwa mu Yakobo 1:22-25 ni wenye kufaa sana?

17 Soma Yakobo 1:22-25. Mufano wa Yakobo wa kioo ni wenye kufaa juu ya sababu fulani. Alikuwa anafundisha kwa kutumia mufano fulani, ni kusema, jambo yenye inaweza kutusaidia kufaidika na Neno ya Mungu. Zaidi ya kusoma Biblia, tunapaswa pia kutumikisha mambo yenye tunasoma. Yakobo alichagula mufano wenye wasikilizaji wake wangeweza kuelewa haraka, ni kusema, mufano wa mutu mwenye kujiangalia kwenye kioo. Alipenda kufundisha somo gani? Inaweza kuwa ujinga kama mutu anajiangalia kwenye kioo na kuona kasoro fulani yenye anaweza kurekebisha, lakini hafanye jambo yoyote juu ya ile. Vilevile, inaweza kuwa ujinga kama tunasoma Neno ya Mungu na kuona jambo fulani yenye tunapaswa kufanyia mabadiliko kuhusu utu wetu, lakini hatufanye jambo yoyote juu ya ile.

18. Ni mambo gani tatu yenye tunapaswa kufanya wakati tuko tunatumia mufano?

18 Wakati uko unatumia mufano, unaweza kuiga mufano wa Yakobo kwa kufanya hii mambo tatu: (1) Hakikisha kama mufano wako ni wenye kufaa kupatana na mambo yenye uko unazungumuzia. (2) Tumia mufano wenye musikilizaji wako anaweza kuelewa kwa wepesi. (3) Fasiria waziwazi somo ya ile mufano. Kama ni nguvu kwako kufikiria mifano yenye kufaa, ona Index des publications des Témoins de Jéhovah. Chini ya kichwa “Exemples,” utapata mifano mingi yenye unaweza kutumia. Kumbuka kama mikro inasaidiaka kupandisha sauti. Mifano nayo iko sawa vile micro. Inasaidia somo fulani yenye uko unafundisha ikuwe wazi. Kwa hiyo, hakikisha kama unatumia mufano wenye kufasiria wazo kubwa yenye unapenda kufundisha. Kusema kweli, kwetu jambo ya maana zaidi yenye inaweza kutusaidia kukomalisha ufundi wetu wa kufundisha haiko kukaza uangalifu juu yetu siye wenyewe, lakini ni kusaidia watu wengi, kadiri inawezekana, wakuwe mu familia ya Yehova yenye furaha.

19. Tunaonyesha namna gani kama tunasamini familia yetu ya kiroho?

19 Yakobo alikuwa na pendeleo ya kuwa na ndugu mukubwa mwenye alikuwa mukamilifu; siye hatuna ile pendeleo. Lakini tuko na pendeleo ya kumutumikia Yehova pamoja na familia kubwa ya ndugu na dada Wakristo. Tunawaonyesha upendo kwa kushirikiana nao, kwa kujifunza mambo fulani kutoka kwao, na kwa kutumika kwa ushikamanifu tena bega kwa bega pamoja nao mu kazi ya kuhubiri na kufundisha. Wakati tunajikaza kuiga mufano wa Yakobo mu tabia yetu, mwenendo wetu, na mu namna yetu ya kufundisha, tunamuletea Yehova utukufu na tunasaidia watu wenye kuwa na mioyo mizuri wamukaribie Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo.

WIMBO 114 “Mukuwe na Uvumilivu”

^ fu. 5 Yakobo alikomalia mu nyumba moya na Yesu. Yakobo alimujua Mwana mukamilifu wa Mungu muzuri sana kuliko watu wenye waliishi ile wakati. Mu hii habari, tutachunguza mambo yenye tunaweza kujifunza kupitia maisha na mafundisho ya ndugu mudogo wa Yesu, mwenye alifikia kuwa nguzo katika kutaniko ya Kikristo ya karne ya kwanza.

^ fu. 1 Juu ya kufanya mambo ikuwe mwepesi, tutamuita Yakobo kuwa ndugu ya Yesu. Lakini kusema kweli, alikuwa ndugu nusu ya Yesu na ni wazi kama yeye njo mwenye aliandika barua yenye kuwa na jina yake.

^ fu. 2 Nathan Knorr alikuwaka mushiriki wa Baraza Yenye Kuongoza. Alimaliza safari yake hapa ku dunia mu 1977.

^ fu. 61 MAFASIRIO YA PICHA: Yakobo alitumia mufano wa moto kidogo, jambo yenye watu wangeweza kuelewa kwa wepesi, ili kuonyesha hatari ya kutumia ulimi mubaya.