MAKALA YA 8

Je, Shauri Unalotoa “Huufanya Moyo Ushangilie”?

Je, Shauri Unalotoa “Huufanya Moyo Ushangilie”?

“Mafuta na uvumba huufanya moyo ushangilie; ndivyo ulivyo urafiki mtamu unaochipuka kutokana na shauri la unyoofu.”​—MET. 27:9.

WIMBO 102 “Mwasaidie Walio Dhaifu”

MUHTASARI a

1-2. Ndugu mmoja alijifunza nini kuhusu kutoa shauri?

 MIAKA mingi iliyopita, wazee wawili wa kutaniko walimtembelea dada ambaye alikuwa hajahudhuria mikutano kwa muda mrefu. Mzee aliyekuwa anaongoza mazungumzo hayo alimsomea maandiko kadhaa yaliyohusu kuhudhuria mikutano. Alifikiri kwamba ziara yao ilikuwa imefanikiwa, lakini yeye na mwandamani wake walipokuwa wakiondoka, dada huyo alisema hivi: “Akina ndugu hamjui mambo ninayopitia.” Ndugu hao walikuwa wametoa shauri bila kumuuliza dada huyo kuhusu matatizo na hali alizokuwa akipitia. Matokeo ni kwamba dada huyo alihisi shauri lao halikumsaidia.

2 Anapokumbuka wakati huo, mzee aliyeongoza mazungumzo hayo, anasema hivi: “Wakati huo nilihisi kwamba dada huyo hakuwa na heshima. Lakini nilipoendelea kufikiria jambo hilo, nilikuja kutambua kwamba nilikuwa nimemsomea maandiko yote yanayofaa, badala ya kumuuliza maswali yanayofaa kama vile, ‘Unakabiliana na hali gani maishani?’ ‘Ninaweza kukusaidiaje?’” Mzee huyo alijifunza somo muhimu kutokana na kisa hicho. Leo, ndugu huyo ni mchungaji mwenye hisia-mwenzi na anayewasaidia wengine.

3. Ni nani kutanikoni wanaoweza kutoa shauri?

 3 Wakiwa wachungaji, wazee wana wajibu wa kutoa shauri linapohitajika. Hata hivyo, kuna nyakati ambazo huenda ndugu na dada wengine kutanikoni wakahitaji kutoa shauri. Kwa mfano, ndugu au dada huenda akampa rafiki yake ushauri unaotegemea Biblia. (Zab. 141:5; Met. 25:12) Au dada mwenye umri mkubwa huenda ‘akawashauri wanawake vijana’ kuhusu mambo yaliyotajwa kwenye Tito 2:3-5. Na bila shaka, mara nyingi wazazi wanahitaji kuwashauri na kuwarekebisha watoto wao. Hivyo, ingawa makala hii inawahusu hasa wazee wa kutaniko, sisi sote tunaweza kunufaika kwa kuchunguza njia ambazo tunaweza kutoa shauri linalomfaa na kumchochea yule anayelipokea na ‘litakalofanya moyo ushangilie.’​—Met. 27:9.

4. Tutazungumzia nini katika makala hii?

4 Katika makala hii, tutazungumzia maswali manne kuhusu jinsi ya kutoa shauri: (1) Tunapaswa kuwa na nia gani? (2) Je, kweli shauri linahitajika? (3) Ni nani anayepaswa kutoa shauri? (4) Unaweza kutoaje shauri kwa njia yenye matokeo?

TUNAPASWA KUWA NA NIA GANI?

5. Kuwa na mtazamo mzuri kunaweza kumsaidiaje mzee wa kutaniko kutoa shauri kwa njia nzuri? (1 Wakorintho 13:4, 7)

5 Wazee wa kutaniko wanawapenda ndugu na dada zao. Nyakati nyingine, wanaonyesha upendo huo kwa kumshauri mtu anayeelekea kuchukua hatua isiyofaa. (Gal 6:1) Hata hivyo, kabla ya kuzungumza na mtu huyo, mzee anapaswa kufikiria baadhi ya mambo ambayo mtume Paulo alitaja kuhusu upendo. “Upendo ni wenye subira na fadhili. . . . Huhimili mambo yote, huamini mambo yote, hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote.” (Soma 1 Wakorintho 13:4, 7.) Kutafakari mistari hiyo ya Biblia, kutamsaidia mzee kuchunguza nia yake ya kutoa shauri na kumfikia ndugu yake akiwa na mtazamo mzuri. Ikiwa yule anayepewa shauri atahisi kwamba mzee anamjali, inaelekea atakubali shauri hilo.​—Rom. 12:10.

6. Mtume Paulo aliweka mfano gani mzuri?

6 Mtume Paulo aliwawekea wazee wa kutaniko mfano mzuri. Kwa mfano, akina ndugu huko Thesalonike walipohitaji shauri, Paulo hakusita kutoa shauri hilo. Hata hivyo, katika barua alizowaandikia, kwanza aliwapongeza kwa kazi yao ya uaminifu, kazi yao ngumu ya upendo, na uvumilivu wao. Pia, alifikiria hali yao, kwa fadhili alitambua kwamba maisha yao hayakuwa rahisi na kwamba walikuwa wakivumilia mateso. (1 The. 1:3; 2 The. 1:4) Hata aliwaambia akina ndugu hao kwamba walikuwa mfano wa kuigwa na Wakristo wengine. (1 The. 1:8, 9) Ni lazima walifurahi sana Paulo alipowapongeza kutoka moyoni! Bila shaka, Paulo aliwapenda sana ndugu zake. Hiyo ndiyo sababu aliweza kutoa mashauri yenye manufaa katika barua zake mbili kwa Wathesalonike.​—1 The. 4:1, 3-5, 11; 2 The. 3:11, 12.

7. Kwa nini huenda mtu asikubali shauri?

7 Ni nini kinachoweza kutokea ikiwa tutatoa shauri kwa njia isiyofaa? Mzee fulani mwenye uzoefu, anasema hivi: “Baadhi ya wahubiri hawaitikii shauri kwa njia nzuri, si kwa sababu kuna jambo fulani baya katika ushauri huo, bali kwa sababu haukutolewa kwa njia yenye upendo.” Tunaweza kujifunza nini kutokana na hilo? Ni rahisi zaidi kukubali shauri ikiwa litatolewa kwa upendo, na si kwa hasira.

JE, KWELI SHAURI LINAHITAJIKA?

8. Mzee anapaswa kujiuliza maswali gani ikiwa anataka kumshauri mtu fulani?

8 Wazee hawapaswi kuwa wepesi katika kutoa shauri. Kabla ya kutoa shauri, mzee anapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, kweli ninahitaji kusema jambo fulani? Je, nina uhakika kwamba jambo ambalo mtu huyo anafanya si sahihi? Je, amevunja kanuni yoyote ya Biblia? Au je, ni kwa sababu tu nina maoni tofauti na yake?’ Kwa hekima wazee wanaepuka ‘kuongea bila kufikiri.’ (Met. 29:20) Kama mzee hana uhakika ikiwa anapaswa kumshauri mtu fulani, anaweza kuzungumza na mzee mwingine ili kuona kama mtu huyo amefanya jambo lililo kinyume na Maandiko na kwamba anahitaji shauri.​—2 Tim. 3:16, 17.

9. Tunajifunza nini kutoka kwa Paulo kuhusu jinsi ya kutoa shauri inapohusu mavazi na mapambo? (1 Timotheo 2:9, 10)

9 Fikiria mfano huu. Tuseme kwamba mzee wa kutaniko anahangaishwa na mavazi au mapambo ya mwamini mwenzake. Mzee huyo anaweza kujiuliza hivi, ‘Je, kuna sababu yoyote ya Kimaandiko ya kumweleza mtu huyo?’ Kwa sababu mzee hataki kutoa maoni yake binafsi, huenda akaomba maoni kutoka kwa mzee mwenzake au mhubiri mkomavu. Wakiwa pamoja wanaweza kupitia shauri la mtume Paulo kuhusu mavazi na mapambo. (Soma 1 Timotheo 2:9, 10.) Paulo alitaja kanuni fulani za ujumla, akisema kwamba mavazi ya Mkristo yanapaswa kuwa yanayofaa, ya kiasi, na yaliyochaguliwa kwa busara. Lakini Paulo hakuorodhesha aina ya mavazi yanayofaa na yasiyofaa. Paulo alitambua kwamba Wakristo wana haki ya kuchagua mavazi wanayopenda maadamu hayakiuki Maandiko. Hivyo, ili kutambua kama shauri linahitajika, wazee wanapaswa kuchunguza ikiwa mtu huyo anaonyesha busara na kiasi inapohusu mavazi yake.

10. Tunapaswa kukumbuka nini inapohusu mapendezi ya kibinafsi ya wengine?

10 Tunapaswa kutambua kwamba Wakristo wawili wakomavu wanaweza kufanya maamuzi mawili tofauti, lakini yote yakiwa yanakubalika. Hatupaswi kusisitiza kwamba waabudu wenzetu wafuate viwango vyetu kuhusu mambo yanayofaa na yasiyofaa.​—Rom. 14:10.

NI NANI ANAYEPASWA KUTOA SHAURI?

11-12. Ikiwa ni muhimu kutoa shauri, mzee anapaswa kujiuliza maswali gani, na kwa nini?

11 Ikiwa ni wazi kwamba shauri linapaswa kutolewa, basi swali ni, Ni nani anayepaswa kulitoa? Kabla ya kumshauri dada aliyeolewa au mtoto, mzee anapaswa kuzungumza na kichwa cha familia ambaye huenda akapendelea kushughulikia jambo hilo yeye mwenyewe. b Au huenda kichwa cha familia akaomba awepo mzee anapotoa shauri hilo. Na kama ilivyotajwa katika  fungu la 3, kuna wakati ambao huenda ikafaa zaidi dada mwenye umri mkubwa kumshauri dada mwenye umri mdogo.

12 Kuna jambo lingine la kufikiria. Huenda mzee akajiuliza hivi, ‘Je, mimi ndiye ninayefaa kutoa shauri hili, au shauri litapokelewa vizuri zaidi ikiwa mwingine atalitoa?’ Kwa mfano, mtu anayepambana na hisia za kujiona hafai huenda akaitikia vizuri zaidi shauri kutoka kwa mzee ambaye amewahi kukabiliana na changamoto hiyo, kuliko kutoka kwa mzee ambaye hajakabiliana nayo. Inaelekea mzee aliyepitia hali kama hiyo atakuwa na hisia-mwenzi zaidi, na yule anayeshauriwa atakubali kwa urahisi zaidi mambo atakayosema. Hata hivyo, wazee wote wa kutaniko wana wajibu wa kuwatia moyo na kuwachochea ndugu na dada zao kufanya marekebisho yoyote ya Kimaandiko. Hivyo, shauri linapohitajika jambo muhimu zaidi ni kwamba shauri hilo litolewe.

UNAWEZA KUTOAJE SHAURI KWA NJIA YENYE MATOKEO?

Kwa nini wazee Wakristo wanapaswa kuwa ‘wepesi wa kusikia’? (Tazama fungu la 13 na 14)

13-14. Kwa nini ni muhimu kwa mzee wa kutaniko kusikiliza?

13 Uwe tayari kusikiliza. Mzee anapojitayarisha kutoa shauri, anapaswa kujiuliza hivi: ‘Ninajua nini kuhusu hali za ndugu yangu? Anapitia hali gani maishani mwake? Je, anapitia changamoto ambazo sijui? Anahitaji nini hasa kutoka kwangu wakati huu?’

14 Bila shaka, kanuni iliyo kwenye Yakobo 1:19 inawahusu wale wanaotoa shauri. Yakobo aliandika hivi: “Kila mtu lazima awe mwepesi wa kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa hasira.” Huenda mzee akafikiri kwamba anajua habari zote zinazohusika, lakini je, ni kweli? Methali 18:13 inatukumbusha hivi: “Yeyote anayejibu kabla ya kusikia ukweli wa mambo, huo ni upumbavu na aibu kwake.” Ni jambo linalofaa zaidi kupata habari kutoka kwa mhusika mwenyewe. Hilo linahusisha kusikiliza kabla ya kusema. Kumbuka somo alilojifunza mzee aliyenukuliwa mwanzoni mwa makala hii. Alitambua kwamba badala ya kuanza ziara yake kwa kuzungumzia habari alizokuwa amejitayarisha, alipaswa kwanza kumuuliza dada huyo maswali kama vile: “Unakabiliana na hali gani maishani?” “Ninaweza kukusaidiaje?” Ikiwa wazee watatumia muda kupata habari zinazohusika, inaelekea watafaulu zaidi kuwasaidia na kuwatia moyo ndugu na dada zao.

15. Wazee wanaweza kutumiaje kanuni inayopatikana katika Methali 27:23?

15 Jitahidi kulifahamu kundi. Kama ilivyotajwa mwanzoni, kutoa shauri kwa njia yenye matokeo kunahusisha mengi zaidi ya kusoma tu maandiko machache, au kutoa pendekezo moja au mawili. Ndugu na dada zetu wanahitaji kuona kwamba tunawajali, kwamba tunawaelewa, na kwamba tunataka kuwasaidia. (Soma Methali 27:23.) Wazee wanapaswa kufanya yote wanayoweza ili kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na ndugu na dada zao.

Ni jambo gani litakalofanya iwe rahisi zaidi kwa wazee kutoa shauri? (Tazama fungu la 16)

16. Ni nini kitakachowasaidia wazee kutoa shauri kwa njia yenye matokeo?

16 Bila shaka, wazee wangependa kuepuka kuwafanya ndugu zao wahisi kwamba wanazungumza nao tu wanapotaka kushughulikia jambo fulani. Badala yake, wao huzungumza kwa ukawaida na ndugu na dada zao na kuonyesha wanawajali wanapopitia changamoto. Mzee mmoja mwenye uzoefu, anasema hivi: “Ukifanya hivyo, utajenga uhusiano mzuri na ndugu na dada zako. Kisha, utakapohitaji kutoa shauri itakuwa rahisi zaidi kufanya hivyo.” Na itakuwa rahisi zaidi kwa yule anayepewa shauri kulikubali.

Kwa nini wazee wanapaswa kuwa wenye subira na fadhili wanapotoa shauri? (Tazama fungu la 17)

17. Ni wakati gani hasa ambao mzee anahitaji kuwa mwenye subira na fadhili?

17 Uwe na subira na fadhili. Tunahitaji kuonyesha subira na fadhili hasa ikiwa mwanzoni mtu huyo alikataa shauri linalotegemea Biblia. Mzee anapaswa kuepuka mwelekeo wa kukasirika ikiwa shauri lake halikubaliwi au kufuatwa kwa haraka. Ilitabiriwa hivi kumhusu Yesu: “Hataponda tete lililovunjika, wala hatazima utambi unaofifia.” (Mt. 12:20) Hivyo, katika sala zake za kibinafsi, mzee anaweza kumwomba Yehova ambariki yule anayehitaji shauri na amsaidie kuelewa sababu ya shauri hilo na kulitumia. Ndugu anayeshauriwa huenda akahitaji muda wa kufikiria kuhusu mambo yaliyozungumziwa. Ikiwa mzee ni mwenye subira na fadhili, yule anayeshauriwa hatakengeushwa na jinsi shauri linavyotolewa, bali atakazia fikira ujumbe ulio katika shauri. Bila shaka, sikuzote shauri linapaswa kutegemea Neno la Mungu.

18. (a) Tunapaswa kukumbuka nini tunapotoa shauri? (b) Kama picha iliyo kwenye sanduku inavyoonyeshwa, wazazi wanazungumzia nini?

18 Jifunze kutokana na makosa yako mwenyewe. Maadamu sisi si wakamilifu, hatutafaulu kutumia mapendekezo ya makala hii kikamili. (Yak. 3:2) Tutakosea, lakini hilo linapotokea, tunapaswa kujitahidi kujifunza kutokana na makosa yetu. Ikiwa ndugu na dada zetu wanaona kwamba tunawapenda, itakuwa rahisi zaidi kwao kutusamehe kwa sababu ya jambo tulilosema au kufanya.—Tazama pia sanduku “ Kikumbusho kwa Wazazi.”

TUMEJIFUNZA NINI?

19. Tunaweza kufanyaje moyo wa ndugu na dada zetu ushangilie?

19 Kama ambavyo tumeona, si rahisi kutoa shauri kwa njia yenye matokeo. Sisi si wakamilifu, na pia wale tunaowashauri si wakamilifu. Kumbuka kanuni tulizozungumzia katika makala hii. Hakikisha kwamba shauri linatolewa kwa nia nzuri. Pia, hakikisha kwamba kwa kweli shauri linahitajika na kwamba wewe ndiye unayefaa kulitoa. Kabla ya kutoa shauri, uliza maswali na usikilize kwa makini ili uweze kuelewa mambo ambayo mtu huyo anapitia. Jaribu kuona mambo kulingana na maoni yake. Uwe mpole, na usitawishe urafiki wa karibu pamoja na ndugu na dada zako. Kumbuka kwamba lengo letu ni hili: Tunataka ushauri wetu uwe wenye matokeo na pia ‘kuufanya moyo ushangilie.’​—Met. 27:9.

WIMBO 103 Wachungaji​—Zawadi Katika Wanadamu

a Si rahisi sikuzote kutoa shauri. Tunapohitaji kutoa shauri, tunaweza kulitoaje kwa njia itakayomnufaisha na kumburudisha yule anayelipokea? Makala hii itawasaidia hasa wazee kutoa shauri kwa njia itakayowafanya wanaolipokea, walikubali na kulitumia.

b Tazama makala “Kuelewa Mpango wa Ukichwa Kutanikoni” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Februari 2021.