Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 9

Mwige Yesu kwa Kuwatumikia Wengine

Mwige Yesu kwa Kuwatumikia Wengine

“Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”​—MDO. 20:35.

WIMBO 17 “Nataka”

MUHTASARI *

1. Ni roho gani nzuri tunayoiona miongoni mwa watu wa Yehova?

 MIAKA mingi iliyopita, Neno la Mungu lilitabiri kwamba watu wa Mungu ‘wangejitoa kwa hiari’ katika utumishi wa Yehova, chini ya mwongozo wa Mwana wake. (Zab. 110:3) Kwa kweli, unabii huo umekuwa ukitimizwa leo. Kila mwaka, watumishi wa Yehova wenye bidii hutumia mamia ya mamilioni ya saa katika kazi ya kuhubiri. Wanafanya hivyo kwa hiari na kwa gharama zao wenyewe. Na pia wanatumia muda wao kuwategemeza waamini wenzao kimwili, kihisia, na kiroho. Akina ndugu waliowekwa rasmi, hutumia saa nyingi wakijitayarisha kuongoza mikutano ya kutaniko na kuwafanyia ziara za uchungaji waamini wenzao. Ni nini kinachowachochea kufanya kazi hizo zote? Ni upendo​—upendo kwa Yehova na upendo kwa jirani.​—Mt. 22:37-39.

2. Kama inavyoonyeshwa kwenye Waroma 15:1-3, Yesu aliweka mfano gani?

2 Yesu aliweka mfano mzuri sana kwa kutanguliza masilahi ya wengine maishani mwake. Tunajitahidi kadiri tunavyoweza kufuata hatua zake. (Soma Waroma 15:1-3.) Wale wote wanaomwiga watanufaika sana. Yesu alisema hivi: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”​—Mdo. 20:35.

3. Tutazungumzia nini katika makala hii?

3 Katika makala hii, tutazungumzia baadhi ya njia ambazo Yesu alijidhabihu ili kuwatumikia wengine na tutachunguza jinsi tunavyoweza kuiga mfano wake. Pia, tutazungumzia jinsi tunavyoweza kuongeza tamaa yetu ya kuwatumikia wengine.

IGA MFANO WA YESU

Ingawa alikuwa amechoka, Yesu alitendaje umati ulipomfuata? (Tazama fungu la 4)

4. Yesu alitangulizaje mahitaji ya wengine maishani?

4 Yesu alijitoa kuwasaidia wengine hata alipokuwa amechoka. Fikiria jinsi Yesu alivyotenda umati wa watu ulipomfuata mlimani, inaelekea karibu na Kapernaumu. Yesu alikuwa amesali usiku mzima. Ni lazima alikuwa amechoka sana, lakini alipoona umati, aliwasikitikia maskini na wagonjwa waliokuwa miongoni mwao. Yesu hakuwaponya tu, bali pia aliwatolea mojawapo ya hotuba yenye kuchochea zaidi, yaani, Mahubiri ya Mlimani.​—Luka 6:12-20.

Tunaweza kuiga jinsi gani roho ya Yesu ya kujidhabihu katika maisha yetu? (Tazama fungu la 5)

5. Vichwa vya familia wanaigaje roho ya Yesu ya kujidhabihu wanapokuwa wamechoka?

5 Jinsi vichwa vya familia wanavyomwiga Yesu. Wazia hali hii: Baada ya kuwa kazini siku nzima, kichwa cha familia anarudi nyumbani akiwa amechoka sana. Ingawa anashawishika kuahirisha Ibada ya Familia iliyopangwa jioni hiyo, anamsihi Yehova ampe nguvu za kuongoza ibada hiyo. Yehova anajibu sala yake, na wanafanya ibada kama kawaida. Watoto wanajifunza somo muhimu jioni hiyo, kwamba wazazi wao wanayaona mambo ya kiroho kuwa muhimu kuliko mambo mengine yote.

6. Toa mfano unaoonyesha jinsi Yesu alivyodhabihu muda wake wa kibinafsi ili kuwasaidia wengine.

6 Yesu alitumia muda wake wa kibinafsi pamoja na wengine hata alipohitaji kuwa peke yake. Je, unaweza kuwazia jinsi Yesu alivyohisi alipojua kwamba Yohana Mbatizaji, rafiki yake, ameuawa? Bila shaka, Yesu alihuzunika sana. Biblia inasema hivi: “Yesu aliposikia hilo [yaani kuhusu kifo cha Yohana] akaondoka hapo kwa mashua, akaenda mahali pasipo na watu ili awe pake yake.” (Mt. 14:10-13) Tunaweza kuelewa kwa nini alitaka kuwa peke yake. Wengi wetu tunapendelea kuomboleza faraghani. Lakini Yesu hakufaulu kufanya hivyo. Umati mkubwa ulifika katika eneo hilo lisilo na watu kabla yake. Yesu alitendaje? Alifikiria mahitaji ya umati huo, naye “akawasikitikia.” Alitambua kwamba walihitaji sana kuburudishwa kiroho, na papo hapo akaanza kuwasaidia. Isitoshe, “akaanza kuwafundisha [si mambo machache, bali] mambo mengi.”​—Marko 6:31-34; Luka 9:10, 11.

7-8. Toa mfano unaoonyesha jinsi wazee wenye upendo wanavyomwiga Yesu uhitaji unapotokea.

7 Jinsi wazee wa kutaniko wenye upendo wanavyomwiga Yesu. Tunathamini sana kazi ambayo wazee wetu wa kutaniko wenye kujidhabihu wanafanya kwa ajili yetu! Ndugu na dada wengi kutanikoni hawaoni kazi zote ambazo wazee hufanya. Kwa mfano, kunapokuwa na dharura ya kimatibabu, washiriki wa Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali hufika haraka hospitalini ili kuwasaidia waabudu wenzao. Mara nyingi hali hizo za dharura hutokea usiku wa manane! Lakini kwa sababu wanawahurumia ndugu na dada zao wanaoteseka, wazee hao wapendwa, pamoja na familia zao, wanatanguliza masilahi ya waamini wenzao badala ya mahitaji yao.

8 Wazee pia wanashiriki katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme na majengo mengine ya kitheokrasi, pia wanashiriki kutoa misaada wakati wa misiba. Tunaweza kusema mengi pia kuhusu saa nyingi ambazo wazee katika kutaniko letu wanatumia kutufundisha, kututia moyo, na kututegemeza. Ndugu hao wote na familia zao wanastahili kupongezwa kutoka moyoni. Yehova na abariki roho wanayoonyesha! Bila shaka kama watu wengine, wazee pia wanahitaji kuwa na usawaziko. Hawapaswi kutumia muda mwingi sana katika utendaji huo wa Kitheokrasi hivi kwamba wanashindwa kutimiza mahitaji ya familia zao.

JINSI YA KUSITAWISHA ROHO YA KUJIDHABIHU

9. Kulingana na Wafilipi 2:4, 5, Wakristo wote wanapaswa kusitawisha mtazamo gani wa akili?

9 Soma Wafilipi 2:4, 5. Ni kweli kwamba si wote ni wazee kutanikoni, hata hivyo, sote tunaweza kujifunza jinsi ya kuiga roho ya kujidhabihu ya Yesu. Biblia inasema kwamba ‘alichukua umbo la mtumwa.’ (Flp. 2:7) Fikiria tunachojifunza kutokana na maneno hayo. Mtumwa au mtumishi aliyependwa, angetafuta fursa za kumfurahisha bwana wake. Ukiwa mtumwa wa Yehova na mtumishi wa ndugu zako, bila shaka unatamani kutumiwa hata zaidi na Yehova na kuwatumikia waabudu wenzako. Unaweza kufanya hivyo kwa kufikiria mapendekezo yafuatayo.

10. Tunaweza kujiuliza maswali gani?

10 Changanua mtazamo wako. Jiulize maswali kama haya: ‘Niko tayari kujidhabihu kwa kadiri gani ili kuwasaidia wengine? Kwa mfano, mimi huitikiaje ninapoombwa kumtembelea ndugu mwenye umri mkubwa aliye katika nyumba ya kutunza waliozeeka au kumpeleka mikutanoni dada mwenye umri mkubwa? Je, niko tayari kujitolea bila kukawia kunapokuwa na uhitaji wa wajitoleaji ili kusafisha eneo la kusanyiko au kudumisha Jumba la Ufalme?’ Yehova anafurahi tunapotumia bila ubinafsi muda na mali zetu—vitu ambavyo tumeweka wakfu kwake​—ili kuwasaidia wengine. Ikiwa tunaona kwamba kuna mahali tunahitaji kuboresha, tunaweza kufanya nini?

11. Sala inaweza kutusaidiaje kusitawisha roho ya kujidhabihu?

11 Sali kwa Yehova kutoka moyoni. Tuseme unatambua kwamba unahitaji kufanya marekebisho fulani, lakini unakosa hamu ya kufanya mabadiliko yanayohitajika. Unapohisi hivyo, msihi Yehova kwa bidii katika sala. Uwe mnyoofu. Mweleze Yehova jinsi unavyohisi, na umwombe akupe “hamu na nguvu za kutenda.”​—Flp. 2:13.

12. Ndugu kijana aliyebatizwa, anaweza kutimiza uhitaji gani?

12 Ikiwa wewe ni ndugu kijana aliyebatizwa, mwombe Yehova akusaidie kusitawisha tamaa ya kutumikia kwa njia kubwa zaidi kutanikoni. Katika baadhi ya nchi, kuna wazee wengi kuliko watumishi wa huduma, na wengi kati ya watumishi hao wa huduma si vijana. Kadiri tengenezo linavyozidi kukua, tunahitaji vijana wengi zaidi ili kutusaidia kuwatunza watu wa Yehova. Ikiwa uko tayari kutumikia mahali popote unapohitajika, utakuwa na furaha. Kwa nini? Kwa sababu utamfurahisha Yehova, utajipatia sifa nzuri, na utaridhika kwa sababu ya kuwasaidia wengine.

Wakristo kutoka Yudea walivuka Mto Yordani na kukimbilia jiji la Pela. Wale waliofika mapema kwenye jiji hilo, wanawapatia chakula Wakristo wenzao ambao wamefika karibuni (Tazama fungu la 13)

13-14. Tunaweza kuchukua hatua gani hususa ili kuwasaidia ndugu na dada zetu? (Tazama picha kwenye jalada.)

13 Uwe macho kuona mahitaji ya wengine. Mtume Paulo aliwahimiza hivi Waebrania: “Msisahau kutenda mema na kushiriki vitu vyenu pamoja na wengine, kwa maana Mungu hupendezwa na dhabihu kama hizo.” (Ebr. 13:16) Huo ulikuwa ushauri mzuri sana! Muda mfupi baada ya kupokea barua hiyo, Wakristo huko Yudea, walilazimika kuacha nyumba zao, biashara zao, na watu wao wa ukoo ambao hawakuwa waamini, na wakaanza “kukimbilia milimani.” (Mt. 24:16) Bila shaka, wakati huo kulikuwa na uhitaji wa haraka wa kusaidiana. Ikiwa kabla ya hapo walikuwa wakitumia ushauri wa Paulo kuhusu kushiriki na wengine vitu walivyokuwa navyo, ingekuwa rahisi zaidi kwao kuzoea maisha yao mapya.

14 Huenda wakati mwingine ndugu na dada zetu wasituambie mahitaji yao. Kwa mfano, mfikirie ndugu anayeomboleza kwa sababu ya kufiwa na mke wake. Je, ndugu huyo anahitaji msaada wa kutayarisha chakula, usafiri, au kusaidiwa kufanya kazi za nyumbani? Huenda asiseme chochote kwa sababu hataki tuhisi kwamba anatusumbua. Lakini anaweza kuthamini sana ikiwa tutachukua hatua ya kwanza ili kumpa msaada anaohitaji. Hatupaswi kutarajia kwamba watu wengine watamsaidia au kwamba sikuzote atatueleza msaada anaohitaji. Jiulize hivi: ‘Ikiwa ningekuwa katika hali kama yake, ningehitaji msaada gani?’

15. Tunapaswa kuazimia kufanya nini tunapotaka kuwasaidia wengine?

15 Uwe mwenye kufikika. Bila shaka, unawajua ndugu na dada katika kutaniko lako ambao sikuzote wako tayari kuwasaidia wengine. Hawatufanyi kamwe tuhisi kwamba tunawasumbua. Tunajua kwamba tunaweza kuwategemea tunapokuwa na uhitaji, na tungependa kuwaiga. Anapofikiria kuhusu mfano wa Yesu, Alan mzee wa kutaniko mwenye umri wa miaka 45, anataka kuwa mwenye kufikika. Alan, anasema hivi: “Yesu alikuwa na shughuli nyingi, lakini watu wa kila umri walimpenda na walijihisi huru kumwomba msaada. Walimwona kuwa mwanamume aliyewajali sana. Ningependa kuiga mtazamo wa Yesu kwa moyo wote na kujulikana kuwa mtu anayefikika, mwenye urafiki, na anayejali.”

16. Kutumia shauri la Zaburi 119:59, 60 kutatusaidiaje kufuata mfano wa Yesu kwa ukaribu?

16 Hatupaswi kuvunjika moyo ikiwa hatutafaulu kumwiga Yesu kikamili. (Yak. 3:2) Mwanafunzi hawezi kumwiga kikamili mwalimu wake. Lakini anapoendelea kujifunza kutokana na makosa yake, na kujitahidi kuiga mfano wa mwalimu wake kwa ukaribu kadiri iwezekanavyo, ataendelea kuboresha ustadi wake. Vivyo hivyo, tukitenda kulingana na mambo ambayo tumejifunza katika funzo la Biblia la kibinafsi, na kujitahidi kabisa kurekebisha kasoro zozote tulizo nazo, tutafanikiwa kufuata kielelezo ambacho Yesu alituachia.—Soma Zaburi 119:59, 60.

MANUFAA YA KUWA NA ROHO YA KUJIDHABIHU

Wazee wa kutaniko wanapoiga mtazamo wa Yesu wa kujidhabihu wanawawekea vijana mfano mzuri (Tazama fungu la 17) *

17-18. Tutapata manufaa gani kwa kuiga roho ya Yesu ya kujidhabihu?

17 Tunaweza kuwachochea wengine waige roho yetu ya kujidhabihu. Mzee wa kutaniko anayeitwa Tim, anasema hivi: “Tuna ndugu vijana ambao wamefanya maendeleo na wamewekwa rasmi kuwa watumishi wa huduma—baadhi yao wakiwa na umri mdogo sana—hasa kwa sababu waliiga roho ya kuwa tayari kuwatumikia wengine ambayo waliiona kwa wengine. Jitihada zao zisizo na ubinafsi zinasaidia kutaniko letu na kuwaunga mkono wazee.”

18 Tunaishi katika ulimwengu uliojaa ubinafsi. Lakini watu wa Yehova wako tofauti kabisa. Tumechochewa na roho ya kujidhabihu ya Yesu, na tumeazimia kufuata mfano wake. Hatuwezi kufuata hatua zake kikamili, lakini tunaweza ‘kufuata hatua zake kwa ukaribu.’ (1 Pet. 2:21) Kadiri tunavyofanya yote tunayoweza ili kuiga roho ya kujidhabihu ya Yesu, ndivyo sisi pia tutakavyojionea shangwe ya kupata kibali cha Yehova.

WIMBO 13 Kristo, Kielelezo Chetu

^ Sikuzote Yesu alitanguliza mahitaji ya wengine badala ya mahitaji yake. Katika makala hii, tutachunguza njia ambazo tunaweza kuiga mfano wake. Pia, tutajifunza jinsi ambavyo kuiga mtazamo wa Yesu wa kujidhabihu kutatuletea manufaa ya kudumu.

^ MAELEZO YA PICHA: Ndugu kijana anayeitwa Dan, anawaona wazee wawili wakimtembelea baba yake hospitalini. Dan anatiwa moyo na jinsi wazee wanavyoonyesha upendo. Yeye pia anachochewa kuwa macho ili kuona mahitaji ya wengine kutanikoni. Ndugu mwingine anayeitwa Ben, anaona jinsi Dan anavyowajali wengine. Mfano wa Dan unamchochea Ben kufanya usafi katika Jumba la Ufalme.