Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Nilipata Kitu Bora Kuliko Udaktari

Nilipata Kitu Bora Kuliko Udaktari

“MMENIAMBIA jambo ambalo nimekuwa nikitazamia tangu utotoni!” Niliwaambia maneno hayo kwa uchangamfu wagonjwa wawili waliokuja kuniona mwaka wa 1971. Nilikuwa nimetoka tu kufungua kliniki yangu nikiwa daktari aliyetoka tu kuhitimu. Wagonjwa hao walikuwa akina nani, na nilikuwa na ndoto gani? Acheni niwasimulie jinsi mazungumzo hayo yalivyobadili mambo niliyotanguliza maishani na kwa nini ninaamini kwamba ndoto yangu ya utotoni itatimia hivi karibuni.

Nilizaliwa mwaka wa 1941, katika familia isiyo tajiri huko Paris, Ufaransa. Nilipenda kusoma lakini nilipokuwa na umri wa miaka kumi, nilipatwa na ugonjwa wa kifua kikuu na hivyo nikaacha kwenda shule! Madaktari walinishauri nipumzike kitandani ili nisiyachoshe mapafu yangu. Hivyo, kwa miezi kadhaa, nilitumia muda wangu kusoma kamusi na kusikiliza vipindi vya Redio Sorbonne vilivyotayarishwa na chuo kikuu cha Paris. Mwishowe, daktari wangu aliposema nilikuwa nimepona na ningeweza kurudi shuleni, nilifurahia sana. Nilijiambia, ‘Madaktari wanafanya kazi nzuri sana!’ Tangu wakati huo na kuendelea, nilitamani kuwatibu watu magonjwa yao. Kila wakati baba yangu aliponiuliza ningependa kufanya kazi gani maishani, sikuzote nilitoa jibu lilelile, “Ninataka kuwa daktari.” Hivyo ndivyo nilivyokuja kuupenda sana udaktari.

SAYANSI ILINISAIDIA KUMKARIBIA ZAIDI MUNGU

Familia yetu ilikuwa ya Wakatoliki. Lakini nilikuwa sijui mambo mengi kumhusu Mungu, na nilikuwa na maswali mengi ambayo hayakujibiwa. Ni baada tu ya kuanza kusomea udaktari katika chuo kikuu ndipo niliposadiki kwamba uhai uliumbwa.

Ninakumbuka mara ya kwanza nilipochunguza chembe au seli za ua la tulip chini ya darubini, nilivutiwa na jinsi chembe hizo zinavyojilinda zenyewe dhidi ya joto na baridi. Pia, nilichunguza jinsi cytoplasm (umajimaji ulio ndani ya chembe au seli) inavyosinyaa inapowekwa kwenye chumvi au kutanuka inapowekwa kwenye maji safi. Kwa sababu ya uwezo huo na mwingine mwingi, viumbe vinaweza kuzoea hali mpya mazingira yanapobadilika. Nilipochunguza utata wa kila seli, ningeweza kuona kwamba uhai haukujitokeza wenyewe tu.

Katika mwaka wangu wa pili wa masomo ya udaktari, niliona uthibitisho mwingine kwamba kuna Mungu. Katika masomo ya anatomia, tulichunguza jinsi mkono unavyotuwezesha kukunja na kunyoosha vidole vyetu. Mpangilio wa misuli, ligamenti, na kano umebuniwa kwa hali ya juu sana. Kwa mfano, nilijifunza kwamba kano zinazounganisha mojawapo ya misuli ya mkono kwenye mfupa wa pili wa kidole inagawanywa mara mbili, na kutokeza madaraja ambayo chini yake kano zinazoenda kwenye sehemu ya mbele ya kidole hupita na kushikiliwa kwenye sehemu yake. Tishu zenye nguvu pia zinashikilia kano karibu na mifupa ya kidole. Bila ufundi huo, kano zilizo kwenye mikono yetu zingekuwa kama kamba iliyokazwa ya upinde wa mshale. Niliweza kuona wazi kabisa kwamba kuna mtu mwenye akili sana aliyebuni mwili wa binadamu.

Nilivutiwa hata zaidi kuhusu kazi ya Muumba, nilipojifunza jinsi mtoto anavyoanza kupumua baada ya kuzaliwa. Nilijifunza kwamba mtoto anapokuwa tumboni anapokea oksijeni kutoka kwa mama kupitia kiunga-mwana au kitovu. Hivyo, alveoli, yaani, mifuko midogo ya hewa kwenye mapafu, inakuwa bado haijawa na hewa. Wakati wa kuzaliwa unapokaribia, umajimaji unaoitwa surfactant hulainisha upande wa ndani wa alveoli. Kisha, baada ya mtoto kuzaliwa matukio ya pekee sana huambatana na pumzi ya kwanza ambayo mtoto aliyetoka kuzaliwa anavuta. Shimo lililo kwenye moyo wa mtoto linajifunga na kuelekeza damu kwenye mapafu. Katika pindi hiyo muhimu, surfactant inazuia alveoli kushikamana hewa inapoingia haraka. Papo hapo mtoto anakuwa na uwezo wa kupumua mwenyewe.

Nilitaka kumjua yule aliyeumba maajabu hayo, hivyo nikaanza kusoma Biblia kwa bidii. Nilivutiwa sana na sheria za usafi zilizokuwa zimetiwa ndani katika agano ambalo Mungu alifanya pamoja na taifa la Israeli zaidi ya miaka elfu tatu iliyopita. Mungu aliwaamuru Waisraeli kufukia kinyesi chao, kuoga kwa ukawaida, na kumtenga mtu yeyote aliyeonyesha dalili za ugonjwa hatari. (Law. 13:50; 15:11; Kum. 23:13) Biblia inazungumzia jinsi magonjwa yanavyoenezwa jambo ambalo wanasayansi wameligundua katika karne za hivi karibuni. Pia, nilitambua kwamba sheria zilizohusu ngono katika kitabu cha Mambo ya Walawi zilisaidia kudumisha usafi wa taifa hilo kwa ujumla. (Law. 12:1-6; 15:16-24) Nilifikia mkataa kwamba Muumba aliwapa sheria hizo Waisraeli kwa manufaa yao wenyewe na kwamba aliwabariki wale waliotii amri zake. Nilikuja kusadiki kwamba Biblia imeongozwa na roho ya Mungu, Mungu ambaye sikulijua jina lake wakati huo.

JINSI NILIVYOKUTANA NA MKE WANGU NA KUMJUA YEHOVA

Mimi na Lydie siku ya harusi yetu, Aprili 3, 1965

Nilipokuwa katika chuo kikuu nikisomea udaktari nilikutana na mwanamke kijana aliyeitwa Lydie, ambaye tulipendana. Tulifunga ndoa mwaka wa 1965 nilipokuwa nimefikia nusu ya masomo yangu. Kufikia mwaka wa 1971, mimi na Lydie tulikuwa tumeshapata watoto watatu kati ya watoto wetu sita. Lydie amenitegemeza sana katika kazi yangu ya udaktari na katika familia yetu pia.

Nilifanya kazi ya udaktari katika hospitali kwa miaka mitatu kabla ya kuanzisha kliniki yangu. Muda mfupi baada ya kuanzisha kliniki, wenzi wa ndoa wawili, yaani, wale wagonjwa wawili niliowataja mwanzoni mwa simulizi hili walikuja ili kupata matibabu. Nilikuwa nataka kumwandikia matibabu mume mke wake alipoomba hivi: “Tafadhali daktari usimwandikie damu kwenye matibabu yake.” Nikamuuliza hivi kwa mshangao: “Kweli? Kwa nini?” Akajibu: “Sisi ni Mashahidi wa Yehova.” Nilikuwa sijawahi kuwasikia Mashahidi wa Yehova au msimamo wao kuhusu damu. Mwanamke huyo alichukua Biblia na kunionyesha msingi wao wa Kimaandiko wa kuamua kutotumia damu. (Mdo. 15:28, 29) Kisha yeye na mume wake waliendelea kunionyesha mambo ambayo Ufalme wa Mungu utatimiza; utaondoa kuteseka, magonjwa, na kifo. (Ufu. 21:3, 4) Nikasema hivi kwa mshangao: “Mambo mnayoniambia yanatimiza ndoto yangu! Nilisomea udaktari ili kuwasaidia watu wanaoteseka.” Nilisisimka sana hivi kwamba tukazungumza kwa muda wa saa moja na nusu. Kufikia wakati ambao wenzi hao walikuwa wanaondoka, moyoni mwangu sikuwa Mkatoliki tena, na nilijifunza kwamba Muumba ambaye nilikuwa nampenda sana alikuwa na jina​—Yehova!

Nilikutana na wenzi hao Mashahidi mara tatu katika kliniki yangu na kila wakati tulipokutana tulizungumza kwa zaidi ya saa moja. Niliwaalika nyumbani ili tuwe na muda mwingi zaidi wa kuzungumzia Biblia. Ingawa Lydie alikubali kujiunga nasi katika funzo la Biblia, hakukubali kwamba baadhi ya mafundisho ya Kikatoliki tuliyokuwa tumefundishwa yalikuwa ya uwongo. Kwa hiyo, nikamwalika kasisi nyumbani kwetu. Tulizungumzia mafundisho ya kanisa hadi usiku sana tukitumia tu Biblia. Mazungumzo hayo yalimsadikisha Lydie kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wanafundisha kweli. Baada ya hapo, upendo wetu kwa Yehova Mungu uliongezeka hivi kwamba sote tukabatizwa mwaka 1974.

KUMTANGULIZA YEHOVA MAISHANI

Mambo ambayo nilijifunza kuhusu kusudi la Mungu kwa wanadamu yalinichochea kubadili mambo niliyotanguliza maishani. Mimi na Lydie tulikazia fikira kumtumikia Yehova maishani mwetu. Tulikuwa tumeazimia kuwalea watoto wetu kulingana na viwango vya Biblia. Tuliwafundisha watoto wetu kumpenda Mungu na jirani na hilo likafanya familia yetu iwe na uhusiano wa karibu zaidi.​—Mt. 22:37-39.

Tunapofikiria wakati huo, mimi na Lydie mara nyingi tunacheka tunapokumbuka jinsi watoto wetu walivyotambua umoja wetu tukiwa wazazi. Walijua kwamba amri ya Yesu ya “[kuacha] ‘Ndiyo’ yenu imaanishe ndiyo, na ‘Siyo’ yenu, siyo” ilikuwa sheria katika nyumba yetu. (Mt. 5:37) Kwa mfano, Lydie hakumruhusu binti yetu aliyekuwa na miaka 17 kwenda matembezi na kikundi cha vijana wa kiume na wa kike. Baadhi ya vijana wa kike walimwambia hivi binti yetu, “Ikiwa mama yako hakuruhusu, zungumza na baba yako!” Lakini binti yetu aliwajibu hivi: “Hilo halitasaidia. Sikuzote wanakubaliana.” Naam, watoto wetu sita waliona kwamba tulikuwa na umoja katika kutumia kanuni za Biblia. Tunamshukuru sana Yehova kwamba leo tuna familia kubwa ya watumishi wa Yehova.

Ingawa kweli ilibadili mambo niliyotanguliza maishani, nilitaka kutumia elimu yangu ya udaktari kuwasaidia watu wa Mungu. Hivyo, nilijitolea kutumikia nikiwa daktari katika makao ya Betheli huko Paris na baadaye katika makao mapya ya Betheli huko Louviers. Nimekuwa nikitumikia nikiwa mjitoleaji anayetoka nje kwa miaka 50 sasa. Katika kipindi hicho, nimejifanyia marafiki wapendwa miongoni mwa familia ya Betheli ambao baadhi yao sasa wana umri wa miaka 90 hivi. Pia, siku moja nilifurahi sana nilipokutana na Mwanabetheli mpya. Nikatambua kwamba nilikuwa nimemsaidia mama yake kujifungua alipomzaa miaka 20 hivi iliyopita!

NIMEJIONEA JINSI YEHOVA ANAVYOWAJALI SANA WATU WAKE

Kwa miaka mingi, upendo wangu kwa Yehova umeongezeka kadiri ambavyo nimeona akiwaongoza na kuwalinda watu wake kupitia tengenezo lake. Mwanzoni mwa miaka 1980, Baraza Linaloongoza lilianzisha programu nchini Marekani ya kuboresha mawasiliano kati ya Mashahidi wa Yehova na madaktari.

Kisha mwaka 1988, Baraza Linaloongoza lilianzisha idara mpya katika Betheli iliyoitwa Huduma za Habari za Hospitali. Mwanzoni idara hiyo ilisimamia Halmashauri za Uhusiano na Hospitali (HLC) zilizoanzishwa nchini Marekani ili kuwasaidia wagonjwa Mashahidi wa Yehova kupata matibabu mazuri. Mpango huo ulipoanzishwa ulimwengu kote, halmashauri hizo zilianzishwa pia nchini Ufaransa. Ninasisimka kuona jinsi tengenezo la Yehova linavyowategemeza kwa upendo ndugu na dada wagonjwa wanapokuwa na uhitaji!

NDOTO YANGU YATIMIA

Tunaendelea kufurahia kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu

Nilipenda udaktari kuliko kitu kingine chochote. Lakini nilipochanganua mambo niliyotanguliza, nilitambua kwamba uponyaji muhimu zaidi ni wa kiroho—kuwasaidia watu wapatanishwe na Chanzo cha uhai, Yehova Mungu. Baada ya kustaafu, mimi na Lydie tulitumia saa nyingi kila mwezi ili kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu tukiwa mapainia wa kawaida. Tunaendelea kushiriki kadiri tunavyoweza katika kazi hii inayookoa uhai.

Nikiwa na Lydie, mwaka wa 2021

Bado ninaendelea kufanya yale ninayoweza ili kuwasaidia wagonjwa. Lakini ninatambua kwamba hata daktari bora hawezi kutibu magonjwa yote au kuzuia kifo. Hivyo, ninatazamia kwa hamu wakati ambapo maumivu, magonjwa, na kifo havitakuwepo. Katika ulimwengu huo mpya unaokaribia haraka sana, nitapata nafasi ya kujifunza milele kuhusu uumbaji wa Mungu, kutia ndani jinsi alivyobuni mwili wa binadamu kwa njia yenye kustaajabisha. Kwa kweli, ndoto yangu ya utotoni imetimia kwa sehemu tu. Ninasadiki kwamba kuna mambo mengi mazuri zaidi yanayokuja!