Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 14

Enyi Wazee wa Kutaniko—Endeleeni Kumwiga Mtume Paulo

Enyi Wazee wa Kutaniko—Endeleeni Kumwiga Mtume Paulo

“Iweni waigaji wangu.”​—1 KOR. 11:1.

WIMBO 99 Ndugu Makumi ya Elfu

MUHTASARI a

1-2. Mfano wa mtume Paulo unaweza kuwasaidiaje wazee wa kutaniko leo?

 MTUME Paulo aliwapenda ndugu zake. Alifanya kazi kwa bidii ili kuwatunza. (Mdo. 20:31) Matokeo ni kwamba waamini wenzake walimpenda sana. Pindi moja, wazee huko Efeso walipotambua kwamba hawangemwona tena kamwe, ‘walilia sana.’ (Mdo. 20:37) Wazee wetu wenye bidii pia wanawapenda ndugu na dada zao sana na wanafanya yote wanayoweza ili kuwasaidia. (Flp. 2:16, 17) Hata hivyo, nyakati nyingine wazee wanakabili changamoto. Ni nini kinachoweza kuwasaidia kushinda changamoto hizo?

2 Wazee wetu wenye bidii wanaweza kufikiria mfano wa Paulo. (1 Kor. 11:1) Paulo hakuwa na uwezo unaopita wa mwanadamu. Paulo alikuwa mwanadamu asiye mkamilifu ambaye nyakati nyingine alipambana sana ili kufanya yaliyo sawa. (Rom. 7:18-20) Na alihitaji kukabiliana na matatizo mbalimbali. Lakini Paulo hakufa moyo au kupoteza shangwe yake. Kwa kumwiga Paulo, wazee wanaweza kushinda changamoto wanazokabiliana nazo na kudumisha shangwe yao wanapomtumikia Yehova. Acheni tuone jinsi wanavyoweza kufanya hivyo.

3. Tutachunguza nini katika makala hii, na tutasaidiwa kufanya nini?

3 Katika makala hii tutachunguza changamoto hizi nne ambazo wazee wanakabiliana nazo: (1) kuwa na usawaziko inapohusu kazi ya kuhubiri na majukumu yao mengine, (2) kuwa wachungaji wenye kujali, (3) kukabiliana na udhaifu wa kibinafsi, (4) kukabiliana na kutokamilika kwa wengine. Tutachunguza jinsi Paulo alivyokabiliana na kila mojawapo ya changamoto hizo, na jinsi wazee wanavyoweza kuiga mfano wake.

KUWA NA USAWAZIKO INAPOHUSU KAZI YA KUHUBIRI NA MAJUKUMU MENGINE

4. Kwa nini inaweza kuwa vigumu kwa wazee kuweka mfano mzuri katika kazi ya kuhubiri?

4 Kwa nini inaweza kuwa changamoto? Zaidi ya kuongoza katika kazi ya kuhubiri, wazee wana majukumu mengine mengi. Kwa mfano, wengi huongoza mikutano ya katikati ya juma na kuongoza Funzo la Biblia la Kutaniko. Pia, wanaweza kushughulikia migawo mingine ya kutoa hotuba. Wana bidii ya kuwazoeza watumishi wa huduma na wanafurahia kuendelea kuwatia moyo ndugu na dada. (1 Pet. 5:2) Baadhi ya wazee wanashiriki katika ujenzi na udumishaji wa Majumba ya Ufalme na majengo mengine ya kitheokrasi. Hata hivyo, kama wengine wote kutanikoni, kazi muhimu zaidi ya wazee ni kuhubiri habari njema.​—Mt. 28:19, 20.

5. Akiwa mhubiri Paulo aliweka mfano gani?

5 Mfano wa Paulo. Katika Wafilipi 1:10, Paulo anatuambia jambo lililomfanya awe mhubiri mwenye mafanikio, anatuhimiza hivi: “Mhakikishe mambo muhimu zaidi.” Paulo alitenda kulingana na ushauri huo. Alikuwa amepewa huduma, na kwa miaka mingi aliiona huduma hiyo kuwa mojawapo ya mambo muhimu zaidi. Alihubiri “hadharani na nyumba kwa nyumba.” (Mdo. 20:20) Hakuhubiri tu muda fulani wa siku au siku moja tu ya juma. Alitumia kila fursa aliyopata ili kuhubiri! Kwa mfano, alipokuwa akiwasubiri wenzake huko Athene, alihubiria habari njema kikundi cha watu fulani mashuhuri, na akapata matokeo mazuri. (Mdo. 17:16, 17, 34) Hata alipokuwa ‘amefungwa gerezani,’ Paulo aliwahubiria wale waliokuwa wamemzunguka.​—Flp. 1:13, 14; Mdo. 28:16-24.

6. Paulo aliwazoeza wengine kufanya nini?

6 Paulo aliutumia vizuri kabisa wakati wake. Mara kwa mara aliwaalika wengine waungane naye katika huduma. Kwa mfano, katika safari yake ya kwanza ya umishonari, alienda na Yohana Marko; na katika safari ya pili na Timotheo. (Mdo. 12:25; 16:1-4) Bila shaka, Paulo alijitahidi kadiri alivyoweza ili kuwafundisha wanaume hao jinsi ya kupanga mambo kutanikoni, kufanya kazi ya uchungaji, na kuwa walimu wenye ustadi.—1 Kor. 4:17.

Mwige Paulo kwa kuwa tayari kutoa Ushahidi (Tazama fungu la 7) b

7. Wazee wanaweza kufuataje himizo la Paulo katika Waefeso 6:14, 15?

7 Somo. Wazee wanaweza kumwiga Paulo kwa kuhubiri nyumba kwa nyumba na pia kuwa tayari kutoa ushahidi kila wanapopata fursa. (Soma Waefeso 6:14, 15.) Kwa mfano, wanaweza kutoa ushahidi wanapofanya ununuzi au wakiwa kazini. Au wanaposhiriki kwenye miradi ya ujenzi ya kitheokrasi, wanaweza kuwahubiria habari njema majirani na watu wanaowauzia vifaa vya ujenzi. Kama Paulo, wazee wanaweza kutumia muda wanaokuwa katika huduma kuwazoeza wengine, kutia ndani watumishi wa huduma.

8. Nyakati nyingine huenda mzee akahitaji kufanya nini?

8 Wazee hawapaswi kamwe kujishughulisha kupita kiasi na migawo ya kutanikoni au ya mzunguko hivi kwamba wanakosa muda wa kuhubiri. Ili wawe na usawaziko, huenda pindi fulani wakahitaji kukataa baadhi ya migawo. Baada ya kufikiria kwa sala, huenda wakatambua kwamba ikiwa watakubali mgawo fulani hawataweza kushughulikia mambo muhimu zaidi. Mambo hayo yanatia ndani kuongoza ibada ya familia kila juma, kushiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri, au kuwazoeza watoto wao katika utendaji huo. Huenda ikawa vigumu kwa baadhi yao kukataa pendeleo fulani la utumishi, lakini wanaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anaelewa tamaa yao ya kuwa na usawaziko katika mambo yote.

KUWA WACHUNGAJI WENYE KUJALI

9. Wazee wenye shughuli nyingi wanakabili changamoto gani?

9 Kwa nini inaweza kuwa changamoto? Watu wa Yehova wanapitia majaribu mengi. Katika siku hizi za mwisho, sisi sote tunahitaji, utegemezo, faraja, na kutiwa moyo. Na nyakati fulani wengine wanahitaji msaada ili kuepuka mwenendo mbaya. (1 The. 5:14) Bila shaka, wazee hawawezi kuondoa majaribu yote ambayo watu wa Mungu wanakabili. Hata hivyo, Yehova anawataka wazee wafanye yote wanayoweza ili kuwatia moyo na kuwalinda kondoo wake. Wazee wa kutaniko wenye shughuli nyingi wanawezaje kupata muda wa kutoa msaada?

Wapongeze na kuwajenga wengine (Tazama fungu la 10 na 12) c

10. Kulingana 1 Wathesalonike 2:7, Paulo alionyeshaje kwamba anawajali watu wa Yehova?

10 Mfano wa Paulo. Paulo alitafuta njia za kuwapongeza ndugu zake na kuwaimarisha. Ni vizuri kwa wazee kuiga mfano wake kwa kuwatendea watu wa Yehova kwa upendo mwororo. (Soma 1 Wathesalonike 2:7.) Paulo aliwahakikishia waabudu wenzake kwamba anawapenda na kwamba Yehova anawapenda pia. (2 Kor. 2:4; Efe. 2:4, 5) Paulo aliwatendea ndugu na dada kutanikoni kama rafiki, akitumia wakati pamoja nao. Alionyesha kwamba aliwatumaini kwa kuzungumza waziwazi kuhusu hofu na udhaifu wake mwenyewe. (2 Kor. 7:5; 1 Tim. 1:15) Hata hivyo, Paulo hakukazia fikira matatizo yake mwenyewe. Badala yake, alitaka kuwasaidia ndugu zake.

11. Paulo aliwashaurije ndugu na dada zake?

11 Nyakati nyingine, Paulo alihitaji kuwashauri ndugu na dada zake. Lakini hakufanya hivyo kamwe kwa kuchochewa na hasira. Aliwashauri kwa sababu aliwapenda na alitaka kuwalinda dhidi ya hatari mbalimbali. Alijitahidi kutoa shauri kwa njia rahisi na inayoeleweka na alitaka walikubali. Kwa mfano, katika barua aliyowaandikia Wakorintho, Paulo aliwapa shauri zito. Baada ya kuandika barua hiyo, alimtuma Tito awatembelee. Paulo alitamani kujua jinsi ambavyo waliitikia ujumbe uliokuwa katika barua yake. Alifurahi sana kujua kwamba walikubali na kufuata shauri hilo!​—2 Kor. 7:6, 7.

12. Wazee wanaweza kuwaimarishaje waabudu wenzao?

12 Somo. Wazee wanaweza kuiga mfano wa Paulo kwa kutumia wakati pamoja na waabudu wenzao. Njia moja ya kufanya hivyo, ni kufika mapema kwenye mikutano ya kutaniko ili kuwa na mazungumzo yenye kujenga na wengine. Mara nyingi inahitaji dakika chache tu kumtia moyo kwa upendo ndugu au dada anayehitaji kutiwa moyo. (Rom. 1:12; Efe. 5:16) Mzee anayefuata mfano wa Paulo, atawaimarisha pia waabudu wenzake kwa kutumia Neno la Mungu ili kuwajenga na kuwahakikishia kwamba bado Mungu anawapenda. Pia, anahakikisha wanajua kwamba anawajali. Anawasiliana nao kwa ukawaida na kutafuta fursa za kuwapongeza. Mzee anapotoa shauri anapaswa kutegemea Neno la Mungu. Anataja mambo hususa kwa fadhili, kwa sababu anataka ndugu na dada wakubali na kutumia shauri lake.​—Gal. 6:1.

KUKABILIANA NA UDHAIFU WA KIBINAFSI

13. Mzee anawezaje kuathiriwa na udhaifu wake mwenyewe?

13 Kwa nini inaweza kuwa changamoto? Wazee si wakamilifu. Kama mtu mwingine yeyote, wao pia wanakosea. (Rom. 3:23) Nyakati nyingine, huenda wakapambana ili kuwa na maoni yaliyosawazika kuhusu udhaifu wao. Baadhi yao huenda wakakazia fikira sana udhaifu wao hivi kwamba wanavunjika moyo. Huenda wengine wakapuuza udhaifu wao na kuhisi kwamba hawahitaji kufanya mabadiliko yoyote.

14. Kulingana na Wafilipi 4:13, unyenyekevu ulimsaidiaje Paulo kukabiliana na udhaifu wake?

14 Mfano wa Paulo. Kwa unyenyekevu Paulo alitambua kwamba hangeweza kushinda udhaifu wake kwa uwezo wake mwenyewe. Alihitaji nguvu zinazotoka kwa Mungu. Mwanzoni, Paulo aliwatesa sana Wakristo. Lakini baadaye, alikubali udhaifu wake na alikuwa tayari kubadili mtazamo na utu wake. (1 Tim. 1:12-16) Kwa msaada wa Yehova, Paulo alikuja kuwa mchungaji mwenye upendo, huruma, na mnyenyekevu. Alitambua kabisa kwamba hakuwa mkamilifu. Hata hivyo, badala ya kukazia fikira udhaifu wake aliamini kabisa kwamba Yehova angeweza kumsamehe. (Rom. 7:21-25) Hakutarajia kuwa mkamilifu. Badala yake, alijitahidi kuboresha utu wake wa Kikristo na kwa unyenyekevu alitegemea msaada wa Yehova ili atimize kazi yake.​—1 Kor. 9:27; soma Wafilipi 4:13.

Jitahidi kushinda udhaifu wa kibinafsi (Tazama fungu la 14 na 15) d

15. Wazee wanapaswa kuwa na maoni gani yaliyosawazika kuhusu udhaifu wao?

15 Somo. Wazee hawawekwi rasmi kwa sababu wao ni wakamilifu. Hata hivyo, Yehova anatarajia wakubali makosa yao na wasitawishe sifa za Kikristo. (Efe. 4:23, 24) Mzee anapaswa kujichunguza kwa kutumia Neno la Mungu na kufanya marekebisho yoyote yanayohitajika. Kisha, Yehova atamsaidia awe mwenye furaha na mafanikio.​—Yak. 1:25.

KUSHUGHULIKA NA HALI YA KUTOKAMILIKA YA WENGINE

16. Ni nini kinachoweza kutokea ikiwa mzee atakazia fikira hali ya kutokamilika ya wengine?

16 Kwa nini inaweza kuwa changamoto? Huenda wazee wakajua udhaifu wa wengine kutanikoni kwa sababu wanashirikiana nao kwa ukaribu. Hata hivyo, ikiwa wazee hawatakuwa waangalifu wanaweza kukasirika, kuwa wakali, na wenye kuhukumu. Paulo aliwaonya Wakristo kwamba Shetani angependa wafanye hivyo.​—2 Kor. 2:10, 11.

17. Paulo aliwaonaje ndugu na dada zake?

17 Mfano wa Paulo. Alikuwa na mtazamo unaofaa kuelekea ndugu na dada zake. Alitambua makosa yao, kwa sababu nyakati nyingine yeye mwenyewe aliumizwa na matendo yao. Hata hivyo, Paulo alijua tofauti kati ya mwenendo mbaya na watu wabaya. Aliwapenda ndugu zake na alikazia fikira sifa zao nzuri. Ilipokuwa vigumu kwa ndugu na dada zake kufanya yaliyo sawa, aliamini kwamba walikuwa na nia nzuri na walihitaji tu msaada.

18. Unajifunza nini kutokana na jinsi Paulo alivyoshughulikia kisa cha Euodia na Sintike? (Wafilipi 4:1-3)

18 Kwa mfano, fikiria jinsi ambavyo Paulo alishughulika na dada wawili katika kutaniko la Filipi. (Soma Wafilipi 4:1-3.) Inaonekana Euodia na Sintike walishindwa kusuluhisha hali yao ya kutoelewana. Paulo hakuwa mkali au mwenye kuhukumu; badala yake, alikazia fikira sifa zao nzuri. Walikuwa dada waaminifu waliomtumikia Yehova kwa miaka mingi. Paulo alijua kwamba Yehova aliwapenda. Kwa kuwa Paulo alikuwa na maoni yanayofaa kuelekea dada hao, aliwatia moyo wasuluhishe tofauti zao. Mtazamo wake pia ulimsaidia kudumisha shangwe yake na kuendelea kuwa na urafiki wa karibu na Wakristo katika kutaniko hilo.

Jitahidi kutowahukumu wengine (Tazama fungu 19) e

19. (a) Wazee wanaweza kudumishaje mtazamo unaofaa kuelekea waabudu wenzao? (b) Unajifunza nini kutokana na picha ya mzee anayefanya usafi katika Jumba la Ufalme?

19 Somo. Enyi wazee, kazieni fikira sifa nzuri za ndugu na dada zenu. Sisi sote si wakamilifu; lakini kila mmoja wetu ana sifa nzuri. (Flp. 2:3) Ni kweli kwamba huenda pindi fulani wazee wakahitaji kumrekebisha ndugu au dada. Hata hivyo, kama Paulo, wazee wanapaswa kujitahidi kuepuka kukazia fikira tu maneno na matendo yanayoudhi ya mtu fulani. Badala yake, wanapaswa kukazia fikira jinsi mtu huyo anavyompenda Yehova, jinsi ambavyo amevumilia katika kumtumikia Mungu, na uwezo wake wa kufanya mambo mazuri. Wazee wenye mtazamo unaofaa, huendeleza mazingira yenye uchangamfu na yanayojenga kutanikoni.

ENDELEA KUMWIGA PAULO

20. Wazee wanaweza kuendeleaje kunufaika kutokana na mfano wa Paulo?

20 Enyi wazee, mtanufaika sana kwa kuendelea kuchunguza mfano wa Paulo. Kwa mfano, katika Fahirisi unaweza kutafuta kichwa “Paulo” na kisha kichwa kidogo “mfano kwa wazee Wakristo.” Unaposoma habari zilizoorodheshwa hapo, jiulize, ‘Mfano wa Paulo unaweza kunisaidiaje kudumisha shangwe yangu ninapotimiza kazi yangu nikiwa mzee?’

21. Wazee wanaweza kuwa na uhakika gani?

21 Enyi wazee, kumbukeni kwamba Yehova hatarajii muwe wakamilifu; badala yake anataka muwe waaminifu. (1 Kor. 4:2) Yehova alithamini bidii ya Paulo na uaminifu wake. Mnaweza kuwa na hakika kwamba Mungu anathamini pia kazi mnayofanya katika utumishi wake. Yehova ‘hatasahau kamwe kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuhudumu na kuendelea kuwahudumia watakatifu.’​—Ebr. 6:10.

WIMBO 87 Njooni! Mburudishwe

a Ni baraka kubwa sana kuwa na wazee wenye bidii wanaotupenda na wanaotujali! Katika makala hii, tutazungumzia changamoto nne wanazokabili. Pia, tutachunguza jinsi mfano wa mtume Paulo, unavyoweza kuwasaidia wazee leo kukabiliana na changamoto hizo. Makala hii, itatusaidia tuwaonyeshe wazee hisia mwenzi na itatuchochea kuwaonyesha upendo na kuwaunga mkono.

b MAELEZO YA PICHA: Anapoondoka kazini ndugu anamhubiria habari njema mfanyakazi mwenzake.

c MAELEZO YA PICHA: Kwa fadhili, mzee anamfanyia uchungaji ndugu mwenye mwelekeo wa kujitenga na wengine.

d MAELEZO YA PICHA: Ndugu anampa ushauri Mkristo ambaye amekasirishwa na jambo fulani.

e MAELEZO YA PICHA: Mzee hamhukumu ndugu ambaye amekengeushwa kutoka kwenye kazi ambayo alijitolea kufanya.