Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 14

Wazee​—Muendelee Kuiga Mutume Paulo

Wazee​—Muendelee Kuiga Mutume Paulo

“Mukuwe waigaji wangu.”​—1 KO. 11:1.

WIMBO 99 Ndugu na Dada Wote

KIFUPI YA HABARI *

1-2. Mufano wa mutume Paulo unaweza kusaidia namna gani wazee leo?

 MUTUME Paulo alipenda sana ndugu zake. Alitumika sana ili kuwahangaikia. (Mdo. 20:31) Njo maana ndugu na dada zake walimupenda sana. Siku moya, wakati wazee wa Efeso walijua kama hawangemuona tena, ‘wote walilia sana.’ (Mdo. 20:37) Wazee wetu wenye kujitolea, wanapenda pia ndugu na dada zao na wanafanya yote yenye wanaweza ili kuwasaidia. (Flp. 2:16, 17) Hata vile, wakati fulani, wazee wanapambana na magumu fulani. Ni nini inaweza kuwasaidia wapiganishe ile magumu?

2 Wazee wetu wenye kutumika kwa bidii wanaweza kufikiria mufano wa Paulo. (1 Ko. 11:1) Paulo hakukuwa na uwezo wenye malaika wako nao. Alikuwa mwanaume mwenye hakamilike. Wakati fulani, ilikuwa nguvu kwake kufanya mambo yenye kuwa sawa. (Ro. 7:18-20) Alikuwa na magumu mingi mbalimbali. Lakini Paulo hakuacha kuendelea kutumikia ndugu zake kwa bidii na hakupoteza furaha yake. Kwa kumuiga Paulo, wazee wanaweza kupiganisha magumu yenye wanakutana nayo na kuendelea kuwa na furaha wakati wako wanamutumikia Yehova. Muache tuone namna wanaweza kufanya vile.

3. Ni mambo gani tutachunguza mu hii habari, na ni mambo gani ingine tutajifunza?

3 Mu hii habari, tutachunguza magumu ine yenye wazee wanazoea kukutana nayo: (1) kuwa na usawaziko kati ya kazi yao ya kuhubiri na madaraka ingine, (2) kuwa wachungaji wazuri, (3) kupambana na uzaifu wa kipekee, na (4) kupambana na uzaifu wa wengine. Tutaona namna Paulo alipiganisha ile magumu yote na namna wazee wanaweza kuiga mufano wake.

KUWA NA USAWAZIKO MU KAZI YA KUHUBIRI NA MADARAKA INGINE

4. Juu ya nini wazee wanaweza kuwa na magumu ya kuongoza kazi ya kuhubiri?

4 Juu ya nini ile inaweza kuwa magumu? Wazee wako na madaraka mingi, zaidi ya kuongoza kazi ya kuhubiri. Kwa mufano, wengi wanasimamia mukutano wa katikati ya juma na wanaongoza Funzo ya Biblia ya Kutaniko. Wanaweza pia kutoa hotuba. Wako nafanya mengi juu ya kuzoeza watumishi wa huduma, na wanafurahia kutolea ndugu na dada zao kitia-moyo. (1 Pe. 5:2) Wazee fulani wanafanya kazi ya kujenga na kutengeneza Majumba ya Ufalme, na kujenga majengo ingine yenye inatumiwa ili kumuabudu Yehova. Sawa vile watu wote mu kutaniko, kazi ya maana sana yenye wazee wanafanya ni kuhubiri.​—Mt. 28:19, 20.

5. Paulo alituachia mufano gani akiwa muhubiri?

5 Mambo yenye wazee wanaweza kujifunza kupitia mufano wa Paulo. Mu Wafilipi 1:10, Paulo anatuambia juu ya nini alipata matokeo ya muzuri mu mahubiri. Anasema hivi: “Muhakikishe mambo ya maana zaidi.” Paulo alifuata shauri yake mwenyewe. Alipewa mugao wa kuhubiri, na kwa miaka mingi aliona kazi ya kuhubiri kuwa jambo ya maana sana mu maisha yake. Alikuwa anahubiri “mbele ya watu wote na nyumba kwa nyumba.” (Mdo. 20:20) Hakuhubiri tu wakati fulani ku siku ao siku moya tu ku juma. Alitumia nafasi yoyote yenye ilijitokeza ili kuhubiri! Kwa mufano, wakati alikuwa anangojea wenzake kule Atene, alianza kuhubiria vikundi mbalimbali vya watu, na alipata matokeo fulani ya muzuri. (Mdo. 17:16, 17, 34) Hata wakati alikuwa mu “vifungo . . . vya gereza,” Paulo alihubiria wale wenye walikuwa pembeni yake.​—Flp. 1:13, 14; Mdo. 28:16-24.

6. Paulo alizoeza wengine kufanya nini?

6 Paulo alitumia muzuri zaidi wakati wake. Mara mingi, alikuwa anaomba wengine wamusindikize mu mahubiri. Kwa mufano, mu safari ya kwanza ya umisionere, alienda na Yohana Marko, na mu safari yake ya pili, alienda na Timoteo. (Mdo. 12:25; 16:1-4) Bila shaka, Paulo alifanya yake yote ili kufundisha wale wanaume namna ya kupanga kutaniko, namna ya kutimiza muzuri kazi ya uchungaji, na namna ya kuwa walimu wenye uzoefu.​—1 Ko. 4:17.

Muige Paulo kwa kuwa tayari kutoa ushahidi (Ona fungu ya 7) *

7. Namna gani wazee wanaweza kufuata shauri ya Paulo yenye kuwa mu Waefeso 6:14, 15?

7 Somo. Wazee wanaweza kuiga Paulo, hapana tu kwa kuhubiri nyumba kwa nyumba, lakini pia kwa kuwa tayari kutoa ushahidi mu kila hali yenye inajitokeza. (Soma Waefeso 6:14, 15.) Kwa mufano, wanaweza kutoa ushahidi wakati wako wanauza vitu, ao fasi kwenye wanatumikiaka. Ao wakati wako wanasaidia kujenga Jumba ya Ufalme, wanaweza kuhubiria watu wenye kuishi pembeni-pembeni pale ao kuhubiria watu wenye kuwauzisha vitu fulani. Kama Paulo, wazee wanaweza kuzoeza wengine, kutia ndani watumishi wa huduma wakati wanahubiri nao.

8. Wakati fulani, muzee anaweza kuwa na lazima ya kufanya nini?

8 Wazee hawapaswe kuacha migao yao mu kutaniko ao mu muzunguko iwafanye wakose wakati wa kuhubiri. Juu ya kuendelea kuwa na usawaziko, mu hali fulani inaweza kuwa lazima kwa wazee kukatala kutimiza migao fulani. Kisha kuwaza na kusali juu ya ile, wanaweza kutambua kama ikiwa wanakubali ile migao, ile itafanya wasihangaikie muzuri jambo ya maana zaidi. Ile mambo inaweza kutia ndani, kuongoza ibada ya familia kila juma, kuwa na bidii mu kazi ya kuhubiri, ao kuzoeza watoto ili kuhubiri. Wamoja wanaona kama ni nguvu kukatala pendeleo fulani ya utumishi. Lakini wanaweza kuwa hakika kama Yehova anaelewa tamaa yao ya kuwa na usawaziko mu mambo yote.

KUWA MUCHUNGAJI MUZURI

9. Wazee wenye kuwa na mambo mingi ya kufanya wanapambana na magumu gani?

9 Juu ya nini ile inaweza kuwa magumu? Watu wa Yehova wako wanapata magumu mingi sana. Mu hizi siku za mwisho, siye wote tuko na lazima ya kutiwa moyo, kusaidiwa, na kufarijiwa. Na wakati fulani, wamoja wako na lazima ya musaada juu waepuke mwenendo mubaya. (1 Te. 5:14) Kusema kweli, wazee hawawezi kuondoa magumu yote yenye watu wa Yehova wanapambana nayo. Hata vile, Yehova anapenda wazee wafanye yote yenye wanaweza ili kutia moyo na kulinda kondoo zake. Namna gani wazee wenye tayari wako na mambo mingi ya kufanya wanaweza kupata wakati wa kutolea ndugu na dada zao musaada wenye wako nao lazima?

Mupongeze wengine na kuwatia moyo (Ona fungu ya 10, 12) *

10. Kulingana na 1 Watesalonike 2:7, namna gani Paulo alihangaikia watu wa Yehova?

10 Mambo yenye wazee wanaweza kujifunza kupitia mufano wa Paulo. Paulo alitafuta njia mbalimbali ili kupongeza ndugu zake na kuwatia moyo. Ni muzuri kwa wazee kuiga mufano wa Paulo na kutendea ndugu na dada kwa upendo na wema. (Soma 1 Watesalonike 2:7.) Paulo alihakikishia waabudu wenzake kama anawapenda na kama Yehova anawapenda. (2 Ko. 2:4; Efe. 2:4, 5) Paulo alitendea wale wenye kuwa mu kutaniko sawa vile marafiki na alipitisha wakati pamoya nao. Alionyesha kama anawatumainia, kwa kuwaelezea waziwazi juu ya woga wake na uzaifu wake. (2 Ko. 7:5; 1 Ti. 1:15) Hata vile, Paulo hakukazia uangalifu magumu yake. Lakini alipenda njo kusaidia ndugu zake.

11. Juu ya nini Paulo alishauria ndugu na dada zake?

11 Wakati fulani, Paulo alikuwa na lazima ya kushauria ndugu na dada zake. Hakufanya vile ili kuonyesha kasirani yake. Alitoa shauri juu alikuwa anawahangaikia na alipenda kuwalinda kutokana na hatari mbalimbali. Alijikaza kufanya shauri yake ikuwe mwepesi kueleweka, na alipenda waikubali. Kwa mufano, mu barua kwa Wakorinto, Paulo alitoa shauri nzito kabisa. Kisha kuandika ile barua, alimutuma Tito kwao. Paulo alikuwa na wasiwasi wa kutaka kujua namna wangetenda wakati walipokea barua yake. Alifurahi sana wakati alisikia kama walikubali shauri yake na kuitumikisha!​—2 Ko. 7:6, 7.

12. Wazee wanaweza namna gani kutia moyo waabudu wenzao?

12 Somo. Wazee wanaweza kufuata mufano wa Paulo kwa kupitisha wakati pamoya na waabudu wenzao. Njia moya ya kufanya vile, ni kufika kwa wakati ku mikutano ili kuwa na mazungumuzo yenye kutia moyo pamoya na wengine. Mara mingi inakamataka wakati kidogo tu ili kutolea ndugu ao dada fulani kitia-moyo yenye alikuwa nayo lazima. (Ro. 1:12; Efe. 5:16) Muzee mwenye anafuata mufano wa Paulo, atatia pia moyo waabudu wenzake kwa kutumia Neno ya Mungu ili kutia nguvu imani yao, na kuwahakikishia kama Mungu anawapenda. Zaidi ya ile, anawahakikishia kama anawapenda. Anazungumuza nao kikawaida na kutafuta nafasi ya kuwapongeza. Wakati inaomba muzee atoe shauri, atahakikisha kama ile shauri inapatana na Neno ya Mungu. Atasema waziwazi lakini mu njia ya muzuri juu anapenda ndugu ao dada fulani atumikishe shauri yake.​—Gal. 6:1.

KUPAMBANA NA UZAIFU WA KIPEKEE

13. Uzaifu wa muzee unaweza kuwa na matokeo gani juu yake?

13 Juu ya nini ile inaweza kuwa magumu? Wazee hawakamilike. Sawa vile siye wote, nao pia wanafanyaka makosa. (Ro. 3:23) Wakati fulani, inaweza kuwa nguvu kwao kuwa na mutazamo wenye kufaa juu ya uzaifu wao. Wamoja wanaweza kuhangaikia sana uzaifu wao na ile inaweza kufanya wafikie kuvunjika moyo. Wengine wanaweza kuwaza kama uzaifu wao hauko wa maana sana na kama hawana lazima ya kufanya mabadiliko yoyote.

14. Kulingana na Wafilipi 4:13, unyenyekevu ulimusaidia namna gani Paulo kupiganisha uzaifu wake?

14 Mambo yenye wazee wanaweza kujifunza kupitia mufano wa Paulo. Kwa unyenyekevu Paulo alitambua kama hangeweza kupiganisha uzaifu wake mwenyewe. Alikuwa na lazima ya nguvu kutoka kwa Mungu. Mbele Paulo alikuwa anatesa sana Wakristo. Lakini kisha alifikia kuelewa kama mambo yenye alikuwa anafanya ilikuwa ya mubaya na alikuwa tayari kubadilisha mutazamo wake na utu wake. (1 Ti. 1:12-16) Kwa musaada wa Yehova, Paulo alifikia kuwa mwenye upendo, huruma, na muchungaji munyenyekevu. Alijua kama alikuwa na uzaifu mingi, lakini hakukaza akili yake juu ya ile. Kuliko kufanya vile, alitumainia kama Yehova angemusamehe. (Ro. 7:21-25) Hakutazamia kuwa mukamilifu. Lakini, alijikaza sana kuwa na utu wa Kikristo na kwa unyenyekevu alitegemea musaada wa Yehova ili kutimiza kazi yake.​—1 Ko. 9:27; soma Wafilipi 4:13.

Ujikaze sana ili kupiganisha uzaifu wa kipekee (Ona fungu ya 14-15) *

15. Namna gani muzee anaweza kuwa na mutazamo wenye kufaa juu ya uzaifu wake?

15 Somo. Wazee hawachaguliwake juu wako wakamilifu. Hata vile, Yehova anatazamia wakubali makosa yao, na kuonyesha utu wa Kikristo. (Efe. 4:23, 24) Muzee anapaswa kujichunguza kupatana na Neno ya Mungu na kufanya mabadiliko yoyote yenye inaombwa. Kisha Yehova atamusaidia kuwa na furaha na kuwa muzee muzuri.​—Yak. 1:25.

KUPAMBANA NA UZAIFU WA WENGINE

16. Ni nini inaweza kutokea kama muzee anakazia uangalifu uzaifu wa wengine?

16 Juu ya nini ile inaweza kuwa magumu? Saa yenye wazee wanapitisha wakati pamoya na ndugu na dada mu kutaniko, inaweza kuwa mwepesi kwao kuona uzaifu wa wale ndugu na dada. Hata vile, kama hawako waangalifu, wazee wanaweza kufikia kukasirika, kutenda kwa ukali, ao kutoa hukumu yenye haifae. Paulo alionya Wakristo kama Shetani angependa wafanye vile.​—2 Ko. 2:10, 11.

17. Paulo aliona namna gani ndugu na dada zake?

17 Mambo yenye wazee wanaweza kujifunza kupitia mufano wa Paulo. Aliendelea kuwa na mutazamo wenye kufaa kwa ajili ya ndugu na dada zake. Alijua muzuri makosa yao, juu wakati fulani mambo yenye walifanya ilimuumiza. Lakini Paulo alijua tofauti kati ya matendo ya mubaya na watu wabaya. Alipenda ndugu zake, na kukazia uangalifu sifa zao za muzuri. Kama ndugu na dada zake walishindwa kufanya mambo ya muzuri, aliamua kufikiri kama walikuwa na nia ya muzuri na kama walikuwa tu na lazima ya musaada.

18. Namna Paulo alisaidia Euodia na Sintike inakufundisha nini? (Wafilipi 4:1-3)

18 Kwa mufano, fikiria namna Paulo alisaidia dada wawili mu kutaniko ya Filipi. (Soma Wafilipi 4:1-3.) Pengine Euodia na Sintike walikosana na hawakukuwa tena marafiki. Paulo hakuwatendea kwa ukali ao kuwahukumu. Lakini alikazia uangalifu sifa zao za muzuri. Wale dada waaminifu walikuwa wamemutumikia Yehova kwa wakati murefu. Paulo alijua kama Yehova aliwapenda. Juu alikuwa na mawazo ya muzuri kuelekea wale dada, aliwatia moyo wafanye amani. Juu Paulo alikazia sifa za muzuri za wengine, aliweza kuendelea kuwa na furaha na kulinda urafiki wa nguvu sana pamoya na wale wa mu ile kutaniko.

Fanya yako yote ili usihukumu wengine (Ona fungu ya 19) *

19. (a) Namna gani wazee wanaweza kuendelea kukazia uangalifu sifa za muzuri za waabudu wenzao? (b) Picha yenye kuonyesha muzee mwenye iko anasafisha Jumba ya Ufalme inaweza kukufundisha nini?

19 Somo. Wazee wanatafuta sifa za muzuri zenye ndugu na dada wako nazo. Siye wote hatukamilike, lakini kila mumoja wetu iko na sifa zenye kupendeza. (Flp. 2:3) Kusema kweli, pengine mara kwa mara wazee wako na lazima ya kurekebisha mawazo ya ndugu ao dada fulani. Kama Paulo, wazee wanapaswa kujikaza kukazia uangalifu hapana maneno na matendo yenye kukasirisha ya ule mutu, lakini wanapaswa kukazia uangalifu upendo wenye ule mutu iko nao kwa Yehova, uvumilivu wenye anaonyesha mu utumishi wa Yehova, na uwezo wake wa kufanya mambo ya muzuri. Wazee wenye wanakazia uangalifu sifa za muzuri za wengine wanasaidia ndugu na dada zao wajisikie kuwa wenye kupendwa na watu wote mu kutaniko.

MUENDELEE KUIGA PAULO

20. Namna gani wazee wanaweza kuendelea kupata faida kupitia mufano wa Paulo?

20 Nyiye wazee mutaona kama ni jambo ya maana kuendelea kujifunza mufano wa Paulo. Kwa mufano, mu Fahirisi ya Machapisho ya Watch Tower, kwenye sehemu “Paulo” chini ya kichwa “mfano kwa wazee Wakristo.” Wakati uko unasoma sehemu fulani zenye kutajwa mule, ujiulize hivi: ‘Mufano wa Paulo unaweza kunisaidia namna gani niendelee kuwa na furaha wakati niko natimiza kazi yangu nikiwa muzee?’

21. Wazee wanaweza kuwa hakika na jambo gani?

21 Wazee, musisahau kama Yehova hawaombe mukuwe wakamilifu; lakini anawaomba mukuwe waaminifu. (1 Ko. 4:2) Yehova alisamini kazi ya bidii ya Paulo na uaminifu wake. Munaweza pia kuwa hakika kama Yehova anasamini mambo yenye munafanya mu utumishi wake. Yehova ‘hatasahau kazi yenu na upendo wenye mulionyesha kwa ajili ya jina lake kwa kutumikia na kuendelea kutumikia watakatifu.’​—Ebr. 6:10.

WIMBO 87 Tunatiana Moyo ku Mikutano

^ Tuko wenye Shukrani sana kwa ajili ya kazi ya bidii yenye wazee wanafanya ili kutusaidia. Mu hii habari, tutazungumuzia magumu ine yenye wazee wanazoea kukutana nayo. Tutaona pia namna mufano wa Paulo unaweza kusaidia wazee leo kupambana na ile magumu. Hii habari itatusaidia siye wote kujiweka pa nafasi ya wazee na itatuchochea kuwaonyesha upendo na kuwategemeza.

^ MAFASIRIO YA PICHA: Wakati ndugu moya anatoka ku kazi, anahubiria mufanyakazi mwenzake habari njema.

^ MAFASIRIO YA PICHA: Muzee moya anamufanyia ndugu fulani mwenye kuwa na muelekeo wa kujitenga na wengine ziara ya uchungaji.

^ MAFASIRIO YA PICHA: Ndugu fulani anatoa shauri yenye kufaa kwa mutu mwenye kukasirikia jambo fulani yenye ilitokea.

^ MAFASIRIO YA PICHA: Muzee moya hahukumu ndugu mwenye alijitolea ili kufanya kazi fulani wakati anafikia kukengeushwa na jambo fulani.