Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 17

Mambo Yenye Mufano wa Eunike Unaweza Kufundisha Mama

Mambo Yenye Mufano wa Eunike Unaweza Kufundisha Mama

“Usiache mafundisho ya mama yako. Ni taji la maua lenye kuvutia kwa ajili ya kichwa chako na pambo la muzuri kwa ajili ya shingo yako.”​—MEZ. 1:8, 9.

WIMBO 137 Wanamuke Wenye Imani

KIFUPI YA HABARI *

Eunike, mama ya Timoteo, na Loisi tate yake wanafurahi sana wakati wako namuangalia saa yenye iko anabatizwa (Ona fungu ya 1)

1-2. (a) Eunike alikuwa nani, na ni magumu gani yenye alipambana nayo wakati alikuwa anafundisha mutoto wake? (b) Fasiria picha yenye kuwa ku jalada.

 HATA kama Biblia haizungumuzie kuhusu ubatizo wa Timoteo, tunaweza kuwazia namna mama ya Timoteo, Eunike, alijisikiaka siku yenye Timoteo alibatizwa. (Mez. 23:25) Wazia furaha yenye Eunike iko nayo wakati anamuangalia Timoteo anasimama mu maji. Eunike anacheka kidogo wakati anakumbatiana na Loisi, tate ya Timoteo. Anashangaa wakati Timoteo anazamishwa mu maji. Anaona vile maji inaruka wakati Timoteo anatoshwa mu maji na iko na furaha. Palepale anatokwa na machozi ya furaha. Hata kama haikukuwa mwepesi, Eunike alifundisha mutoto wake kumupenda Yehova na Mwana wake, Yesu Kristo. Ni magumu gani yenye alipambana nayo wakati alikuwa anafundisha mutoto wake?

2 Wazazi wa Timoteo hawakukuwa mu dini moya. Baba yake alikuwa Mugiriki, mama yake na tate yake walikuwa Wayahudi. (Mdo. 16:1) Inawezekana Timoteo alikuwa kijana wakati Eunike na Loisi walibadilisha dini yao na kuwa Wakristo. Lakini baba yake hakukuwa Mukristo. Sasa, Timoteo angeingia mu dini gani? Alipaswa kujiamulia juu hakukuwa mutoto. Angeingia mu dini ya baba yake? Angefuata desturi za Kiyahudi zenye alifundishwa wakati alikuwa angali mutoto? Ao angeamua kuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo?

3. Kulingana na Mezali 1:8, 9, Yehova anaona namna gani kazi yenye mama wako wanafanya juu ya kusaidia watoto wao wakuwe marafiki wake?

3 Mama Wakristo nao pia wanapendaka familia zao. Wanapendaka sana kusaidia watoto wao wakuwe na urafiki wa karibu pamoya na Yehova. Na Mungu wetu anasamini sana bidii yao. (Soma Mezali 1:8, 9.) Yehova alishasaidia mama wengi wafundishe watoto wao kweli.

4. Ni magumu gani yenye mama wako wanapambana nayo leo?

4 Wakati fulani, ni kawaida kwa mama kujiuliza ikiwa watoto wao watachagua kumutumikia Yehova sawa vile Timoteo alifanya. Kusema kweli, wazazi wanajua mikazo yenye watoto wao wako napambana nayo mu hii dunia yenye kutawaliwa na Shetani. (1 Pe. 5:8) Zaidi ya ile, mama wengi hawana bwana na wengine wako na bwana mwenye haiko muabudu wa Yehova. Na ile inafanya ikuwe nguvu kwao kukomalisha watoto muzuri. Kwa mufano, dada mwenye kuitwa Christine * anasema hivi: “Bwana yangu alikuwa baba muzuri, na alisimamia muzuri familia. Nilipenda watoto wetu wakuwe pia Mashahidi wa Yehova. Lakini bwana yangu alikatala kabisa. Kwa miaka mingi nilikuwa nalia na niko najiuliza kama kweli watoto wangu watafikia kuwa waabudu wa Yehova.”

5. Tutazungumuzia nini mu hii habari?

5 Kama uko mama Mukristo, unaweza kusaidia watoto wako, sawa vile Eunike. Mu hii habari, tutajifunza namna unaweza kuiga mufano wake kwa kufundisha watoto wako kupitia mambo yenye unasema na mambo yenye unafanya. Tutazungumuzia pia namna Yehova anaweza kukusaidia.

FUNDISHA WATOTO WAKO KUPITIA MAMBO YENYE UNASEMA

6. Vile 2 Timoteo 3:14, 15 inaonyesha, namna gani Timoteo alifikia kuwa Mukristo?

6 Wakati Timoteo alikuwa kijana mudogo, mama yake alifanya yake yote ili kumusaidia aelewe “maandishi matakatifu,” sawa vile Wayahudi waliielewa. Ni kweli Eunike hakujua mambo mingi juu hakujua kitu kuhusu Yesu Kristo. Lakini, mambo yenye Timoteo alijifunza mu Maandiko, ilikuwa musingi ya muzuri yenye ingemusaidia akuwe Mukristo. Sasa, angekuwa Mukristo kweli? Kwa kuwa alikuwa kijana, alikuwa na haki ya kuamua kama atakuwa Mukristo. Bila shaka, Timoteo alifikia “kusadikishwa kuamini” kweli kuhusu Yesu, juu mama yake alimusaidia pia. (Soma 2 Timoteo 3:14, 15.) Eunike alifurahi sana juu aliweza kufundisha mutoto wake kuhusu Yehova hata kama haikukuwa mwepesi! Eunike aliishi kabisa kulingana na jina yake, yenye inatokana na neno yenye inamaanisha “kushinda.”

7. Eunike angefanya nini ili kusaidia mutoto wake afanye maendeleo kisha ubatizo?

7 Ubatizo ni hatua ya maana yenye Timoteo alifikia mu maisha, lakini Eunike aliendelea tu kuhangaika juu ya maisha ya Timoteo. Timoteo angetumia namna gani maisha yake kisha ubatizo? Je, angeanza kushirikiana na marafiki wabaya? Angeenda ku masomo ya Atene, na kuanza kuamini mafundisho ya wafilozofe wapagani? Angepoteza wakati, nguvu, na ujana wake juu ya kutafuta utajiri? Eunike hangemukamatia Timoteo maamuzi, lakini angemusaidia tu akamate maamuzi ya hekima. Namna gani? Kwa kuendelea kumusaidia amupende sana Yehova na akuwe mwenye shukrani kwa Mwana Wake. Haiko tu wazazi wenye kuwa mu dini tofauti njo wanakuwaka na magumu ya kufundisha watoto wao wamupende Yehova. Hata kama wazazi wote wako mu kweli, inaweza tu kuwa nguvu kugusa mioyo ya vijana ili wafikie kuwa watumishi waaminifu wa Yehova. Mufano wa Eunike, unaweza kufundisha wazazi nini?

8. Namna gani mama anaweza kusaidia bwana yake Shahidi kuhangaikia mahitaji ya kiroho ya watoto wao?

8 Ujifunze Biblia pamoya na watoto wako. Dada, kama bwana yako iko Shahidi, Yehova anapenda umusaidie kuhangaikia mahitaji ya kiroho ya watoto wenu. Njia moya ya kufanya vile ni kuunga mukono kwa ukawaida programu ya Ibada ya Familia. Useme mambo ya muzuri juu ya Ibada ya Familia, na ufikirie ni nini unaweza kufanya juu ipite mu njia ya kufurahisha. Kwa mufano, unaweza kusaidia bwana yako kupanga programu fulani ya pekee ya kujifunza Biblia. Zaidi ya ile, kama inaomba kuanza kufundisha watoto fulani Biblia kipekee mu kitabu Furahia Maisha Milele! pengine unaweza kusaidiana na bwana yako kupanga namna watafikia kujifunza.

9. Mama mwenye kuwa na bwana mwenye haiko Shahidi, anaweza kupata wapi musaada?

9 Mama fulani wako na daraka ya kufundisha watoto wao Biblia juu wako nawachunga peke yao ao juu bwana zao hawako Mashahidi. Kama uko mu ile hali usihangaike sana. Yehova atakusaidia. Tumia vyombo vya kufundishia vyenye anatupatia kupitia tengenezo yake ili kujifunza na watoto wako. Unaweza pia kuuliza wazazi wenye kuwa na uzoefu juu ya namna wako natumia hivi vyombo mu ibada yao ya familia? * (Mez. 11:14) Yehova anaweza pia kukusaidia ujue namna ya kuzungumuza na watoto wako. Umuombe akusaidie kujua mambo yenye kuwa mu akili na mu moyo wao. (Mez. 20:5) Ulizo ya mwepesi sawa hii: ‘Ni jaribu gani ya nguvu sana yenye uko napata ku masomo?’ inaweza kukusaidia muanze mazungumuzo yenye itakusaidia ujue mambo mingi juu ya mutoto wako.

10. Ni mu njia gani ingine unaweza kusaidia watoto wako wajifunze juu ya Yehova?

10 Utafute nafasi mbalimbali za kufundisha watoto wako kumuhusu Yehova. Ambia watoto wako juu ya Yehova na juu ya mambo mingi yenye alishakufanyia. (Kum. 6:6, 7; Isa. 63:7) Ile ni ya lazima zaidi kama hauwezi kujifunza nao kwa ukawaida ku nyumba. Christine, mwenye tulishataya anasema hivi: “Sikukuwa na nafasi mingi za kuzungumuzia mambo ya kiroho, kwa hiyo nilikuwa nafanya vile wakati wowote wenye tulijikuta pamoya. Tulikuwa natembea ao kutembeza mutumbwi na tuko nazungumuzia kuhusu uumbaji wa Yehova wa ajabu na kuhusu mambo mingi ya kiroho. Wakati watoto wangu walikomala, niliwatia moyo waanze kujifunza Biblia wao peke.” Tena, uzungumuzie mambo ya muzuri juu ya tengenezo ya Yehova na juu ya ndugu na dada. Usichambue wazee. Mambo yenye uko nasema juu yao inaweza kufanya watoto wako wawaendee ao wasiwaendee wakati wako na lazima yao.

11. Kulingana na Yakobo 3:18, juu ya nini ni jambo ya lazima kufanya mu nyumba yako mukuwe amani?

11 Ufanye mu nyumba yako mukuwe amani. Onyesha bwana yako na watoto wako upendo kwa ukawaida. Zungumuza kuhusu bwana yako kwa fazili na kwa heshima, na uzoeze watoto wako wakuwe nafanya vile. Kama unafanya vile, utafanya kukuwe hali ya amani yenye itasaidia watoto wako wajifunze juu ya Yehova. (Soma Yakobo 3:18.) Fikiria mufano wa Jozsef, painia wa pekee mu Romania. Wakati alikuwa nakomala, baba yake alifanya ikuwe nguvu sana kwake, kwa mama yake, kwa dada yake mukubwa, na kwa wadogo wake wawili kumutumikia Yehova. Jozsef anasema hivi: “Mama yangu alikuwa najikaza sana juu ya kufanya mu nyumba yetu mukuwe amani. Kadiri baba yangu alikuwa mukali, ni vile mama yangu alitenda kwa fazili. Wakati aliona kama tunaanza kushindwa kuheshimia na kutii baba yetu, alikuwa natusomea Waefeso 6:1-3. Kisha alikuwa natuelezea kuhusu sifa za muzuri za baba yetu na alikuwa natusaidia tuelewe juu ya nini tunapaswa kumupenda. Ni vile alikuwa nafanya juu ya kutuliza hali mbalimbali zenye zingefanya kukuwe muvurugo mu familia.”

FUNDISHA WATOTO WAKO KUPITIA MAMBO YENYE UNAFANYA

12. Kulingana na 2 Timoteo 1:5, mufano wa Eunike ulimusaidia namna gani Timoteo?

12 Soma 2 Timoteo 1:5. Eunike alimuwekea Timoteo mufano muzuri. Inawezekana alimufundisha kama imani ya kweli inaonekana kupitia matendo. (Yak. 2:26) Bila shaka, Timoteo aliona kama matendo ya mama yake ilichochewa na upendo wa nguvu wenye alikuwa nao kwa Yehova. Kwa kweli, Timoteo alikuwa hakika kama mama yake alikuwa na furaha juu alikuwa namutumikia Yehova. Mufano wa Eunike ulimusaidia namna gani Timoteo? Sawa vile mutume Paulo alionyesha, Timoteo alikuwa na imani ya nguvu sawa mama yake. Timoteo hakupata ile imani ya nguvu kwa muujiza. Aliona mufano wa mama yake na akaamua kumuiga. Vilevile leo, mama wengi walishasaidia “bila neno,” watu wa familia yao wamutumikie Yehova. (1 Pe. 3:1, 2) Na weye unaweza. Namna gani?

13. Juu ya nini mama anapaswa kutia pa nafasi ya kwanza urafiki wake pamoya na Yehova?

13 Tia pa nafasi ya kwanza urafiki wako pamoya na Yehova. (Kum. 6:5, 6) Sawa vile mama wengi, uko najitolea sana. Unatoaka vitu sawa vile, wakati, makuta, na hata wakati ingine unakosa usingizi, juu ya kuhangaikia mahitaji ya kimwili ya watoto wako. Lakini haupaswe kutumika sana juu ya kuhangaikia ile mambo hivi kwamba unakosa na wakati wa kufanya urafiki wako pamoya na Yehova ukuwe nguvu. Panga kwa ukawaida wakati kwa ajili ya sala, funzo ya Biblia ya kipekee na kwa ajili ya mikutano ya kutaniko. Ukifanya vile, utakuwa nguvu kiroho na utawekea mufano muzuri familia yako na hata watu wengine.

14-15. Mufano wa Leanne, Maria, na João unakufundisha nini?

14 Fikiria mifano fulani ya vijana wenye walijifunza kumupenda Yehova na kumutumainia kwa kuona mufano wa mama zao. Leanne, mutoto mwanamuke wa Christine anasema hivi: “Hatukukuwa najifunza Biblia wakati baba alikuwa ku nyumba. Lakini mama hakukuwa nakosa mikutano. Matendo yake ilifanya tukuwe na imani ya nguvu hata kama hatukujua mambo mingi juu ya Biblia. Hata mbele tuanze kukusanyika, tulijua kama Mashahidi wa Yehova wanafundishaka kweli.”

15 Maria, mwenye baba yake, wakati fulani alikuwa napatia watu wa familia yake malipizi juu walikusanyika, anasema hivi: “Mama yangu iko kati ya dada wenye kuwa na uhodari sana wenye najua. Wakati nilikuwa mutoto, wakati fulani nilikuwa nakatala kufanya mambo fulani juu nilikuwa naogopa mambo yenye wengine wangesema. Lakini kuona uhodari wenye mama alikuwa nao, na namna sikuzote alikuwa namutia Yehova pa nafasi ya kwanza mu maisha yake, kulinisaidia nisikuwe naogopa tena watu.” João, mwenye baba yake alikataza watu wa familia yake kuzungumuzia mambo ya kiroho ku nyumba, anasema hivi: “Nawaza kitu yenye ilinigusa moyo sana ni kuona namna mama alikuwa tayari kuacha kila kitu juu ya kumufurahisha baba. Lakini kitu yenye hakuacha ni kumupenda Yehova.”

16. Namna gani mama mwenye kuwa mufano muzuri anaweza kusaidia wengine?

16 Mama, kumbuka kama mufano wako unaweza kusaidia wengine. Namna gani? Fikiria namna mufano wa Eunike ulimusaidia mutume Paulo. Aliandika kama imani ya Timoteo yenye haikukuwa na unafiki, “ilikaa kwanza ndani ya . . . Eunike.” (2 Ti. 1:5) Ni wakati gani mutume Paulo aliona imani ya Eunike kwa mara ya kwanza? Inawezekana ni mu safari yake ya kwanza ya umisionere njo alikutana na Loisi na Eunike mu muji wa Listra, na inawezekana aliwasaidia wakuwe Wakristo. (Mdo. 14:4-18) Waza kidogo: Wakati alimuandikia Timoteo, kisha miaka 15 hivi, Paulo alikuwa angali anakumbuka matendo ya uaminifu ya Eunike na alionyesha kama Eunike alikuwa mufano muzuri wa kuiga! Kusema kweli, mufano wa Eunike ulimutia sana moyo mutume Paulo na inawezekana ulitia moyo hata Wakristo wengine wengi wa ile wakati. Kama uko nakomalisha watoto weye peke ao kama bwana ao bibi yako haiko Shahidi, ukuwe hakika kama mufano wako wa uaminifu uko nachochea na kutia moyo wengine.

Kusaidia mutoto akomale kiroho kunaomba wakati. Usichoke! (Ona fungu ya 17)

17. Unaweza kufanya nini kama mutoto wako hapendi kumutumikia Yehova hata kama uko najikaza sana kumusaidia?

17 Unaweza kufanya nini kama mutoto wako hapendi kumutumikia Yehova hata kama uko najikaza sana ili kumusaidia? Kumbuka kama kuzoeza mutoto inaomba wakati. Sawa vile picha inaonyesha, wakati unapanda mbegu fulani, wakati fulani unaweza kujiuliza kama ile mbegu itakomala na kuwa mumea wenye utatokeza matunda ao hapana. Hata kama haujue ikiwa ule mumea utatokeza matunda ao hapana, utaendelea kuumwangia maji juu ukomale. (Mk. 4:26-29) Vilevile, vile uko mama, wakati fulani unaweza kujiuliza ikiwa uko nagusa kabisa moyo wa watoto wako. Hauwezi kujua maamuzi yenye watoto wako watakamata. Lakini kama unaendelea kufanya yako yote ili kuwazoeza, utawapatia nafasi ya kuwa marafiki wa Mungu.​—Mez. 22:6.

TEGEMEA MUSAADA WA YEHOVA

18. Yehova anaweza kufanya nini ili kusaidia watoto wako wakomale kiroho?

18 Tangu zamani, Yehova amesaidia vijana wengi sana wakuwe marafiki wake. (Zb. 22:9, 10) Anaweza pia kusaidia watoto wako wakomale kiroho kama wanapenda kufanya vile. (1 Ko. 3:6, 7) Hata kama watoto wako hawamutumikie Yehova kwa ukamili, ataendelea kuwapenda. (Zb. 11:4) Wakati wanaonyesha hata alama kidogo ya “mwelekeo wenye kufaa,” Yehova atawasaidia wakuwe marafiki wake. (Mdo. 13:48; 2 Ny. 16:9) Anaweza kukusaidia useme jambo yenye kufaa kwa wakati wenye kufaa, wakati watoto wako wako na lazima sana ya kusikia ile jambo. (Mez. 15:23) Ao anaweza kuchochea ndugu ao dada mu kutaniko awahangaikie mu njia ya pekee. Hata wakati watoto wako watakuwa wakubwa, Yehova anaweza kuwakumbusha jambo fulani yenye uliwafundishaka zamani. (Yoh. 14:26) Yehova atakubariki kama unaendelea kuzoeza watoto wako kupitia maneno na mufano wako.

19. Ni nini inaweza kufanya ukuwe hakika kama Yehova anakukubali?

19 Yehova anakupenda, haiko juu ya maamuzi yenye watoto wako wanaweza kukamata, lakini anakupenda juu unamupenda. Kama uko nachunga watoto weye peke, Yehova anaahidi kama atakuwa Baba ya watoto wako na mulinzi wako. (Zb. 68:5) Hauwezi kujua ikiwa watoto wako watachagua kumutumikia Yehova ao hapana. Lakini kama unaendelea kutegemea musaada wa Yehova na kufanya yako yote, atakukubali.

WIMBO 134 Watoto Ni Zawadi Yenye Mungu Anatupatia

^ fu. 5 Hii habari inazungumuzia mambo yenye mama Wakristo wanaweza kujifunza kupitia mufano wa mama ya Timoteo, Eunike, na namna wanaweza kusaidia watoto wao wafikie kumujua na kumupenda Yehova.

^ fu. 4 Majina fulani imebadilishwa.

^ fu. 9 Kwa mufano, ona somo ya 50 yenye kuwa mu kitabu Furahia Maisha Milele! na habari yenye kichwa, “Mapendekezo ya Kufanya Ibada ya Familia na Funzo la Kibinafsi,” yenye kuwa mu Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 8, 2011, uku. 6-7.