Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Ikiwa Mkristo atamtaliki mke wake bila msingi wa Kimaandiko na kufunga ndoa na mtu mwingine, kutaniko litaonaje ndoa yake ya mwanzoni na ndoa yake mpya?

Katika hali hiyo, kutaniko litaona kwamba ndoa ya kwanza ilikwisha mwanamume huyo alipofunga ndoa nyingine, na litaona ndoa yake mpya kuwa halali. Ili kuelewa sababu ya msimamo huo, acheni tuchunguze jambo ambalo Yesu alisema kuhusu talaka na kufunga ndoa tena.

Kama inavyotajwa kwenye Mathayo 19:9, Yesu alitoa msingi pekee wa Kimaandiko wa kutalikiana. Alisema hivi: “Mtu yeyote anayemtaliki mke wake isipokuwa kwa sababu ya uasherati, na kumwoa mwingine, anafanya uzinzi.” Kutokana na maneno ya Yesu, tunajifunza (1) kwamba uasherati ndio msingi pekee wa Kimaandiko wa kutalikiana na (2) kwamba mwanamume anayemtaliki mke wake bila msingi huo wa Kimaandiko na kumwoa mwanamke mwingine anafanya uzinzi. *

Je, maneno ya Yesu yanamaanisha kwamba mwanamume anayefanya uasherati na kumtaliki mke wake yuko huru Kimaandiko kufunga ndoa tena? Si mara zote. Mume anapofanya uzinzi, mwenzi asiye na hatia anaweza kuamua ikiwa atamsamehe mume wake au hatamsamehe. Akikataa kumsamehe, kisha watalikiane kisheria, wote wawili wako huru kufunga ndoa baada ya talaka kukamilishwa.

Kwa upande mwingine, huenda mwenzi asiye na hatia akatamani sana kudumisha ndoa yake na hivyo kumwambia mume wake kwamba yuko tayari kumsamehe. Hata hivyo, namna gani ikiwa mume aliyefanya uzinzi hakubaliani na uamuzi wa mke wake na anatafuta talaka ya kisheria bila kumhusisha mke wake? Kwa kuwa mke wake yuko tayari kumsamehe na kuendelea na ndoa, mume huyo hatakuwa huru Kimaandiko kufunga ndoa tena. Akisisitiza kwamba atafunga ndoa na mtu mwingine bila kuwa huru Kimaandiko, anafanya uzinzi tena, na hivyo kutaniko litahitaji kumchukulia hatua ya kihukumu.​—1 Kor. 5:1, 2; 6:9, 10.

Ikiwa mwanamume ambaye hayuko huru Kimaandiko anafunga ndoa tena, kutaniko litaonaje ndoa yake ya mwanzoni na ndoa yake mpya? Je, bado ndoa yake ya mwanzoni ni halali Kimaandiko? Je, bado mwenzi asiye na hatia anaweza kuamua kumsamehe au kumkataa yule aliyekuwa mume wake? Je, ndoa mpya itaonwa kuwa ndoa ya uzinzi?

Zamani, kutaniko liliiona ndoa mpya kuwa ndoa ya uzinzi maadamu mwenzi asiye na hatia yuko hai, hajafunga ndoa tena, na hana hatia ya kufanya uasherati. Hata hivyo, Yesu hakumtaja mwenzi asiye na hatia alipozungumzia talaka na kufunga ndoa tena. Badala yake, alieleza kwamba mwanamume anayetoa talaka bila msingi wa Kimaandiko na kumwoa mwanamke mwingine, anafanya uzinzi. Katika kisa hicho, talaka na ndoa mpya, ambayo Yesu aliilinganisha na uzinzi, inakomesha ndoa ya mwanzoni.

“Mtu yeyote anayemtaliki mke wake isipokuwa kwa sababu ya uasherati, na kumwoa mwingine, anafanya uzinzi.”​—Mt. 19:9

Ndoa inapokwisha kwa sababu ya talaka na mume kufunga ndoa tena, haiwezekani tena kwa mwenzi asiye na hatia kumsamehe au kukataa kumsamehe yule aliyekuwa mume wake. Hivyo, hatalazimika kufanya uamuzi mgumu wa kuamua kumsamehe au kukataa kumsamehe yule aliyekuwa mume wake. Isitoshe, maoni ya kutaniko kuelekea ndoa hiyo mpya hayatategemea ikiwa mwenzi asiye na hatia amekufa, amefunga ndoa tena, au ana hatia ya kufanya uasherati. *

Katika mfano uliotajwa hapo juu, mume alifanya uzinzi kisha akatalikiana na mke wake. Namna gani ikiwa mume hakufanya uzinzi bali alitafuta talaka kisha akafunga ndoa tena? Au namna gani ikiwa mume hakufanya uasherati kabla ya talaka, lakini alifanya uasherati baada ya talaka, kisha akafunga ndoa nyingine ingawa mke wake alikuwa tayari kumsamehe? Katika visa hivyo vyote, talaka na kufunga ndoa tena, ambako ni sawa na kufanya uzinzi, kunakomesha ndoa ya mwanzoni. Ndoa hiyo mpya ni muungano ulio halali kisheria. Kama ilivyotajwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Kiingereza la Novemba 15, 1979, kwenye ukurasa wa 32, “sasa ameingia katika ndoa mpya na hivyo hawezi tu kuivunja na kumrudia mke wake wa zamani; ndoa ya kwanza ilikwisha baada ya talaka, uzinzi, na kufunga ndoa nyingine.”

Uelewaji huu uliorekebishwa haupuuzi utakatifu wa ndoa au kupunguza uzito wa kufanya uzinzi. Mwanamume anayemtaliki mke wake bila msingi wa Kimaandiko na kumwoa mwanamke mwingine bila kuwa huru kufanya hivyo Kimaandiko, atachukuliwa hatua ya kihukumu kwa hatia ya kosa la uzinzi. (Ikiwa mwenzi mpya wa ndoa ni Mkristo, yeye pia atachukuliwa hatua ya kihukumu kwa hatia ya kosa la uzinzi.) Ingawa ndoa hiyo mpya haitaonwa kuwa ya uzinzi, mwanamume huyo hatastahili kupewa mapendeleo ya pekee ya utumishi kutanikoni kwa miaka mingi, na hadi maoni ya watu yawe yamebadilika kumwelekea kwa sababu ya suto iliyosababishwa na makosa yake ya zamani. Wazee watachunguza pia hali ya sasa ya mwenzi wake wa zamani ambaye huenda alitendewa kwa hila, na hali ya watoto wadogo ambao huenda waliachwa na mwenzi mwenye hatia.​—Mal. 2:14-16.

Kwa sababu ya matokeo mabaya sana ya talaka isiyo ya Kimaandiko na kufunga ndoa nyingine, kwa hekima Wakristo wanasitawisha maoni ya Yehova kwa kudumisha utakatifu wa mpango wa ndoa.​—Mhu. 5:4, 5; Ebr. 13:4.

^ Ili kurahisisha mambo, tutamzungumzia mwenzi anayefanya uzinzi kuwa mwanamume na mwenzi asiye na hatia kuwa mwanamke. Hata hivyo, kama ilivyoandikwa kwenye Marko 10:11, 12, Yesu alionyesha wazi kwamba shauri hilo linawahusu wanaume na wanawake pia.

^ Hili linabadili uelewaji wetu wa zamani kwamba ndoa kama hiyo itaonwa kuwa ndoa ya uzinzi mpaka mwenzi asiye na hatia afe, afunge ndoa tena, au awe na hatia ya kufanya uasherati.