Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 16

Pata Shangwe kwa Kumpa Yehova Kilicho Bora Kulingana na Uwezo Wako

Pata Shangwe kwa Kumpa Yehova Kilicho Bora Kulingana na Uwezo Wako

“Kila mmoja na achunguze matendo yake mwenyewe.”​—GAL. 6:4.

WIMBO 37 Kumtumikia Yehova kwa Nafsi Yote

MUHTASARI *

1. Ni nini kinachotupatia shangwe nyingi?

 YEHOVA anataka tuwe na furaha. Tunajua hilo kwa sababu shangwe ni mojawapo ya sifa za tunda la roho yake takatifu. (Gal. 5:22) Kwa kuwa kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea, tunapata shangwe nyingi tunaposhiriki kikamili katika huduma ya Kikristo na kuwasaidia ndugu zetu katika njia mbalimbali.​—Mdo. 20:35.

2-3. (a) Kama inavyoonyeshwa kwenye Wagalatia 6:4, ni mambo gani mawili yanayoweza kutusaidia kuwa na shangwe katika utumishi wa Yehova? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

2 Kama inavyoonyeshwa kwenye Wagalatia 6:4, mtume Paulo anataja mambo mawili yanayoweza kutusaidia kuendelea kuwa na shangwe. (Soma.) Kwanza, lengo letu linapaswa kuwa kumpa Yehova kilicho bora kulingana na uwezo wetu. Ikiwa tunampa kilicho bora kabisa kulingana na uwezo wetu, tunapaswa kuwa na furaha. (Mt. 22:36-38) Pili, tunapaswa kuepuka kujilinganisha na wengine. Tunapaswa kumshukuru Yehova kwa mambo yote tunayoweza kutimiza kulingana na afya yetu, mazoezi tuliyopata, au vipawa vyetu. Isitoshe, kila kitu tulicho nacho tumepata kutoka kwake. Kwa upande mwingine, ikiwa wengine wanapata matokeo zaidi kuliko sisi katika aina fulani ya huduma, tunapaswa kushangilia kwamba wanatumia vipawa vyao kumsifu Yehova, na si kwa masilahi yao wenyewe au sababu za kibinafsi. Hivyo, badala ya kushindana nao, tunapaswa kujifunza kutoka kwao.

3 Katika makala hii, tutaona jambo linaloweza kutusaidia tunapohisi kwamba hatuwezi kutimiza mengi katika utumishi wetu. Pia, tutachunguza jinsi tunavyoweza kutumia kwa njia nzuri kabisa zawadi zozote ambazo huenda tunazo, na mambo tunayoweza kujifunza kwa kuiga mifano ya wengine.

TUNAPOHISI HATUWEZI KUTIMIZA MENGI

Kufanya yote tunayoweza katika kila hatua ya maisha yetu humfurahisha Yehova (Tazama fungu la 4 hadi 6) *

4. Ni hali gani inayoweza kutufanya tuvunjike moyo? Toa mfano.

4 Ni vigumu kwa baadhi ya watumishi wa Yehova kuzoea hali zinazowazuia kutimiza mengi, ambazo zinasababishwa na kusonga kwa umri au afya mbaya. Carol alipitia hali hiyo. Wakati fulani alikuwa na pendeleo la kutumikia katika eneo lenye uhitaji. Wakati huo, aliongoza mafunzo ya Biblia 35 na aliwasaidia watu kadhaa kufanya maendeleo na kufikia hatua ya kujiweka wakfu na kubatizwa. Carol alikuwa na matokeo mazuri katika huduma! Baadaye afya yake ilizorota, na alihitaji kukaa nyumbani karibu muda wote. Carol anasema hivi: “Ninajua kwamba kwa sababu ya matatizo ya afya, siwezi kufanya mambo ambayo wengine wanaweza kufanya, lakini ninahisi kwamba mimi si mwaminifu kama wao. Siwezi kufanya mambo yote ninayotaka, na hilo linanivunja moyo.” Carol anataka kufanya yote anayoweza kwa ajili ya Yehova. Kwa kweli, anastahili pongezi! Tunaweza kuwa na hakika kwamba Mungu wetu mwenye upendo anathamini roho yake nzuri.

5. (a) Tunapaswa kukumbuka nini ikiwa tunavunjika moyo kwa sababu hatuwezi kufanya mengi? (b) Kama picha zinavyoonyesha, ndugu huyo ameendeleaje kutoa kilicho bora kulingana na uwezo wake katika utumishi wa Yehova?

5 Ikiwa nyakati nyingine unavunjika moyo kwa sababu huwezi kufanya mengi kama ilivyokuwa awali, jiulize hivi, ‘Yehova anataka nifanye nini?’ Nifanye yote niwezayo kulingana na hali zangu za sasa. Fikiria kisa hiki: Dada aliye na umri wa miaka 80 anahisi kuvunjika moyo kwa sababu hawezi kufanya mengi katika huduma kama alivyofanya alipokuwa na umri wa miaka 40. Anafikiri kwamba hata ingawa anatoa kilicho bora kulingana na uwezo wake, bado hamfurahishi Yehova. Je, hilo ni kweli? Hebu wazia. Ikiwa dada huyo alitoa kilicho bora kulingana na uwezo wake alipokuwa na umri wa miaka 40 na bado anatoa kilicho bora kulingana na uwezo wake akiwa na umri wa miaka 80, basi hajaacha kamwe kutoa kilicho bora kulingana na uwezo wake. Ikiwa tunaanza kuhisi kwamba kiwango chetu cha utumishi ni kidogo na hatuwezi kumfurahisha Yehova, tunahitaji kukumbuka kwamba Yehova ndiye anayeweka kiwango cha mambo yanayomfurahisha. Ikiwa tunafanya yote tunayoweza, Yehova atafurahishwa nasi na kusema: “Vema!”​—Linganisha Mathayo 25:20-23.

6. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Maria?

6 Itakuwa rahisi zaidi kuwa na shangwe, ikiwa tutakazia fikira mambo tunayoweza kutimiza badala ya mambo tusiyoweza kutimiza. Mfikirie dada anayeitwa Maria, mwenye ugonjwa unaomzuia kufanya mengi katika huduma. Mwanzoni, alishuka moyo na kujihisi hafai. Lakini baadaye alimfikiria dada kutanikoni aliyekuwa hawezi kutoka kitandani na akaamua kumsaidia. Maria anasema hivi: “Nilifanya mpango wa kuhubiri naye kwa simu na kuandika barua. Kila wakati nilipohubiri naye, nilirudi nyumbani nikiwa mwenye furaha na kuridhika kwamba nilifaulu kumsaidia dada yangu.” Sisi pia tunaweza kuongeza shangwe yetu tunapokazia fikira mambo tunayoweza kutimiza, badala ya kufikiria mambo ambayo hatuwezi kutimiza. Lakini namna gani ikiwa tunaweza kufanya mengi zaidi au tunafanya vizuri katika aina fulani ya utumishi wa Yehova?

IKIWA UNA ZAWADI​—‘ITUMIE’!

7. Mtume Petro aliwapa shauri gani hususa Wakristo?

7 Katika barua yake ya kwanza, mtume Petro aliwahimiza ndugu zake watumie zawadi na vipawa vyote walivyokuwa navyo ili kuwajenga waamini wenzao. Petro aliandika hivi: “Kwa kadiri ambayo kila mmoja amepokea zawadi, itumieni kuhudumiana kama wasimamizi wazuri wa fadhili zisizostahiliwa za Mungu.” (1 Pet. 4:10) Hatupaswi kuogopa kutumia kikamili zawadi zetu na kuhisi kwamba huenda wengine watatuonea wivu au watavunjika moyo. Ikiwa tutafanya hivyo, hatutakuwa tukimpa Yehova kilicho bora kulingana na uwezo wetu.

8. Kulingana na 1 Wakorintho 4:6, 7, kwa nini tunapaswa kuepuka kujisifu kuhusu zawadi zetu?

8 Tunahitaji kutumia zawadi zetu kikamili, lakini ni lazima tuwe makini tusijisifu kwa sababu ya zawadi tulizo nazo. (Soma 1 Wakorintho 4:6, 7.) Kwa mfano, huenda ukawa na matokeo mazuri inapohusu kuanzisha funzo la Biblia. Usisite kutumia zawadi hiyo! Lakini kuna tofauti kati ya kutumia zawadi, na kujisifu kuhusiana na zawadi hiyo. Tuseme kwamba hivi karibuni ulijionea jambo zuri katika huduma lililotokana na kuanzisha funzo la Biblia. Unatamani kuwaambia walio kwenye kikundi chako cha utumishi kuhusu jambo hilo. Hata hivyo unapokutana nao, unamsikia dada akisimulia kuhusu mazungumzo aliyofanya na mwenye nyumba yaliyomwezesha kumwachia gazeti. Yeye alimwachia mwenye nyumba gazeti; wewe ulianzisha funzo la Biblia. Utafanya nini? Unajua kwamba kikundi kitatiwa moyo na jambo ulilojionea, lakini huenda ukaamua kusubiri wakati mwingine unaofaa ili usimulie jambo hilo, na hivyo usipunguze shangwe ya dada yako aliyemwachia mwenye nyumba gazeti. Hilo ni tendo la fadhili. Hata hivyo, kwa vyovyote vile usiache kuanzisha mafunzo ya Biblia. Una zawadi​—itumie!

9. Tunapaswa kutumiaje zawadi tulizo nazo?

9 Tunapaswa kukumbuka kwamba vipawa vyovyote ambavyo huenda tukawa navyo ni zawadi kutoka kwa Mungu. Tunapaswa kutumia zawadi hizo kuliimarisha kutaniko, na si kujitafutia sifa. (Flp. 2:3) Tunapotumia nguvu na uwezo wetu ili kufanya mapenzi ya Mungu, tutakuwa na sababu ya kushangilia​—si kwa sababu tunashindana na wengine au kuthibitisha kwamba sisi ni bora kuliko wao, bali kwa sababu tunatumia zawadi zetu ili kumletea sifa Yehova.

10. Kwa nini hatupaswi kujilinganisha na wengine?

10 Mtu asipokuwa mwangalifu, anaweza kuanguka kwenye mtego wa kulinganisha vipawa vyake na mapungufu ya mtu mwingine. Kwa mfano, huenda ndugu ana uwezo wa kutoa hotuba nzuri sana. Hicho ni kipawa chake. Hata hivyo, moyoni mwake huenda akamdharau ndugu ambaye si mtoaji mzuri wa hotuba. Lakini huenda ndugu huyo anafanya vizuri sana katika ukaribishaji wageni, kuwazoeza watoto wake, au ni mwenye bidii katika huduma. Tunathamini sana kwamba tuna ndugu na dada wengi wenye vipawa mbalimbali wanaotumia zawadi zao kumtumikia Yehova na kuwasaidia wengine!

JIFUNZE KUTOKANA NA MFANO WA WENGINE

11. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kufuata mfano wa Yesu?

11 Ingawa tunapaswa kuepuka kujilinganisha na wengine, tunaweza kunufaika kwa kujifunza kutokana na mifano ya watumishi waaminifu wa Yehova. Acheni tuchunguze mfano wa Yesu. Hata ingawa alikuwa mkamilifu, tunaweza kujifunza kutokana na sifa zake maridadi na mambo mazuri aliyofanya. (1 Pet. 2:21) Tunapojitahidi kabisa kufuata mfano wake kwa ukaribu kadiri tunavyoweza, tutakuwa watumishi bora wa Yehova na wenye matokeo zaidi katika huduma yetu.

12-13. Tunaweza kujifunza nini kutoka kwa Mfalme Daudi?

12 Katika Neno la Mungu, tunapata mifano mingi ya wanaume na wanawake waaminifu ambao tunaweza kuiga mfano wao, ingawa hawakuwa wakamilifu. (Ebr. 6:12) Mfikirie Mfalme Daudi ambaye Yehova alimwita “mtu anayeupendeza moyo wangu.” (Mdo. 13:22) Ingawa hivyo, Daudi hakuwa mkamilifu. Isitoshe, alifanya dhambi nzito sana. Pamoja na hayo, yeye ni mfano mzuri kwetu. Kwa nini? Kwa sababu aliporekebishwa hakujaribu kujitetea. Badala yake, alikubali shauri zito alilopewa, naye akajutia kutoka moyoni jambo alilokuwa amefanya. Kwa sababu hiyo, Yehova alimsamehe.​—Zab. 51:3, 4, 10-12.

13 Tunaweza kujifunza kutoka kwa Daudi kwa kujiuliza hivi: ‘Ninatendaje ninapopewa shauri? Je, ninakubali haraka makosa yangu, au ninajaribu kujitetea? Je, mimi ni mwepesi wa kuwalaumu wengine? Je, ninajitahidi kufanya yote ninayoweza ili nisirudie makosa yangu?’ Unaweza kujiuliza maswali kama hayo unaposoma masimulizi ya wanaume na wanawake wengine waaminifu katika Biblia. Je, walipitia changamoto kama unazopitia? Walionyesha sifa gani nzuri? Katika kila kisa jiulize: ‘Ninaweza kumwigaje mtumishi huyu mshikamanifu wa Yehova?’

14. Tunaweza kunufaikaje kwa kuwatazama waamini wenzetu?

14 Pia, tunaweza kunufaika kwa kuwatazama waabudu wenzetu, iwe ni vijana au wenye umri mkubwa. Kwa mfano, je, unaweza kumfikiria mtu fulani katika kutaniko lenu ambaye kwa uaminifu anavumilia jaribu—labda anashinikizwa na wengine, anapata upinzani kutoka kwa watu wa familia, au ana afya mbaya? Je, unaona sifa fulani nzuri katika mtu huyo ambazo ungependa kusitawisha kwa kadiri kubwa zaidi? Kwa kuchunguza mfano wake mzuri, huenda ukajifunza njia hususa za kuvumilia majaribu yako mwenyewe. Tunashukuru sana kuwa na mifano halisi ya imani ambayo tunaweza kuiga—kwa kweli tuna sababu ya kushangilia!​—Ebr. 13:7; Yak. 1:2, 3.

FURAHIA UTUMISHI WAKO KWA YEHOVA

15. Mtume Paulo alitoa shauri gani linaloweza kutusaidia kuendelea kushangilia katika utumishi wetu kwa Yehova?

15 Ili kudumisha amani na umoja kutanikoni, kila mmoja wetu anahitaji kufanya yote anayoweza kulingana na uwezo wake. Wafikirie Wakristo wa karne ya kwanza. Walikuwa na zawadi na migawo mbalimbali. (1 Kor. 12:4, 7-11) Lakini jambo hilo halikuwafanya wawe na mashindano na migawanyiko. Badala yake, mtume Paulo alimhimiza kila mmoja kufanya mambo yaliyohitajika ili “kuujenga mwili wa Kristo.” Paulo aliwaandikia hivi Waefeso: “Kila kiungo kinapofanya kazi vizuri, hilo linafanya mwili ukue na kujijenga katika upendo.” (Efe. 4:1-3, 11, 12, 16) Wale waliofanya hivyo, walichangia amani na umoja​—sifa ambazo tunaona katika makutaniko yetu leo.

16. Tunapaswa kuazimia kufanya nini? (Waebrania 6:10)

16 Azimia kuepuka kujilinganisha na wengine. Badala yake, jifunze kutoka kwa Yesu, na ujitahidi kuiga sifa zake. Iga mifano ya imani ya watu wanaotajwa katika Biblia na ya nyakati zetu. Unapoendelea kufanya yote unayoweza, uwe na uhakika kwamba Yehova “hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi [yako].” (Soma Waebrania 6:10.) Endelea kushangilia katika utumishi wa Yehova, ukijua kwamba anathamini jitihada zako za moyo wote za kumfurahisha yeye.

WIMBO 65 Songa Mbele!

^ Sisi sote tunaweza kunufaika kwa kuchunguza mifano inayowekwa na wengine. Hata hivyo, kuna hatari ambazo tunapaswa kuepuka. Makala hii, itatusaidia kudumisha shangwe yetu na kuepuka mtego wa kuwa na kiburi au kuvunjika moyo tunapofikiria mambo ambayo wengine wanaweza kutimiza.

^ MAELEZO YA PICHA: Ndugu alitumikia Betheli alipokuwa kijana. Kisha akafunga ndoa na kufanya upainia pamoja na mke wake. Baada ya kupata watoto, aliwazoeza katika huduma. Sasa akiwa na umri mkubwa, anaendelea kufanya yote anayoweza kulingana na uwezo wake, akitoa ushahidi kwa kuandika barua.