Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI JUU YA MAISHA YA WATU

Nimefurahia Kujifunza na Kufundisha Wengine Juu ya Yehova

Nimefurahia Kujifunza na Kufundisha Wengine Juu ya Yehova

WAKATI nilikuwa nakomalia mu Easton, Pennsylvania, Amerika, nilipenda sana kuenda ku masomo ya juu sababu nilipenda kuwa mutu wa maana sana. Nilipenda sana masomo na nilikuwa naweza matematike na sayansi. Mu mwaka wa 1956, tengenezo ya kutetea haki za watu ilinipatia dolare 25 juu miye njo niliweza sana kati ya wanafunzi weusi. Kisha, miradi yangu ilibadilika. Juu ya nini?

NAMNA NILIJIFUNZA JUU YA YEHOVA

Wakati kidogo kisha mwaka wa 1940, wazazi wangu walikuwa wanajifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Hata kama hawakuendelea kujifunza Biblia, mama yangu aliendelea kupokea magazeti Munara wa Mulinzi na Amuka! Mu mwaka wa 1950, mukusanyiko wa kimataifa ulifanywa mu muji wa New York, na familia yangu ilikubali kukusanyika.

Wakati kidogo kisha pale, Ndugu Lawrence Jeffries alianza kututembelea. Alijikaza kunisaidia nijifunze kweli. Ku mwanzo, sikukubaliana na musimamo wa Mashahidi wa Yehova, ni kusema, kutounga mukono mambo ya politike na kutokuwa maaskari. Nilimuambia kama, ikiwa kila mutu mu Amerika anakatala kuenda ku vita, maadui wanaweza kuya na kukamata inchi yetu. Kwa uvumilivu, ndugu Jeffries alifikiri na miye hivi: “Unawaza Yehova anaweza kufanya nini kama watu wote mu Amerika wangekuwa namutumikia na maadui wanakuya kuwashambulia?” Mawazo yake juu ya ile jambo na mambo ingine ilinisaidia nione kama mawazo yangu haikukuwa na musingi. Ile ilifanya nipende zaidi kujifunza kweli ya Biblia.

Siku yenye nilibatizwa

Nilipitisha wakati mingi na niko nasoma magazeti ya zamani ya Munara wa Mulinzi na Amuka! yenye mama yangu aliwekaka mu chumba yenye tulikuwa nawekea vitu. Kisha, nilifikia kutambua kama mambo yenye nilijifunza ilikuwa kweli, njo maana nilikubali kujifunza Biblia pamoya na Ndugu Jeffries. Nilianza pia kuenda ku mikutano kwa ukawaida. Nilipenda sana mambo yenye nilikuwa najifunza, na nikafikia kuwa muhubiri wa habari njema. Miradi yangu ilibadilika wakati nilijua kama “ile siku kubwa ya Yehova [ilikuwa] karibu.” (Sef. 1:14) Sikufurahia tena kuenda ku masomo. Lakini, nilipenda kusaidia wengine wajifunze kweli ya Biblia.

Nilimaliza masomo ya segondere tarehe 13, Mwezi wa 6, 1956, na kisha siku tatu, nilibatizwa ku mukusanyiko wa muzunguko. Ile wakati, sikukuwa najua kama kutumia maisha yangu ili kujifunza na kufundisha wengine kungeniletea baraka mingi sana.

KUJIFUNZA NA KUFUNDISHA WENGINE JUU YA YEHOVA WAKATI NILIKUWA PAINIA

Miezi sita kisha kubatizwa, nilikuwa painia wa kawaida. Mu Huduma ya Ufalme ya Mwezi wa 12, 1956 mulikuwa hii habari: “Unaweza Kutumikia Fasi Kwenye Kuwa Lazima Kubwa ya Wahubiri?” Ningeweza pia kufanya vile. Nilipenda kusaidia fasi kwenye kulikuwa wahubiri kidogo.​—Mt. 24:14.

Nilihamia Edgefield, Caroline du Sud. Kule kulikuwa kutaniko yenye ilikuwa tu na wahubiri ine. Miye njo nilikuwa sasa wa tano. Tulikuwa nafanyia mikutano mu nyumba ya ndugu. Kila mwezi, nilikuwa nafanya saa 100 mu mahubiri. Nilikuwa na mambo mingi ya kufanya, juu miye njo nilikuwa nasimamia mahubiri, na kupitisha hotuba na vipindi. Na jambo ya kufurahisha, kadiri nilikuwa na mambo mingi ya kufanya, ni vile nilijifunza mambo mingi zaidi juu ya Yehova.

Mwanamuke fulani mwenye nilijifunza naye Biblia alikuwa na fasi ya kutayarishia maiti mbele izikwe mu muji wa Johnston, muji wenye ulikuwa napatikana ku kilometre fulani. Alikuwa nanipatia kazi fulani yenye haikukuwa nanikamata wakati mingi na alitupatia nyumba fulani ya kidogo juu tukuwe nafanyia ndani mikutano.

Ndugu Jolly Jeffries, mutoto wa ule ndugu mwenye alijifunzaka na miye Biblia, alitoka Brooklyn, New York, na kuhamia kwenye nilikuwa naishi na tukafanya naye kazi ya upainia. Tuliishi mu gari ya kidogo, yenye ndugu fulani alitupatiaka.

Watu hawakukuwa nalipwa makuta mingi mu Caroline du Sud. Tulikuwa napata dolare 2 ao 3 ku siku. Siku moya, makuta ilikuwa imeniisha. Nilikuwa nimetumia makuta kidogo yenye nilikuwa nayo juu ya kuuza chakula kidogo. Wakati nilitoka, mwanaume fulani alinikaribia na kuniuliza: “Unapenda kutumika? Nitakulipa dolare moya ku saa.” Alinipatia kazi ya siku tatu ya kusafisha fasi kwenye walikuwa najenga. Ile ilionyesha wazi kama Yehova alikuwa nanisaidia juu nibakie Edgefield. Hata kama sikukuwa na makuta mingi, niliweza kuenda ku mukusanyiko wa kimataifa wenye ulifanywa mu muji wa New York mu 1958.

On our wedding day

Siku ya pili ya mukusanyiko, jambo fulani ya pekee ilitokea. Nilikutana na Ruby Wadlington, mwenye alikuwa painia wa kawaida mu muji wa Gallatin, Tennessee. Juu siye wote wawili tulipenda kuwa wamisionere, tulihuzuria mukutano kwa ajili ya wale wenye wanapenda kusoma Masomo ya Gileadi wenye ulifanywa ku ule mukusanyiko wa kimataifa. Kisha, tulianza kuandikiana. Na kisha pale, nilialikwa ili kutoa hotuba kule Gallatin. Nilitumia ile nafasi juu ya kumuuliza Ruby kama tunaweza kuoana. Nilihamia mu kutaniko ya Ruby, na tulioana mu 1959.

KUJIFUNZA NA KUFUNDISHA WENGINE JUU YA YEHOVA MU KUTANIKO

Wakati nilikuwa na miaka 23, niliwekwa kuwa mutumishi wa kutaniko (sasa anaitwa muratibu wa baraza ya wazee) mu Gallatin. Kutaniko yetu njo ilikuwa ya kwanza yenye Charles Thompson alitembelea kisha tu kuwa mwangalizi wa muzunguko. Hata kama alikuwa na uzoefu sana, aliniuliza ikiwa ndugu na dada wako na lazima ya nini na kama waangalizi wengine wa muzunguko wanafanyaka nini juu ya kusaidia makutaniko. Ile ilinifundisha kama ni muzuri kuuliza maulizo na kupata habari zote mbele ya kuhangaikia jambo fulani.

Mu Mwezi wa 5, 1964, nilialikwa ku Masomo ya Huduma ya Ufalme katika South Lansing, New York. Ile masomo ilifanya mwezi moya. Ndugu wenye walikuwa naongoza ile masomo walinifanya nipende sana kujifunza mambo mingi zaidi na nijikaze kuwa mutu wa kiroho.

KUJIFUNZA NA KUFUNDISHA WENGINE JUU YA YEHOVA WAKATI NILIKUWA MWANGALIZI WA MUZUNGUKO NA MWANGALIZI WA WILAYA

Mu Mwezi wa 1, 1965, biro ya tawi ilituomba miye na Ruby tufanye kazi ya muzunguko. Muzunguko wetu wa kwanza ulikuwa na eneo kubwa sana. Ulikuwa naanzia Knoxville, Tennessee, mupaka Richmond, Virginia. Mu muzunguko wetu mulikuwa makutaniko ya Caroline du Nord, Kentucky, na Virginie Occidentale. Nilikuwa natembelea tu makutaniko ya watu weusi juu ile wakati kulikuwa ubaguzi sana mu Amerika ya Kusini; weusi hawangekusanyika na wazungu. Ndugu walikuwa maskini, na tulijifunza kusaidia wale wenye walikuwa na lazima ya musaada. Mwangalizi fulani wa muzunguko mwenye alikuwa amefanya ile kazi kwa miaka mingi alinifundisha hii somo ya maana sana: “Ukuwe tu sawa kila ndugu. Usifike mu kutaniko na kujifanya sawa vile weye njo mukubwa wa kutaniko. Unaweza kuwasaidia ikiwa wanakuona kuwa ndugu yao.”

Wakati tulitembelea kutaniko fulani ya kidogo, Ruby alianza kujifunza na kijana fulani mwanamuke mwenye alikuwa na mutoto mwanamuke wa mwaka moya. Wakati mu kutaniko hamukukuwa mutu mwenye angeweza kujifunza naye, Ruby aliendelea kujifunza naye kupitia barua. Wakati tulitembelea tena ile kutaniko, ule mwanamuke alikuya ku mikutano yote. Na wakati dada wawili mapainia wa pekee walihamia mu ile kutaniko, waliendelea kujifunza naye na kisha wakati kidogo, alibatizwa. Kisha kupita miaka 30 hivi, mu 1995, ku Beteli ya Patterson, dada fulani kijana alikuya kuzungumuza na Ruby. Alikuwa mutoto wa ule mwanamuke mwenye Ruby alijifunzaka naye Biblia. Ule dada na bwana yake walikuwa wanafunzi mu somo ya 100 ya Masomo ya Gileadi.

Muzunguko wetu wa pili ulikuwa mu Florida ya katikati. Ile wakati tulikuwa na lazima ya gari, njo maana tuliuza gari moya ku bei ya muzuri kabisa. Lakini, mu juma ya kwanza, pompe ya maji ilikufa. Hatukukuwa na makuta ya kuitengeneza. Niliita ndugu fulani mwenye niliwaza kama anaweza kutusaidia. Ule ndugu aliomba mufanyakazi wake moya atutengenezee ile gari, na kisha ule ndugu hakupenda tumulipe makuta. Alisema tu hivi: “Hamutanilipa kitu.” Na hata alitupatia makuta kidogo! Ile ilituonyesha kabisa namna Yehova anahangaikiaka watumishi wake. Ilitukumbusha kama tunapaswa pia kuonyesha wengine ukarimu.

Fasi yote kwenye tulikuwa natembelea makutaniko, tulikuwa naikala mu nyumba za ndugu. Ile ilifanya tukuwe na marafiki wengi. Siku moya, nilianza kuandika na mashini ripoti kuhusu kutaniko fulani, lakini sikuimaliza na nikaiacha mu mashini yangu ya kuandikia na kuenda. Mangaribi wakati nilirudia, waliniambia kama mutoto mwanaume wa miaka tatu wa mu ile familia kwenye tulikuwa aligusa-gusa ku mashini yangu ya kuandikia na kwa hiyo, nilipaswa kuandika tena ile ripoti. Kwa miaka mingi, nilikuwa namufanyia muzaha juu ya ile jambo.

Mu 1971, nilipata barua ya kuniomba niende kuwa mwangalizi wa wilaya mu muji wa New York. Tulishituka! Wakati tulihamia kule, nilikuwa na miaka 34 tu. Ndugu walinikaribisha kwa furaha. Miye njo nilikuwa mwangalizi wao wa kwanza wa wilaya mwenye alikuwa mweusi.

Juu nilikuwa mwangalizi wa wilaya, nilifurahia kufundisha wengine juu ya Yehova ku mwisho wa kila juma ku mukusanyiko wa muzunguko. Waangalizi wengi wa muzunguko, walikuwa na uzoefu kunipita. Mwangalizi moya kati yao njo mwenye alifanyaka hotuba ya ubatizo wakati nilibatizwaka. Ndugu mwingine, Theodore Jaracz, alifikiaka kuwa mushiriki wa Baraza Yenye Kuongoza. Kulikuwa pia ndugu wengi wenye uzoefu wenye walikuwa natumikia ku Beteli ya Brooklyn. Nilifurahi sana kuona vile waangalizi wa muzunguko na wanabeteli walifanya nijisikie muzuri. Nilijionea namna walikuwa wachungaji wenye upendo, namna walitegemea Neno ya Mungu na kutegemeza kwa ushikamanifu tengenezo yake. Unyenyekevu wao ulifanya ikuwe mwepesi kwangu kutumika kama mwangalizi wa wilaya.

KUFANYA TENA KAZI YA MUZUNGUKO

Mu 1974, Baraza Yenye Kuongoza iliomba kikundi ingine ya waangalizi wa muzunguko wakuwe waangalizi wa wilaya, na miye niliombwa nikuwe tena mwangalizi wa muzunguko. Na mara hii nilitumikia mu Caroline du Sud. Jambo ya kufurahisha, ile wakati ndugu na dada wazungu na ndugu na dada weusi mu sehemu ya kusini mwa Amerika walikuwa nakusanyika pamoya, na ile ilifurahisha sana ndugu na dada.

Ku mwisho wa 1976, nilitumwa mu muzunguko fulani wa Georgie kati ya Atlanta na Columbus. Ninakumbuka wakati nilitoa hotuba ya maziko ya watoto tano weusi wenye walikufa wakati watu fulani waliunguza nyumba yao. Mama yao alienda ku hopitale juu alikuwa na vidonda. Mashahidi wengi wa Yehova, weusi na wazungu, waliendelea kufika ku hopitale juu ya kufariji wazazi wa wale watoto. Niliona kama ndugu walikuwa na upendo sana. Wakati watumishi wa Yehova wanaonyeshana upendo, wanaweza kuvumilia hata magumu ya nguvu sana.

KUJIFUNZA NA KUFUNDISHA WENGINE JUU YA YEHOVA KU BETELI

Mu 1977, tulialikwa ku Beteli ya Brooklyn kwa miezi kidogo juu ya kusaidia mu kazi fulani. Wakati ile kazi ilikaribia kumalizika, ndugu wawili wa Baraza Yenye Kuongoza waliongea na miye na Ruby na kutuuliza kama tutafurahia kuendelea kutumikia ku Beteli. Tuliitika.

Kwa miaka 24, nilitumika mu Idara ya Utumishi, kwenye mara mingi ndugu wanahangaikiaka maulizo ya nguvu. Kwa miaka mingi, Baraza Yenye Kuongoza imetoa maagizo yenye inapatana na kanuni za Biblia. Ile maagizo inasaidiaka Idara ya Utumishi kujibia maulizo yenye ndugu wanaulizaka, na pia inatumiwaka juu ya kuzoeza waangalizi wa muzunguko, wazee, na mapainia. Ile mazoezi imesaidia ndugu wengi wakomale kiroho. Na imetia nguvu tengenezo ya Yehova.

Kuanzia 1995 mupaka 2018, nilitembelea biro mbalimbali za tawi juu nilikuwa mujumbe wa makao makubwa, mwenye zamani alikuwa naitwa mwangalizi wa eneo ya dunia. Nilikutana na ndugu wa Halmashauri za Tawi, wanabeteli, na wamisionere juu ya kuwatia moyo na kuwasaidia kupambana na magumu yenye wanakutanaka nayo. Ndugu na dada walikuwa natuelezea mambo yenye walikutana nayo, na kila mara ile ilikuwa natutia moyo. Kwa mufano, tulitembelea Rwanda mu 2000. Tuliguswa sana wakati tulisikia namna ndugu na familia ya Beteli waliokoka mauaji ya 1994. Wengi walipoteza wapendwa wao. Hata kama walipambana na ile magumu, waliendelea kuwa na imani, tumaini, na furaha.

Siku yenye tulikumbuka miaka 50 ya ndoa yetu

Tuko sasa na miaka zaidi ya 80. Kwa miaka 20 yenye imepita, nimetumikia mu Halmashauri ya Tawi ya Amerika. Siyasomaka masomo ya juu. Lakini, nimepata elimu ya juu sana kutoka kwa Yehova na tengenezo yake. Imenisaidia niweze kufundisha wengine kweli za Biblia zenye zinaweza kuwasaidia milele. (2 Ko. 3:5; 2 Ti. 2:2) Nimejionea namna Biblia imesaidia watu wakuwe na maisha ya muzuri na wakuwe marafiki wa Muumbaji wao. (Yak. 4:8) Kadiri tunaweza, miye na Ruby tunaendelea kutia wengine moyo wafurahie sana pendeleo ya kujifunza juu ya Yehova na kufundisha wengine kweli za Biblia. Ile njo pendeleo kubwa sana ya kila mutumishi wa Yehova!