Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Mtume Paulo alimaanisha nini alipojirejelea kuwa “yule aliyezaliwa kabla ya wakati wake”? (1 Wakorintho 15:8)

▪ Kulingana na 1 Wakorintho 15:8, Paulo alisema: “Mwisho kabisa alinitokea mimi pia kana kwamba kwa yule aliyezaliwa kabla ya wakati wake.” Zamani, tulifafanua kwamba huenda Paulo alikuwa akirejelea hali yake mwenyewe alipoona maono ya Yesu aliyetukuzwa mbinguni. Ni kana kwamba alikuwa amepewa pendeleo la kuzaliwa, au kufufuliwa, kwenye uhai wa kiroho kabla ya wakati, karne nyingi kabla ya ufufuo wa aina hiyo kuanza kufanywa. Hata hivyo, baada ya kuchunguza mstari huu kwa undani inaonekana kwamba tunahitaji kurekebisha ufafanuzi wa mstari huu.

Ni kweli kwamba hapa Paulo anarejelea jambo lililotokea alipogeuzwa imani na kuwa Mkristo. Lakini alimaanisha nini aliposema ‘alizaliwa kabla ya wakati wake’? Maneno yake yanaweza kueleweka kwa njia kadhaa.

Paulo aligeuzwa imani ghafla kwa njia yenye kushtua. Mtoto anayezaliwa kabla ya wakati wake, huzaliwa bila kutarajiwa. Sauli (ambaye baadaye alijulikana kuwa Paulo) alipokuwa akisafiri kwenda Damasko ili kuwatesa Wakristo huko, hakutarajia kwamba angeona maono ya Yesu aliyefufuliwa. Kugeuzwa imani kwa Paulo kulikuwa jambo lisilotarajiwa kwake mwenyewe na pia kwa Wakristo ambao alikusudia kuwatesa katika jiji hilo. Isitoshe, tukio hilo lilikuwa lenye kushtua sana hivi kwamba alipoteza uwezo wake wa kuona kwa muda fulani.​—Mdo. 9:1-9, 17-19.

Aligeuzwa imani “wakati usiofaa.” Neno la awali la Kigiriki linalotafsiriwa “yule aliyezaliwa kabla ya wakati wake” linaweza pia kutafsiriwa “yule aliyezaliwa wakati usiofaa.” Tafsiri ya The Jerusalem Bible inasema hivi: “Ni kana kwamba nilizaliwa wakati ambao hakuna aliyetarajia.” Paulo alipogeuzwa imani, tayari Yesu alikuwa amerudi mbinguni. Tofauti na wale ambao Paulo alikuwa amewarejelea katika mistari inayotangulia, yeye hakuwa amemwona Yesu aliyefufuliwa kabla ya kurudi mbinguni. (1 Kor. 15:4-8) Yesu alipomtokea Paulo bila kutarajia, Paulo alipata nafasi ya kumwona Yesu, ingawa ni kana kwamba ulikuwa “wakati usiofaa.”

Alikuwa akizungumza kujihusu yeye mwenyewe kwa njia ya kiasi. Kulingana na wasomi fulani, maneno ambayo Paulo alitumia hapa yanaweza kuwa na maana yenye dharau. Ikiwa Paulo alimaanisha hivyo, alikuwa akikubali kwamba hakustahili kupata pendeleo alilopewa. Hata alisema hivi: “Mimi ni mdogo zaidi kati ya mitume, nami sistahili kuitwa mtume, kwa sababu nililitesa kutaniko la Mungu. Lakini kwa fadhili zisizostahiliwa za Mungu mimi niko kama nilivyo.”​—1 Kor. 15:9, 10.

Basi, inaonekana kwamba huenda Paulo alikuwa akirejelea jinsi Yesu alivyomtokea ghafla na kwa njia isiyotarajiwa, wakati usiotarajiwa ambao aligeuzwa imani, au kwamba hakustahili kiroho kupata ufunuo huo wenye kustaajabisha. Vyovyote vile, ni wazi kwamba Paulo alithamini tukio hilo. Lilimthibitishia kwa uhakika kabisa kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa. Haishangazi kwamba mara nyingi alirejelea tukio hilo lisilotarajiwa alipokuwa akiwahubiria wengine kuhusu ufufuo wa Yesu.​—Mdo. 22:6-11; 26:13-18.