MAKALA YA 3

Yehova Anakusaidia Ili Ufanikiwe

Yehova Anakusaidia Ili Ufanikiwe

“Yehova alikuwa pamoja na Yosefu . . . , akifanikisha kila jambo alilokuwa akifanya.”​—MWA. 39:2, 3.

WIMBO 30 Baba Yangu, Mungu Wangu, Rafiki Yangu

MUHTASARI a

1-2. (a) Kwa nini hatushangai kwamba tunapatwa na majaribu? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

 TUKIWA watu wa Yehova, hatushangai tunapokabili majaribu. Tunatambua kwamba kama Biblia inavyosema, “ni lazima tuingie katika Ufalme wa Mungu kupitia dhiki nyingi.” (Mdo. 14:22) Pia, tunatambua kwamba baadhi ya matatizo yetu hayataondolewa kabisa mpaka tutakapoishi katika ulimwengu mpya wa Mungu, ambapo “kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.”​—Ufu. 21:4.

2 Yehova hatukingi ili tusipatwe na majaribu. Hata hivyo, anatusaidia tuyavumilie. Ona jambo ambalo mtume Paulo aliwaambia Wakristo walioishi huko Roma. Kwanza, alitaja baadhi ya majaribu ambayo yeye na ndugu zake walikabili. Kisha akaandika hivi: “Tunatoka tukiwa tumeshinda kabisa kupitia yule aliyetupenda.” (Rom. 8:35-37) Hilo linamaanisha kwamba Yehova anaweza kukusaidia ufanikiwe hata wakati ambapo jaribu linaendelea. Acheni tuone jinsi Yehova alivyomsaidia Yosefu afanikiwe na jinsi anavyoweza kukusaidia wewe.

MAMBO YANAPOBADILIKA GHAFLA

3. Ni badiliko gani la ghafla ambalo lilitokea katika maisha ya Yosefu?

3 Yakobo alionyesha wazi kwamba alimpenda sana Yosefu mwanaye. (Mwa. 37:3, 4) Matokeo ni kwamba wana wakubwa wa Yakobo walimwonea wivu ndugu yao. Walipopata nafasi, walimuuza Yosefu kwa kikundi cha wafanyabiashara Wamidiani. Wafanyabiashara hao walimpeleka Yosefu mamia ya kilometa huko Misri, ambako aliuzwa tena—wakati huu kwa Potifa, mkuu wa walinzi wa Farao. Maisha ya Yosefu yalibadilika upesi, kutoka kuwa mwana aliyependwa zaidi na baba yake, na kuwa mtumwa wa hali ya chini huko Misri!—Mwa. 39:1.

4. Huenda tukakabili changamoto gani inayofanana na ya Yosefu?

4 Biblia inasema kwamba “mambo mabaya humpata kila mtu.” (Mhu. 9:11, Holy Bible—Easy-to-Read Version) Wakati mwingine tunakabili matatizo yaliyo “ya kawaida kwa watu,” yaani, majaribu ambayo huwapata wanadamu wote. (1 Kor. 10:13) Au huenda tukateseka kwa sababu tu sisi ni wanafunzi wa Yesu. Kwa mfano, huenda tukadhihakiwa, kupingwa, au hata kuteswa kwa sababu ya imani yetu. (2 Tim. 3:12) Hata upatwe na jaribu gani, Yehova anaweza kukusaidia ufanikiwe. Alimsaidiaje Yosefu?

Yehova alimsaidia Yosefu afanikiwe hata wakati alipouzwa na kuwa mtumwa wa Potifa huko Misri (Tazama fungu la 5)

5. Potifa alifikia mkataa gani kuhusu mafanikio ya Yosefu? (Mwanzo 39:2-6)

5 Soma Mwanzo 39:2-6. Potifa alitambua kwamba Yosefu alikuwa kijana mwenye ustadi sana na mfanyakazi mwenye bidii. Na alijua sababu. Potifa aliona kwamba “Yehova alikuwa akifanikisha kila jambo alilokuwa akifanya [Yosefu].” b Mwishowe, Potifa alimfanya Yosefu kuwa mhudumu wake binafsi. Pia, alimweka Yosefu kuwa msimamizi wa nyumba yake yote. Matokeo yalikuwaje? Potifa alisitawi.

6. Huenda Yosefu alihisije kuhusu hali yake?

6 Jaribu kuona hali hiyo kwa maoni ya Yosefu. Ni jambo gani alilotamani sana? Je, alitamani kutambuliwa na kuthawabishwa na Potifa? Inaelekea kwamba alitamani kuwekwa huru na kurudi kwa baba yake. Kwa sababu licha ya mapendeleo yote aliyokuwa nayo katika nyumba ya Potifa, bado Yosefu alikuwa mtumwa wa bwana aliyeabudu miungu ya uwongo. Yehova hakumfanya Potifa amweke Yosefu huru. Na baada ya muda mfupi, hali ya Yosefu ingekuwa mbaya zaidi.

HALI INAPOKUWA MBAYA ZAIDI

7. Hali ya Yosefu ilizidi kuwa mbaya jinsi gani? (Mwanzo 39:14, 15)

7 Kama vile inavyoonyeshwa kwenye Mwanzo sura ya 39, mke wa Potifa alivutiwa na Yosefu na alijaribu tena na tena kumshawishi Yosefu. Kila mara, Yosefu alipinga vishawishi hivyo. Mwishowe, alimkasirikia sana Yosefu na akadai kwamba Yosefu alijaribu kumbaka. (Soma Mwanzo 39:14, 15.) Potifa aliposikia kuhusu jambo hilo, alimtupa Yosefu gerezani, ambako alikaa kwa miaka kadhaa. (Mwa. 39:19, 20) Maisha yalikuwaje gerezani? Neno la Kiebrania ambalo Yosefu alitumia kurejelea “gereza” linaweza kumaanisha “tangi,” au “shimo,” hilo linadokeza kwamba alikuwa kwenye mazingira yenye giza na alihisi kwamba hana tumaini. (Mwa. 40:15; maelezo ya chini) Pia, Biblia inaonyesha kwamba kwa muda fulani miguu ya Yosefu ilikuwa imefungwa kwa pingu na shingo yake ilitiwa katika vyuma. (Zab. 105:17, 18) Hali ya Yosefu ilikuwa ikizidi kuwa mbaya. Alitoka kuwa mtumwa aliyeaminika na kuwa mfungwa wa hali ya chini.

8. Tunaweza kuwa na uhakika kuhusu jambo gani hata jaribu linapozidi kuwa gumu?

8 Je, umewahi kukabili hali ngumu iliyozidi kuwa mbaya hata ingawa ulisali kwa bidii? Hilo linaweza kutokea. Yehova hatukingi ili tusipatwe na majaribu katika ulimwengu huu unaotawaliwa na Shetani. (1 Yoh. 5:19) Hata hivyo, unaweza kuwa na uhakika kuhusu jambo hili: Yehova anaelewa kikamili mambo unayopitia, na anakujali. (Mt. 10:29-31; 1 Pet. 5:6, 7) Isitoshe, ameahidi hivi: “Sitakuacha wala kukutupa kamwe.” (Ebr. 13:5) Yehova anaweza kukusaidia ili uvumilie hata inapoonekana kwamba hakuna tumaini. Acheni tuone jambo hilo katika kisa cha Yosefu.

Yehova alikuwa pamoja na Yosefu hata alipokuwa gerezani na kuwekwa kuwa msimamizi wa wafungwa wote (Tazama fungu la 9)

9. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova alikuwa pamoja na Yosefu alipokuwa gerezani? (Mwanzo 39:21-23)

9 Soma Mwanzo 39:21-23. Hata katika kipindi kigumu alichokuwa gerezani, Yehova alimsaidia Yosefu kufanikiwa. Jinsi gani? Baada ya muda, Yosefu alitumainiwa na kuheshimiwa na ofisa mkuu wa gereza, kama ilivyokuwa na Potifa. Baada ya muda, ofisa huyo mkuu alimweka Yosefu kuwa msimamizi wa wafungwa wenzake. Hata Biblia inasema kwamba “ofisa mkuu wa gereza hakujishughulisha na jambo hata moja lililokuwa chini ya usimamizi wa Yosefu.” Sasa Yosefu alikuwa na jambo ambalo angejishughulisha nalo​—kazi yenye kuridhisha. Hayo yalikuwa mabadiliko yasiyo ya kawaida! Ingewezekanaje kwa mfungwa aliyeshtakiwa kwamba alijaribu kumbaka mke wa ofisa wa makao ya mfalme apewe cheo hicho cha kuaminika? Kuna sababu moja tu. Kama Mwanzo 39:23 inavyosema, “Yehova alikuwa pamoja na Yosefu na Yehova alifanikisha jambo lolote alilofanya.”

10. Eleza ni kwa nini huenda Yosefu hakuhisi kwamba alifanikiwa katika kila jambo.

10 Jaribu tena kuona hali hiyo kwa maoni ya Yosefu. Baada ya kushtakiwa kwa uwongo na kufungwa gerezani, je, unafikiri alihisi kwamba alikuwa amefanikiwa katika kila jambo? Ni jambo gani ambalo Yosefu alitamani zaidi? Je, alitamani kupata kibali machoni pa ofisa mkuu wa gereza? Inaelekea kwamba Yosefu alitamani aondolewe mashtaka na kuwekwa huru. Hata alimwomba mfungwa mmoja ambaye alikuwa karibu kuwekwa huru azungumze na Farao kwa niaba yake ili amweke huru kutoka kwenye gereza hilo lenye kukatisha tamaa. (Mwa. 40:14) Hata hivyo, mwanamume huyo hakuzungumza na Farao wakati huo. Matokeo ni kwamba Yosefu aliendelea kuwa gerezani kwa miaka miwili zaidi. (Mwa. 40:23; 41:1, 14) Ingawa hivyo, Yehova aliendelea kumsaidia afanikiwe. Jinsi gani?

11. Yehova alimpa Yosefu uwezo gani wa pekee, na hilo lilisaidiaje kutimiza kusudi la Yehova?

11 Yosefu alipokuwa gerezani, Yehova alimfanya mfalme wa Misri aote ndoto mbili zilizomhangaisha. Farao alitamani sana kujua maana ya ndoto hizo. Mfalme alipotambua kwamba Yosefu alikuwa na uwezo wa kutafsiri ndoto, aliagiza kwamba aletwe. Kwa msaada wa Yehova, Yosefu alieleza maana ya ndoto hizo na Farao akafurahishwa na ushauri unaofaa ambao Yosefu alitoa. Farao alipoona kwamba Yehova alikuwa pamoja na kijana huyo, alimweka Yosefu awe msimamizi wa chakula katika nchi yote ya Misri. (Mwa. 41:38, 41-44) Baadaye, njaa kali ilitokea ambayo haikuathiri tu nchi ya Misri, bali pia nchi ya Kanaani ambako familia ya Yosefu ilikuwa ikiishi. Sasa Yosefu angeweza kuiokoa familia yake na hivyo kulinda ukoo ambao ungemtokeza Masihi.

12. Ni kwa njia gani Yehova alimfanya Yosefu afanikiwe?

12 Fikiria matukio hayo yasiyo ya kawaida katika maisha ya Yosefu. Ni nani ambaye alimfanya Potifa amtambue Yosefu aliyekuwa mtumwa tu? Ni nani ambaye alimfanya ofisa mkuu wa gereza amwonyeshe Yosefu kibali ingawa alikuwa mfungwa wa hali ya chini? Ni nani ambaye alimfanya Farao aote ndoto zilizomhangaisha na kumpa Yosefu uwezo wa kuzitafsiri? Ni nani ambaye alimfanya Farao amweke Yosefu kuwa msimamizi wa chakula nchini Misri? (Mwa. 45:5) Bila shaka, Yehova ndiye aliyefanya kila jambo ambalo Yosefu alifanya lifanikiwe. Mwishowe, Yehova alibadili njama ya ukatili ya ndugu za Yosefu iwe njia ya kutimiza kusudi lake.

JINSI YEHOVA ANAVYOKUSAIDIA UFANIKIWE

13. Je, Yehova huingilia kati kila jambo tunalokabili? Eleza.

13 Tunaweza kufikia mkataa gani kutokana na simulizi la Yosefu? Je, Yehova anaingilia kati kila hali tunayokabili? Je, anaongoza kila tukio katika maisha yetu, hivi kwamba mambo yote mabaya yanayotokea yawe na kusudi zuri? Hapana, Biblia haiungi mkono maoni hayo. (Mhu. 8:9; 9:11) Hata hivyo, tunajua jambo hili: Tunapokabili jaribu, Yehova anatambua jambo hilo, naye husikia tunapomlilia ili kumwomba msaada. (Zab. 34:15; 55:22; Isa. 59:1) Zaidi ya hilo, Yehova anaweza kutusaidia tufanikiwe kuvumilia majaribu. Jinsi gani?

14. Yehova hutusaidiaje tunapokabili hali ngumu?

14 Njia moja ambayo Yehova hutusaidia ni kwa kutufariji na kututia moyo, na mara nyingi ni kwa wakati unaofaa kabisa. (2 Kor. 1:3, 4) Ilikuwa hivyo kwa Eziz, ndugu kutoka Turkmenistan aliyehukumiwa kufungwa miaka miwili gerezani kwa sababu ya imani yake. Anasema hivi: “Asubuhi ambayo kesi yangu ilisikilizwa, ndugu mmoja alinionyesha andiko la Isaya 30:15, ambalo linasema: ‘Mtakuwa na nguvu mkiendelea kuwa watulivu na kuwa na tumaini.’ Andiko hilo limenisaidia sikuzote kuendelea kuwa mtulivu na kumtegemea Yehova katika kila jambo. Kutafakari andiko hilo kulinisaidia kipindi chote nilichokuwa gerezani.” Je, unaweza kukumbuka wakati fulani maishani mwako ambapo Yehova alikusaidia kwa kukufariji na kukutia moyo wakati ambapo ulihitaji zaidi kutiwa moyo?

15-16. Unajifunza nini kutokana na kisa cha Tori?

15 Mara nyingi, tunapokumbuka jinsi tulivyokabiliana na hali ngumu, ndipo tunapotambua jinsi Yehova alivyotusaidia kuvumilia. Dada anayeitwa Tori alijionea ukweli wa jambo hilo. Mwanaye anayeitwa Mason, alikabiliana na ugonjwa wa kansa kwa miaka sita hadi alipokufa. Inaeleweka kwamba Tori alivunjika moyo sana. Anasema hivi: “Sidhani kuna hali nyingine yenye maumivu makali kuliko hii ambayo ningeweza kukabili nikiwa mama.” Anaendelea kusema hivi: “Nina uhakika wazazi wengine watakubaliana nami kwamba kumwona mtoto wako akiteseka ni jambo baya zaidi kuliko wewe mwenyewe kuteseka.”

16 Ingawa jaribu hilo lilikuwa lenye kuvunja moyo sana, baadaye Tori alitafakari jinsi ambavyo Yehova alimsaidia kukabiliana nalo. Anasema hivi: “Ninapokumbuka kipindi hicho, ninaona jinsi ambavyo mkono wa Yehova ulinisaidia katika kipindi chote ambacho mwanangu alikuwa mgonjwa. Kwa mfano, hata kipindi ambacho Mason alikuwa mgonjwa sana hivi kwamba hangeweza kuwaona wageni, ndugu na dada wangeendesha gari kwa saa mbili ili kuja hospitalini. Sikuzote kulikuwa na mtu kwenye chumba cha kusubiria—ambaye alikuwa tayari kutoa msaada. Pia, tuliandaliwa mahitaji yetu ya kimwili. Hata hali ilipokuwa ngumu sana, hatukukosa kamwe mahitaji yetu.” Yehova alimpatia Tori msaada aliohitaji ili kuvumilia, na pia alimsaidia Mason.​—Tazama sanduku “ Yehova Alitupatia Hasa Kile Tulichohitaji.”

HESABU BARAKA ZAKO

17-18. Ni nini kitakachotusaidia kutambua na kuthamini msaada wa Yehova wakati tunapokabili majaribu? (Zaburi 40:5)

17 Soma Zaburi 40:5. Lengo la mtu anayepanda mlima ni kufika kileleni. Hata hivyo, kuna vituo mbalimbali njiani ambapo anaweza kusimama na kutazama mandhari. Vivyo hivyo, tenga muda kwa ukawaida ili kutua na kutafakari jinsi Yehova anavyokusaidia kufanikiwa hata unapokabili hali ngumu. Mwishoni mwa kila siku, jiulize hivi: ‘Leo, nimeona baraka za Yehova katika njia gani? Ingawa bado jaribu linaendelea, Yehova ananisaidiaje kulivumilia?’ Jaribu kutambua hata baraka moja kutoka kwa Yehova ambayo imekusaidia ufanikiwe.

18 Ni kweli kwamba huenda unasali ili jaribu lako liishe. Jambo hilo linaeleweka na linafaa. (Flp. 4:6) Lakini pia, tunapaswa kutambua baraka tulizo nazo sasa. Kwa kweli, Yehova anaahidi kwamba atatuimarisha na kutusaidia kuvumilia. Basi, sikuzote onyesha kwamba unathamini msaada kutoka kwa Yehova. Kisha utaona jinsi anavyokusaidia ufanikiwe, hata wakati unapokabili majaribu, kama alivyomsaidia Yosefu.​—Mwa. 41:51, 52.

WIMBO 32 Simama Upande wa Yehova!

a Tunapokabiliana na jaribu gumu, huenda tukahisi kwamba hatuwezi “kufanikiwa.” Huenda tukafikiri kwamba tunaweza kusema tumefanikiwa ikiwa tu jaribu hilo litakwisha. Hata hivyo, matukio yaliyotokea katika maisha ya Yosefu yanatufundisha somo muhimu​—kwamba Yehova anaweza kutusaidia tufanikiwe hata wakati tunapokabili majaribu. Makala hii itaonyesha jinsi anavyotusaidia.

b Biblia inataja katika mistari michache tu mabadiliko hayo yaliyotokea mwanzoni Yosefu alipokuwa mtumwa, lakini huenda yalitokea katika kipindi cha miaka kadhaa.