MAKALA YA 9

Thamini Zawadi ya Mungu ya Uhai

Thamini Zawadi ya Mungu ya Uhai

“Kupitia kwake tuko hai, tunatembea, na tunaishi.”​—MDO. 17:28.

WIMBO 141 Muujiza wa Uhai

MUHTASARI a

1. Uhai wetu ni wenye thamani kadiri gani kwa Yehova?

 WAZIA kwamba rafiki yako amekupatia nyumba ambayo rangi yake imechakaa kidogo na baadhi ya sehemu za paa zinavuja, lakini licha ya kasoro hizo thamani ya nyumba hiyo ni mamilioni ya dola. Bila shaka ungeithamini na kuitunza nyumba hiyo. Vivyo hivyo, Yehova ametupatia zawadi yenye thamani. Zawadi ya uhai. Kwa kweli, Yehova ameonyesha jinsi anavyothamini uhai wetu kwa kumtoa Mwana wake kuwa fidia kwa ajili yetu.​—Yoh. 3:16.

2. Kama andiko la 2 Wakorintho 7:1 linavyosema, Yehova anatarajia tufanye nini?

2 Yehova ndiye Chanzo cha uhai. (Zab. 36:9) Mtume Paulo alikubaliana na ukweli huo aliposema hivi: “Kupitia kwake tuko hai, tunatembea, na tunaishi.” (Mdo. 17:25, 28) Basi, tunaweza kusema kwa uhakika kwamba uhai wetu ni zawadi kutoka kwa Mungu. Anatuandalia kwa upendo mambo tunayohitaji ili kuendelea kuishi. (Mdo. 14:15-17) Lakini Yehova haendelezi uhai wetu kimuujiza. Badala yake, anatarajia tufanye yote tunayoweza ili kutunza afya yetu ya kimwili na ya kiroho. (Soma 2 Wakorintho 7:1.) Kwa nini tunapaswa kulinda afya na uhai wetu, na tunawezaje kufanya hivyo?

THAMINI ZAWADI YA UHAI

3. Ni sababu gani moja inayotuchochea kutunza afya yetu?

3 Sababu moja inayofanya tujitahidi kutunza afya yetu ni ili tumtumikie Yehova kwa uwezo wetu wote. (Marko 12:30) Tunatamani kuitoa “miili [yetu] iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, na yenye kukubalika kwa Mungu,” hivyo tunaepuka kufanya jambo lolote ambalo tunajua litadhuru afya yetu. (Rom. 12:1) Ukweli ni kwamba hatuwezi kuepuka kabisa kupatwa na ugonjwa. Lakini tunafanya yote tunayoweza ili kutunza afya yetu kwa sababu tunataka kumwonyesha Baba yetu wa mbinguni kwamba tunathamini zawadi ya uhai.

4. Mfalme Daudi alitamani kufanya nini?

4 Mfalme Daudi alieleza kwa nini alithamini zawadi ya Mungu ya uhai alipoandika hivi: “Kuna faida gani nikifa, nikishuka shimoni? Je, mavumbi yatakusifu? Je, yatasimulia kuhusu uaminifu wako?” (Zab. 30:9) Huenda Daudi aliandika maneno hayo karibu na mwisho wa maisha yake. Lakini alikuwa ameazimia kuendelea kuwa hai na mwenye afya njema ili aweze kumsifu Yehova. Bila shaka sisi sote tumeazimia kufanya hivyo pia.

5. Hata iwe tumezeeka au sisi ni wagonjwa kadiri gani, tunaweza kufanya nini?

5 Huenda ugonjwa na kuzeeka kukatuzuia kufanya mambo mengi ambayo tulifanya zamani. Matokeo ni kwamba huenda tukavunjika moyo na kuhuzunika. Lakini hatupaswi kamwe kukata tamaa na kupuuza afya yetu. Kwa nini? Kwa sababu hata iwe tumezeeka au ni wagonjwa kadiri gani, bado tunaweza kumsifu Yehova kama alivyofanya Mfalme Daudi. Inafariji sana kujua kwamba Mungu wetu anatuthamini hata ingawa sisi si wakamilifu! (Mt. 10:29-31) Hata tukifa, atatamani kutufufua. (Ayu. 14:14, 15) Maadamu tuko hai, tunataka kufanya yote tunayoweza ili kulinda afya na uhai wetu.

EPUKA MAZOEA YENYE KUDHURU

6. Yehova angependa tuwe na mazoea gani kuhusu kula na kunywa?

6 Ingawa Biblia si kitabu kinachozungumzia kihususa mambo ya afya au vyakula, kinafunua mawazo ya Yehova kuhusu mambo hayo. Kwa mfano, anatuhimiza ‘tujiepushe na mambo yanayodhuru’ ambayo yanaweza kuathiri mwili wetu. (Mhu. 11:10) Ulafi na ulevi, ni mambo ambayo yanahatarisha uhai, na Biblia inasema tunapaswa kuyaepuka. (Met. 23:20) Yehova anataka tuwe na sifa ya kujizuia tunapoamua tutakula na kunywa nini, na kwa kiasi gani.​—1 Kor. 6:12; 9:25.

7. Shauri linalopatikana kwenye Methali 2:11, linatusaidiaje kufanya maamuzi mazuri kuhusu afya yetu?

7 Tunaweza kufanya maamuzi yanayoonyesha tunathamini sana zawadi ya Mungu ya uhai kwa kutumia uwezo wetu wa kufikiri. (Zab. 119:99, 100; soma Methali 2:11.) Kwa mfano, tunachagua kwa makini kile tutakachokula. Ikiwa tunapenda aina fulani ya chakula lakini tunajua kwamba kitatusababishia ugonjwa, kwa busara tutaepuka kula chakula hicho. Pia, tunathibitisha kwamba tuna utimamu wa akili tunapohakikisha tunalala vya kutosha, tunafanya mazoezi kwa ukawaida, tunadumisha ratiba nzuri ya usafi wa kimwili, na kudumisha nyumba zetu zikiwa safi.

ZINGATIA USALAMA

8. Biblia inafunua nini kuhusu mawazo ya Yehova kuelekea kudumisha usalama wetu?

8 Sheria ambayo Yehova alilipatia taifa la Israeli ilitia ndani miongozo ambayo ingewasaidia kuzuia aksidenti mbaya zisitokee nyumbani na kazini. (Kut. 21:28, 29; Kum. 22:8) Aksidenti zilizosababisha kifo zilikuwa na matokeo mabaya kwa wauaji wasiokusudia. (Kum. 19:4, 5) Pia, Sheria iliagiza kwamba hata wale ambao walimuumiza bila kukusudia mtoto ambaye bado hajazaliwa walipaswa kuadhibiwa. (Kut. 21:22, 23) Maandiko yanaonyesha wazi kwamba Yehova anataka tuzingatie usalama.

Tunawezaje kuonyesha kwamba tunaheshimu uhai katika hali hizi mbalimbali? (Tazama fungu la 9)

9. Tunaweza kuchukua tahadhari gani ili kuepuka aksidenti? (Tazama pia picha.)

9 Tunaonyesha kwamba tunathamini zawadi ya Mungu ya uhai kwa kujitahidi kuzingatia usalama nyumbani na kazini. Kwa mfano, tunatupa vitu vyenye ncha kali, kemikali hatari, au dawa kwa njia iliyo salama, na tunaweka vitu kama hivyo mahali ambapo watoto wadogo hawawezi kuvifikia. Tunakuwa makini tunaposhughulika na moto, maji moto, na vifaa vinavyotumia umeme, na hatuviachi bila mtu wa kuvisimamia. Hatuendeshi gari ikiwa uwezo wetu wa kufanya maamuzi umeathiriwa na dawa, pombe, au kukosa usingizi, na hatujiruhusu tukengeushwe kwa kutumia vifaa vya kielektroni vinavyoshikwa mkononi tunapoendesha gari.

MAJANGA YANAPOTOKEA

10. Tunaweza kufanya nini kabla na wakati wa majanga yanayohatarisha uhai?

10 Wakati mwingine, hatuwezi kuzuia mambo yanayohatarisha uhai. Hilo ni kweli hasa kuhusiana na misiba ya asili, milipuko ya magonjwa, na mapigano ya kijamii. Hata hivyo, majanga kama hayo yanapotokea, tunaweza kujitahidi kupunguza hatari na kuongeza uwezekano wetu wa kuokoka kwa kutii amri za kutotoka nje, amri za kuondoka nyumbani, na vizuizi vya dharura. (Rom. 13:1, 5-7) Tunaweza kujitayarisha mapema kwa ajili ya hali fulani za dharura, hivyo tunapaswa kufuata mwongozo unaotolewa na wenye mamlaka ili kujitayarisha kwa ajili ya janga. Kwa mfano, huenda ikafaa kuwa na akiba ya maji, vyakula visivyoharibika upesi, na vifaa vya huduma ya kwanza.

11. Tunapaswa kuwa tayari kufanya nini ikiwa ugonjwa wenye kuambukiza unaenea katika eneo letu?

11 Tunapaswa kufanya nini ikiwa ugonjwa wenye kuambukiza unaenea katika eneo letu? Tunapaswa kutii miongozo ya dharura, kama vile kunawa mikono, kudumisha umbali unaofaa kutoka kwa watu wengine, kuvaa barakoa, na kujitenga na watu wengine. Tunapofanya mambo hayo, tunaonyesha kwamba tunathamini sana zawadi ya Mungu ya uhai.

12. Kanuni iliyo kwenye Methali 14:15 inatusaidiaje kuchagua habari tunazopaswa kuamini wakati wa janga fulani?

12 Wakati wa dharura, huenda habari zisizo sahihi zikasambazwa kati ya marafiki, majirani, na katika vyombo vya habari. Badala ya kuamini “kila neno” tunalosikia, ni vizuri kusikiliza habari zinazotegemeka zaidi kutoka kwa serikali na wahudumu wa afya. (Soma Methali 14:15.) Baraza Linaloongoza na ofisi za tawi, hufanya yote wanayoweza ili kupata habari sahihi kabla ya kutoa mwongozo kuhusu mikutano ya kutaniko na kazi ya kuhubiri. (Ebr. 13:17) Tunapofuata mwongozo huo, tunajilinda sisi wenyewe na wengine ili tusipatwe na madhara. Pia, huenda tukawasaidia watu katika jamii wawe na maoni mazuri kuhusu Mashahidi wa Yehova.​—1 Pet. 2:12.

JITAYARISHE ILI UJIEPUSHE NA DAMU

13. Tunaonyeshaje kwamba tunathamini zawadi ya Mungu ya uhai inapohusu masuala ya damu?

13 Mashahidi wa Yehova wanajulikana kwa msimamo wao wa kuheshimu utakatifu wa damu. Tunatii sheria ya Yehova kuhusu damu kwa kuepuka kutiwa damu mishipani, hata wakati wa matibabu ya dharura. (Mdo. 15:28, 29) Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba tunataka kufa. Kinyume chake, tunathamini zawadi ya Mungu ya uhai. Tunatafuta matibabu kutoka kwa madaktari walio tayari kutoa matibabu ya kiwango cha juu ambayo hayahusishi kutiwa damu mishipani.

14. Tunawezaje kupunguza uwezekano wa kuhitaji kufanyiwa matibabu ya dharura?

14 Tunaweza kuepuka uhitaji wa kufanyiwa matibabu ya dharura kwa kufuata mapendekezo yaliyotajwa mwanzoni mwa makala hii kuhusu kutunza afya. Kadiri tunavyokuwa na afya nzuri, ndivyo tutakavyokuwa na nguvu za kuhimili wakati na baada ya kufanyiwa upasuaji wowote. Pia, tunaweza kupunguza uwezekano wa kufanyiwa upasuaji wa dharura kwa kudumisha nyumba zetu na mahali tunapofanyia kazi pakiwa salama na kwa kutii kabisa sheria za barabarani.

Kwa sababu tunathamini zawadi ya uhai, tunajaza hati ya mamlaka ya kudumu ya uwakilishi na kuibeba nyakati zote (Tazama fungu la 15) d

15. (a) Kwa nini ni muhimu kubeba hati ya mamlaka ya kudumu ya uwakilishi yenye habari za karibuni zaidi? (Tazama pia picha.) (b) Kama inavyoonyeshwa kwenye video, tunawezaje kufanya maamuzi mazuri kuhusu matibabu yanayohusisha damu?

15 Kwa kuwa tunathamini zawadi ya uhai, tunajaza hati ya mamlaka ya kudumu ya uwakilishi (mwelekezo wa mapema kuhusu tiba) na kuibeba nyakati zote. b Kupitia hati hiyo, tunaonyesha maamuzi yetu kuhusu kutiwa damu mishipani na kuhusu matibabu mengine. Je, hati yako ya mamlaka ya kudumu ya uwakilishi ina habari za karibuni zaidi? Ikiwa unahitaji kujaza au kurekebisha habari zilizopo, usiahirishe jambo hilo. Tukieleza waziwazi maamuzi yetu kwa kuyaandika, hilo litatusaidia kuepuka kuchelewesha matibabu yetu isivyo lazima. Pia, kufanya hivyo kutaepusha madaktari kutupatia matibabu yanayoweza kutudhuru. c

16. Tunaweza kufanya nini ikiwa hatuna uhakika wa jinsi ya kujaza hati ya mamlaka ya kudumu ya uwakilishi?

16 Hata iwe sisi ni vijana au tuna afya kadiri gani, sisi sote tunaweza kupatwa na ugonjwa au aksidenti. (Mhu. 9:11) Hivyo, kwa hakika ni jambo la hekima kujaza hati ya mamlaka ya kudumu ya uwakilishi. Kama huna uhakika wa jinsi ya kujaza hati hiyo, waombe msaada wazee wa kutaniko lenu. Wanajitahidi kufahamu vizuri jinsi ya kujaza hati hiyo, lakini hawatakufanyia maamuzi ya kitiba. Hilo ni jukumu lako. (Gal. 6:4, 5) Hata hivyo, wanaweza kukusaidia unapojaza hati hiyo.

UWE MWENYE USAWAZIKO

17. Tunaweza kuonyeshaje usawaziko inapohusu suala la afya?

17 Maamuzi mengi tunayofanya kuhusu afya yetu na matibabu, yanaongozwa na dhamiri yetu iliyozoezwa na Biblia. (Mdo. 24:16; 1 Tim. 3:9) Tunapofanya maamuzi na kuyazungumzia pamoja na wengine, ni vema kutumia kanuni hii inayopatikana kwenye Wafilipi 4:5: “Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote.” Tunapokuwa na usawaziko, hatuhangaikii kupita kiasi afya yetu ya kimwili, au kuwashinikiza wengine wafuate maoni yetu kuhusu afya. Tunawapenda na kuwaheshimu ndugu na dada zetu, hata ikiwa wanafanya maamuzi tofauti na yetu.​—Rom. 14:10-12.

18. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunathamini zawadi ya uhai?

18 Tunaonyesha uthamini wetu kwa Yehova, Chanzo cha uhai, kwa kulinda uhai wetu na kumpa kilicho bora kulingana na uwezo wetu. (Ufu. 4:11) Kwa sasa, ni lazima tukabiliane na magonjwa na majanga mbalimbali. Lakini haya si maisha ambayo Muumba wetu alikusudia tuwe nayo. Hivi karibuni atatupatia uzima wa milele bila maumivu na kifo. (Ufu. 21:4) Hata hivyo, kwa sasa tunafurahi sana kuwa hai na kumtumikia Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo, Yehova!

WIMBO 140 Uzima wa Milele—Hatimaye!

a Makala hii itatusaidia kusitawisha uthamini kwa ajili ya zawadi ya Mungu ya uhai. Tutaona hatua hususa ambazo tunaweza kuchukua ili kulinda afya na uhai wetu msiba wa asili unapotokea na pia kupunguza uwezekano wa aksidenti mbaya kutokea. Pia, tutazungumzia mambo tunayopaswa kufanya ili kujitayarisha kwa ajili ya matibabu ya dharura.

b Pia, hati hiyo inaitwa DPA.

d MAELEZO YA PICHA: Ndugu kijana akijaza hati ya mamlaka ya kudumu ya uwakilishi na anahakikisha kwamba anaibeba.