Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 12

Jifunze Mengi Zaidi Kumhusu Yehova Kupitia Uumbaji Wake

Jifunze Mengi Zaidi Kumhusu Yehova Kupitia Uumbaji Wake

“Sifa zake zisizoonekana, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kupitia vitu vilivyoumbwa.”​—ROM. 1:20.

WIMBO 6 Mbingu Zatangaza Utukufu wa Mungu

MUHTASARI a

1. Taja njia moja iliyomsaidia Ayubu kumjua Yehova vizuri zaidi.

 KATI ya mazungumzo yote ambayo Ayubu alikuwa nayo maishani, pindi moja kihususa ilikuwa yenye kutokeza, yaani, mazungumzo aliyokuwa nayo pamoja na Yehova Mungu. Ili kuimarisha uhakika wa Ayubu katika hekima na uwezo Wake wa kuwatunza watumishi Wake, Yehova alimwambia Ayubu aangalie baadhi ya vitu vyenye kustaajabisha alivyoumba. Kwa mfano, Ayubu alikumbushwa kwamba Mungu anaandalia wanyama mahitaji yao, hivyo angeweza pia kumtunza Ayubu. (Ayu. 38:39-41; 39:1, 5, 13-16) Kwa kuchunguza uumbaji, Ayubu alijifunza mambo mengi kuhusu sifa za Mungu wake.

2. Kwa nini nyakati nyingine huenda isiwe rahisi kuchunguza uumbaji wa Yehova?

2 Sisi pia tunaweza kujifunza mengi zaidi kumhusu Mungu wetu kwa kuchunguza kazi zake za uumbaji. Hata hivyo, huenda sikuzote isiwe rahisi kufanya hivyo. Ikiwa tunaishi jijini, huenda isiwe rahisi kuona vitu vingi ambavyo Yehova ameumba. Hata ikiwa tunaishi nje ya mji, huenda tukahisi kwamba tuna muda mchache wa kuchunguza uumbaji wa Yehova. Hivyo, acheni tuzungumzie kwa nini ni muhimu kutenga wakati na kufanya jitihada ili kuchunguza uumbaji. Tutachunguza jinsi Yehova na Yesu walivyotumia uumbaji kufundisha na mambo tunayoweza kufanya ili kujifunza zaidi kutokana na uumbaji.

KWA NINI TUNAPASWA KUCHUNGUZA UUMBAJI?

Yehova alitaka Adamu afurahie uumbaji Wake na awape majina wanyama (Tazama fungu la 3)

3. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova alitaka Adamu afurahie uumbaji?

3 Yehova alitaka mwanadamu wa kwanza afurahie uumbaji Wake. Mungu alipomuumba Adamu, alimpatia paradiso maridadi ili aichunguze na alimpa mgawo wa kuilima na kuongeza eneo la paradiso hiyo. (Mwa. 2:8, 9, 15) Wazia Adamu alivyosisimka alipoona mbegu zikiota na maua yakichanua. Adamu alikuwa na pendeleo kubwa sana la kutunza bustani ya Edeni! Pia, Yehova alimpa Adamu mgawo wa kuwapa majina wanyama. (Mwa. 2:19, 20) Yehova angeweza kuwapatia majina mwenyewe; lakini alimpatia mgawo huo Adamu. Bila shaka, kabla ya kuamua jina la kuwapa, Adamu aliwachunguza kwa makini wanyama hao, akiangalia kihususa sifa na tabia zao. Ni lazima Adamu alifurahia kazi hiyo. Bila shaka, kufanya kazi hiyo kulimpatia fursa ya kuongeza uthamini wake kwa hekima na ubunifu wa Baba yake.

4. (a) Kwa nini tunapaswa kuchunguza uumbaji? (b) Unathamini hasa kazi gani za uumbaji?

4 Sababu moja inayotufanya tuchunguze uumbaji ni kwamba Yehova anataka tufanye hivyo. Anatuambia hivi: “Inueni macho yenu mbinguni mwone.” Kisha anauliza: “Ni nani aliyeviumba vitu hivi?” Jibu liko wazi. (Isa. 40:26) Yehova hakujaza tu mbingu, bali pia dunia na bahari zikiwa na kazi zenye kustaajabisha za uumbaji ambazo zinaweza kutufundisha kumhusu yeye. (Zab. 104:24, 25) Hebu wazia jinsi Mungu alivyotuumba. Alitupatia uwezo wa kuthamini na kufurahia vitu maridadi alivyoumba. Pia, alituwezesha kufurahia uumbaji wake mbalimbali kupitia hisi zetu tano—kuona, kusikia, kugusa, kuonja, na kunusa.

5. Kulingana na Waroma 1:20, tunanufaikaje tunapochunguza uumbaji wa Yehova?

5 Biblia inafunua sababu nyingine muhimu inayotufanya tuchunguze uumbaji. Uumbaji unatufundisha kuhusu sifa za Yehova. (Soma Waroma 1:20.) Kwa mfano, fikiria kazi za ubuni ambazo Yehova ameumba. Je, hazifunui hekima ya Yehova? Na fikiria kuhusu vyakula mbalimbali tunavyoweza kufurahia. Huo ni uthibitisho ulio wazi wa upendo wake kwa wanadamu. Tunapotambua utu wa Yehova kupitia vitu alivyoumba, tunamjua vizuri zaidi na tunachochewa kumkaribia zaidi. Sasa, acheni tuzungumzie baadhi ya njia ambazo Yehova ametumia uumbaji kuwafundisha wanadamu masomo muhimu.

MUNGU ANATUMIA UUMBAJI KUTUFUNDISHA KUMHUSU

6. Tunajifunza somo gani kwa kuchunguza ndege wanaohama?

6 Yehova ana ratiba yake. Kila mwaka kati ya mwisho wa mwezi wa Februari na katikati ya mwezi wa Mei, Waisraeli wangeona ndege aina ya korongo wakipaa juu walipohama kuelekea Kaskazini. Mungu aliwaambia Waisraeli hivi: “Hata korongo angani anajua majira yake.” (Yer. 8:7) Kama tu Yehova alivyowawekea ratiba ndege hao, pia ameweka wakati hususa wa kutekeleza hukumu zake. Leo, tunapotazama ndege wanaohama, tunakumbushwa kwamba tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova ana “wakati wake uliowekwa” wa kukomesha ulimwengu huu mwovu.​—Hab. 2:3.

7. Kutazama upaaji wa ndege angani kunaweza kutupatia uhakikisho gani? (Isaya 40:31)

7 Yehova anawapa nguvu watumishi wake. Kupitia Isaya, Yehova aliahidi kwamba angewaimarisha watu wake ili “[wapae] juu kwa mabawa kama tai” wanapohisi ni dhaifu au wamevunjika moyo. (Soma Isaya 40:31.) Waisraeli walizoea kuwaona tai wakipaa juu bila kutumia jitihada nyingi. Hicho ni kikumbusho kizuri sana kwamba kama tu vile ambavyo Yehova amewapatia ndege hao nguvu, ndivyo anavyoweza pia kuwapatia nguvu watumishi wake! Unapomwona ndege mkubwa akipaa juu na juu zaidi angani bila kutumia sana mabawa yake, kumbuka kwamba Yehova anaweza kukupatia nguvu ya kukabiliana na matatizo yako.

8. Ayubu alijifunza nini kwa kuchunguza uumbaji wa Mungu, nasi tunaweza kujifunza nini?

8 Yehova anastahili kutumainiwa. Yehova alimsaidia Ayubu amtumaini zaidi. (Ayu. 32:2; 40:6-8) Katika mazungumzo pamoja na Ayubu, Mungu alirejelea kazi nyingi za uumbaji, kutia ndani nyota, mawingu, na umeme wa radi. Pia, Yehova aliwataja wanyama kama vile fahali mwitu na farasi. (Ayu. 38:32-35; 39:9, 19, 20) Vitu hivyo vyote havikuthibitisha tu nguvu kubwa ya Mungu, bali pia upendo na hekima yake kuu. Kwa sababu ya mazungumzo hayo, Ayubu alimtumaini zaidi Yehova kuliko wakati mwingine wowote. (Ayu. 42:1-6) Vivyo hivyo, tunapochunguza uumbaji, tunakumbushwa kwamba Yehova ana hekima na nguvu nyingi sana kuliko sisi. Pia, anaweza na atayaondoa majaribu yetu yote. Ukweli huo unaweza kutusaidia kumtumaini zaidi.

YESU ALITUMIA UUMBAJI KUFUNDISHA KUMHUSU BABA YAKE

9-10. Tunajifunza nini kumhusu Yehova kupitia jua na mvua?

9 Yesu alifahamu mengi sana kuhusu uumbaji. Akiwa “mfanyakazi stadi” alikuwa na pendeleo la kufanya kazi na Baba yake alipouumba ulimwengu. (Met. 8:30) Baadaye, Yesu alipokuwa duniani, alitumia uumbaji kuwafundisha wanafunzi wake kumhusu Baba yake. Fikiria masomo machache aliyofundisha.

10 Yehova anaonyesha upendo wake kwa kila mtu. Katika Mahubiri ya Mlimani, Yesu aliwasaidia wanafunzi wake wakazie fikira kuhusu mambo mawili katika uumbaji ambayo watu wengi wanachukulia kivivi hivi: mvua na jua. Mambo hayo mawili ni muhimu ili kuendeleza uhai. Yehova angeweza kuwanyima vitu hivyo wanadamu wasiostahili. Badala yake, kwa upendo anawaangazia jua na kuwapatia mvua watu wote. (Mt. 5:43-45) Yesu alitumia somo hilo kuwafundisha wanafunzi wake kwamba Yehova anataka tumwonyeshe upendo kila mtu. Tunapofurahia machweo ya jua yenye kupendeza au mvua yenye kuburudisha, tunaweza kutafakari kuhusu upendo wa Yehova usio na ubaguzi. Mfano wake unatuchochea kuonyesha upendo kama huo kwa kuwahubiria watu wote.

11. Kuwatazama ndege wa angani kunawezaje kututia moyo?

11 Yehova anatuandalia mahitaji yetu ya kimwili. Katika mahubiri hayohayo, Yesu alisema hivi pia: “Waangalieni kwa makini ndege wa angani; hawapandi mbegu, hawavuni, wala kukusanya ghalani, na bado Baba yenu wa mbinguni huwalisha.” Inawezekana kwamba wale waliokuwa wakimsikiliza Yesu wangeweza kuona ndege wakipaa juu alipowauliza hivi: “Je, ninyi si wenye thamani kuliko wao?” (Mt. 6:26) Hiyo ni njia yenye upendo sana ya kutuhakikishia kwamba Yehova atatuandalia mahitaji yetu ya kimwili! (Mt. 6:31, 32) Somo hilo tunalojifunza kutokana na uumbaji linaendelea kuwatia moyo watumishi waaminifu. Dada kijana painia kutoka nchini Hispania, alikuwa amevunjika moyo kwa sababu hakuweza kupata sehemu nzuri ya kuishi. Lakini alipoona ndege wakila mbegu na beri, alitiwa moyo. Anasema, “Ndege hao walinikumbusha kwamba Yehova alikuwa anawatunza na kwamba atanitunza mimi pia.” Muda mfupi baada ya hapo dada huyo alipata mahali pa kuishi.

12. Kulingana na Mathayo 10:29-31, shore wanatufundisha nini kumhusu Yehova?

12 Yehova anatuthamini tukiwa mtu mmoja-mmoja. Kabla ya kuwatuma mitume wake kwenda kuhubiri, Yesu aliwasaidia wasiogope upinzani. (Soma Mathayo 10:29-31.) Alifanya hivyo kwa kuzungumzia ndege waliojulikana sana huko Israeli: shore. Ndege hao walikuwa na thamani ndogo katika siku za Yesu. Lakini aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Hakuna hata mmoja wao atakayeanguka chini bila Baba yenu kujua.” Kisha akasema hivi: “Ninyi ni wenye thamani kuliko shore wengi.” Hivyo, Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake kwamba Yehova aliwathamini wakiwa mtu mmoja-mmoja, kwa hiyo hawakuwa na sababu yoyote ya kuogopa mateso. Hapana shaka kwamba wanafunzi hao walikumbuka maneno ya Yesu walipoona shore wakati wakihubiri katika miji na vijiji. Kila unapomwona ndege mdogo, kumbuka kwamba Yehova anakuthamini wewe binafsi kwa sababu wewe pia “ni [mwenye] thamani kuliko shore wengi.” Kwa msaada wa Yehova, unaweza kukabili upinzani bila woga.​—Zab. 118:6.

TUNAWEZAJE KUJIFUNZA MENGI ZAIDI KUMHUSU MUNGU KUPITIA UUMBAJI?

13. Ni nini kitakachotusaidia kujifunza kutokana na uumbaji?

13 Tunaweza kujifunza masomo mengi zaidi kumhusu Yehova kupitia uumbaji. Jinsi gani? Kwanza, tunapaswa kutenga wakati ili kuchunguza uumbaji. Kisha, tunahitaji kutafakari kile ambacho unatufundisha kumhusu Yehova. Huenda sikuzote isiwe rahisi kwetu kufanya hivyo. Géraldine, dada kutoka nchini Kamerun, anasema, “Nililelewa jijini, hivyo nilitambua kwamba nilihitaji kujitahidi zaidi ili kuchunguza uumbaji.” Mzee wa kutaniko anayeitwa Alfonso anasema hivi: “Nimejifunza kwamba ninahitaji kutenga wakati wa kuwa peke yangu ili kuchunguza uumbaji wa Yehova na kutafakari kile ambacho unanifundisha kumhusu.”

Alipotazama uumbaji uliomzunguka, Daudi alitafakari kuhusu kile ambacho ulimfundisha kumhusu Yehova (Tazama fungu la 14)

14. Daudi alijifunza nini alipotafakari kuhusu uumbaji wa Mungu?

14 Daudi alitafakari kwa kina kuhusu uumbaji wa Mungu. Alimwambia Yehova hivi: “Ninapoziona mbingu zako, kazi za vidole vyako, mwezi na nyota ambazo umetayarisha, mwanadamu anayeweza kufa ni nini hivi kwamba unamweka akilini?” (Zab. 8:3, 4) Naam, Daudi alipotazama anga la usiku hakufurahia tu kutazama nyota, bali pia alitafakari kuhusu mambo ambayo nyota zilimfundisha kumhusu Mungu. Alijifunza jinsi Yehova alivyo mkuu. Nyakati nyingine, Daudi alitafakari kuhusu jinsi mwili wake ulivyokua tumboni mwa mama yake. Alipotafakari kuhusu mambo hayo yenye kustaajabisha, alithamini hata zaidi hekima ya Yehova.​—Zab. 139:14-17.

15. Toa mifano ya jinsi ambavyo umejionea sifa za Yehova katika uumbaji. (Zaburi 148:7-10)

15 Kama Daudi, huhitaji kwenda mbali ili upate jambo la kutafakari katika uumbaji. Ukitazama mazingira yako, unaweza kutambua sifa nyingi za Yehova. Kwa mfano, unaweza kutambua nguvu za Yehova unapohisi joto la jua kwenye ngozi yako. (Yer. 31:35) Fikiria kuhusu hekima ya Yehova unapomwona ndege akijenga kiota chake. Fikiria kuhusu ucheshi wa Yehova unapomwona mtoto wa mbwa akikimbiza mkia wake. Na mshukuru Yehova kwa upendo wake unapomwona mama akicheza na mtoto wake mchanga. Tuna fursa nyingi sana za kujifunza kumhusu Yehova kwa sababu uumbaji wake wote—mkubwa na mdogo, ulio karibu na ulio mbali—unamtukuza yeye.​—Soma Zaburi 148:7-10.

16. Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

16 Mungu wetu ana hekima, upendo, na nguvu zisizo na kifani, na kila kitu alichoumba kinapendeza. Sifa hizo na nyingine nyingi zinaonekana wazi ikiwa tutazitafuta katika uumbaji. Acheni sote tutenge wakati kwa ukawaida ili kufurahia uumbaji na kutafakari kuhusu kile ambacho unatufundisha kumhusu Yehova. Kwa kufanya hivyo, tutamkaribia Muumba wetu hata zaidi. (Yak. 4:8) Katika makala inayofuata, tutaona jinsi wazazi wanavyoweza kutumia uumbaji kuwasaidia watoto wao wamkaribie Yehova.

WIMBO 5 Kazi za Mungu za Ajabu

a Uumbaji wa Yehova ni wenye kustaajabisha. Tunastaajabishwa na kazi zake kama vile jua lenye nguvu nyingi na maua maridadi. Mambo tunayojifunza kutokana na uumbaji yanaweza pia kutusaidia kutambua sifa za utu wa Yehova. Katika makala hii, tutazungumzia kwa nini tunapaswa kutenga wakati ili kuchunguza uumbaji na pia jinsi kufanya hivyo kunavyoweza kutusaidia kumkaribia Mungu zaidi.