Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

1923​—⁠Miaka Mia Moja Iliyopita

1923​—⁠Miaka Mia Moja Iliyopita

GAZETI la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1923, lilisema hivi: “Tunatarajia mwaka wa 1923 uwe wenye kusisimua sana. Tuna pendeleo kubwa la kuutolea ushahidi . . . ulimwengu uliokandamizwa na kuwaonyesha watu kwamba kutakuwa na wakati ujao mzuri.” Mwaka huo Wanafunzi wa Biblia walitiwa moyo sana kwa sababu kulianza kuwa na umoja zaidi katika ibada yao na kazi yao ya kuhubiri, umoja unaotambulisha ibada ya kweli leo.

UMOJA WA IBADA

Kalenda yenye maandiko na namba za nyimbo

Mwaka huo, tengenezo lilifanya baadhi ya mabadiliko ambayo yalisaidia kuendeleza umoja wa ibada miongoni mwa Wanafunzi wa Biblia. Gazeti Mnara wa Mlinzi lilianza kuchapisha maelezo yaliyofafanua maandiko ambayo wangezungumzia kwenye mkutano wao wa kila juma wa Sala, Sifa, na Ushuhuda. Isitoshe, Wanafunzi wa Biblia walichapisha kalenda iliyoorodhesha maandiko kwa ajili ya kila juma na pia nyimbo ambazo wangeimba wakati wa funzo lao la kibinafsi na ibada ya familia.

Katika mikutano yao, Wanafunzi wa Biblia walitoa “ushuhuda” uliotia ndani mambo waliyojionea katika utumishi wa shambani, maelezo ya kumshukuru Yehova, wimbo, na hata sala. Eva Barney, aliyebatizwa mwaka wa 1923 akiwa na umri wa miaka 15, anakumbuka hivi: “Ikiwa ungetaka kutoa ushuhuda ungesimama na kuanza kusema, ‘Ningependa kumshukuru Bwana kwa wema wake wote kunielekea.’” Baadhi ya akina ndugu walipenda kutoa ushuhuda lakini Dada Barney aliendelea kusema hivi: “Ndugu mpendwa Godwin aliyekuwa amezeeka alikuwa na mambo mengi ya kumshukuru Bwana. Lakini mke wake alipoona kwamba ndugu aliyekuwa akiongoza ameanza kuhangaika, alikuwa akivuta koti la mume wake naye angeketi.”

Mara moja kwa mwezi, kila darasa (kutaniko) lilikuwa na mkutano wa pekee wa Sala, Sifa, na Ushuhuda. Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Aprili 1, 1923, lilifafanua hivi mkutano huo: “Nusu ya mkutano huu inapaswa kutumiwa kutoa ushuhuda kuhusu kazi ya kuhubiri na kuwatia moyo wafanyakazi. . . . Tunaamini kwamba utendaji huu wa umoja utawasaidia akina ndugu na dada wawe na uhusiano wa karibu zaidi.”

Charles Martin, mfanyakazi wa darasa (au mhubiri wa kutaniko) mwenye umri wa miaka 19, kutoka Vancouver, Kanada, alinufaika sana na mikutano hiyo. Baadaye, alikumbuka hivi: “Katika mikutano hiyo ndipo nilipojifunza mambo ya kusema katika utumishi wa nyumba kwa nyumba. Mara kwa mara, watu wangesimulia mambo ambayo walijionea katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Hilo lilinisadia kujua mambo ninayoweza kusema na jinsi ya kujibu vipingamizi mbalimbali.”

WAABUDU KWA UMOJA

Chapisho la Bulletin la Mei 1, 1923

“Siku za utumishi” pia zilichangia umoja katika tengenezo. Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Aprili 1, 1923, lilitangaza hivi: “Ili kuwe na umoja katika utendaji . . . , Jumanne, Mei 1, 1923, imechaguliwa kuwa siku ya kushiriki katika utumishi. Baada ya hapo, itakuwa hivyo pia kwa Jumanne ya kwanza ya kila mwezi . . . Kila mshiriki katika kila darasa anapaswa kushiriki katika kazi hiyo.”

Hata Wanafunzi wa Biblia wenye umri mdogo walishiriki katika kazi hiyo. Dada Hazel Burford, ambaye alikuwa na umri wa miaka 16 tu, anakumbuka hivi: “Chapisho la Bulletin liliandaa mapendekezo ya kutumia katika utumishi ambayo tuliyakariri. a Nikiwa pamoja na babu yangu, nilishiriki kwa bidii katika utendaji huo wote.” Hata hivyo, Dada Burford alipata upinzani kutoka katika chanzo kisichotarajiwa. Alisema hivi: “Ndugu mmoja mpendwa aliyezeeka hakutaka kabisa nizungumze na watu. Wakati huo, baadhi ya watu hawakuelewa kwamba Wanafunzi wote wa Biblia, kutia ndani ‘vijana wa kiume na kike’ wanapaswa kushiriki katika kumsifu Muumba wetu Mkuu.” (Zab. 148:​12, 13) Lakini Dada Burford aliendelea kuhubiri. Baadaye, alihudhuria darasa la pili la Shule ya Gileadi na akatumikia akiwa mmishonari huko Panama. Baada ya muda kupita, ndugu hao walibadili mtazamo wao kuhusu vijana kushiriki katika huduma.

MAKUSANYIKO YALILETA UMOJA

Makusanyiko yaliwasaidia pia akina ndugu wawe na umoja. Makusanyiko mengi kati ya hayo yalikuwa na siku za utumishi, kama vile kusanyiko lililofanywa huko Winnipeg, Kanada. Katika kusanyiko hilo, siku ya Machi 31, wahudhuriaji wote walialikwa kuhubiri katika jiji hilo. Siku hizo za utumishi ziliweka msingi wa ukuzi wa baadaye. Inakadiriwa kwamba watu 7,000 walihudhuria kusanyiko lingine huko Winnipeg, Agosti 5, 1923. Wakati huo, hilo ndilo lilikuwa hudhurio la juu zaidi katika kusanyiko huko Kanada.

Kusanyiko muhimu sana la watu wa Yehova mwaka wa 1923 lilifanywa Agosti 18-26 huko Los Angeles, California. Katika majuma yaliyotangulia kusanyiko hilo, magazeti ya habari yalikuwa na matangazo ya tukio hilo na Wanafunzi wa Biblia waligawa mialiko zaidi ya 500,000. Mabango ya matangazo yaliwekwa kwenye magari ya umma na magari ya watu binafsi.

Kusanyiko la Wanafunzi wa Biblia la mwaka wa 1923 huko Los Angeles

Jumamosi, Agosti 25, Ndugu Rutherford alitoa hotuba yenye kichwa “Kondoo na Mbuzi,” ambayo ilitambulisha waziwazi “kondoo” kuwa watu wenye mwelekeo unaofaa ambao wangeishi katika paradiso duniani. Pia, alitoa azimio lililoitwa “Onyo.” Azimio hilo lilifunua uwongo wa dini zinazodai kuwa za Kikristo na kuwahimiza watu wenye mioyo minyoofu wajitenge na “Babiloni Mkubwa.” (Ufu. 18:​2, 4) Baadaye, Wanafunzi wa Biblia wenye bidii ulimwenguni kote walisambaza mamilioni ya nakala za azimio hilo.

“Utendaji huu wa umoja utawasaidia akina ndugu na dada wawe na uhusiano wa karibu zaidi”

Siku ya mwisho ya kusanyiko hilo, wahudhuriaji zaidi ya 30,000 walimsikiliza Ndugu Rutherford akitoa hotuba yenye kichwa “Mataifa Yote Yapiga Mwendo Kuelekea Har–​Magedoni, Lakini Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe.” Kwa kuwa walitarajia idadi kubwa ya wahudhuriaji, Wanafunzi wa Biblia walikodi uwanja mpya wa Los Angeles Coliseum. Ili kuhakikisha kila mtu anasikia, akina ndugu walitumia mfumo wa kupaza sauti katika uwanja huo, hiyo ilikuwa teknolojia mpya wakati huo. Wengine wengi walisikiliza programu hiyo kupitia redio.

UKUZI WA KIMATAIFA

Mwaka wa 1923, kulikuwa na ukuzi mkubwa wa kazi ya kuhubiri barani Afrika, Ulaya, India, na Amerika Kusini. Huko India, A. J. Joseph ambaye alikuwa na mke na watoto sita, alisimamia kutokezwa kwa machapisho katika Kihindi, Kitamili, Kitelugu, na Kiurdu.

William R. Brown na familia yake

Huko Sierra Leone, Wanafunzi wa Biblia Alfred Joseph na Leonard Blackman waliandika barua kwa makao makuu ya ulimwenguni pote huko Brooklyn, New York, wakiomba msaada. Aprili 14, 1923, ombi lao lilijibiwa. Alfred alisema hivi: “Jumamosi moja usiku, nilipokea simu ambayo sikutarajia.” Alisikia sauti nzito ikimuuliza hivi: “Je, wewe ndiye uliyeandika barua kwa Shirika la Watch Tower ukiuliza kuhusu wahubiri?” Alfred akajibu: “Ndiyo.” Sauti kwenye simu ikajibu: “Basi wamenituma mimi.” Ilikuwa sauti ya William R. Brown. Alikuwa amewasili siku hiyo kutoka Karibea pamoja na mke wake, Antonia, na binti zao wadogo Louise na Lucy. Akina ndugu hawakuhitaji kusubiri muda mrefu ili kukutana na Ndugu Brown na familia yake.

Alfred aliendelea kusema hivi: “Asubuhi iliyofuata, mimi na Leonard tulikuwa tukifanya funzo letu la kila juma la Biblia, kisha ghafla tukamwona mwanamume mrefu mlangoni. Alikuwa Ndugu Brown. Alikuwa na bidii sana katika kweli hivi kwamba alitaka kutoa hotuba ya watu wote siku iliyofuata.” Katika muda usiozidi mwezi mmoja, Ndugu Brown alikuwa amewaachia watu machapisho yote ambayo alikuwa amekuja nayo. Baada ya muda mfupi, alipokea vitabu 5,000 zaidi, na punde si punde alihitaji vitabu vingine vingi zaidi. Lakini Ndugu Brown hakujulikana kuwa muuzaji wa vitabu. Katika miaka mingi ambayo alitumikia akiwa mtumishi wa Yehova mwenye bidii, mara nyingi alirejelea Maandiko katika hotuba zake na hivyo akajulikana kama Bible Brown.

Betheli ya Magdeburg, miaka ya 1920

Wakati huohuo, ofisi ya tawi iliyokuwa huko Barmen, Ujerumani, ilikuwa imejaa watu wengi, na jiji hilo lilikabili hatari ya kuvamiwa na nchi jirani ya Ufaransa. Wanafunzi wa Biblia walipata jengo fulani huko Magdeburg ambalo lilionekana kwamba linafaa kwa ajili ya shughuli za uchapishaji. Juni 19, akina ndugu walimaliza kupakia vifaa vya uchapishaji na vifaa vingine na wakahamia katika Betheli mpya huko Magdeburg. Siku moja baada ya makao makuu ya ulimwenguni pote kujulishwa kwamba shughuli za kuhama zilikuwa zimekamilika, magazeti ya habari yalitangaza kwamba Ufaransa ilikuwa imeteka jiji la Barmen. Akina ndugu waliona jambo hilo kuwa uthibitisho wa ulinzi na baraka za Yehova.

George Young pamoja na Sarah Ferguson (kulia) na dada yake

Huko Brazili, George Young, ambaye alisafiri sana ili kutangaza habari njema, alianzisha ofisi mpya ya tawi na akaanza kuchapisha gazeti la Mnara wa Mlinzi katika Kireno. Katika muda wa miezi michache tu, aliwaachia watu zaidi ya machapisho 7,000. Sarah Ferguson alisisimka sana Ndugu Young alipotembelea familia yao huko Brazili. Sarah alikuwa akisoma gazeti Mnara wa Mlinzi tangu mwaka wa 1899, lakini hakuwa amefaulu kuonyesha wakfu wake kwa kubatizwa kwenye maji. Miezi michache baadaye, hatimaye Dada Ferguson na watoto wake wanne walifaulu kuchukua hatua hiyo muhimu.

“KUSHANGILIA TUNAPOMTUMIKIA MUNGU”

Mwishoni mwa mwaka huo, matokeo ya jitihada za Wanafunzi wa Biblia za kuwa na umoja katika ibada yalitajwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Desemba 15, 1923: “Inaonekana wazi kwamba madarasa . . . yako katika hali nzuri ya kiroho . . . Acheni tuwe tayari, tuongeze bidii, tuazimie kusonga mbele katika mwaka unaokuja, na kushangilia tunapomtumikia Mungu.”

Mwaka uliofuata ulikuwa mwaka wa kusisimua sana kwa Wanafunzi wa Biblia. Akina ndugu huko Betheli walikuwa wakifanya kazi kwa miezi mingi kwenye eneo fulani huko Staten Island, mwendo mfupi kutoka makao makuu huko Brooklyn. Majengo yaliyojengwa kwenye eneo hilo jipya yalikamilishwa mwanzoni mwa mwaka wa 1924, na yalisaidia kuleta umoja kati ya akina ndugu na kueneza habari njema kwa njia ambazo hazingewezekana kabla ya hapo.

Kikundi cha wajenzi huko Staten Island

a Sasa ni Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo.