Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 43

“Atawatia Nguvu”​—⁠Jinsi Gani?

“Atawatia Nguvu”​—⁠Jinsi Gani?

“[Yehova] atawafanya muwe imara, atawatia nguvu, atawapa msingi imara.”—1 PET. 5:10.

WIMBO 38 Atakupa Nguvu

MUHTASARI a

1. Waabudu wa Yehova walitiwaje nguvu nyakati za kale?

 MARA nyingi, Neno la Mungu huwafafanua wanaume waaminifu kuwa wenye nguvu. Lakini hata wale waliokuwa na nguvu zaidi miongoni mwao hawakuhisi kwamba wana nguvu sikuzote. Kwa mfano, pindi fulani Mfalme Daudi alihisi kwamba alikuwa “imara kama mlima,” lakini katika pindi nyingine ‘aliogopa.’ (Zab. 30:7) Ingawa Samsoni alikuwa na nguvu nyingi zisizo za kawaida alipochochewa na roho ya Mungu, alitambua kwamba bila kupata nguvu zinazotoka kwa Mungu, angekuwa dhaifu kama wanadamu wengine wote. (Amu. 14:​5, 6; 16:17) Wanaume hao waaminifu walikuwa na nguvu kwa sababu tu Yehova aliwapa nguvu.

2. Kwa nini mtume Paulo alisema kwamba alikuwa dhaifu na pia mwenye nguvu? (2 Wakorintho 12:​9, 10)

2 Mtume Paulo alisema kwamba yeye pia alihitaji nguvu kutoka kwa Yehova. (Soma 2 Wakorintho 12:​9, 10.) Kama wengi kati yetu, Paulo alipambana na matatizo ya kiafya. (Gal. 4:​13, 14) Pia, wakati mwingine ilikuwa vigumu kwake kufanya mambo yaliyo sawa. (Rom. 7:​18, 19) Na wakati mwingine alikuwa na wasiwasi na hakuwa na uhakika kuhusu mambo ambayo yangempata. (2 Kor. 1:​8, 9) Ingawa hivyo, Paulo alipokuwa dhaifu, alikuwa mwenye nguvu. Jinsi gani? Yehova alimpa Paulo nguvu alizohitaji. Alimwimarisha Paulo.

3. Tutajibu maswali gani katika makala hii?

3 Yehova anaahidi kwamba atatutia nguvu pia. (1 Pet. 5:10) Lakini hatuwezi kutarajia kupata nguvu hizo bila kufanya jitihada zozote. Kwa mfano, injini inaweza kulipa gari nguvu za kusonga mbele. Hata hivyo, ni lazima dereva akanyage pedali ya mafuta ili gari lisonge. Vivyo hivyo, Yehova yuko tayari kutupa nguvu tunazohitaji, lakini tunapaswa kuchukua hatua fulani ili tunufaike kutokana na nguvu hizo. Ni nini ambacho Yehova ametuandalia ili kutupatia nguvu? Na tunahitaji kufanya nini ili tupokee nguvu hizo? Tutapata majibu ya maswali hayo kwa kuchunguza jinsi Yehova alivyowatia nguvu watu watatu wanaotajwa katika Biblia, yaani, nabii Yona, Maria mama ya Yesu, na mtume Paulo. Pia, tutaona jinsi Yehova anavyowatia nguvu watumishi wake leo kwa njia kama hizo.

PATA NGUVU KUPITIA SALA NA KUJIFUNZA

4. Tunawezaje kupokea nguvu kutoka kwa Yehova?

4 Njia moja ambayo tunaweza kupokea nguvu kutoka kwa Yehova ni kwa kusali kwake. Yehova anajibu sala zetu kwa kutupatia “nguvu zinazopita zile za kawaida.” (2 Kor. 4:7) Pia, tunaweza kutiwa nguvu kwa kusoma Neno lake na kulitafakari. (Zab. 86:11) Ujumbe ambao Yehova ametupatia katika Biblia ni ‘wenye nguvu.’ (Ebr. 4:12) Unaposali kwa Yehova na kusoma Neno lake, utapata nguvu unazohitaji ili uendelee kuvumilia, kudumisha shangwe yako, na kutimiza mgawo mgumu. Ona jinsi Yehova alivyomtia nguvu nabii Yona.

5. Kwa nini nabii Yona alihitaji kutiwa nguvu?

5 Nabii Yona alihitaji kutiwa nguvu. Alikuwa amekimbia mgawo mgumu ambao Yehova alikuwa amempa. Matokeo ni kwamba alikuwa karibu kupoteza uhai wake katika dhoruba kali sana na alihatarisha uhai wa wasafiri wenzake katika meli. Alipotupwa baharini, alijikuta mahali ambapo hakuwahi kufika kabla ya hapo—alikuwa gizani ndani ya tumbo la samaki mkubwa. Unafikiri Yona alihisije? Je, alitarajia kwamba angekufa akiwa humo ndani? Je, alihisi kwamba Yehova amemwacha? Ni wazi kwamba Yona alikuwa na wasiwasi mwingi.

Kama nabii Yona, tunawezaje kupata nguvu tunapokabili jaribu? (Tazama fungu la 6-9)

6. Kulingana na Yona 2:​1, 2, 7, ni nini kilichomwimarisha Yona alipokuwa katika tumbo la samaki?

6 Yona alifanya nini ili apate nguvu akiwa katika tumbo la samaki? Jambo moja alilofanya ni kusali. (Soma Yona 2:​1, 2, 7.) Ingawa alikuwa amekosa kumtii Yehova, Yona alikuwa na uhakika kwamba Yehova angesikiliza sala yake ya unyenyekevu na kukubali toba yake. Yona pia alitafakari kuhusu Maandiko. Kwa nini tunasema hivyo? Katika sala yake iliyoandikwa kwenye Yona sura ya 2, anatumia maneno na misemo kama ile inayopatikana katika kitabu cha Zaburi. (Kwa mfano, linganisha Yona 2:​2, 5 na Zaburi 69:1; 86:7.) Ni wazi kwamba Yona alifahamu maandiko hayo vizuri. Na alipoyatafakari wakati alipopatwa na taabu, alipata uhakika kwamba Yehova angemsaidia. Baadaye, Yona alirudishwa kwenye nchi kavu na alikuwa tayari kukubali na kutimiza mgawo ambao angepewa.—Yona 2:10–3:4.

7-8. Ndugu mmoja nchini Taiwan amepokeaje nguvu anapokabiliana na matatizo mbalimbali?

7 Mfano wa Yona unaweza kutusaidia tunapokabili majaribu mbalimbali. Kwa mfano, Zhiming, b ndugu anayeishi nchini Taiwan, anakabili matatizo mbalimbali makubwa ya kiafya. Isitoshe, anavumilia upinzani mkali kutoka kwa watu wa familia yake kwa sababu ya imani yake katika Yehova. Anapata nguvu kutoka kwa Yehova kupitia kusali na kujifunza. Anasema hivi: “Wakati mwingine matatizo yanapotokea, ninakuwa na mahangaiko sana hivi kwamba inakuwa vigumu kuwa mtulivu na ninashindwa kujifunza kibinafsi.” Lakini hakati tamaa. Anasema hivi: “Kwanza, ninasali kwa Yehova, kisha ninasikiliza nyimbo zetu za Ufalme. Wakati mwingine, hata ninaimba kwa sauti ya chini hadi ninapopata utulivu. Halafu ninaanza kujifunza.”

8 Kujifunza kibinafsi kumemwimarisha Zhiming kwa njia ambazo hakutarajia. Kwa mfano, baada ya kufanyiwa upasuaji mkubwa, muuguzi alikuja na kumwambia kwamba kwa sababu alikuwa na kiwango kidogo cha chembe nyekundu, angehitaji kuongezwa damu mwilini. Usiku kabla ya kufanyiwa upasuaji, Zhiming alikuwa amesoma kuhusu dada ambaye alifanyiwa upasuaji kama huo. Dada huyo alikuwa na kiwango cha chini hata zaidi cha chembe nyekundu za damu; ingawa hivyo, hakukubali kuongezwa damu mwilini na alipona. Kisa cha dada huyo kilimwimarisha Zhiming ili aendelee kuwa mwaminifu.

9. Ikiwa jaribu fulani limekudhoofisha, unaweza kufanya nini? (Tazama pia picha.)

9 Unapokabili jaribu je, umewahi kuhisi kwamba kwa sababu ya mahangaiko ni vigumu kujieleza waziwazi katika sala? Au unahisi umechoka sana hivi kwamba huwezi kujifunza? Kumbuka kwamba Yehova anaelewa hali yako kikamilifu. Basi, hata unapotoa sala fupi, unaweza kuwa na uhakika kwamba atakupatia kile hasa unachohitaji. (Efe. 3:20) Ikiwa maumivu yako ya kimwili au kihisia yanafanya iwe vigumu kwako kusoma na kujifunza, unaweza kusikiliza rekodi za sauti za Biblia au machapisho yanayotegemea Biblia. Pia, unaweza kusikiliza wimbo wetu mmoja au kutazama video kwenye jw.org. Ukisali kwa Yehova na kutafuta majibu ya sala zako katika maandalizi ya kiroho ambayo ametupatia, utaonyesha kwamba unataka Yehova akupe nguvu.

PATA NGUVU KUTOKA KWA WAABUDU WENZAKO

10. Ndugu na dada zetu Wakristo wanatutiaje nguvu?

10 Yehova anaweza kutumia ndugu na dada zetu Wakristo ili kututia nguvu. Wanaweza kuwa “chanzo cha faraja nyingi” tunapokabili jaribu au tunapopambana ili kutimiza mgawo mgumu. (Kol. 4:​10, 11) Tunahitaji marafiki hasa katika “nyakati za taabu.” (Met. 17:17) Tunapokuwa dhaifu, waabudu wenzetu wanaweza kutusaidia kimwili, kihisia, na kiroho. Fikiria jinsi Maria, mama ya Yesu, alivyotiwa nguvu na wengine.

11. Kwa nini Maria alihitaji kutiwa nguvu?

11 Maria alihitaji kutiwa nguvu. Fikiria jinsi alivyolemewa na hisia baada ya kupokea mgawo mzito kutoka kwa malaika Gabrieli. Angekuwa mjamzito, ingawa hakuwa amefunga ndoa wakati huo. Hakuwa na uzoefu wa kulea watoto wake mwenyewe, lakini angemtunza mvulana ambaye baadaye angekuwa Masihi. Na kwa kuwa hakuwa amefanya ngono, Maria angemwelezaje jambo hilo Yosefu, mchumba wake?—Luka 1:​26-33.

12. Kulingana na Luka 1:​39-45, Maria alipokeaje nguvu alizohitaji?

12 Maria alipataje nguvu alizohitaji ili kutimiza mgawo huo mzito na usio wa kawaida? Alitafuta msaada kutoka kwa watu wengine. Kwa mfano, alimwomba malaika Gabrieli ampe habari zaidi kuhusu mgawo huo. (Luka 1:34) Muda mfupi baada ya hapo, alisafiri kwenda kwenye “eneo lenye milima” la Yuda ili kumtembelea Elisabeti, mtu wake wa ukoo. Safari hiyo ilikuwa na matokeo mazuri. Elisabeti alimpongeza Maria na aliongozwa na Yehova kusema unabii wenye kutia moyo kumhusu mwana wa Maria ambaye bado hakuwa amezaliwa. (Soma Luka 1:​39-45.) Maria alisema kwamba Yehova alikuwa “amefanya mambo makuu kwa mkono wake.” (Luka 1:​46-51) Kupitia malaika Gabrieli na Elisabeti, Yehova alimwimarisha Maria.

13. Dada mmoja nchini Bolivia alithawabishwaje kwa kutafuta msaada kutoka kwa waabudu wenzake?

13 Kama Maria, wewe pia unaweza kutiwa nguvu na waabudu wenzako. Dasuri, dada anayeishi nchini Bolivia, alihitaji kutiwa nguvu kwa njia hiyo. Baba yake alipopatikana na ugonjwa usio na tiba na kulazwa hospitalini, kwa hiari Dasuri alikubali jukumu la kumtunza. (1 Tim. 5:4) Hali haikuwa rahisi sikuzote. Anasema hivi: “Mara nyingi nilihisi kwamba siwezi kuendelea.” Je, aliomba msaada? Mwanzoni hakuomba msaada. Anasema hivi: “Sikutaka kuwasumbua ndugu zangu, nilijiambia kwamba ‘Yehova ndiye atakayenipatia msaada ninaohitaji.’ Lakini nikatambua kwamba kwa kujitenga na wengine, nilikuwa nikijaribu kutatua matatizo yangu nikiwa peke yangu.” (Met. 18:1) Dasuri aliamua kuwaandikia ujumbe baadhi ya rafiki zake na kuwaeleza hali yake. Anasema hivi: “Maneno hayatoshi kueleza jinsi nilivyotiwa nguvu na Wakristo wenzangu wapendwa. Walileta chakula hospitalini na kushiriki pamoja nami maandiko yenye kutia moyo katika Biblia. Inafurahisha sana kujua hatuko peke yetu. Sisi ni sehemu ya familia kubwa ya Yehova—familia ambayo iko tayari kukusaidia, kulia pamoja nawe, na kukutia moyo unapopambana.”

14. Kwa nini tunapaswa kukubali msaada kutoka kwa wazee wa kutaniko?

14 Njia moja ambayo Yehova anatupatia nguvu ni kupitia wazee wa kutaniko. Wao ni zawadi ambazo anatumia ili kutuimarisha na kutufariji. (Isa. 32:​1, 2) Basi unapohisi wasiwasi, waeleze wazee wa kutaniko mambo yanayokuhangaisha. Wanapokupatia msaada, usisite kuukubali. Kupitia kwao, Yehova anaweza kukupa nguvu.

PATA NGUVU KUTOKANA NA TUMAINI LAKO LA WAKATI UJAO

15. Wakristo wote wana tumaini gani lenye thamani?

15 Tumaini letu linalotegemea Biblia linaweza kutujaza nguvu. (Rom. 4:​3, 18-20) Tukiwa Wakristo, tuna tumaini lenye thamani sana la kuishi milele—iwe ni katika dunia iliyofanywa kuwa paradiso au katika Ufalme wa mbinguni. Tumaini letu linatutia nguvu ili tuendelee kuvumilia majaribu, tuhubiri habari njema, na tutimize migawo mbalimbali kutanikoni. (1 The. 1:3) Tumaini hilohilo lilimtia nguvu mtume Paulo.

16. Kwa nini mtume Paulo alihitaji kutiwa nguvu?

16 Paulo alihitaji nguvu. Katika barua yake kwa Wakorintho alijilinganisha na chombo dhaifu cha udongo. Alikuwa ‘amekandamizwa,’ ‘kufadhaishwa,’ ‘kuteswa,’ na ‘kuangushwa chini.’ Hata uhai wake ulikuwa hatarini. (2 Kor. 4:​8-10) Paulo aliandika maneno hayo katika safari yake ya tatu ya umishonari. Huenda wakati huo hakujua kwamba bado angekabili matatizo zaidi. Angeshambuliwa na umati wenye hasira, angekamatwa, angevunjikiwa na meli baharini, na kufungwa gerezani.

17. Kulingana na 2 Wakorintho 4:​16-18, nini ambacho kilimtia nguvu Paulo ili avumilie majaribu?

17 Paulo alipata nguvu za kuvumilia kwa kukazia fikira tumaini lake. (Soma 2 Wakorintho 4:​16-18.) Aliwaambia Wakorintho kwamba hata ikiwa mwili wake ulikuwa ‘ukichakaa,’ hangeruhusu hilo limvunje moyo. Paulo alikazia fikira wakati wake ujao. Tumaini lake la kuishi milele mbinguni lilikuwa “[kuu] na bora zaidi na zaidi,” hivi kwamba alikuwa tayari kuvumilia jaribu lolote. Paulo alitafakari kuhusu tumaini hilo. Na matokeo ni kwamba alihisi “anafanywa upya siku kwa siku.”

18. Tumaini limemtiaje nguvu Tihomir na familia yake?

18 Tihomir, ndugu anayeishi nchini Bulgaria, anapata nguvu kutokana na tumaini lake. Miaka michache iliyopita, ndugu yake mdogo, Zdravko, alikufa katika aksidenti. Kwa muda fulani baada ya hapo, Tihomir alipambana na hisia kali za majonzi. Ili kukabiliana na hali hiyo, yeye na familia yake wamewazia jinsi ufufuo utakavyokuwa. Anaeleza hivi: “Kwa mfano, tunazungumzia mahali ambapo tutakutana na Zdravko, chakula ambacho tutamwandalia, watu ambao tutawakaribisha kwenye tafrija ya kwanza atakaporudi, na mambo ambayo tutamwambia kuhusu siku za mwisho.” Tihomir anasema kwamba kukazia fikira tumaini lao kunaimarisha familia yake iendelee kuvumilia na kuendelea kungojea wakati ambapo Yehova atamfufua ndugu yake.

Unawazia maisha yako yatakuwaje katika ulimwengu mpya? (Tazama fungu la 19) c

19. Unaweza kufanya nini ili kuimarisha tumaini lako? (Tazama pia picha.)

19 Unawezaje kuimarisha tumaini lako? Kwa mfano, ikiwa una tumaini la kuishi milele duniani, soma ufafanuzi wa Biblia kuhusu Paradiso na utafakari kuhusu mambo hayo. (Isa. 25:8; 32:​16-18) Fikiria jinsi maisha yatavyokuwa katika ulimwengu mpya. Jiwazie ukiwa huko. Unamwona nani huko? Unasikia sauti gani? Unahisije? Ili kuchochea uwezo wako wa kuwazia, tazama picha katika machapisho yetu zinazoonyesha Paradiso au utazame video ya muziki kama vile, Ulimwengu Mpya, Paradiso Ipo Karibu Sana, au Wazia Maisha Paradiso. Ikiwa tutaendelea kufikiria kuhusu tumaini la ulimwengu mpya, matatizo yetu yatakuwa ya ‘muda mfupi na mepesi.’ (2 Kor. 4:17) Tumaini ambalo Yehova amekupatia linaweza kukutia nguvu.

20. Tunapohisi kwamba sisi ni dhaifu tunawezaje kupata nguvu?

20 Hata tunapokuwa dhaifu, “kwa msaada wa Mungu tutapata nguvu.” (Zab. 108:13) Tayari Yehova amekuandalia mambo unayohitaji ili upate nguvu kutoka kwake. Basi, unapohitaji msaada ili kutimiza mgawo fulani, kuvumilia jaribu, au kudumisha shangwe yako, sali kwa Yehova kwa bidii na utafute mwongozo wake kupitia funzo la kibinafsi. Waruhusu ndugu na dada zako Wakristo wakutie moyo. Dumisha tumaini lako likiwa jangavu na wazi akilini. Kisha utaimarishwa “kwa nguvu zote kwa uwezo [wa Mungu] wenye utukufu ili uvumilie kikamili kwa subira na shangwe.”—Kol. 1:11.

WIMBO 33 Mtupie Yehova Mzigo Wako

a Makala hii itawasaidia wale ambao huenda wakahisi wamelemewa na jaribu fulani au na mgawo ambao wanahisi kwamba unapita uwezo wao. Tutajifunza jinsi Yehova anavyoweza kututia nguvu na mambo tunayoweza kufanya ili tupate msaada wake.

b Baadhi ya majina yamebadilishwa.

c MAELEZO YA PICHA: Dada ambaye ni kiziwi anatafakari ahadi za Biblia na anacheza video ya muziki ili kumsaidia kuwazia jinsi maisha yake yatakavyokuwa katika ulimwengu mpya.