Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 44

Ujifunze Neno ya Mungu kwa Undani Kabisa

Ujifunze Neno ya Mungu kwa Undani Kabisa

‘Elewa kwa ukamili upana na urefu na urefu kuenda juu na urefu kuenda chini.’—EFE. 3:18.

WIMBO 95 Mwangaza Unaendelea Kuongezeka

KIFUPI YA HABARI a

1-2. Njia ya muzuri zaidi ya kusoma na kujifunza Biblia ni gani? Toa mufano.

 WAZIA unataka kuamua ikiwa utauza nyumba fulani ao hapana. Utakuwa na lazima ya kuona nini mbele ukamate ule uamuzi? Picha tu ya mbele ya nyumba? Bila shaka utapenda kufika na ujionee nyumba weye peke, uizunguke, uingie ndani, uchunguze kila chumba, na uchunguze kwa uangalifu kila sehemu ya nyumba. Unaweza hata kupenda kuchunguza plan ya ile nyumba na kuona namna ilijengwa. Kusema kweli, utapenda kuona kila sehemu ya nyumba yenye unapenda kuuza.

2 Tunaweza pia kufanya vile wakati tuko nasoma na kujifunza Biblia. Mutu moya alilinganisha ujumbe wa Biblia na “jengo kubwa, yenye kuwa murefu sana, na yenye musingi wake unaingia ndani kabisa.” Sasa, namna gani tunaweza kujua muzuri mambo yote yenye kuwa mu Biblia? Kama unaisoma mbiombio pengine utajifunza tu kweli za musingi, ni kusema “mambo ya musingi ya maneno matakatifu ya Mungu.” (Ebr. 5:12) Kuliko kufanya vile, sawa vile mutu anaweza kufanya kuhusu nyumba, ingia “ndani” ili uchunguze mambo yote ya maana. Njia ya muzuri ya kujifunza Biblia ni kuona namna sehemu zake mbalimbali zinapatana. Usitafute tu kujua ni kweli gani unaamini, lakini pia juu ya nini unaziamini.

3. Mutume Paulo aliomba Wakristo wenzake wafanye nini, na juu ya nini? (Waefeso 3:14-19)

3 Ili kuelewa Neno ya Mungu kwa undani kabisa, unapaswa kujifunza mafundisho mazito ya Biblia. Mutume Paulo alitia moyo ndugu na dada zake wajifunze Neno ya Mungu kwa uangalifu ili waweze ‘kuelewa kwa ukamili upana na urefu na urefu kuenda juu na urefu kuenda chini’ wa kweli. Na ile ingefanya wafikie kuwa “na mizizi na kufanywa imara” katika imani yao. (Soma Waefeso 3:14-19.) Siye pia tunapaswa kufanya vile. Tuone namna tunaweza kujifunza kwa uangalifu Neno ya Mungu ili tuelewe muzuri maana yake.

UJIFUNZE KWA UANGALIFU MAFUNDISHO MAZITO YA BIBLIA

4. Unaweza kufanya nini ili kumukaribia Yehova zaidi? Toa mufano.

4 Siye Wakristo hatutosheke tu na mafundisho ya musingi ya Biblia. Kwa musaada wa roho takatifu ya Mungu tunapenda sana kujifunza “hata mambo mazito ya Mungu.” (1 Ko. 2:9, 10) Juu ya nini usijiwekee programu ya kujifunza habari zenye zitakusaidia umukaribie Yehova zaidi? Kwa mufano, unaweza kuchunguza namna alionyesha upendo watumishi wake wa zamani na namna ile inaonyesha kama anakupenda na weye. Unaweza kuchunguza mipango yenye Yehova aliweka kwa ajili ya ibada mu Israeli na kuona namna inalingana na vile Yehova anapenda Wakristo wamuabudu leo. Ao pengine unaweza kujifunza kwa undani maunabii yenye Yesu alitimiza mu maisha na utumishi wake hapa ku dunia.

5. Ungependa kuchunguza habari gani mu funzo yako ya kipekee?

5 Wakristo fulani wenye wanajifunzaka sana Biblia, waliulizwa kuhusu mambo mazito yenye kila mumoja wao angependa kuchunguza mu Neno ya Mungu. Majibu fulani yenye walitoa iko mu kisanduku “ Habari Zenye Tunaweza Kujifunza mu Funzo Yetu ya Kipekee.” Tutafurahi sana kama tunajifunza zile habari kwa kutumia Index ao Musaada wa Kutafuta Habari kwa Ajili ya Mashahidi wa Yehova. Kujifunza Biblia kwa undani kunaweza kukusaidia kutia nguvu imani yako, na kukusaidia ‘upate ujuzi juu ya Mungu.’ (Mez. 2:4, 5) Tuzungumuzie sasa mafundisho fulani mazito ya Biblia yenye unaweza kujifunza kwa uangalifu.

FIKIRIA SANA KUSUDI YA MUNGU

6. (a) Kuko tofauti gani kati ya mupango na kusudi? (b) Juu ya nini tunaweza kusema kama kusudi ya Yehova kwa ajili ya wanadamu na dunia ni ya “milele”? (Waefeso 3:11)

6 Kwa mufano, angalia mambo yenye Biblia inasema kuhusu kusudi ya Mungu. Kuko tofauti kubwa kati ya mupango na kusudi. Mupango iko sawa barabara fulani yenye itatuongoza fasi kwenye tunapenda kuenda. Lakini kama kitu fulani inazuia barabara, hatutaweza kufika ile fasi. Lakini kusudi inaweza kulinganishwa na fasi kwenye tuko naenda. Tunajua kwenye tuko naenda, kwa hiyo tunaweza kukamata njia tofauti juu ya kufika kule. Kama tunapata kizuizi mu njia fulani tunaweza kutumia njia ingine. Tunamushukuru sana Yehova juu ametufunulia mu Biblia hatua kwa hatua “kusudi [lake] la milele.” (Efe. 3:11) Hata kama anaweza kutumia njia tofauti, mambo inakuwaka tu vile anapenda kwa sababu “amefanya kila kitu kitimize kusudi lake.” (Mez. 16:4) Na matokeo ya mambo yenye Yehova iko nafanya itadumu milele. Kusudi ya Yehova ni nini, na ni njia gani tofauti zenye alitumia ili kuitimiza?

7. Kisha Adamu na Eva kuasi, Yehova alifanya mabadiliko gani ili afikie kutimiza kusudi yake? (Matayo 25:34)

7 Mungu aliambia wanadamu wa kwanza kusudi yake kwa ajili yao. Walipaswa ‘kuzaa na kuwa wengi, kujaza dunia na kuitawala, na kutawala . . . kila kiumbe chenye uzima’ ku dunia. (Mwa. 1:28) Wakati Adamu na Eva waliasi, ile ilifanya zambi iingie mu familia ya wanadamu. Lakini ile haikuzuia Yehova kutimiza kusudi yake. Alitafuta njia ingine ya kutimiza kusudi yake. Palepale alisema kama atasimamisha Ufalme mbinguni wenye utatimiza kusudi yenye alikuwa nayo ku mwanzo kwa ajili ya wanadamu na dunia. (Soma Matayo 25:34.) Kwa wakati wenye kufaa, kwa upendo Yehova alituma Mwana wake muzaliwa wa kwanza ku dunia ili afundishe watu kuhusu Ufalme na atoe uzima wake ili kutukomboa kutoka katika zambi na kifo. Kisha Yesu alifufuliwa na kuenda mbinguni ili akuwe Mufalme wa Ufalme wa Mungu. Lakini kuko mambo mingi ya kufikiria kuhusu kusudi ya Mungu.

Wazia wakati wenye viumbe wote wenye akili wa mbinguni na wa ku dunia watamutumikia Yehova pamoja kwa ushikamanifu! (Ona fungu ya 8)

8. (a) Habari kubwa ya Biblia ni nini? (b) Sawa vile inaonyeshwa mu Waefeso 1:8-11, kusudi kubwa ya Yehova ni nini? (Ona picha ku jalada.)

8 Habari kubwa ya Biblia ni kwamba jina ya Yehova itatetewa wakati atakuwa natimiza kusudi yake kwa ajili ya dunia, kupitia Ufalme wake wenye kutawaliwa na Yesu Kristo. Kusudi ya Yehova haiwezi kubadilishwa. Amehakikisha kama ataitimiza kabisa. (Isa. 46:10, 11, maelezo ya chini; Ebr. 6:17, 18) Kadiri siku zitaendelea, dunia itageuzwa na kuwa paradiso kwenye kutaishi wazao wa Adamu na Eva wenye haki na wakamilifu, wenye ‘watafurahia maisha milele.’ (Zb. 22:26) Lakini kusudi ya Yehova itatimiza mambo mingi zaidi. Kusudi yake kubwa ni kuunganisha viumbe vyake vyote vyenye akili vya mbinguni na vya ku dunia. Kwa hiyo, wote wenye kuishi watajitiisha kwake kwa uaminifu akiwa Mutawala wao Mwenye Mamlaka Makubwa Zaidi. (Soma Waefeso 1:8-11.) Je, haikushangaze kuona njia ya muzuri yenye Yehova anatumia ili kutimiza kusudi yake?

FIKIRIA SANA WAKATI WAKO WENYE KUYA

9. Wakati tunasoma Biblia, tunajifunza mambo gani juu ya wakati wenye kuya?

9 Fikiria unabii wenye Yehova alitoa mu bustani ya Edeni, wenye kuwa mu Mwanzo 3:15. b Ule unabii unazungumuzia matukio yenye ingetimiza kusudi ya Mungu. Lakini ile mambo ingetimia kisha maelfu ya miaka. Ile matukio ingetia ndani kutokeza uzao wa Abrahamu wenye ungeongoza mupaka kuzaliwa kwa Kristo. (Mwa. 22:15-18) Kisha sawa vile ilitabiriwa, mu mwaka wa 33 Yesu alipigwa kwenye kisigino. (Mdo. 3:13-15) Tukio ya mwisho ya ule unabii, ni kusema kuponda Shetani kichwa, itatimia kisha zaidi ya miaka 1000 wakati wenye kuya. (Ufu. 20:7-10) Biblia inafunua mambo mingi kuhusu mambo yenye itatokea kadiri uadui kati ya mupangilio wa Shetani na tengenezo ya Yehova unaendelea kuongezeka.

10. (a) Ni matukio gani yenye itatokea hivi karibuni? (b) Namna gani tunaweza kutayarisha moyo wetu na akili yetu? (Ona maelezo ya chini.)

10 Fikiria kuhusu hii matukio ya ajabu yenye Biblia ilitabiri. Kwanza mataifa itatangaza “amani na usalama!” (1 Te. 5:2, 3) ‘Kwa kushitukia,’ taabu kubwa itaanza wakati mataifa itashambulia dini zote za uongo. (Ufu. 17:16) Kisha pale, inawezekana kuonekane alama yenye haiko ya kawaida ya “Mwana wa binadamu akikuja juu ya mawingu ya mbinguni akiwa na nguvu na utukufu mwingi.” (Mt. 24:30) Yesu atahukumu wanadamu kwa kutenganisha kondoo na mbuzi. (Mt. 25:31-33, 46) Lakini mu ile wakati, Shetani ataendelea na upinzani wake. Juu anachukia sana watu wa Mungu, atachochea muungano wa mataifa wenye Biblia inaita Gogu wa Magogu kushambulia watumishi waaminifu wa Yehova. (Eze. 38:2, 10, 11) Wakati fulani mu ile kipindi, watiwa-mafuta wenye watakuwa wangali ku dunia watakusanywa mbinguni pamoya na Kristo na jeshi yake ya mbinguni ili kupigana vita ya Armagedoni. Vita ya Armagedoni njo tukio ya mwisho ya taabu kubwa. c (Mt. 24:31; Ufu. 16:14, 16) Kisha Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Yesu utaanza.—Ufu. 20:6.

Utamukaribia Yehova kwa kadiri gani wakati utakuwa umejifunza kumuhusu kwa mamilioni ya miaka? (Ona fungu ya 11)

11. Tumaini ya uzima wa milele inamaanisha nini kwako? (Ona pia picha.)

11 Sasa fikiria namna mambo itakuwa kisha ile Miaka Elfu. Biblia inasema kama Muumbaji wetu “ametia umilele katika moyo [wetu].” (Muh. 3:11) Fikiria ile inamaanisha nini juu yako na juu ya uhusiano wako pamoya na Yehova. Mu Kitabu Mkaribie Yehova, ukurasa wa 319, tunapata hii maneno yenye kugusa moyo: “Baada ya kuishi mamia, maelfu, mamilioni au hata mabilioni ya miaka, tutajua mengi zaidi kumhusu Yehova Mungu kuliko tujuavyo sasa. Lakini bado tutatambua kwamba kuna mambo mengi mazuri tutakayohitaji kujifunza. . . . Uhai udumuo milele utakuwa na kusudi na utapendeza isivyowazika—kwa sababu tutazidi kumkaribia Yehova daima.” Mbele ile wakati ifike tunaendelea kujifunza Neno ya Mungu. Ni mambo gani ingine yenye tunaweza kuchunguza kwa undani?

ANGALIA JUU MBINGUNI

12. Namna gani tunaweza kuangalia juu mbinguni? Toa mufano.

12 Neno ya Mungu inatuelezea kidogo kuhusu mambo yenye inafanyikaka kwenye Yehova iko, ni kusema “katika nafasi za juu zenye kuwa juu.” (Isa. 33:5) Biblia inatufunulia mambo yenye kushangaza kuhusu Yehova na kuhusu sehemu ya mbinguni ya tengenezo yake. (Isa. 6:1-4; Da. 7:9, 10; Ufu. 4:1-6) Kwa mufano tunaweza kusoma kuhusu mambo ya ajabu yenye Ezekieli aliona wakati “mbingu zilifunguka na [akaanza] kuona maono ya Mungu.”—Eze. 1:1.

13. Ni nini inakugusa moyo kuhusu daraka ya Yesu mbinguni, sawa vile inaonyeshwa mu Waebrania 4:14-16?

13 Fikiria pia kuhusu daraka ya Yesu mbinguni akiwa Mufalme wetu mwenye kutawala na Kuhani Mukubwa mwenye huruma. Kupitia yeye tunaweza kukaribia katika sala “kiti cha ufalme [cha Mungu] cha fazili zenye hazistahiliwe” na tunaweza kumuomba rehema na musaada “wakati wenye kufaa.” (Soma Waebrania 4:14-16.) Tusipitishe hata siku moya bila kufikiria mambo yenye Yehova na Yesu wametufanyia na wanaendelea kutufanyia wakiwa mbinguni. Upendo wao kwetu unapaswa kugusa sana moyo wetu na kutulazimisha kumuabudu Yehova na kumutumikia kwa bidii.—2 Ko. 5:14, 15.

Wazia furaha yenye utakuwa nayo mu dunia mupya, juu unajua kama ulisaidia watu wengine wakuwe Mashahidi wa Yehova na wanafunzi wa Yesu! (Ona fungu ya 14)

14. Ni jambo gani ya maana sana yenye tunaweza kufanya ili kuonyesha Yehova na Yesu shukrani? (Ona pia picha.)

14 Njia moya ya kuonyesha kama tuko wenye shukrani kwa Mungu na kwa Mwana wake ni kujikaza kusaidia wengine wakuwe Mashahidi wa Yehova na wafuasi wa Yesu. (Mt. 28:19, 20) Ni vile mutume Paulo alifanya juu ya kuonyesha shukrani Yehova na Yesu. Alijua kama mapenzi ya Yehova ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe na wapate ujuzi wenye hauna makosa wa ile kweli.” (1 Ti. 2:3, 4) Alitumika sana mu kazi ya kuhubiri ili kusaidia watu wengi kadiri aliweza juu ‘kwa njia yoyote aokoe wengine.’—1 Ko. 9:22, 23.

FURAHIA KUCHUNGUZA KWA UANGALIFU NENO YA MUNGU

15. Kulingana na Zaburi 1:2, nini njo itafanya tukuwe na furaha?

15 Mutunga-zaburi hakukosea wakati alisema kama mwenye furaha na mwenye kufanikiwa ni mutu mwenye “anapendezwa na sheria ya Yehova” na mwenye “anatafakari juu ya sheria Yake muchana na usiku.” (Zb. 1:1-3; maelezo ya chini) Mutafsiri wa Biblia, Joseph Rotherham, alifasiria ile andiko mu kitabu fulani (Studies in the Psalms). Alisema kama ule mutu anapaswa “kupenda sana muongozo wa Mungu, kwa hiyo anautafuta, anajifunza kuuhusu, na anapitisha wakati mwingi na iko naufikiria.” Aliongeza kama musomaji wa Biblia “mwenye amepitisha siku bila kusoma Biblia anapaswa kuona kama ile siku imepotea bure.” Unaweza kufurahia kujifunza Biblia kwa kukazia uangalifu mambo yote yenye kuwa mu Biblia, hata mambo ya kidogo-kidogo na kuona namna ile mambo yote inapatana. Inafurahisha sana kuchunguza kwa undani Neno ya Mungu!

16. Tutazungumuzia nini mu habari yenye kufuata?

16 Kweli za muzuri zenye Yehova anatufundisha mu Neno yake haziko nguvu sana, tunaweza kuzielewa. Mu habari yenye kufuata tutajifunza moya kati ya mafundisho mazito, ni kusema hekalu kubwa ya Yehova ya kiroho, yenye Paulo alizungumuzia mu barua yake kwa Wakristo Waebrania. Tunatumaini kama kujifunza ile habari kutakuletea furaha.

WIMBO 94 Aksanti Yehova kwa Kutupatia Neno Yako

a Kujifunza Biblia kunaweza kutuletea furaha mu maisha yetu yote. Kunaweza kutuletea faida na kufanya tukuwe karibu zaidi na Baba yetu wa mbinguni. Mu hii habari tutaona namna tunaweza kuchunguza “upana na urefu na urefu kuenda juu na urefu kuenda chini” wa Neno ya Mungu.

b Ona habari “Unabii wa Zamani Wenye Unakuhusu” mu Munara wa Mulinzi wa Mwezi wa 7, 2022.

c Ili kujua namna unaweza kujitayarisha kwa ajili ya matukio ya wakati wenye kuya yenye itatikisa ulimwengu, ona kitabu Ufalme wa Mungu Unatawala! uku. 230.