MAKALA YA 44

Chunguza kwa Undani Sehemu Zote za Neno la Mungu

Chunguza kwa Undani Sehemu Zote za Neno la Mungu

‘Fahamu kikamili upana na urefu na kimo na kina.’—EFE. 3:18.

WIMBO 95 Nuru Inazidi Kuongezeka

MUHTASARI a

1-2. Ni njia gani bora ya kusoma na kujifunza Biblia? Toa mfano.

 WAZIA kwamba unataka kununua nyumba. Utaangalia mambo gani kabla ya kufanya uamuzi huo? Je, inatosha tu kuona picha ya upande wa mbele wa nyumba hiyo? Bila shaka, ungependa kuiona nyumba hiyo jinsi ilivyo kihalisi ili utembee ndani yake, kuchunguza vyumba vyote, na kuona sehemu zake zote. Pia, huenda ukachunguza mchoro wa ramani ya nyumba hiyo ili ujue jinsi ilivyojengwa. Kwa hakika, ungependa kuifahamu kwa kina nyumba ambayo unataka kununua.

2 Tunaweza kufanya jambo kama hilo tunaposoma na kujifunza Biblia. Kitabu kimoja cha marejezo kinafananisha ujumbe wa Biblia na “jengo kubwa sana, lenye kimo kirefu sana na msingi wenye kina kirefu.” Basi, tunawezaje kuelewa vizuri ujumbe wote ulio katika Biblia? Ikiwa utaisoma haraka-haraka, huenda ukajifunza habari za msingi tu, yaani, “mambo ya msingi ya maneno matakatifu ya Mungu.” (Ebr. 5:12) Badala yake, kama ile nyumba, unapaswa kuingia “ndani” na kuichunguza kwa makini ili uielewe kikamili zaidi. Njia bora ya kujifunza Biblia ni kuona jinsi sehemu mbalimbali za ujumbe wake zinavyohusiana. Jitahidi kuelewa ni kweli gani ambazo unaamini na kwa nini unaamini kweli hizo.

3. Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo wenzake wafanye nini, na kwa nini? (Waefeso 3:​14-19)

3 Ili kuelewa kikamili Neno la Mungu na sehemu zake zote, tunapaswa kujifunza kweli zenye kina za Biblia. Mtume Paulo aliwahimiza ndugu na dada zake Wakristo wajifunze Neno la Mungu kwa bidii ili “[wafahamu] kikamili upana na urefu na kimo na kina” cha ile kweli, kisha wangekuwa na “mizizi na kuimarishwa” katika imani yao. (Soma Waefeso 3:​14-19.) Sisi tunahitaji kufanya hivyo pia. Acheni tuone jinsi tunavyoweza kuchunguza kwa undani Neno la Mungu ili tuelewe kikamili zaidi ujumbe wake wenye thamani.

CHUNGUZA KWA UNDANI KWELI ZENYE KINA ZA BIBLIA

4. Tunaweza kufanya nini ili tumkaribie zaidi Yehova? Toa mifano.

4 Tukiwa Wakristo, haturidhiki kujua mambo ya msingi tu kuhusu Biblia. Kwa msaada wa roho takatifu ya Mungu, tunatamani kujifunza “hata mambo mazito ya Mungu.” (1 Kor. 2:​9, 10) Kwa nini usianze mradi wa kujifunza kibinafsi ambao utakusaidia kumkaribia Yehova hata zaidi? Kwa mfano, unaweza kuchunguza jinsi alivyowaonyesha upendo watumishi wake wa zamani na jinsi hilo linavyothibitisha kwamba anakupenda wewe pia. Unaweza kuchunguza mpango wa ibada ambao Yehova aliweka katika Israeli la kale na jinsi tunavyomwabudu leo tukiwa Wakristo. Au labda unaweza kujifunza kwa undani unabii mbalimbali ambao Yesu alitimiza wakati wa maisha na huduma yake hapa duniani.

5. Je, una habari ambayo ungependa kufanya utafiti kuihusu katika mradi wa funzo lako la kibinafsi?

5 Baadhi ya wanafunzi wenye bidii wa Biblia waliulizwa ni kweli gani zenye kina ambazo wao binafsi wangependa kuchunguza katika Neno la Mungu. Baadhi ya majibu yao yameorodheshwa kwenye sanduku “ Habari kwa Ajili ya Miradi ya Kujifunza Kibinafsi.” Unaweza kupata shangwe nyingi kwa kujifunza habari hizo kwa msaada wa Fahirisi au Mwongozo wa Utafiti wa Mashahidi wa Yehova. Kujifunza Biblia kwa kina kunaweza kuimarisha imani yako na kukusaidia upate “ujuzi kumhusu Mungu.” (Met. 2:​4, 5) Acheni sasa tuchunguze baadhi ya kweli zenye kina za Biblia ambazo unaweza kujifunza kwa undani.

TAFAKARI KUHUSU KUSUDI LA MUNGU

6. (a) Kuna tofauti gani kati ya mpango na kusudi? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba kusudi la Yehova kwa ajili ya wanadamu na dunia ni la “milele”? (Waefeso 3:11)

6 Kwa mfano, fikiria mambo ambayo Biblia inasema kuhusu kusudi la Mungu. Kuna tofauti kubwa kati ya mpango na kusudi. Mpango ni kama kuchagua njia moja hususa inayokuongoza mahali ambapo unataka kwenda. Hata hivyo, huenda mpango huo usifaulu ikiwa utakutana na kizuizi barabarani. Kuwa na kusudi kunaweza kulinganishwa na kukazia fikira mahali ambapo unataka kwenda. Tunajua kihususa mwisho wa safari yetu, lakini tunaweza kutumia njia mbalimbali ili kufika huko. Tunaweza kubadili njia ikiwa hilo linahitajika. Tunashukuru kwamba Yehova amefunua hatua kwa hatua ‘kusudi lake la milele’ katika Biblia. (Efe. 3:11) Kwa njia moja au nyingine, sikuzote anafanikiwa kwa sababu “amefanya kila kitu kitimize kusudi lake.” (Met. 16:4) Na matokeo ya mambo ambayo Yehova anatimiza yatadumu milele. Kusudi la Yehova ni nini, na amefanya mabadiliko gani ili kulitimiza?

7. Baada ya wanadamu wa kwanza kuasi, Yehova alifanya mabadiliko gani ili atimize kusudi lake? (Mathayo 25:34)

7 Mungu aliwaambia wanadamu wa kwanza kusudi lake kwa ajili yao. Aliwaambia, “Zaeni, muwe wengi, muijaze dunia na kuitiisha, na mtawale . . . kila kiumbe aliye hai” duniani. (Mwa. 1:28) Adamu na Hawa walipoasi na kufanya dhambi iingie katika familia ya wanadamu, hilo halikumzuia Yehova kutimiza kusudi lake. Alifanya mabadiliko katika njia ambayo kusudi lake lingetimizwa. Mara moja, aliamua kwamba atasimamisha Ufalme mbinguni ambao ungetimiza kusudi lake la mwanzoni kwa ajili ya wanadamu na dunia. (Soma Mathayo 25:34.) Wakati wake ulipofika, kwa upendo Yehova alimtuma Mwana wake mzaliwa wa kwanza aje duniani ili kuwafundisha watu kuhusu Ufalme na kutoa uhai wake uwe fidia kwa ajili ya kutukomboa kutoka katika dhambi na kifo. Kisha Yesu akafufuliwa na kurudi mbinguni ili atawale akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Lakini tunaweza kujifunza mengi zaidi kuhusu kusudi la Mungu.

Wazia wakati ambapo viumbe wote wenye akili mbinguni na duniani wataunganishwa na kumwabudu Yehova kwa ushikamanifu! (Tazama fungu la 8)

8. (a) Kichwa kikuu cha Biblia ni nini? (b) Kama inavyoelezwa kwenye Waefeso 1:​8-11, hatimaye kusudi la Mungu ni nini? (Tazama picha kwenye jalada.)

8 Kichwa kikuu cha Biblia ni kwamba jina la Yehova litatetewa anapoendelea kutimiza kusudi lake kwa ajili ya dunia kupitia Ufalme wake unaoongozwa na Kristo. Kusudi la Yehova haliwezi kubadilishwa. Ametoa uhakikisho kwamba atafanikiwa kulitimiza. (Isa. 46:​10, 11, maelezo ya chini; Ebr. 6:​17, 18) Hatimaye, dunia itabadilishwa na kuwa paradiso ambamo wazao wakamilifu na waadilifu wa Adamu na Hawa ‘watafurahia maisha milele.’ (Zab. 22:26) Lakini Yehova atatimiza mambo mengi zaidi, kusudi lake ni hatimaye kuunganisha viumbe wake wote wenye akili walio mbinguni na duniani. Kisha wote walio hai watajitiisha chini yake kwa ushikamanifu akiwa Mwenye Enzi Kuu wao. (Soma Waefeso 1:​8-11.) Je, hustaajabishwi na jinsi Yehova anavyotimiza kusudi lake kwa njia yenye kupendeza?

TAFAKARI KUHUSU WAKATI WAKO UJAO

9. Kwa kusoma Biblia, tunaweza kuona mbali kadiri gani katika wakati ujao?

9 Fikiria unabii ambao Yehova alitoa katika bustani ya Edeni, unaopatikana kwenye Mwanzo 3:15. b Unabii huo ulitaja matukio ambayo yangetimiza kusudi lake lakini yangetokea maelfu ya miaka baadaye. Matukio hayo yalitia ndani kutokeza uzao wa Abrahamu, ukoo ambao ungeongoza kwenye kuzaliwa kwa Kristo. (Mwa. 22:​15-18) Kisha mwaka wa 33 W.K., Yesu aliumwa kisigino kama ilivyotabiriwa. (Mdo. 3:​13-15) Tukio la mwisho la unabii huo, yaani, kupondwa kwa kichwa cha Shetani, litatokea baada ya zaidi ya miaka 1,000 ijayo. (Ufu. 20:​7-10) Na Biblia inafunua mengi zaidi kuhusu mambo yatakayotokea kadiri uadui kati ya mfumo wa Shetani na tengenezo la Yehova unavyofikia mwisho wake.

10. (a) Ni matukio gani ambayo yatatokea wakati ujao hivi karibuni? (b) Tunawezaje kutayarisha akili na mioyo yetu? (Tazama maelezo ya chini.)

10 Fikiria kuhusu matukio haya ya kustaajabisha ambayo Biblia ilitabiri. Kwanza, mataifa yatatoa tangazo la “amani na usalama!” (1 The. 5:​2, 3) Kisha “ghafla” dhiki kuu itaanza, mataifa yatakaposhambulia dini zote za uwongo. (Ufu. 17:16) Baada ya hapo, huenda kutakuwa na tukio lisilo la kawaida la “Mwana wa binadamu akija juu ya mawingu ya mbinguni akiwa na nguvu na utukufu mwingi.” (Mt. 24:30) Yesu atawahukumu wanadamu, akitenganisha kondoo na mbuzi. (Mt. 25:​31-33, 46) Hata hivyo, bado Shetani ataendelea kumpinga Yehova. Akiongozwa na chuki, atachochea muungano wa mataifa ambao Biblia inauita Gogu wa nchi ya Magogu ili kuwashambulia waabudu wa kweli wa Yehova. (Eze. 38:​2, 10, 11) Kufikia pindi fulani, watiwa-mafuta waliobaki duniani watakusanywa na kwenda mbinguni ili wajiunge na Kristo na jeshi lake la mbinguni kupigana vita vya Har–​Magedoni, sehemu ya mwisho ya ile dhiki kuu. c (Mt. 24:31; Ufu. 16:​14, 16) Kisha Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo juu ya dunia utaanza.—Ufu. 20:6.

Utajihisi ukiwa karibu na Yehova kwa kadiri gani baada ya kujifunza kumhusu kwa mabilioni ya miaka? (Tazama fungu la 11)

11. Tumaini la uzima wa milele lina maana gani kwako? (Tazama pia picha.)

11 Sasa fikiria kuhusu wakati ujao ulio mbali hata zaidi. Biblia inasema kwamba Muumba wetu ‘hata ameweka umilele katika mioyo yetu.’ (Mhu. 3:11) Fikiria jinsi jambo hilo litakavyokusaidia kuimarisha uhusiano wako pamoja na Yehova. Kitabu Mkaribie Yehova, ukurasa wa 319, kinachochea fikira zetu kwa kusema hivi: “Baada ya kuishi mamia, maelfu, mamilioni au hata mabilioni ya miaka, tutajua mengi zaidi kumhusu Yehova Mungu kuliko tujuavyo sasa. Lakini bado tutatambua kwamba kuna mambo mengi mazuri tutakayohitaji kujifunza. . . . Uhai udumuo milele utakuwa na kusudi na utapendeza isivyowazika—kwa sababu tutazidi kumkaribia Yehova daima.” Hata hivyo kwa sasa, tunapoendelea kujifunza Neno la Mungu, ni nini kingine ambacho tunaweza kuchunguza kwa undani? 

TAZAMA JUU MBINGUNI

12. Tunawezaje kutazama juu mbinguni? Toa mfano.

12 Neno la Mungu linatufunulia kuhusu kuwepo kwa Yehova “katika vilele vilivyo juu.” (Isa. 33:5) Biblia inafunua mambo yenye kustaajabisha kumhusu Yehova na sehemu ya mbinguni ya tengenezo lake. (Isa. 6:​1-4; Dan. 7:​9, 10; Ufu. 4:​1-6) Kwa mfano, tunaweza kusoma kuhusu mambo yenye kustaajabisha ambayo Ezekieli aliona ‘mbingu zilipofunguliwa naye akaanza kuona maono ya Mungu.’—Eze. 1:1.

13. Unahisije kuhusu jukumu analotimiza Yesu akiwa mbinguni kama linavyoelezwa kwenye Waebrania 4:​14-16?

13 Pia, fikiria kuhusu jukumu la Yesu akiwa Mfalme wetu anayetawala mbinguni na Kuhani Mkuu mwenye huruma. Kupitia kwake, tunaweza kukikaribia ‘kiti cha Ufalme cha Mungu cha fadhili zisizostahiliwa’ katika sala na kumwomba rehema na msaada kwa “wakati unaofaa.” (Soma Waebrania 4:​14-16; maelezo ya chini.) Acheni kila siku tuendelee kutafakari kuhusu mambo ambayo Yehova na Yesu wametufanyia na yale ambayo wanatufanyia kutoka mbinguni. Upendo wao kwetu unapaswa kugusa kabisa mioyo yetu na kutuchochea kuwa wenye bidii katika utumishi na ibada yetu.—2 Kor. 5:​14, 15.

Wazia jinsi utakavyokuwa na shangwe katika ulimwengu mpya kwa kujua kwamba uliwasaidia wengine wawe Mashahidi wa Yehova na wanafunzi wa Yesu! (Tazama fungu la 14)

14. Ni jambo gani bora zaidi ambalo tunaweza kufanya ili kuonyesha kwamba tunashukuru kwa mambo ambayo Yehova na Yesu wametufanyia? (Tazama pia picha.)

14 Mojawapo ya njia bora zaidi ya kuonyesha kwamba tunamshukuru Yehova na Mwana wake ni kujitahidi kuwasaidia wengine wawe Mashahidi wa Yehova na wanafunzi wa Yesu. (Mt. 28:​19, 20) Hivyo ndivyo mtume Paulo alivyofanya akichochewa na shukrani kumwelekea Mungu na Kristo. Alijua mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:​3, 4) Alifanya kazi kwa bidii sana katika huduma yake na kuwasaidia watu wengi iwezekanavyo “ili kwa vyovyote [awaokoe] wengine.”—1 Kor. 9:​22, 23.

FURAHIA KULICHUNGUZA KWA UNDANI NENO LA MUNGU

15. Kulingana na Zaburi 1:​2, ni nini ambacho kitatuletea furaha?

15 Kwa kufaa, mtunga zaburi anamfafanua mtu mwenye furaha na mwenye mafanikio kuwa mtu ambaye “anapendezwa na sheria ya Yehova” na ambaye “huitafakari sheria Yake mchana na usiku.” (Zab. 1:​1-3; maelezo ya chini) Akitoa maelezo kuhusu andiko hilo katika kitabu Studies in the Psalms, mtafsiri wa Biblia Joseph Rotherham alisema kwamba mtu anapaswa “kupendezwa sana na mwongozo wa Mungu hivi kwamba atautafuta, atajifunza kuuhusu, na kuendelea kuutafakari.” Aliongezea kwamba msomaji wa Biblia atahisi “amepoteza siku ikiwa hatatumia siku hiyo kuelewa zaidi hekima ya Biblia.” Unaweza kupendezwa na kujifunza Biblia kwa kusoma mambo yote unayoweza kuhusu ujumbe wake wenye thamani na kuona jinsi sehemu zake zote zinavyoungana. Tunapata shangwe nyingi kwa kuchunguza kwa undani kila sehemu ya Neno la Mungu!

16. Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

16 Si vigumu sana kwetu kuelewa kweli maridadi ambazo Yehova anatufundisha katika Neno lake. Katika makala inayofuata, tutachunguza mojawapo ya kweli zenye kina zaidi, yaani, hekalu kubwa la kiroho la Yehova, ambalo Paulo alilifafanua katika barua yake kwa Wakristo Waebrania. Tunatumaini kwamba utapendezwa sana kwa kuchunguza habari hiyo.

WIMBO 94 Kulithamini Neno la Mungu

a Kusoma Biblia kunaweza kuwa jambo lenye kufurahisha, tunaloweza kufanya katika maisha yetu yote na linalotusaidia kumkaribia hata zaidi Baba yetu wa mbinguni. Katika makala hii, tutaona jinsi tunavyoweza kuchunguza kwa undani “upana na urefu na kimo na kina” cha Neno la Mungu.

b Tazama makala “Unabii wa Kale Unaokuhusu” kwenye gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 2022.

c Ili ujifunze jinsi unavyoweza kujitayarisha kwa ajili ya matukio yenye kustaajabisha yatakayotokea hivi karibuni, tazama kitabu Ufalme wa Mungu Unatawala! uku. 230.