Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 45

Furahia Pendeleo Yako ya Kumutumikia Yehova mu Hekalu Yake ya Kiroho

Furahia Pendeleo Yako ya Kumutumikia Yehova mu Hekalu Yake ya Kiroho

“Mumuabudu Ule mwenye alifanya mbingu na dunia.”—UFU. 14:7.

WIMBO 93 Bariki Mikutano Yetu

KIFUPI YA HABARI a

1. Malaika iko nasema nini, na ile iko na maana gani kwetu?

 KAMA malaika angezungumuza na weye, ungesikiliza mambo yenye angekuambia? Leo, malaika iko nasema na “wale wenye wanakaa katika dunia, kwa kila taifa na kabila na luga na watu.” Iko nasema nini? “Mumuogope Mungu na kumupatia utukufu . . . Mumuabudu Ule mwenye alifanya mbingu na dunia.” (Ufu. 14:6, 7) Yehova njo Mungu pekee wa kweli mwenye kila mutu anapaswa kuabudu. Tuko wenye shukrani sana juu alitupatia pendeleo ya pekee ya kumuabudu mu hekalu yake kubwa ya kiroho!

2. Hekalu ya kiroho ya Yehova ni nini? (Ona pia kisanduku “ Hekalu ya Kiroho Haiko Nini?”)

2 Hekalu ya kiroho nini kabisa, na ni wapi tutapata mafasirio kuhusu ile hekalu? Hekalu ya kiroho haiko jengo yenye kuwa fasi fulani. Lakini, hekalu ya kiroho ni mupango wenye Yehova ameweka wa kumuabudu mu njia yenye anakubali kwa musingi wa zabihu ya Yesu ya ukombozi. Mutume Paulo alifasiria ule mupango mu barua yenye aliandikia Wakristo Waebrania wa karne ya kwanza wenye walikuwa wanaishi Yudea. b

3-4. Ni mambo gani njo ilihangaisha Paulo kuhusu Wakristo Waebrania wa Yudea, na aliwasaidia namna gani?

3 Juu ya nini Paulo aliandika barua yake kwa Wakristo Waebrania wa Yudea? Inawezekana ni kwa sababu mbili kubwa. Sababu ya kwanza ilikuwa juu ya kuwatia moyo. Wengi kati yao walikomalia mu dini ya Wayahudi. Inawezekana wakubwa wa dini yao ya zamani walikuwa wanawachekelea juu sasa walikuwa Wakristo. Juu ya nini? Juu Wakristo hawakukuwa na hekalu kwa ajili ya ibada, hawakukuwa na mazabahu kwenye wangemutolea Mungu zabihu, na hawakukuwa na makuhani wa kuwatumikia. Ile ingevunja moyo wanafunzi wa Yesu na kuregeza imani yao. (Ebr. 2:1; 3:12, 14) Na wengine hata wangejaribiwa kurudilia dini ya Wayahudi.

4 Sababu ya pili, Paulo alionyesha kama wale Wakristo Waebrania hawakukuwa wanajikaza kuelewa mafundisho ya mupya ao mafundisho mazito, ni kusema “chakula kigumu” chenye kupatikana mu Neno ya Mungu. (Ebr. 5:11-14) Kwa kweli, wamoja kati yao walikuwa wangali wanafuata Sheria ya Musa. Lakini Paulo alifasiria kama zabihu zenye Sheria iliomba haziondoe zambi kabisa-kabisa. Kwa hiyo, Sheria ‘iliwekwa pembeni.’ Kisha Paulo akazungumuzia mafundisho fulani mazito. Alikumbusha Wakristo wenzake “tumaini la muzuri zaidi” lenye linategemea zabihu ya Yesu yenye ingeweza kuwasaidia kabisa ‘kumukaribia Mungu.’—Ebr. 7:18, 19.

5. Kitabu ya Waebrania inazungumuzia nini yenye tunapaswa kuelewa, na juu ya nini?

5 Paulo alifasiria ndugu zake Waebrania juu ya nini ibada ya Kikristo ilikuwa ya hali ya juu zaidi kuliko ibada yao ya zamani. Mambo yenye ilikuwa mu dini ya Wayahudi ilikuwa tu “kivuli cha mambo yenye yatakuja, lakini ukweli wa mambo ni wa Kristo.” (Kol. 2:17) Kivuli ya kitu haiko kile kitu, lakini inaonyesha tu kijuu-juu umbo ya kile kitu. Kwa hiyo pia, namna ya kuabudu ya Wayahudi wa zamani ilikuwa tu kivuli ya ukweli wa mambo wenye ulipaswa kuya. Tunapaswa kuelewa mupango wenye Yehova ameweka juu zambi zetu ziweze kusamehewa ili tuweze kumuabudu mu njia yenye anakubali. Sasa, kwa kutumia mafasirio yenye kuwa mu kitabu ya Waebrania tulinganishe “kivuli” (ni kusema, namna ya kuabudu ya Wayahudi wa zamani) na “ukweli wa mambo” (ni kusema, namna ya kuabudu ya Wakristo). Kwa kufanya vile, tunaweza kuelewa muzuri zaidi hekalu ya kiroho na namna inatuhusu.

TABENAKULO

6. Tabenakulo ilitumiwa namna gani?

6 Kivuli. Paulo alizungumuzia tabenakulo ya wakati wa Musa, yenye ilianza kutumiwa mu 1512 M.K.Y. (Ona muchoro “Kivuli—Ukweli wa Mambo.”) Tabenakulo ilikuwa hema yenye Waisraeli walikuwa wanahamisha wakati walikuwa wanatoka fasi moya kuenda fasi ingine. Waliitumikisha kwa miaka karibu 500 mupaka wakati hekalu ilijengwa Yerusalemu. (Kut. 25:8, 9; Hes. 9:22) Ile “hema ya mukutano” njo ilikuwa fasi yenye Waisraeli walikuwa wanamukaribia Mungu, kumutolea zabihu zao, na kumuabudu. (Kut. 29:43-46) Lakini, tabenakulo ilifananisha pia kitu kubwa zaidi yenye ingekuja kwa ajili ya Wakristo.

7. Hekalu ya kiroho ilianza wakati gani?

7 Ukweli wa mambo. Tabenakulo ilikuwa “kivuli cha vitu vya mbinguni,” na inafananisha hekalu kubwa ya kiroho ya Yehova. Paulo alisema kama “hema [tabenakulo] hii ni mufano kwa ajili ya wakati wa sasa.” (Ebr. 8:5; 9:9) Kwa hiyo, wakati Paulo aliandikia Waebrania, hekalu ya kiroho tayari ilikuwa. Hekalu ya kiroho ilianza mu mwaka wa 29 K.K.Y. Ile mwaka, Yesu alibatizwa, alitiwa mafuta na roho takatifu, na akaanza kumutumikia Yehova akiwa “kuhani mukubwa” mu hekalu ya kiroho. cEbr. 4:14; Mdo. 10:37, 38.

KUHANI MUKUBWA

8-9. Kulingana na Waebrania 7:23-27, kuko tofauti gani kubwa kati ya makuhani wakubwa wa mu Israeli na Kuhani Mukubwa zaidi Yesu Kristo?

8 Kivuli. Kuhani mukubwa aliruhusiwa kuwakilisha watu mbele ya Mungu. Ni wakati tabenakulo ilianza kutumika njo Yehova aliweka Haruni kuwa kuhani mukubwa wa kwanza wa Waisraeli. Lakini, Paulo alifasiria kama “watu wengi walikuwa makuhani mumoja kisha mwingine kwa sababu kifo kiliwazuia kuendelea kuwa makuhani.” d (Soma Waebrania 7:23-27.) Juu hawakukuwa wakamilifu, wale makuhani walipaswa kutoa zabihu kwa ajili ya zambi zao wenyewe. Ile ni tofauti kubwa kati ya makuhani wakubwa wa Waisraeli na Kuhani Mukubwa zaidi, Yesu Kristo.

9 Ukweli wa mambo. Kuhani wetu Mukubwa Yesu Kristo ni “mutumishi . . . wa hema ya kweli, yenye imesimamishwa na Yehova, hapana na mwanadamu.” (Ebr. 8:1, 2) Paulo alifasiria kama “kwa sababu yeye [Yesu] anaendelea kuishi milele, hakuna wale wenye wanariti ukuhani wake.” Paulo aliongeza kama Yesu “hana uchafu, alitenganishwa na watenda-zambi,” na tofauti na makuhani wakubwa wa Waisraeli, “yeye hana lazima ya kutoa zabihu kila siku” kwa ajili ya zambi zake. Mu namna Wayahudi walikuwa wanaabudu zamani tuone namna walitumia mazabahu na zabihu na tuone inamaanisha nini mu namna Wakristo wanaabudu leo.

MAZABAHU NA ZABIHU

10. Zabihu zenye zilitolewa ku mazabahu ya shaba zilikuwa kivuli ya nini?

10 Kivuli. Inje ya mwingilio wa tabenakulo kulikuwa mazabahu ya shaba kwenye wanyama walikuwa natolewa kwa Yehova. (Kut. 27:1, 2; 40:29) Lakini zile zabihu hazikutoa musamaha kamili kwa ajili ya zambi za watu. (Ebr. 10:1-4) Zabihu za wanyama zenye ziliendelea kutolewa ku tabenakulo zilikuwa kivuli ya zabihu yenye ingeokoa kikamili wanadamu kutoka katika zambi.

11. Ni ku mazabahu gani njo Yesu alijitoa kuwa zabihu? (Waebrania 10:5-7, 10)

11 Ukweli wa mambo. Yesu alijua kama Yehova alimutuma hapa ku dunia ili kutoa uzima wake wa kibinadamu kuwa bei ya ukombozi kwa ajili ya wanadamu. (Mt. 20:28) Kwa hiyo, wakati alibatizwa, Yesu alionyesha kama alikuwa tayari kufanya mapenzi ya Yehova. (Yoh. 6:38; Gal. 1:4) Yesu alijitoa ku mazabahu ya mufano yenye ilifananisha “mapenzi” ya Mungu; mapenzi ya Mungu ilikuwa kwamba Mwana wake atoe uzima wake mukamilifu wa kibinadamu. Yesu alitoa uzima wake “mara moja kwa wakati wote” ili kufunika kikamili zambi za watu wote wenye wanaonyesha imani katika Kristo. (Soma Waebrania 10:5-7, 10.) Tuone sasa maana ya sehemu mbalimbali zenye kuwa mu tabenakulo.

PATAKATIFU NA PATAKATIFU ZAIDI

12. Nani njo aliruhusiwa kuingia Patakatifu na nani njo aliruhusiwa kuingia Patakatifu Zaidi?

12 Kivuli. Sehemu fulani zenye zilikuwa mu tabenakulo zilikuwa nafanana na sehemu fulani zenye zilikuwa mu hekalu yenye ilifikia kujengwa Yerusalemu. Ndani mulikuwa vyumba viwili, ni kusema, “Patakatifu” na “Patakatifu Zaidi,” vyenye vilitenganishwa na pazia. (Ebr. 9:2-5; Kut. 26:31-33) Ndani ya Patakatifu mulikuwa kinara cha taa cha zahabu, mazabahu ya kuchomea uvumba, na meza ya mikate ya wonyesho. “Makuhani wenye kutiwa mafuta” tu njo waliruhusiwa kuingia ndani ya Patakatifu ili kutimiza utumishi mutakatifu. (Hes. 3:3, 7, 10) Ndani ya Patakatifu Zaidi mulikuwa sanduku la agano la zahabu lenye lilifananisha kuwapo kwa Yehova. (Kut. 25:21, 22) Ni kuhani mukubwa tu njo mwenye aliruhusiwa kupita pazia na kuingia Patakatifu Zaidi mara moya ku mwaka, Siku ya Kufunika Zambi. (Law. 16:2, 17) Kila mwaka aliingia Patakatifu Zaidi ili kutoa damu ya wanyama juu zambi zake na zambi za taifa yote zifunikwe. Kisha wakati, kupitia roho yake takatifu, Yehova alionyesha wazi maana ya zile sehemu za tabenakulo.—Ebr. 9:6-8. e

13. Patakatifu na Patakatifu Zaidi panafananisha nini?

13 Ukweli wa mambo. Hesabu kidogo ya wanafunzi wa Kristo wametiwa mafuta na roho takatifu, na wanafurahia uhusiano wa pekee pamoya na Yehova. Wale wanafunzi 144000 watatumika kama makuhani mbinguni pamoya na Yesu. (Ufu. 1:6; 14:1) Mahali Patakatifu yenye ilikuwa mu tabenakulo inafananisha hali yao ya kufanywa kuwa wana wa Mungu wakati wangali ku dunia. (Ro. 8:15-17) Mahali Patakatifu Zaidi ya mu tabenakulo inafananisha mbinguni, kwenye Yehova anakuwaka. “Pazia” yenye ilitenganisha Patakatifu na Patakatifu Zaidi ilifananisha mwili wa kibinadamu wa Yesu wenye ulimuzuia kuingia mbinguni akiwa Kuhani Mukubwa zaidi wa hekalu ya kiroho. Kwa kutoa mwili wake wa kibinadamu kuwa zabihu kwa ajili ya wanadamu, Yesu alifanya iwezekane kwa Wakristo wote watiwa-mafuta kuenda mbinguni. Wanapaswa pia kuacha miili yao ya kibinadamu ili wapate zawabu ya kuishi mbinguni. (Ebr. 10:19, 20; 1 Ko. 15:50) Kisha Yesu kufufuliwa, aliingia Patakatifu Zaidi mu hekalu ya kiroho, kwenye watiwa-mafuta wote watafikia kujiunga naye.

14. Kulingana na Waebrania 9:12, 24-26, nini njo inafanya mupango wa Yehova kwa ajili ya hekalu ya kiroho ukuwe wa hali ya juu zaidi?

14 Tunaona wazi kama mupango wa Yehova wa ibada safi wenye kutegemea zabihu ya bei ya ukombozi na ukuhani wa Yesu Kristo ni wa hali ya juu sana. Kuhani mukubwa katika Israeli aliingia Patakatifu Zaidi penye kutengenezwa na wanadamu na aliingia na damu ya zabihu za wanyama, lakini Yesu “aliingia mbinguni kwenyewe,” mahali patakatifu zaidi kupita zote, ili kuonekana mbele ya Yehova. Pale alitoa samani ya uzima wake mukamilifu wa kibinadamu kwa ajili yetu “ili kuondoa zambi kupitia zabihu yake mwenyewe.” (Soma Waebrania 9:12, 24-26.) Zabihu ya Yesu njo zabihu kubwa sana yenye inatosha zambi milele. Sawa vile tutaona, ikiwa tuko na tumaini ya kuishi mbinguni ao ku dunia, siye wote tunaweza kumuabudu Yehova katika hekalu yake ya kiroho.

VIWANJA

15. Nani njo walikuwa natumikia mu kiwanja cha tabenakulo?

15 Kivuli. Tabenakulo ilikuwa na kiwanja moya, ni kusema fasi kubwa yenye kuzungukwa na lupango kwenye makuhani walikuwa nafanyia kazi zao. Mazabahu kubwa ya shaba ya toleo ya kuteketezwa ilkuwa pia mu ile kiwanja, mulikuwa pia beseni ya shaba ya maji yenye makuhani walitumia ili kujisafisha mbele ya kufanya utumishi wao mutakatifu. (Kut. 30:17-20; 40:6-8) Lakini hekalu zenye zilifikia kujengwa zilikuwa pia na kiwanja cha inje kwenye wale wenye hawakukuwa makuhani wangesimama na kumuabudu Yehova.

16. Nani njo anatumikia mu kiwanja cha ndani na nani njo anatumikia mu kiwanja cha inje ya hekalu ya kiroho?

16 Ukweli wa mambo. Mbele ya kuenda mbinguni ili kuwa makuhani pamoya na Yesu, mabaki ya Wakristo watiwa-mafuta wanatumika kwa uaminifu ku dunia mu kiwanja cha ndani cha hekalu ya kiroho. Ile beseni kubwa ya maji inakumbusha Wakristo watiwa-mafuta na Wakristo wengine wote kama ni jambo ya maana waendelee kuwa safi kiroho na waendelee kuwa na mwenendo safi. Sasa ni wapi njo “kundi kubwa,” wenye wanategemeza kwa uaminifu ndugu za Kristo wanamutumikia Yehova? Mutume Yohana aliwaona “wamesimama mbele ya kile kiti cha ufalme,” chenye ku dunia kinalingana na kiwanja cha inje, kwenye “wanamutolea [Mungu] utumishi mutakatifu muchana na usiku katika hekalu lake.” (Ufu. 7:9, 13-15) Tunafurahi sana juu tuko na fasi yetu mu mupango wa Yehova wa ibada safi!

PENDELEO YETU YA KUMUABUDU YEHOVA

17. Tuko na pendeleo ya kumutolea Yehova zabihu gani?

17 Leo, Wakristo wote wako na pendeleo ya kumutolea Yehova zabihu kwa kutumia wakati wao, nguvu yao, na vitu vyenye wako navyo ili kusaidia kazi ya Ufalme iendelee mbele. Sawa vile mutume Paulo aliambia Wakristo Waebrania, “sikuzote tumutolee Mungu zabihu ya sifa, ni kusema, tunda la midomo yetu yenye inatangaza jina lake.” (Ebr. 13:15) Tunaweza kuonyesha kama tunafurahia pendeleo yenye tuko nayo ya kumuabudu Yehova kwa kumutolea zabihu kwa uwezo wetu wote.

18. Kulingana na Waebrania 10:22-25, hatupaswe kupuuza nini na hatupaswe kusahau nini hata kidogo?

18 Soma Waebrania 10:22-25. Ku mwisho-mwisho wa barua yake kwa Waebrania, Paulo alizungumuzia sehemu mbalimbali za ibada yetu zenye hatupaswe kupuuza. Ile inatia ndani kumukaribia Yehova katika sala, kufanya tangazo ya mbele ya watu wote ya tumaini yetu, kukusanyika pamoya mu kutaniko, na kutiana moyo ‘na kufanya vile zaidi sana kwa kadiri tunaona siku ya Yehova kuwa inakaribia.’ Ku mwisho wa kitabu ya Ufunuo, malaika wa Yehova anasema hivi mara mbili: “Abudu Mungu!” (Ufu. 19:10; 22:9) Tusisahau hata siku moya hii mafundisho mazito kuhusu hekalu kubwa ya kiroho ya Yehova, na pendeleo ya muzuri sana yenye tuko nayo ya kumuabubu Mungu wetu mukubwa!

WIMBO 88 Unijulishe Njia Zako

a Moya kati ya mafundisho mazito ya Neno ya Mungu ni fundisho kuhusu hekalu kubwa ya kiroho ya Yehova. Ile hekalu ni nini? Hii habari inazungumuzia mambo mbalimbali yenye inapatikana mu kitabu ya Waebrania kuhusu ile hekalu. Tunatumainia kama hii habari itakusaidia ufurahie zaidi pendeleo yenye uko nayo ya kumuabudu Yehova.

b Ili kuona kifupi ya Kitabu ya Waebrania, angalia ku jw.org video Utangulizi wa Kitabu cha Waebrania.

c Waebrania njo tu kitabu moya ya Maandishi ya Kigiriki ya Kikristo yenye inamuita Yesu kuwa Kuhani Mukubwa.

d Kulingana na kitabu fulani, inawezekana mu Israeli mulifikia kuwa makuhani wakubwa 84 kufikia wakati hekalu ya Yerusalemu iliharibiwa mu mwaka wa 70 K.K.Y.

e Ili kujua maana ya mambo yenye kuhani mukubwa alikuwa anafanya kwenye Siku ya Kufunika Zambi, angalia ku jw.org video Hema.

g Ona kisanduku “Jinsi Roho Ilivyofunua Maana ya Hekalu la Kiroho” mu Munara wa Mulinzi wa tarehe 15, Mwezi wa 7, 2010, uku. 22.