MAKALA YA 45

Thamini Pendeleo Lako la Kuabudu Katika Hekalu la Kiroho la Yehova

Thamini Pendeleo Lako la Kuabudu Katika Hekalu la Kiroho la Yehova

“Mwabuduni Yule aliyeziumba mbingu na dunia.”—UFU. 14:7.

WIMBO 93 Bariki Kukutana Kwetu

MUHTASARI a

1. Malaika anatangaza ujumbe gani, na hilo linamaanisha nini kwetu?

 IKIWA malaika angezungumza nawe, je, ungesikiliza mambo ambayo angekwambia? Leo, malaika anazungumza na “kila taifa na kabila na lugha na watu.” Anasema nini? “Mwogopeni Mungu na kumpa utukufu . . . Mwabuduni Yule aliyeziumba mbingu na dunia.” (Ufu. 14:​6, 7) Yehova ndiye Mungu wa pekee wa kweli ambaye kila mtu anapaswa kumwabudu. Tunashukuru kwamba ametupatia pendeleo lenye thamani sana la kumwabudu katika hekalu lake kubwa la kiroho!

2. Hekalu la kiroho la Yehova ni nini? (Pia tazama sanduku “ Maana Isiyo Sahihi ya Hekalu la Kiroho.”)

2 Hekalu la kiroho ni nini hasa, na tunaweza kupata wapi ufafanuzi kulihusu? Hekalu la kiroho si jengo halisi. Ni mpango wa Yehova wa kumtolea ibada inayokubalika kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Yesu. Mtume Paulo alifafanua mpango huo katika barua aliyoandikia Wakristo Waebrania katika karne ya kwanza walioishi huko Yudea. b

3-4. Ni mambo gani ambayo yalimhangaisha Paulo kuhusu Wakristo Waebrania huko Yudea, naye aliwasaidiaje?

3 Kwa nini Paulo aliwaandikia barua Wakristo Waebrania huko Yudea? Inaelekea ni kwa sababu mbili kuu. Kwanza, ili kuwatia moyo. Wengi wao walishirikiana na dini ya Kiyahudi kabla ya kuwa Wakristo. Huenda viongozi wa dini ya Kiyahudi waliwadhihaki kwa kuwa Wakristo. Kwa nini? Kwa sababu Wakristo hawakuwa na hekalu la kifahari ambamo wangeabudu, na hawakuwa na madhabahu ambayo wangetumia kumtolea Mungu dhabihu, wala hawakuwa na makuhani wa kuwahudumia. Huenda hilo lingewavunja moyo Wanafunzi wa Kristo na kudhoofisha imani yao. (Ebr. 2:1; 3:​12, 14) Hata huenda baadhi yao walishawishiwa kurudi katika dini ya Kiyahudi.

4 Pili, Paulo aliwaambia Wakristo hao Waebrania kwamba hawakuwa wakijitahidi kuelewa mafundisho mapya au mafundisho ya kiroho yenye kina, yaani, “chakula kigumu” kinachopatikana katika Neno la Mungu. (Ebr. 5:​11-14) Inaonekana kwamba bado baadhi yao walikuwa wakifuata Sheria ya Musa. Hata hivyo, Paulo alieleza kwamba dhabihu zilizotolewa kulingana na Sheria ya Musa hazingeweza kuondoa kabisa dhambi. Kwa sababu hiyo, Sheria ilikuwa ‘imewekwa kando.’ Basi, Paulo akawafundisha baadhi ya kweli zenye kina zaidi. Aliwakumbusha Wakristo wenzake kuhusu “tumaini bora” linalotegemea dhabihu ya Yesu ambayo kwa kweli ingewasaidia ‘wamkaribie Mungu.’—Ebr. 7:​18, 19.

5. Tunahitaji kuelewa jambo gani katika kitabu cha Biblia cha Waebrania, na kwa nini?

5 Paulo aliwaeleza ndugu zake Waebrania kwa nini ibada ya Kikristo ilikuwa bora zaidi kuliko jinsi walivyoabudu zamani. Utaratibu uliotumiwa katika dini ya Kiyahudi ulikuwa “kivuli cha mambo yanayokuja, bali uhalisi ni wa Kristo.” (Kol. 2:17) Kivuli kinachoonekana kwa kawaida ni umbo la kitu halisi ambacho kinatokeza kivuli hicho. Vivyo hivyo, njia ambayo Wayahudi walitumia kuabudu zamani, ilikuwa kivuli tu cha uhalisi ambao ungekuja. Tunahitaji kuelewa mpango ambao Yehova ameweka ili tusamehewe dhambi zetu na ili tumwabudu kwa njia inayokubalika. Acheni tulinganishe “kivuli” (njia ambayo Wayahudi walitumia kuabudu zamani) na “uhalisi” (njia ya Wakristo ya kuabudu), kama inavyofafanuliwa katika Waebrania. Kufanya hivyo kutatusaidia kuelewa vizuri zaidi hekalu la kiroho na jinsi linavyotuhusu.

HEMA LA IBADA

6. Hema la ibada lilitumiwa jinsi gani?

6 Njia ya zamani ya ibada. Mazungumzo ya Paulo yalitegemea hema la ibada ambalo Musa alianzisha katika mwaka wa 1512 K.W.K. (Tazama chati “Njia ya Zamani ya Ibada—Uhalisi wa Kikristo.”) Mwanzoni, Waisraeli walibeba hema la ibada walipoondoka sehemu moja kwenda nyingine. Walilitumia kwa karibu miaka 500 hadi hekalu la kudumu lilipojengwa huko Yerusalemu. (Kut. 25:​8, 9; Hes. 9:22) “Hema [hilo] la mkutano” lilikuwa kituo ambacho Waisraeli wangemkaribia Mungu na kumtolea dhabihu zao na ibada yao. (Kut. 29:​43-46) Hata hivyo, hema la ibada liliwakilisha jambo bora zaidi kwa ajili ya Wakristo.

7. Hekalu la kiroho lilianzishwa wakati gani?

7 Uhalisi wa Kikristo. Hema la kale la ibada lilikuwa “kivuli cha vitu vya mbinguni,” na lilifananisha hekalu kubwa la kiroho la Yehova. Paulo alisema kwamba “hema hili ni mfano kwa ajili ya wakati huu.” (Ebr. 8:5; 9:9) Basi, wakati alipowaandikia Waebrania barua, tayari hekalu la kiroho lilikuwa jambo halisi kwa Wakristo. Hekalu hilo lilianzishwa mwaka wa 29 W.K. Mwaka huo, Yesu alibatizwa, akatiwa mafuta kwa roho takatifu, na akaanza kutumikia akiwa “kuhani mkuu sana” wa Yehova katika hekalu la kiroho. cEbr. 4:14; Mdo. 10:​37, 38.

KUHANI MKUU

8-9. Kulingana na Waebrania 7:​23-27, kuna tofauti gani kubwa kati ya makuhani wakuu wa Israeli na Kuhani Mkuu sana, Yesu Kristo?

8 Njia ya zamani ya ibada. Kuhani mkuu alikuwa na jukumu la kuwawakilisha watu mbele za Mungu. Haruni kuhani mkuu wa kwanza wa Israeli, alichaguliwa na Yehova mpango wa hema la ibada ulipoanzishwa. Hata hivyo, kama Paulo alivyoeleza, “wengi walikuwa makuhani mmoja baada ya mwingine kwa sababu kifo kiliwazuia wasiendelee kuwa makuhani.” d (Soma Waebrania 7:​23-27.) Na kwa sababu walikuwa wanadamu wasio wakamilifu, makuhani hao wakuu walihitaji kutoa dhabihu kwa ajili ya dhambi zao wenyewe. Hiyo ni tofauti kubwa sana kati ya makuhani wakuu wa Israeli na Kuhani Mkuu sana, Yesu Kristo. 

9 Uhalisi wa Kikristo. Akiwa Kuhani wetu Mkuu, Yesu Kristo ni “mhudumu . . . wa hema la kweli, ambalo limesimamishwa na Yehova, na si mwanadamu.” (Ebr. 8:​1, 2) Paulo alieleza kwamba “kwa sababu [Yesu] anaendelea kuishi milele, hakuna anayerithi ukuhani wake.” Paulo aliongezea kwamba Yesu ni kuhani “asiye na unajisi, aliyetenganishwa na watenda dhambi” na tofauti na makuhani wakuu wa Israeli, “hahitaji kutoa dhabihu kila siku” kwa ajili ya dhambi zake mwenyewe. Sasa fikiria kuhusu tofauti kati ya madhabahu na dhabihu katika njia ya zamani ya ibada na mpango ulio katika uhalisi wa Kikristo.

MADHABAHU NA DHABIHU

10. Dhabihu zilizotolewa kwenye madhabahu ya shaba ziliwakilisha nini?

10 Njia ya zamani ya ibada. Nje ya mwingilio wa hema la ibada kulikuwa na madhabahu ya shaba ambayo ilitumiwa kumtolea Yehova dhabihu za wanyama. (Kut. 27:​1, 2; 40:29) Hata hivyo, dhabihu hizo hazingeandaa msamaha kamili kwa ajili ya dhambi za watu. (Ebr. 10:​1-4) Mpango wa kutoa dhabihu za wanyama kwa kuendelea kwenye hema la ibada ulifananisha dhabihu moja ambayo ingewakomboa wanadamu kikamili.

11. Yesu alijitoa mwenyewe kuwa dhabihu juu ya madhabahu gani? (Waebrania 10:​5-7, 10)

11 Uhalisi wa Kikristo. Yesu alijua kwamba Yehova alikuwa amemtuma duniani ili atoe uhai wake wa kibinadamu uwe dhabihu ya fidia kwa ajili ya wanadamu. (Mt. 20:28) Hivyo, wakati wa ubatizo wake, Yesu alijitoa mwenyewe ili kufanya mapenzi ya Yehova. (Yoh. 6:38; Gal. 1:4) Yesu alijitoa mwenyewe kwenye madhabahu ya mfano ambayo iliwakilisha “mapenzi” ya Mungu kwa ajili ya Mwana wake ili atoe uhai wake mkamilifu wa kibinadamu uwe dhabihu. Yesu alitoa uhai wake “mara moja kwa wakati wote” ili kutoa fidia au kufunika kabisa dhambi za kila mtu ambaye anaonyesha imani katika Kristo. (Soma Waebrania 10:​5-7, 10.) Sasa, tutachunguza maana ya sehemu za ndani za hema la ibada.

PATAKATIFU NA PATAKATIFU ZAIDI

12. Ni nani ambao waliruhusiwa kuingia katika vyumba vya hema la ibada?

12 Njia ya zamani ya ibada. Hema la ibada na mahekalu ambayo baadaye yalijengwa huko Yerusalemu, kimsingi yalikuwa na mpangilio uleule. Ndani kulikuwa na sehemu mbili—“Patakatifu” na “Patakatifu Zaidi”—na sehemu hizo zilitenganishwa na pazia lililotariziwa. (Ebr. 9:​2-5; Kut. 26:​31-33) Ndani ya Patakatifu kulikuwa na kinara cha taa cha dhahabu, madhabahu iliyotumiwa kuchoma uvumba, na meza ya mikate ya wonyesho. “Makuhani waliotiwa mafuta” ndio tu walioruhusiwa kuingia Patakatifu ili kutimiza majukumu yao ya kikuhani. (Hes. 3:​3, 7, 10) Patakatifu Zaidi palikuwa na sanduku la agano la dhahabu ambalo liliwakilisha kuwepo kwa Yehova. (Kut. 25:​21, 22) Kuhani mkuu peke yake ndiye aliyeruhusiwa kuvuka pazia na kuingia Patakatifu Zaidi kila mwaka katika Siku ya Kufunika Dhambi. (Law. 16:​2, 17) Mwaka baada ya mwaka, aliingia akiwa na damu ya wanyama ili kufunika dhambi zake mwenyewe na dhambi za taifa zima. Mwishowe Yehova kupitia roho yake takatifu, alionyesha wazi maana ya sehemu hizo mbalimbali za hema la ibada.—Ebr. 9:​6-8. e

13. Patakatifu na Patakatifu zaidi katika hema la ibada panafananisha nini katika uhalisi wa Kikristo?

13 Uhalisi wa Kikristo. Idadi hususa ya wanafunzi wa Kristo wametiwa mafuta kwa roho takatifu, nao wana uhusiano wa pekee pamoja na Yehova. Wakristo hao 144,000 watatumikia wakiwa makuhani mbinguni pamoja na Yesu. (Ufu. 1:6; 14:1) Patakatifu pa hema la ibada panafananisha hali yao ya kuzaliwa kwa roho na kuwa wana wa Mungu wakiwa bado duniani. (Rom. 8:​15-17) Patakatifu Zaidi pa hema la ibada panafananisha mbinguni, ambako Yehova anaishi. “Pazia” lililotenganisha Patakatifu na Patakatifu Zaidi lilifananisha mwili wa kibinadamu wa Yesu ambao ulikuwa kizuizi cha kuingia mbinguni akiwa Kuhani Mkuu sana wa hekalu la kiroho. Kwa kuutoa uhai wake wa kibinadamu uwe dhabihu kwa ajili ya wanadamu, Yesu alifungua njia ya uhai wa mbinguni kwa ajili ya Wakristo watiwa-mafuta. Ili wapokee thawabu yao ya mbinguni, ni lazima wao pia wavue miili yao ya kibinadamu. (Ebr. 10:​19, 20; 1 Kor. 15:50) Baada ya kufufuliwa Yesu aliingia Patakatifu zaidi pa hekalu la kiroho ambako hatimaye watiwa-mafuta wanajiunga naye.

14. Kulingana na Waebrania 9:​12, 24-26, ni nini kinachofanya mpango wa hekalu la kiroho la Yehova uwe bora zaidi?

14 Basi, tunaona mpango bora wa Yehova wa ibada unaotegemea fidia ya dhabihu na ukuhani wa Yesu Kristo. Kuhani mkuu wa Israeli aliingia katika Patakatifu Zaidi palipotengenezwa na wanadamu, akiwa na damu ya dhabihu za wanyama, lakini Yesu “aliingia mbinguni kwenyewe,” mahali patakatifu zaidi, ili kuwa mbele za Yehova. Akiwa huko, alitoa thamani ya uhai wake mkamilifu wa kibinadamu kwa ajili yetu “ili kuondoa dhambi kupitia dhabihu yake mwenyewe.” (Soma Waebrania 9:​12, 24-26.) Dhabihu ya Yesu ndiyo dhabihu pekee ambayo inafuta dhambi milele. Sasa tutajifunza kwamba iwe tuna tumaini la kwenda mbinguni au kuishi duniani, sote tunaweza kumwabudu Yehova katika hekalu lake la kiroho.

NYUA

15. Ni nani waliotumikia kwenye ua wa hema la ibada?

15 Njia ya zamani ya ibada. Hema la ibada lilikuwa na ua mmoja—eneo lililo wazi ambalo lilikuwa limezungushiwa wigo au ukingo, mahali ambapo makuhani walitimiza majukumu yao. Madhabahu kubwa ya shaba ya dhabihu za kuteketezwa ilikuwa katika ua pamoja na beseni kubwa la maji la shaba ambalo makuhani walitumia kujitakasa kabla ya kutimiza utumishi wao mtakatifu. (Kut. 30:​17-20; 40:​6-8) Hata hivyo, mahekalu yaliyojengwa baadaye, yalikuwa pia na ua wa nje mahali ambapo wale ambao hawakuwa makuhani wangeweza kusimama na kumwabudu Mungu.

16. Ni nani wanaotumikia katika nyua mbalimbali za hekalu la kiroho?

16 Uhalisi wa Kikristo. Kabla ya kwenda kutumikia wakiwa makuhani na Yesu mbinguni, watiwa-mafuta waliobaki duniani ambao ni ndugu za Kristo wanatumikia kwa uaminifu katika ua wa ndani wa hekalu la kiroho duniani. Kuwepo kwa beseni kubwa la maji ni kikumbusho muhimu kwao, na kwa Wakristo wote cha kuendelea kuwa safi kiadili na kiroho. Basi, wale wanaofanyiza “umati mkubwa,” unaounga mkono kwa ushikamanifu ndugu za Kristo, wanamwabudu Yehova wakiwa wapi? Mtume Yohana aliwaona wakiwa “wamesimama mbele ya kiti cha ufalme,” sehemu ambayo inalingana na ua wa nje duniani, ambapo “wanamtolea [Mungu] utumishi mtakatifu mchana na usiku katika hekalu lake.” (Ufu. 7:​9, 13-15) Tunathamini sana pendeleo la kushiriki katika mpango wa ibada safi ya Yehova!

PENDELEO LETU LA KUMWABUDU YEHOVA

17. Tuna pendeleo la kumtolea Yehova dhabihu gani mbalimbali?

17 Leo, Wakristo wote wana pendeleo la kumtolea Yehova dhabihu kwa kutumia wakati, nguvu, na mali zao, ili kuendeleza kazi ya Ufalme wa Mungu. Kama mtume Paulo alivyowaambia Wakristo Waebrania, sikuzote tunaweza kumtolea “Mungu dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo yetu ambalo hulitangaza jina lake hadharani.” (Ebr. 13:15) Tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini pendeleo letu la kumwabudu Yehova kwa kumtolea dhabihu zetu zilizo bora kabisa.

18. Kulingana na Waebrania 10:​22-25, ni mambo gani ambayo hatupaswi kamwe kuyapuuza, na ni nini ambacho hatupaswi kusahau?

18 Soma Waebrania 10:​22-25. Karibu na mwisho wa barua yake kwa Waebrania, Paulo anataja mambo mbalimbali kuhusu ibada yetu ambayo hatupaswi kamwe kuyapuuza. Mambo hayo yanatia ndani kumkaribia Yehova katika sala, kutoa tangazo la hadharani la tumaini letu, kukutana pamoja tukiwa kutaniko, na kutiana moyo “zaidi kwa kadiri [tunavyoona] siku ile [ya Yehova] ikikaribia.” Karibu na mwisho wa simulizi la Ufunuo, malaika wa Yehova anasema maneno yafuatayo mara mbili ili kusisitiza: “Mwabudu Mungu!” (Ufu. 19:10; 22:9) Acheni tuendelee kukumbuka kweli hizi zenye kina za kiroho kuhusu hekalu kubwa la kiroho la Yehova na pendeleo letu lenye thamani la kumwabudu Mungu wetu Mkuu!

WIMBO 88 Nijulishe Njia Zako

a Mojawapo ya mafundisho yenye kina zaidi katika Neno la Mungu, ni kuhusu hekalu kubwa la kiroho la Yehova. Hekalu hilo ni nini? Katika makala hii tutachunguza habari kuhusu hekalu hilo ambazo zinapatikana katika kitabu cha Biblia cha Waebrania. Tunatarajia kwamba makala hii itakusaidia kuthamini zaidi pendeleo lako la kumwabudu Yehova.

b Ili kuona muhtasari wa kitabu cha Biblia cha Waebrania, tazama video, Utangulizi wa Waebrania kwenye jw.org.

c Waebrania ndicho kitabu pekee katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ambacho kinamrejelea Yesu kuwa Kuhani Mkuu.

d Kulingana na kitabu kimoja cha marejezo, huenda kulikuwa na jumla ya makuhani wakuu 84 huko Israeli kufikia wakati ambapo hekalu huko Yerusalemu liliharibiwa mwaka wa 70 W.K.

e Ili ujifunze maana ya mambo ambayo Kuhani Mkuu alifanya katika siku ya kufunika dhambi, tazama video ya Kiingereza The Tent, yaani, Hema la Ibada kwenye jw.org.

f Tazama kitabu Hatimaye Ibada Safi ya Yehova Yarudishwa! uku. 240.

g Tazama sanduku “Jinsi Roho Ilivyofunua Maana ya Hekalu la Kiroho” katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 2010, uku. 22.