MAKALA YA 2

WIMBO 19 Mlo wa Jioni wa Bwana

Je, Uko Tayari kwa Ajili ya Siku Muhimu Zaidi Katika Mwaka?

Je, Uko Tayari kwa Ajili ya Siku Muhimu Zaidi Katika Mwaka?

“Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka.”​—LUKA 22:19.

JAMBO KUU

Chunguza kwa nini siku ya Ukumbusho ni ya pekee, jinsi tunavyoweza kujitayarisha kwa ajili ya siku hiyo, na jinsi tunavyoweza kuwasaidia wengine wahudhurie.

1. Kwa nini Ukumbusho ndiyo siku muhimu zaidi katika mwaka? (Luka 22:19, 20)

 UKUMBUSHO wa kifo cha Kristo ndiyo siku muhimu zaidi kwa watu wa Yehova. Ndilo tukio pekee ambalo Yesu aliagiza kihususa wafuasi wake waadhimishe. (Soma Luka 22:19, 20.) Tuna sababu nyingi za kutazamia kwa hamu Ukumbusho. Acheni tuchunguze baadhi ya sababu hizo.

2. Ni baadhi ya sababu gani zinazofanya tutarajie kwa hamu Ukumbusho?

2 Ukumbusho unatusaidia kutafakari thamani ya fidia. Unatukumbusha njia ambazo tunaweza kuonyesha shukrani zetu kwa ajili ya dhabihu ya Yesu. (2 Kor. 5:14, 15) Pia, unatupatia nafasi ya kufurahia “ubadilishanaji wa kitia moyo” pamoja na ndugu na dada zetu. (Rom. 1:12, maelezo ya chini) Kila mwaka, wahubiri wengi wasiotenda huhudhuria Ukumbusho. Baadhi yao, hata wamechochewa kumrudia Yehova kwa sababu wamekaribishwa kwa uchangamfu kwenye Ukumbusho. Na watu wengi wanaopendezwa wamechochewa kuanza kufuata barabara ya uzima kwa sababu ya mambo waliyosikia na waliyojionea. Hivyo, haishangazi kwamba Ukumbusho ni siku ya pekee sana kwetu!

3. Ukumbusho unauunganishaje undugu wetu wa ulimwenguni pote? (Tazama pia picha.)

3 Fikiria pia jinsi Ukumbusho unavyouunganisha undugu wetu wa ulimwenguni pote. Kadiri jua linavyotua siku hiyo, Mashahidi wa Yehova hukusanyika kwa ajili ya Ukumbusho ulimwenguni pote. Sisi sote husikiliza hotuba inayokazia umuhimu wa fidia. Tunaimba nyimbo mbili za sifa, tunapitisha mifano, na kwa moyo wote tunaitikia “amina” baada ya kutolewa kwa sala nne. Katika muda wa saa 24 hivi, makutaniko yote ulimwenguni yatakuwa yamefuata hatua hizohizo. Je, unaweza kuwazia shangwe ambayo Yehova na Yesu wanahisi wanapoona tukiwaheshimu kwa umoja kwa njia hiyo?

Ukumbusho unauunganisha undugu wetu wa ulimwenguni pote (Tazama fungu la 3) f



4. Tutazungumzia nini katika makala hii?

4 Katika makala hii, tutachunguza maswali haya: Tunawezaje kuutayarisha moyo wetu kwa ajili ya Ukumbusho? Tunaweza kuwasaidiaje wengine wanufaike na Ukumbusho? Na tunawezaje kuwasaidia wahubiri wasiotenda? Majibu ya maswali hayo yatatusaidia kuwa tayari kwa ajili ya tukio hilo muhimu sana.

TUNAWEZAJE KUUTAYARISHA MOYO WETU KWA AJILI YA UKUMBUSHO?

5. (a) Kwa nini tunapaswa kutafakari kuhusu thamani ya fidia? (Zaburi 49:7, 8) (b) Umejifunza nini kutokana na video Kwa Nini Yesu Alikufa?

5 Njia moja muhimu zaidi ambayo tunaweza kuutayarisha moyo wetu kwa ajili ya Ukumbusho ni kwa kutafakari thamani ya dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. Hatungeweza kujikomboa kutoka kwenye dhambi na kifo kwa uwezo wetu wenyewe. (Soma Zaburi 49:7, 8; tazama pia video Kwa Nini Yesu Alikufa?) a Hivyo, Yehova alipanga Yesu atoe uhai wake kwa ajili yetu, jambo ambalo lilimgharimu sana Yeye na Mwana wake mpendwa. (Rom. 6:23) Kadiri tunavyotafakari mambo ambayo Yehova na Yesu wamejidhabihu kwa ajili yetu, ndivyo tutakavyoithamini zaidi fidia. Tutachunguza mambo machache ambayo Yehova na Yesu walijidhabihu kwa ajili yetu. Lakini kwanza tuchunguze fidia ilihusisha nini.

6. Fidia ilihusisha nini?

6 Fidia ni bei inayolipwa ili kurudisha kitu. Mwanadamu wa kwanza, Adamu, alikuwa mkamilifu alipoumbwa. Alipofanya dhambi, alipoteza tumaini lake la kuishi milele na pia la watoto wake wote. Ili kulipia kile ambacho Adamu alipoteza, Yesu alitoa uhai wake mkamilifu kuwa dhabihu. Wakati wa maisha yake yote akiwa duniani, Yesu “hakufanya dhambi wala udanganyifu haukupatikana kinywani mwake.” (1 Pet. 2:22) Wakati wa kifo cha Yesu, uhai wake mkamilifu ulilingana kabisa na uhai ambao Adamu alipoteza.—1 Kor. 15:45; 1 Tim. 2:6.

7. Ni baadhi ya majaribu gani ambayo Yesu alikabili alipokuwa duniani?

7 Alipokuwa duniani, Yesu alimtii Baba yake wa mbinguni kikamilifu licha ya kukabili majaribu mengi. Ingawa Yesu alikuwa mtoto mkamilifu, aliwatii wazazi wake ambao hawakuwa wakamilifu. (Luka 2:51) Akiwa kijana, alihitaji kukataa kushinikizwa na wengine ili aendelee kuwa mtiifu na mwaminifu. Na akiwa mtu mzima, Yesu alihitaji kusimama imara dhidi ya vishawishi vya Shetani Ibilisi, kutia ndani mashambulizi ya moja kwa moja ambayo yangeweza kufanya aache kuwa mshikamanifu kwa Mungu. (Mt. 4:1-11) Shetani alikuwa ameazimia kumfanya Yesu atende dhambi ili asiweze kulipia fidia.

8. Yesu alivumilia majaribu gani mengine?

8 Wakati wa huduma yake duniani, Yesu alivumilia majaribu mengine pia. Maadui wake walimtesa na walijaribu kumuua. (Luka 4:28, 29; 13:31) Alihitaji kuvumilia udhaifu wa wafuasi wake. (Marko 9:33, 34) Alipokuwa akihukumiwa kifo, aliteswa na kudhihakiwa. Kisha aliuawa kwa njia ya kuaibisha na yenye maumivu makali sana. (Ebr. 12:1-3) Alipokuwa kwenye mti wa mateso alilazimika kuvumilia mateso makali, bila kuwa na ulinzi wa Yehova. bMt. 27:46.

9. Tunahisije kuhusu dhabihu ya Yesu? (1 Petro 1:8)

9 Ni wazi kwamba Yesu alijidhabihu sana ili kutoa uhai wake kuwa fidia. Je, hatuchochewi kumpenda sana Yesu tunapotafakari jinsi alivyojidhabihu sana kwa hiari kwa ajili yetu?—Soma 1 Petro 1:8.

10. Yehova alijidhabihu jinsi gani ili kutoa fidia?

10 Namna gani Yehova? Alijidhabihu kwa hiari jinsi gani ili Yesu atoe uhai wake kuwa fidia? Uhusiano wa Yehova na Yesu ni uhusiano wa karibu zaidi kati ya baba na mwana. (Met. 8:30) Hivyo, hebu wazia jinsi Yehova alivyohisi alipomwona Yesu akivumilia majaribu mengi sana alipokuwa duniani. Bila shaka, Yehova aliumia sana alipoona Mwana wake akitendewa kwa njia isiyofaa, akikataliwa, na kuteswa.

11. Toa mfano unaoonyesha jinsi Yehova alivyohisi Yesu alipouawa.

11 Mzazi yeyote aliyefiwa na mtoto anaelewa vizuri hisia kali za huzuni zinazotokana na kifo cha mtoto. Tuna imani yenye nguvu katika ufufuo, lakini hilo haliondoi maumivu tunayohisi tunapofiwa na mtu tunayempenda. Mfano huo, unatusaidia kuelewa jinsi Yehova alivyohisi alipoona Mwana wake mpendwa akiteseka na kufa katika majira ya kuchipua ya mwaka wa 33 W.K. cMt. 3:17.

12. Tunaweza kufanya nini kabla ya Ukumbusho?

12 Kuanzia sasa hadi wakati wa Ukumbusho, jitahidi kujifunza zaidi kuhusu fidia kwenye funzo lako la kibinafsi au katika Ibada ya Familia. Tumia Mwongozo wa Utafiti wa Mashahidi wa Yehova (ikiwa unapatikana katika lugha yenu) au machapisho mengine ya kujifunzia Biblia ili ujifunze kwa kina kuhusu fidia. d Pia, jitahidi kufuata ratiba ya usomaji wa Biblia ya Ukumbusho katika Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha ya Kikristo. Na katika siku ya Ukumbusho, usisahau kutazama programu ya pekee ya Ibada ya Asubuhi. Tunapotayarisha moyo wetu kwa ajili ya Ukumbusho, tutaweza kuwasaidia wengine wanufaike pia na Ukumbusho.—Ezra 7:10.

WASAIDIE WENGINE WANUFAIKE

13. Hatua ya kwanza ya kuwasaidia wengine wanufaike na Ukumbusho ni ipi?

13 Tunaweza kuwasaidiaje wengine wanufaike na Ukumbusho? Bila shaka, hatua ya kwanza ni kwa kuwaalika. Zaidi ya kuwaalika wale tunaokutana nao katika huduma kwa ukawaida, tunaweza kuandika orodha ya watu tutakaowaalika. Orodha hiyo inaweza kutia ndani watu wetu wa ukoo, wafanyakazi wenzetu, wanafunzi wenzetu, na watu wengine tunaowajua. Hata ikiwa hatuna mialiko ya kutosha iliyochapishwa, tunaweza kuwatumia kiunganishi cha mwaliko wa kielektroni. Huenda tukashangaa kuona jinsi watu wengi watakavyoitikia vizuri!—Mhu. 11:6.

14. Toa mfano unaoonyesha nguvu za mwaliko wa kibinafsi.

14 Usipuuze kamwe nguvu za mwaliko wa kibinafsi. Siku moja, dada ambaye mume wake si Shahidi alishangaa mume wake alipomwambia kwa furaha kwamba angehudhuria Ukumbusho. Kwa nini dada huyo alishangaa? Kwa sababu wakati uliopita alikuwa akimtia moyo mara nyingi ahudhurie, lakini mume wake hakuhudhuria. Kwa nini wakati huu alikubali kuhudhuria? Mume huyo alisema hivi: “Nimepewa mwaliko wa kibinafsi.” Kisha akaeleza kwamba mzee wa kutaniko anayefahamiana naye alimwalika ahudhurie Ukumbusho. Mume wake alihudhuria Ukumbusho mwaka huo na miaka mingi iliyofuata.

15. Tunahitaji kukumbuka nini tunapowaalika watu kwenye Ukumbusho?

15 Kumbuka kwamba wale tunaowaalika wanaweza kuwa na maswali—hasa ikiwa hawakuwahi kuhudhuria mikutano yetu. Itafaa kufikiria mapema maswali watakayouliza na kutayarisha majibu. (Kol. 4:6) Kwa mfano, huenda wengine wakauliza: ‘Ni mambo gani yatakayofanyika katika tukio hilo?’ ‘Tukio hilo litachukua muda gani?’ ‘Nivae mavazi ya aina gani?’ ‘Je, kuna kiingilio?’ ‘Je, sadaka zitakusanywa?’ Tunapomwalika mtu kwa ajili ya Ukumbusho, tunaweza kumuuliza moja kwa moja, “Je, una swali lolote?” kisha tujibu maswali yoyote atakayouliza. Pia, tunaweza kutumia video Kumbuka Kifo cha Yesu na Ni Nini Hutendeka Katika Jumba la Ufalme? ili kumsaidia kuelewa jinsi mikutano yetu inavyofanywa. Na somo la 28 la kitabu Furahia Maisha Milele! lina mambo mengi mazuri tunayoweza kushiriki na mtu huyo.

16. Wale wanaohudhuria Ukumbusho wanaweza kuwa na maswali gani mengine?

16 Baada ya kuhudhuria ukumbusho, watu wapya wanaopendezwa wanaweza kuuliza maswali mengine. Wanaweza kuuliza hivi: Kwa nini ni watu wachache tu walioshiriki mifano (au hakuna mtu yeyote aliyeshiriki)? Pia, huenda wakauliza tunaadhimisha Ukumbusho mara ngapi. Na huenda wangependa kujua ikiwa mikutano yote ya Mashahidi wa Yehova inafanywa kama Ukumbusho unavyofanywa. Hata ingawa mambo mengi yatakuwa yamezungumziwa kwenye hotuba ya Ukumbusho, huenda wapya wakahitaji ufafanuzi zaidi. Makala kwenye jw.org yenye kichwa “Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Wanaadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana kwa Njia Tofauti na Dini Nyingine?” inaweza kutusaidia kujibu baadhi ya maswali yao. Tungependa kufanya yote tuwezayo—kabla, wakati, na baada ya Ukumbusho—ili kuwasaidia wale “walio na mwelekeo unaofaa” wanufaike na mwadhimisho huo.—Mdo. 13:48.

WASAIDIE WAHUBIRI WASIOTENDA

17. Wazee wa kutaniko wanaweza kuwasaidiaje wahubiri wasiotenda? (Ezekieli 34:12, 16)

17 Wakati wa majira ya Ukumbusho, wazee wa kutaniko wanaweza kuwasaidiaje wahubiri wasiotenda? Kwa kuwaonyesha kwamba wanawajali. (Soma Ezekieli 34:12, 16.) Kabla ya Ukumbusho, jitahidi kuwasiliana na wengi iwezekanavyo. Wahakikishie kwamba unawapenda na uko tayari kuwasaidia kwa njia yoyote unayoweza. Waalike wahudhurie Ukumbusho. Ikiwa watahudhuria wakaribishe kwa uchangamfu. Baada ya Ukumbusho, endelea kuwatembelea au kuwapigia simu ndugu na dada hao wapendwa, na kuwapa msaada wowote wa kiroho wanaohitaji ili wamrudie Yehova.—1 Pet. 2:25.

18. Sisi sote tunaweza kuwasaidiaje wahubiri wasiotenda? (Waroma 12:10)

18 Ndugu na dada kutanikoni wanaweza kuwasaidia wahubiri wasiotenda wahudhurie Ukumbusho. Jinsi gani? Kwa kuwatendea kwa upendo, fadhili, na heshima. (Soma Waroma 12:10.) Kumbuka kwamba huenda kondoo hao wapendwa walisita kurudi kwenye mikutano. Labda waliogopa kwamba hawatakaribishwa vizuri. e Hivyo, epuka kuwauliza maswali yatakayowaaibisha au kusema jambo litakalowaumiza. (1 The. 5:11) Ndugu na dada hao ni waamini wenzetu. Tunafurahi kuabudu pamoja nao tena!—Zab. 119:176; Mdo. 20:35

19. Tunapata manufaa gani kwa kukumbuka kifo cha Yesu?

19 Tunashukuru sana kwamba Yesu alituambia tuadhimishe Ukumbusho wa kifo chake kila mwaka. Na tunaelewa kwa nini jambo hilo ni muhimu sana. Tunapohudhuria Ukumbusho tunajinufaisha wenyewe na wengine katika njia nyingi. (Isa. 48:17, 18) Upendo wetu kwa Yehova na Yesu unaongezeka. Tunaonyesha jinsi tunavyoshukuru kwa mambo yote ambayo wametufanyia. Tunaimarisha uhusiano wetu pamoja na ndugu na dada zetu. Na huenda tukawasaidia wengine wajifunze jinsi wanavyoweza kufurahia baraka tunazopata kwa sababu ya fidia. Hivyo, acheni tufanye yote tunayoweza ili kuwa tayari kwa ajili ya siku ya Ukumbusho wa mwaka huu—siku muhimu zaidi katika mwaka!

TUNAWEZAJE . . .

  • kuutayarisha moyo wetu kwa ajili ya Ukumbusho?

  • kuwasaidia wengine wanufaike na Ukumbusho?

  • kuwasaidia wahubiri wasiotenda?

WIMBO 18 Tunathamini Fidia

a Tumia sehemu ya tafuta kwenye jw.org ili kupata makala na video zilizorejelewa katika makala hii.

b Tazama makala ya “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Aprili 2021.

c Tazama kitabu Mkaribie Yehova, sura ya 23, fu. 8-9.

d Tazama sanduku lenye kichwa “ Habari Unazoweza Kufanyia Utafiti.”

e Tazama picha na sanduku lenye kichwa “ Kutaniko Lilitendaje?” Ndugu asiyetenda anasita kuingia katika Jumba la Ufalme, lakini anashinda hali hiyo. Anakaribishwa kwa uchangamfu na anafurahia kushirikiana na ndugu na dada.

f MAELEZO YA PICHA: Watu wa Yehova wanapoadhimisha Ukumbusho katika eneo moja la dunia, ndugu na dada zao katika maeneo mengine ya dunia wanajitayarisha kwa ajili ya tukio hilo la pekee.