Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unawatendea Wanawake Kama Yehova Anavyowatendea?

Je, Unawatendea Wanawake Kama Yehova Anavyowatendea?

TUNA pendeleo la kutumikia pamoja na wanawake wengi waaminifu. Na tunampenda na kumthamini kila mmoja wa dada hao washikamanifu na wenye bidii! a Hivyo, akina ndugu, jitahidini kuwatendea kwa fadhili, haki, na heshima. Lakini kwa sababu sisi si wakamilifu, huenda nyakati nyingine tukashindwa kufanya hivyo. Baadhi ya akina ndugu huenda wakakabili changamoto nyingine.

Baadhi ya watu wamelelewa katika utamaduni ambao wanaume wengi wanawaona wanawake kuwa duni. Kwa mfano, Hans, mwangalizi wa mzunguko nchini Bolivia, anasema kwamba baadhi ya wanaume wamelelewa katika utamaduni unaowachochea wanaume watende kwa kiburi sana. Wanaume hao wanaamini kwamba wao ni bora kuliko wanawake na mara nyingi wanawatendea kwa njia isiyo ya heshima. Shengxian, mzee wa kutaniko anayeishi Taiwan, anasema hivi: “Mahali ninapoishi wanaume wanahisi kwamba mwanamke hapaswi kuwaeleza wanaume maoni yake au kuingilia mambo yao. Ikiwa mwanamume atataja maoni ya mwanamke kuhusu jambo fulani, wanaume wenzake wanaweza kumdharau.” Wanaume wengine wanaonyesha ubaguzi wao kupitia njia zisizo wazi. Kwa mfano, wanaweza kusema jambo fulani la utani linalowashushia heshima wanawake.

Tunashukuru kwamba hata ikiwa mwanamume amelelewa katika utamaduni gani, anaweza kubadilika. Anaweza kushinda hisia za kwamba wanaume ni bora kuliko wanawake. (Efe. 4:22-24) Hilo linawezekana ikiwa ataiga mfano wa Yehova. Katika makala hii, tutajifunza jinsi Yehova anavyowatendea wanawake, jinsi akina ndugu wanavyoweza kujifunza kuwatendea wanawake kama Yehova anavyowatendea, na jinsi wazee wanavyoweza kuongoza katika kuwaonyesha heshima akina dada.

YEHOVA ANAWATENDEAJE WANAWAKE?

Yehova ametuwekea kielelezo bora cha jinsi ya kuwatendea wanawake. Akiwa Baba mwenye huruma, anaipenda familia yake. (Yoh. 3:16) Na akina dada waaminifu ni kama mabinti wenye thamani machoni pake. Chunguza njia zifuatazo ambazo Yehova anawaonyesha heshima wanawake.

Anawatendea bila ubaguzi. Yehova aliwaumba wanaume na wanawake kwa mfano wake. (Mwa. 1:27) Hakuwaumba wanaume wakiwa na akili zaidi au uwezo zaidi kuliko wanawake; wala hawaoni wanaume kuwa bora kuliko wanawake. (2 Nya. 19:7) Aliwaumba wanaume na wanawake wakiwa na uwezo unaofanana wa kiakili wa kuelewa kweli za Biblia na kuiga sifa nzuri za Mungu. Pia, Yehova anaona imani ya wanaume na wanawake kuwa sawa​—iwe wana tumaini la kuishi milele katika paradiso duniani au kutumikia wakiwa wafalme na makuhani mbinguni. (2 Pet. 1:1, maelezo ya chini) Ni wazi kwamba Yehova hawabagui wanawake.

Anawasikiliza. Yehova anajali kuhusu jinsi wanawake wanavyohisi na matatizo wanayokabili. Kwa mfano, alisikiliza na kujibu sala za Raheli na Hana. (Mwa. 30:22; 1 Sam. 1:10, 11, 19, 20) Pia, Yehova aliwaongoza waandikaji wa Biblia watie ndani masimulizi ya wanaume waliowasikiliza wanawake. Kwa mfano, Abrahamu alifuata maagizo ya Yehova kwamba amsikilize mke wake, Sara. (Mwa. 21:12-​14) Mfalme Daudi alimsikiliza Abigaili. Kwa kweli, alihisi kwamba Yehova alikuwa amemtuma Abigaili azungumze naye. (1 Sam. 25:32-​35) Yesu, aliyeiga sifa za Baba yake kikamilifu, alimsikiliza Maria, mama yake. (Yoh. 2:3-​10) Mifano hiyo inakazia kwamba njia moja ambayo Yehova anatumia kuwaonyesha heshima wanawake ni kwa kuwasikiliza.

Anawaamini. Kwa mfano, Yehova alimwamini Hawa kwa kumpa mgawo wa kusaidia kuitunza dunia nzima. (Mwa. 1:28) Kwa kufanya hivyo, hakumwona Hawa kuwa duni kwa mume wake, Adamu, bali msaidizi wake. Pia, Yehova aliwaamini manabii wa kike Debora na Hulda kwa kuwapa mgawo wa kuwashauri watu wake, kutia ndani mwamuzi na mfalme. (Amu. 4:4-9; 2 Fal. 22:14-​20) Leo, Yehova amewapa wanawake migawo mbalimbali ya kutimiza kwenye utumishi wake. Akina dada hao waaminifu wanatumikia wakiwa wahubiri, mapainia, na wamishonari. Wanasaidia katika kazi ya usanifu-majengo, ujenzi, na udumishaji wa Majumba ya Ufalme na majengo ya ofisi za tawi. Baadhi yao wanatumikia Betheli; wengine wanatumikia kwenye ofisi za utafsiri. Akina dada hao ni kama jeshi kubwa ambalo Yehova analitumia kutimiza mapenzi yake. (Zab. 68:11) Ni wazi kwamba Yehova hawaoni wanawake kuwa dhaifu au wasio na uwezo.

AKINA NDUGU WANAWEZA KUJIFUNZAJE KUWATENDEA WANAWAKE KAMA YEHOVA ANAVYOWATENDEA?

Akina ndugu, ili kujua ikiwa tunawatendea akina dada Wakristo kama Yehova anavyowatendea, tunahitaji kuchunguza kwa unyoofu mawazo na matendo yetu. Ili kufanya hivyo tunahitaji msaada. Kama mashine ya eksirei inavyoweza kutambua ugonjwa fulani kwenye moyo halisi, ndivyo ambavyo rafiki wa karibu na Neno la Mungu linavyoweza kutusaidia kutambua ikiwa tuna hisia zisizofaa kuhusu wanawake ambazo huenda zimekita mizizi ndani ya moyo wetu. Tunaweza kufanya nini ili tupate msaada huo?

Muulize rafiki wa karibu. (Met. 18:17) Ni vema kumfuata rafiki tunayemwamini ambaye anajulikana kuwa mwenye fadhili na usawaziko na kumuuliza maswali kama vile: “Ninawatendeaje akina dada? Je, wanahisi kwamba ninawaheshimu? Je, kuna jambo lolote ninaloweza kufanya ili niwatendee kwa njia nzuri zaidi? ” Ikiwa rafiki yako atataja baadhi ya mambo ambayo unahitaji kuboresha, epuka kujitetea. Badala yake, uwe tayari kufanya mabadiliko yanayohitajika.

Jifunze Neno la Mungu. Njia bora ya kutambua ikiwa tunawatendea akina dada kwa njia nzuri ni kwa kuchunguza mtazamo wetu na matendo yetu kwa kutumia Neno la Mungu. (Ebr. 4:12) Tunapochunguza Biblia, tunajifunza kuhusu wanaume waliowatendea vizuri wanawake na wanaume ambao hawakuwatendea vizuri. Kisha tunaweza kulinganisha mifano hiyo na jinsi sisi tunavyowatendea wanawake. Pia, kulinganisha mistari ya Biblia kunaweza kutusaidia kuepuka kutumia vibaya maandiko bila kujua, ili yaunge mkono maoni yetu yasiyo sahihi kuhusu wanawake. Kwa mfano, kulingana na 1 Petro 3:7, mke anapaswa kupewa “heshima kama chombo dhaifu zaidi.” b Je, hilo linamaanisha kwamba yeye ni duni, yaani, hana akili nyingi au uwezo kama mwanamume? La hasha! Linganisha maneno ya Petro na andiko la Wagalatia 3:26-​29 linaloonyesha kwamba Yehova amewachagua wanawake na pia wanaume watawale pamoja na Yesu mbinguni. Tunapojifunza Neno la Mungu na kumuuliza rafiki wa karibu kuhusu jinsi tunavyowatendea wanawake, tunaweza kujifunza kuwaonyesha heshima inayofaa dada zetu Wakristo.

WAZEE WA KUTANIKO WANAWAONYESHAJE HESHIMA AKINA DADA?

Akina ndugu kutanikoni wanaweza pia kujifunza jinsi ya kuwatendea kwa heshima akina dada, kwa kufuata mfano mzuri wa wazee wa kutaniko wenye upendo. Wazee wa kutaniko wanawezaje kuongoza katika kuwaonyesha heshima akina dada? Fikiria baadhi ya njia zifuatazo.

Wanawapongeza akina dada. Mtume Paulo amewawekea wazee wa kutaniko mfano mzuri wa kuiga. Aliwapongeza hadharani dada kadhaa katika barua aliyoandikia kutaniko la Roma. (Rom. 16:12) Je, unaweza kuwazia shangwe ambayo dada hao walihisi waliposikia barua ya Paulo ikisomwa kutanikoni? Vivyo hivyo, wazee wa kutaniko huwapongeza sana akina dada kwa sababu ya sifa zao nzuri na kwa ajili ya kazi wanayofanya kwa Yehova. Jambo hilo huwafanya akina dada watambue jinsi wanavyothaminiwa na kuheshimiwa sana. Maneno yenye kutia moyo ya mzee wa kutaniko ndiyo ambayo huenda dada hao wanahitaji ili waendelee kumtumikia Yehova kwa uaminifu.​—Met. 15:23.

Wapongeze

Wanapowapongeza akina dada, wazee wa kutaniko hutoa maelezo yao kwa unyoofu na kihususa. Kwa nini? Dada anayeitwa Jessica anasema hivi: “Inapendeza kusikia ndugu akimwambia dada ‘umefanya kazi nzuri.’ Lakini tunatiwa moyo zaidi akina ndugu wanapotupongeza kwa jambo fulani hususa, kama vile kuwafundisha watoto wetu kukaa kimya wakati wa mikutano au kwenda kumchukua mwanafunzi wa Biblia na kumleta mkutanoni.” Wazee wanapowapongeza akina dada kwa jambo fulani hususa, wanawafanya wahisi wanahitajika na ni wenye thamani kutanikoni.

Wanawasikiliza akina dada. Wazee wanyenyekevu wanatambua kwamba si wao tu ndio wenye maoni mazuri. Wazee hao wanawaomba akina dada watoe maoni yao na wanawasikiliza kwa makini wanapozungumza. Kwa kufanya hivyo, wazee hao wanawatia moyo akina dada na wanajinufaisha wao wenyewe. Jinsi gani? Mzee wa kutaniko anayeitwa Gerardo, ambaye anatumikia Betheli, anasema hivi: “Nimejionea kwamba kuwauliza akina dada maoni yao hunisaidia kufanya kazi yangu iwe bora zaidi. Mara nyingi, wamefanya kazi hiyo kwa muda mrefu zaidi kuliko akina ndugu wengi.” Katika kutaniko, akina dada wengi wanatumikia wakiwa mapainia, hivyo wanawajua vizuri watu katika eneo lao. Mzee wa kutaniko anayeitwa Bryan anasema hivi: “Akina dada wana sifa nyingi nzuri na ujuzi ambao tengenezo linahitaji. Hivyo, nufaika na uzoefu wao! ”

Wasikilize

Wazee wenye hekima hawapuuzi maoni ya akina dada. Kwa nini? Mzee wa kutaniko anayeitwa Edward, anasema hivi: “Maoni na uzoefu wa akina dada unaweza kumsaidia ndugu aone jambo kwa njia pana zaidi na hilo litamsaidia aelewe vizuri hisia za wengine.” (Met. 1:5) Hata ikiwa mzee hatatumia pendekezo la dada, bado anaweza kumshukuru kwa maoni na utambuzi wake.

Wanawazoeza akina dada. Wazee wenye utambuzi hutafuta fursa za kuwazoeza akina dada. Kwa mfano, wanaweza kuwafundisha akina dada jinsi ya kuongoza mikutano ya utumishi wa shambani ili wawe tayari kuiongoza akina ndugu waliobatizwa wasipokuwepo. Wanaweza kuwazoeza kutumia vifaa na mashine ili waweze kusaidia kwenye miradi ya udumishaji na ujenzi. Waangalizi walio Betheli wamewazoeza akina dada kushughulikia migawo mbalimbali kutia ndani, udumishaji, ununuzi, hesabu, kutayarisha programu za kompyuta, na kadhalika. Wazee wanapowazoeza akina dada, wanaonyesha kwamba wanawaona akina dada kuwa wenye uwezo na wanategemeka.

Wazoeze

Akina dada wengi hutumia mazoezi waliyopata kutoka kwa wazee wa kutaniko ili kuwanufaisha wengine. Kwa mfano, baadhi ya akina dada hutumia mazoezi waliyopata ya ujenzi kuwasaidia wengine kujenga nyumba zao upya janga la asili linapotokea. Akina dada wengine hutumia mbinu walizofundishwa za mahubiri ya hadharani kuwazoeza dada wengi zaidi kufanya aina hiyo ya utumishi. Akina dada wanahisije kuhusu wazee waliowazoeza? Dada anayeitwa Jennifer, anasema hivi: “Niliposhiriki kwenye mradi wa ujenzi wa Jumba la Ufalme, mwangalizi wa ujenzi alitenga wakati ili kunizoeza. Alitambua kazi niliyofanya na alinipongeza. Nilifurahia kufanya kazi pamoja naye kwa sababu nilihisi ninathaminiwa na kuaminiwa.”

MANUFAA YA KUWATENDEA AKINA DADA KAMA WATU WA FAMILIA YETU

Tunawapenda dada zetu waaminifu kama Yehova anavyowapenda! Hivyo tunawatendea kama watu wa familia yetu. (1 Tim. 5:1, 2) Tunawathamini na tunajivunia kufanya kazi pamoja nao. Na tunafurahi sana wanapojua kwamba tunawapenda na kuwaunga mkono. Dada anayeitwa Vanessa, anasema hivi: “Ninamshukuru sana Yehova kwa kuwa sehemu ya tengenezo hili ambalo lina akina ndugu wengi ambao wamenitia moyo sana.” Dada anayeishi Taiwan anasema hivi: “Ninamshukuru sana Yehova na tengenezo lake kwa kuwathamini wanawake na kuheshimu hisia zao. Hilo huimarisha imani yangu na kunifanya nithamini hata zaidi pendeleo nililo nalo la kuwa sehemu ya tengenezo la Yehova.”

Yehova anafurahi sana anapowaona wanaume Wakristo waaminifu wanapojitahidi kuwaona na kuwatendea wanawake waaminifu kama anavyofanya! (Met. 27:11) Mzee wa kutaniko anayeishi Scotland, anayeitwa Benjamin anasema hivi: “Maoni ya ulimwengu kuhusu wanawake yanaweza kuwashushia heshima sana. Hivyo, wanawake wanapokuja kwenye Jumba la Ufalme tunataka wahisi wanaheshimiwa na kupendwa.” Acheni sisi sote tufanye yote tunayoweza kumwiga Yehova kwa kuwatendea dada zetu wapendwa kwa upendo na heshima wanayostahili.​—Rom. 12:10.

a Katika makala hii, neno “dada” linapotumiwa, linarejelea akina dada Wakristo, si mtu wa familia.

b Ili kupata habari zaidi kuhusu msemo “chombo dhaifu zaidi,” tazama makala yenye kichwa “Thamani ya ‘Chombo Dhaifu Zaidi’” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 2006, na “Mwongozo Wenye Hekima kwa Wenzi wa Ndoa” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 2005.