MAKALA YA 6

WIMBO 10 Msifuni Yehova Mungu Wetu!

“Lisifuni Jina la Yehova”

“Lisifuni Jina la Yehova”

“Msifuni, enyi watumishi wa Yehova, lisifuni jina la Yehova.”ZAB. 113:1.

JAMBO KUU

Kukazia mambo yanayotuchochea kulisifu jina takatifu la Yehova kila tunapopata fursa.

1-2. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuelewa jinsi Yehova anavyohisi kuhusu jina lake kuchongewa?

 WAZIA jambo hili: Mtu unayempenda anasema jambo fulani baya kukuhusu. Unajua kwamba jambo alilosema ni uwongo, lakini baadhi ya watu wanamwamini. Jambo baya hata zaidi, wanaanza kuwaambia wengine uwongo huo, na wengine wengi wanaamini jambo hilo. Ungehisije? Ikiwa unawajali watu na sifa yako nzuri, uchongezi huo utakufanya ujihisi vibaya, sivyo?—Met. 22:1.

2 Mfano huo unaweza kutusaidia kuelewa jinsi Yehova alivyohisi sifa yake nzuri ilipochafuliwa. Mmoja kati ya wana wake wa kiroho alimweleza mwanamke wa kwanza, Hawa, uwongo kumhusu. Naye Hawa aliamini uwongo huo. Kwa sababu ya uwongo huo, wazazi wetu wa kwanza walimwasi Yehova. Matokeo ni kwamba dhambi na kifo vikaenea katika familia ya wanadamu. (Mwa. 3:​1-6; Rom. 5:12) Matatizo yote tunayoona ulimwenguni leo—vifo, vita, huzuni—yametokana na uwongo ambao Shetani alianza kueneza katika bustani ya Edeni. Je, Yehova anaumia kwa sababu ya uchongezi huo na matokeo yake mabaya? Bila shaka. Hata hivyo, Yehova hana kinyongo. Isitoshe, anaendelea kuwa “Mungu mwenye furaha.”—1 Tim. 1:11.

3. Tuna pendeleo gani?

3 Tuna pendeleo la kusaidia kulitetea jina la Yehova kwa kutii amri hii rahisi: “Lisifuni jina la Yehova.” (Zab. 113:1) Tunafanya hivyo kwa kuwaambia wengine mambo mazuri kumhusu Yule anayeitwa kwa jina hilo takatifu. Je, wewe utafanya hivyo? Acheni tuchunguze mambo matatu muhimu yatakayotuchochea kulisifu jina la Mungu wetu kwa moyo wote.

TUNAMFURAHISHA YEHOVA TUNAPOLISIFU JINA LAKE

4. Kwa nini Yehova anafurahi tunapomsifu? Toa mfano. (Tazama pia picha.)

4 Tunamfurahisha Baba yetu wa mbinguni tunapolisifu jina lake. (Zab. 119:108) Je, hilo linamaanisha kwamba Mungu Mweza-Yote ni kama wanadamu wanaotamani kusifiwa kwa sababu hawajiamini na wanahitaji kuhakikishiwa wanathaminiwa? Hapana. Fikiria mfano huu. Msichana mdogo anamkumbatia baba yake kwa upendo na kumwambia, “Wewe ni baba mzuri zaidi katika ulimwengu wote!” Baba yake anafurahi na kuguswa moyo na maneno hayo ya kutoka moyoni. Kwa nini? Je, ni kwa sababu yeye ni mtu asiyejiamini na anayetamani sana au hata kutegemea sifa kutoka kwa mtoto wake? Hapana. Ni kwa sababu anampenda binti yake na anafurahi sana kuona akimwonyesha upendo na kumthamini. Anajua kwamba sifa hizo zitamsaidia binti yake kuwa na furaha anapoendelea kukua. Kwa sababu hizohizo, Yehova, Baba aliye bora zaidi, anafurahi tunapomsifu.

Kama tu baba wa kibinadamu anavyofurahi mtoto wake anapomwonyesha anampenda na kumthamini, ndivyo Yehova anavyofurahi tunapolisifu jina lake (Tazama fungu la 4)


5. Tunaweza kusaidia kupinga uwongo gani kwa kulisifu jina la Mungu?

5 Tunapomsifu Baba yetu wa mbinguni, tunasaidia kupinga uwongo unaotuhusu kibinafsi. Shetani anadai kwamba hakuna mwanadamu atakayelitetea jina la Mungu kwa ushikamanifu. Anadai kuwa hakuna yeyote kati yetu aliye mtimilifu. Anasema kwamba sisi sote tutaacha kumtumikia Mungu ikiwa tunahisi kuwa tutanufaika kwa kufanya hivyo. (Ayu. 1:​9-11; 2:4) Lakini Ayubu aliyekuwa mwaminifu alithibitisha kwamba Shetani ni mwongo. Namna gani wewe? Kila mmoja wetu ana pendeleo la kutetea kwa ushikamanifu jina la Baba yetu na kumfurahisha kwa kumtumikia kwa utimilifu. (Met. 27:11) Kwa kweli, ni pendeleo kubwa sana kufanya hivyo.

6. Tunawezaje kumwiga Mfalme Daudi na Walawi? (Nehemia 9:5)

6 Kwa kuwa wanampenda Mungu, watu waaminifu wanachochewa kulisifu jina lake kwa moyo wote. Mfalme Daudi aliandika hivi: “Nafsi yangu na imsifu Yehova; kila kitu kilicho ndani yangu na kilisifu jina lake takatifu.” (Zab. 103:1) Daudi alielewa kwamba kulisifu jina la Yehova ni sawa na kumsifu Yehova mwenyewe. Jina la Yehova linahusisha sifa yake nzuri, hivyo linatukumbusha sifa zake zote maridadi na matendo yake yenye kustaajabisha. Daudi aliliona jina la Baba yake kuwa takatifu na alitamani kulisifu. Alitaka kufanya hivyo na “kila kitu kilicho ndani” yake—yaani, kwa moyo wote. Vivyo hivyo, Walawi waliongoza katika kumsifu Yehova. Kwa unyenyekevu, walikubali kwamba maneno yao hayangeweza kamwe kueleza kikamili sifa ambayo jina hilo takatifu linastahili. (Soma Nehemia 9:5.) Hapana shaka kwamba sifa hizo za kutoka moyoni zilimletea shangwe Yehova.

7. Tunawezaje kumsifu Yehova katika huduma na maisha yetu ya kila siku?

7 Leo, tunaweza kumfurahisha Yehova kwa kuzungumza kumhusu kwa njia inayoonyesha kwamba tunamthamini na tunampenda sana. Tunapokuwa katika huduma, tunakumbuka kwamba lengo letu kuu ni kuwasaidia watu wamkaribie Yehova, na wahisi kama sisi tunavyohisi kumhusu Baba yetu mwenye upendo. (Yak. 4:8) Tunafurahi sana kuwaonyesha watu jinsi Biblia inavyomfafanua Yehova, inavyofunua upendo wake, haki, hekima, na sifa zake nyingine zenye kuvutia. Pia, tunamsifu Yehova na kumfurahisha kwa kujitahidi kumwiga. (Efe. 5:1) Tunapofanya hivyo, tunakuwa tofauti kabisa na watu katika ulimwengu huu mwovu. Huenda watu wakatambua kwamba tuko tofauti na kujiuliza kwa nini. (Mt. 5:​14-16) Tunaposhughulika nao katika maisha ya kila siku, huenda tukapata fursa ya kuwaeleza kwa nini tunatenda kwa njia tofauti. Matokeo ni kwamba watu wanyoofu wanatamani kumkaribia Mungu wetu. Tunapomsifu Yehova kwa njia hizo, tunaufurahisha moyo wake.—1 Tim. 2:​3, 4.

TUNAMFURAHISHA YESU TUNAPOLISIFU JINA LA YEHOVA

8. Yesu ametuonyeshaje mfano bora wa kulisifu jina la Yehova?

8 Hakuna kiumbe yeyote mbinguni au duniani anayemjua Baba vizuri zaidi kuliko Mwana wake. (Mt. 11:27) Yesu anampenda Baba yake, na anaongoza katika kulisifu jina la Yehova. (Yoh. 14:31) Katika sala aliyotoa kwa Baba yake usiku kabla ya kifo chake, Yesu alitaja jambo muhimu zaidi alilotimiza katika huduma yake duniani. Alisema hivi: “Nimewajulisha jina lako.” (Yoh. 17:26) Alimaanisha nini?

9. Yesu alitumiaje mfano kueleza sifa za Baba yake kwa njia iliyo wazi kabisa?

9 Yesu alifanya mengi zaidi ya kuwaambia tu watu kwamba jina la Mungu ni Yehova. Wayahudi ambao Yesu aliwafundisha tayari walilijua jina la Mungu. Lakini Yesu ndiye aliyekuwa mstari wa mbele akiwa yule ‘aliyeeleza kumhusu.’ (Yoh. 1:​17, 18) Kwa mfano, Maandiko ya Kiebrania yanafunua kwamba Yehova ni mwenye rehema na huruma. (Kut. 34:​5-7) Yesu alifafanua kweli hiyo hata zaidi aliposimulia kuhusu mfano wa mwana mpotevu na baba yake. Tunaposoma kuhusu jinsi baba huyo anavyomwona mwana wake aliyetubu “akiwa mbali,” anavyokimbia ili kukutana naye, anavyomkumbatia, na kumsamehe kutoka moyoni, tunapata picha kamili zaidi ya rehema na huruma ya Yehova. (Luka 15:​11-32) Yesu aliwasaidia wengine waelewe vizuri kabisa utu wa Baba yake.

10. (a) Tunajuaje kwamba Yesu alilitumia jina la kibinafsi la Baba yake na alitaka wengine wafanye hivyo pia? (Marko 5:19) (Tazama pia picha.) (b) Yesu anataka tufanye nini leo?

10 Je, Yesu alitaka wengine pia watumie jina la kibinafsi la Baba yake? Bila shaka. Huenda baadhi ya viongozi wa dini wa siku za Yesu waliamini kwamba jina la Mungu lilikuwa takatifu sana hivi kwamba halikupaswa kutamkwa, lakini Yesu hakuruhusu desturi hizo zisizo za kimaandiko zimzuie kuliheshimu jina la Baba yake. Fikiria wakati ambapo Yesu alimponya mwanamume mwenye roho waovu katika eneo la Wagerasene. Watu katika eneo hilo waliogopa na kumsihi Yesu aondoke, hivyo hakubaki katika eneo hilo. (Marko 5:​16, 17) Lakini bado Yesu alitaka jina la Yehova lijulikane huko. Hivyo, alimwambia mwanamume aliyemponya awaambie watu mambo ambayo Yehova alikuwa amefanya, si mambo ambayo Yesu alikuwa amefanya. (Soma Marko 5:19.) a Leo pia, anataka tufanye vivyo hivyo, yaani, tuwajulishe watu ulimwenguni pote kuhusu jina la Baba yake! (Mt. 24:14; 28:​19, 20) Tunapofanya sehemu yetu, tunamfurahisha Mfalme wetu, Yesu.

Yesu alimwambia mwanamume ambaye awali alikuwa na roho waovu awaambie watu kuhusu jinsi Yehova alivyomsaidia (Tazama fungu la 10)


11. Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali kuhusu nini, na kwa nini hilo ni muhimu? (Ezekieli 36:23)

11 Yesu alijua kwamba kusudi la Yehova ni kulitakasa jina Lake, na kuliondolea shutuma zote. Hiyo ndiyo sababu Bwana wetu aliwafundisha wafuasi wake wasali hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.” (Mt. 6:9) Yesu alielewa kwamba hilo ndilo suala kuu zaidi linalokabili uumbaji wote. (Soma Ezekieli 36:23.) Hakuna kiumbe yeyote mbinguni au duniani ambaye amefanya mengi zaidi ya Yesu ili kulitakasa jina la Yehova. Hata hivyo, Yesu alipokamatwa, maadui wake walimshtaki kwa kosa gani? Kukufuru! Bila shaka, Yesu aliona kuwa kulitumia vibaya au kulichongea jina takatifu la Baba yake kuwa dhambi mbaya sana. Alihangaishwa sana kujua kwamba angeshtakiwa na kuhukumiwa kwa kosa hilo. Huenda hiyo ndiyo ilikuwa sababu kuu kwa nini Yesu “alikuwa na maumivu makali” saa chache kabla ya kukamatwa.—Luka 22:​41-44.

12. Yesu alitakasaje jina la Baba yake kwa njia kubwa zaidi?

12 Ili kulitakasa jina la Baba yake, Yesu alivumilia mateso, matukano, na uchongezi wa kila aina. Alijua kwamba alikuwa amemtii Baba yake katika mambo yote; hakuwa na sababu yoyote ya kuaibika. (Ebr. 12:2) Pia, alijua kwamba Shetani alikuwa akimshambulia moja kwa moja katika kipindi hicho kigumu. (Luka 22:​2-4; 23:​33, 34) Bila shaka Shetani alitamani sana kuvunja utimilifu wa Yesu; hata hivyo, Shetani alishindwa kabisa! Yesu alithibitisha kabisa kwamba Shetani ni mwongo mbaya sana na kwamba Yehova ana watumishi washikamanifu, ambao wanadumisha utimilifu wao hata chini ya majaribu makali zaidi!

13. Unaweza kumfurahishaje Mfalme wako anayetawala?

13 Je, unataka kumfurahisha Mfalme wako anayetawala? Endelea kulisifu jina la Yehova, na kuwasaidia wengine waujue vizuri kabisa utu wa Mungu. Kwa kufanya hivyo, utakuwa unafuata hatua za Yesu. (1 Pet. 2:21) Kama Yesu, utamfanya Yehova ashangilie na kuthibitisha kwamba adui Yake, Shetani, ni mwongo mwovu sana!

TUNASAIDIA KUOKOA UHAI WA WATU TUNAPOLISIFU JINA LA YEHOVA

14-15. Huenda mambo gani mazuri yakatokea tunapowafundisha watu kumhusu Yehova?

14 Tunapolisifu jina la Yehova, tunasaidia kuokoa uhai wa watu. Jinsi gani? Shetani “amezipofusha akili za wasioamini.” (2 Kor. 4:4) Matokeo ni kwamba wanaamini uwongo wa Shetani kama vile: hakuna Mungu, Mungu yuko mbali sana na sisi na hajali kuhusu wanadamu, Mungu ni mkatili na anawatesa watenda dhambi milele. Uwongo wa aina hiyo unalificha au kulichafua jina la Yehova na sifa yake, ili watu wasitamani kumkaribia. Lakini kazi yetu inamzuia Shetani kutimiza kusudi lake. Tunawafundisha watu ukweli kumhusu Baba yetu, na kulisifu jina takatifu la Mungu wetu. Matokeo ni nini?

15 Kweli za Neno la Mungu zina nguvu nyingi. Tunapowafundisha watu kuhusu Yehova na kuwasaidia waujue kabisa utu wa Yehova, tunajionea jambo zuri sana. Hatua kwa hatua watu hawadanganywi tena na uwongo wa Shetani, wanaanza kumwona Baba yetu mpendwa kama sisi tunavyomwona. Wanastaajabishwa sana na nguvu zake zisizo na kifani. (Isa. 40:26) Wanajifunza kumtumaini kwa sababu ya haki yake kamilifu. (Kum. 32:4) Wanaelimishwa na hekima yake nyingi. (Isa. 55:9; Rom. 11:33) Na wanafarijika kujua kwamba sifa yake kuu ni upendo. (1 Yoh. 4:8) Kadiri wanavyomkaribia Yehova zaidi, tumaini lao la kuishi milele wakiwa watoto wake linakuwa la hakika zaidi. Ni pendeleo lililoje kuwasaidia watu wamkaribie Baba yao! Tunapofanya hivyo, Yehova anatuona kuwa “wafanyakazi wenzi.”—1 Kor. 3:​5, 9.

16. Baadhi ya watu walichochewaje walipojifunza kuhusu jina la Mungu? Toa mifano.

16 Huenda mwanzoni, tukawafundisha tu watu kwamba jina la Mungu ni Yehova. Jambo hilo pekee linaweza kubadili maisha ya mtu mwenye moyo mnyoofu. Kwa mfano, mwanamke kijana anayeitwa Aaliyah b alilelewa katika dini ambayo mafundisho yake hayatoki katika Biblia. Lakini hakuridhika na dini yake na hakuhisi akiwa karibu na Mungu. Hali hiyo ilibadilika alipoanza kujifunza na Mashahidi. Alianza kumwona Mungu kuwa Rafiki yake. Na alishangaa kuona kwamba jina la Mungu limeondolewa kutoka katika Biblia nyingi na badala yake majina ya cheo, kama vile Bwana yalitumiwa. Kujifunza kuhusu jina la Mungu kulibadili maisha yake kabisa. Alisema hivi kwa msisimko: “Rafiki yangu mpendwa zaidi ana jina!” Matokeo yalikuwaje? Anasema hivi: “Sasa nina amani nyingi sana moyoni. Ninahisi nimebarikiwa sana.” Mwanamume anayeitwa Steve alikuwa mwanamuziki, na alilelewa katika familia ya Kiyahudi iliyoshikilia sana imani yao. Alikataa kuwa sehemu ya shirika la kidini kwa sababu alikuwa amejionea unafiki mwingi. Hata hivyo, baada ya kifo cha mama yake, alikubali kusikiliza wakati funzo la Biblia lilipokuwa likiongozwa na Mashahidi wa Yehova. Aliguswa moyo sana alipojifunza jina la Mungu. Anasema hivi: “Sikuwahi kujua jina la Mungu.” Anaendelea kusema hivi: “Kwa mara ya kwanza, nilielewa kwamba Mungu ni Mtu halisi! Hapo ndipo nilipotambua kwamba nimepata Rafiki.”

17. Kwa nini umeazimia kuendelea kulisifu jina la Yehova? (Tazama pia picha.)

17 Je, unawaeleza wengine kuhusu jina takatifu la Yehova unapohubiri na kufundisha? Je, unawasaidia kuona jinsi Mungu wetu alivyo? Unapofanya hivyo, unalisifu jina la Mungu. Na uendelee kulisifu jina takatifu la Yehova kwa kuwasaidia watu wamjue Yule anayeitwa kwa jina hilo. Kwa kufanya hivyo, utaokoa uhai wa watu. Utakuwa ukifuata mwongozo wa Mfalme wako, Kristo Yesu. Zaidi ya yote, utamfurahisha Baba yako mpendwa, Yehova. Na ‘ulisifu jina lake milele na milele’!—Zab. 145:2.

Tunalisifu jina la Yehova kwa kuwafundisha watu kulihusu na kuwaonyesha jinsi utu wa Yehova ulivyo (Tazama fungu la 17)

KULISIFU JINA LA MUNGU . . .

  • kunamfurahishaje Yehova?

  • kunamfurahishaje Kristo Yesu?

  • kunaokoaje uhai wa watu?

WIMBO 2 Jina Lako Ni Yehova

a Kuna sababu nzuri za kuamini kwamba Marko alitumia jina la Mungu aliponukuu maneno haya ya Yesu. Hivyo, jina hilo limerudishwa katika Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

b Majina yamebadilishwa.