Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uwe Mwenye Furaha Unapomngojea Yehova kwa Subira

Uwe Mwenye Furaha Unapomngojea Yehova kwa Subira

JE, UNATAZAMIA kwa hamu wakati ambapo Yehova ataondoa uovu wote na kufanya vitu vyote kuwa vipya? (Ufu. 21:​1-5) Bila shaka! Hata hivyo, si rahisi sikuzote kuendelea kumngojea Yehova kwa subira, hasa tunapokabili matatizo. Tumaini lililoahirishwa linaweza kuufanya moyo uwe mgonjwa.—Met. 13:​12, maelezo ya chini.

Ingawa hivyo, bado Yehova anatarajia tungoje kwa subira hadi wakati wake uliowekwa wa kutenda ufike. Kwa nini anatarajia tufanye hivyo? Ni mambo gani yatakayotusaidia tuwe wenye furaha tunapoendelea kungoja?

KWA NINI YEHOVA ANATARAJIA TUNGOJE?

Biblia inasema hivi: “Yehova anangoja kwa subira ili kuwaonyesha kibali, naye atainuka ili kuwaonyesha rehema. Kwa maana Yehova ni Mungu wa haki. Wenye furaha ni wote wanaoendelea kumtarajia.” (Isa. 30:18) Mwanzoni maneno hayo ya Isaya yalikusudiwa kwa ajili ya Wayahudi waliokuwa wakaidi. (Isa. 30:1) Lakini baadhi ya Wayahudi walikuwa waaminifu, na maneno hayo yaliwapa tumaini. Maneno hayo yanawapatia tumaini pia watumishi waaminifu wa Yehova leo.

Hivyo, ni lazima tungoje kwa subira kwa sababu Yehova anangoja kwa subira. Ana wakati uliowekwa ambapo atakomesha mfumo huu, na anangojea hadi siku na saa hiyo ifike. (Mt. 24:36) Wakati huo, itakuwa wazi kabisa kwamba mashtaka ya Ibilisi dhidi ya Yehova na wale wanaomtumikia ni ya uwongo. Kisha, Yehova atamwondoa Shetani na wote wanaomuunga mkono, lakini ‘atatuonyesha sisi rehema.’

Tunapoendelea kungoja, huenda Yehova asiondoe majaribu yetu, lakini anatuhakikishia kwamba tunaweza kuwa na furaha tunapomngojea. Kama Isaya alivyosema, tunaweza kuwa wenye furaha tunaposubiri kwa hamu au kutarajia jambo fulani zuri litukie. (Isa. 30:18) a Tunawezaje kuipata furaha hiyo? Mambo manne yanaweza kutusaidia.

JINSI YA KUWA WENYE FURAHA TUNAPONGOJA

Kazia fikira mambo mazuri. Mfalme Daudi alikuwa amejionea uovu mwingi maishani mwake. (Zab. 37:35) Hata hivyo, aliandika hivi: “Nyamaza mbele za Yehova na umngojee kwa matumaini. Usikasirishwe na mtu anayefanikiwa kutekeleza njama zake.” (Zab. 37:7) Daudi alitumia maishani mwake ushauri huo kwa kukazia fikira ahadi ya Yehova ya kumwokoa. Pia, alithamini kila baraka aliyopokea kutoka kwa Yehova. (Zab. 40:5) Ikiwa sisi pia tutakazia fikira mambo mazuri katika maisha yetu bila kulemewa na mambo mabaya yanayotuzunguka, itakuwa rahisi zaidi kumngojea Yehova.

Tumia kila fursa kumsifu Yehova. Mwandikaji wa Zaburi ya 71, ambaye inaelekea ni Daudi, alimwambia hivi Yehova: “Nitaendelea kungoja; nitakusifu hata zaidi.” (Zab. 71:14) Angemsifu Yehova jinsi gani? Kwa kuwaambia wengine kumhusu Yehova na kumwimbia sifa. (Zab. 71:​16, 23) Kama Daudi, tunaweza kuwa wenye furaha tunapomngojea Yehova. Tunamsifu kupitia huduma yetu, mazungumzo ya kila siku, na nyimbo zetu za ibada. Wakati mwingine utakapoimba wimbo wa Ufalme, kwa nini usikazie fikira ujumbe wenye kufariji wa wimbo huo?

Waruhusu ndugu na dada zako wakutie moyo. Alipokabili changamoto, Daudi alimwambia hivi Yehova: “Mbele ya washikamanifu wako, nitalitumaini jina lako.” (Zab. 52:9) Sisi pia tunaweza kutiwa moyo na waabudu wenzetu washikamanifu, tunapokuwa kwenye mikutano yetu na katika huduma, lakini pia wakati wa tafrija.—Rom. 1:​11, 12.

Imarisha tumaini lako. Zaburi 62:5 inasema: “Ninamngojea Mungu kimyakimya kwa sababu tumaini langu linatoka kwake.” Kuwa na tumaini lenye nguvu kunatia ndani kuwa na matarajio hakika—jambo ambalo ni muhimu sana ikiwa tutahitaji kuendelea kuvumilia katika mfumo huu kwa muda mrefu kuliko tulivyowazia. Ni lazima tusadiki kabisa kwamba ahadi za Yehova zitakuwa halisi haidhuru tutahitaji kuzingoja kwa muda mrefu kadiri gani. Tunaweza kuimarisha tumaini letu kwa kujifunza Neno la Mungu—upatano wake, unabii mbalimbali, na habari ambazo Yehova anafunua kujihusu. (Zab. 1:​2, 3) Pia, tunahitaji kuendelea ‘kusali tukiwa na roho takatifu’ ili tuendelee kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova wakati tukingojea atimize ahadi yake ya uzima wa milele.—Yuda 20, 21.

Kama Mfalme Daudi, uwe na hakika kwamba Yehova anawalinda wale wanaomngojea na anawaonyesha upendo Wake mshikamanifu. (Zab. 33:​18, 22) Endelea kumngoja Yehova kwa subira kwa kukazia fikira mambo mazuri maishani mwako, kumsifu, kuwaruhusu waabudu wenzako wakutie moyo, na kwa kuendelea kuimarisha tumaini lako lenye thamani.

a Neno la lugha ya awali lililotafsiriwa kuwa “wanaoendelea kumtarajia” pia linaweza kumaanisha “kutumaini au kutamani jambo fulani litukie,” hilo linaonyesha kwamba ni jambo la kawaida kutamani Yehova atukomboe.