Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Washiriki Wapya Wawili wa Baraza Linaloongoza

Washiriki Wapya Wawili wa Baraza Linaloongoza

SIKU ya Jumatano, Januari 18, 2023, tangazo la pekee liliwekwa kwenye jw.org, likieleza kwamba Ndugu Gage Fleegle na Jeffrey Winder walikuwa wamewekwa rasmi kutumikia wakiwa washiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Ndugu hao wametumikia kwa uaminifu katika utumishi wa Yehova kwa muda mrefu.

Gage Fleegle na Nadia, mke wake

Ndugu Fleegle alilelewa mashariki mwa jimbo la Pennsylvania, Marekani, na wazazi wake waliokuwa katika kweli. Alipokuwa tineja, familia yao ilihamia kwenye mji mdogo wa mashambani ambako kulikuwa na uhitaji mkubwa wa wahubiri. Alibatizwa muda mfupi baadaye, Novemba 20, 1988.

Sikuzote wazazi wa Ndugu Fleegle walimtia moyo awe mtumishi wa wakati wote. Mara nyingi waliwaalika nyumbani waangalizi wa mzunguko na Wanabetheli, na Ndugu Fleegle angeweza kuona jinsi ndugu na dada hao walivyo na furaha sana. Muda mfupi baada ya kubatizwa—Septemba 1, 1989—alianza kutumikia akiwa painia wa kawaida. Miaka miwili baadaye, alifikia lengo alilojiwekea alipokuwa na umri wa miaka 12—lengo la kuwa Mwanabetheli. Alianza kutumikia katika Betheli ya Brooklyn, mwezi wa Oktoba 1991.

Akiwa Betheli, Ndugu Fleegle alifanya kazi ya kujalidi vitabu kwa miaka minane, na baada ya hapo alipewa mgawo kwenye Idara ya Utumishi. Wakati huo, alitumikia katika kutaniko la lugha ya Kirusi kwa miaka michache. Mwaka wa 2006, alimwoa Nadia, mke wake, ambaye alijiunga naye katika utumishi wa Betheli. Pamoja, wametumikia katika makutaniko ya lugha ya Kireno na kwa zaidi ya miaka kumi katika makutaniko ya lugha ya Kihispania. Baada ya miaka mingi ya kutumikia katika Idara ya Utumishi, Ndugu Fleegle alipewa mgawo wa kufanya kazi katika Ofisi ya Halmashauri ya Ufundishaji na baadaye katika Ofisi ya Halmashauri ya Utumishi. Mwezi wa Machi 2022 aliwekwa rasmi kuwa msaidizi wa Halmashauri ya Utumishi ya Baraza Linaloongoza.

Jeffrey Winder na Angela, mke wake

Ndugu Winder alilelewa huko Murrieta, California, Marekani. Wazazi wake walimlea katika kweli, naye alibatizwa Machi 29, 1986. Mwezi uliofuata aliamua kuanza upainia msaidizi. Alifurahia sana upainia hivi kwamba alitamani kuendelea. Baada ya miezi kadhaa ya kufanya upainia msaidizi, alianza upainia wa kawaida Oktoba 1, 1986.

Akiwa tineja, Ndugu Winder aliwatembelea ndugu zake wawili wakubwa waliokuwa wakitumikia Betheli wakati huo. Matembezi hayo yalimchochea kujaza ombi la utumishi wa Betheli alipokuwa na umri mkubwa zaidi. Na mwezi wa Mei 1990, alialikwa kutumikia katika Betheli ya Wallkill.

Akiwa Betheli, Ndugu Winder amefanya kazi kwenye idara mbalimbali, kutia ndani Idara ya Usafi, Idara ya Kutunza Shamba, na Ofisi ya Betheli. Mwaka wa 1997, alimwoa Angela, mke wake, na wamekuwa wakitumikia Betheli pamoja tangu wakati huo. Mwaka wa 2014, walihamishiwa huko Warwick, ambako Ndugu Winder alisaidia katika ujenzi wa makao makuu ya ulimwenguni pote. Mwaka wa 2016, walihamia katika Kituo cha Elimu cha Watchtower huko Patterson, ambako Ndugu Winder alifanya kazi katika Idara ya Huduma za Sauti na Video. Miaka minne baadaye, walirudi tena Warwick, na Ndugu Winder alipewa mgawo wa kutumika katika Ofisi ya Halmashauri ya Wafanyakazi. Mwezi wa Machi 2022 aliwekwa rasmi kuwa msaidizi wa Halmashauri ya Wafanyakazi ya Baraza Linaloongoza.

Tunasali kwamba Yehova aendelee kuwabariki sana ‘wanaume hao walio zawadi’ wanapoendelea kufanya kazi kwa bidii kwa ajili ya masilahi ya Ufalme.—Efe. 4:8.