Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Biblia inafunua nini kuhusu uwezo wa Yehova wa kutabiri wakati ujao?

Biblia inaonyesha wazi kwamba Yehova anaweza kutabiri kuhusu wakati ujao. (Isa. 45:21) Biblia haitaji kila jambo kuhusu jinsi au wakati anaoamua kufanya hivyo au hata kiasi cha habari anachochagua kujua. Hivyo, hatujui kila jambo kuhusu uwezo wa Yehova wa kutabiri wakati ujao. Hata hivyo, fikiria mambo haya machache.

Uwezo wa Yehova hauna mipaka isipokuwa ile anayojiwekea mwenyewe. Kwa sababu ana hekima isiyo na kifani, anaweza kutabiri kuhusu chochote anachochagua. (Rom. 11:33) Kwa sababu anaonyesha sifa ya kujizuia kikamilifu, anaweza pia kuchagua kutojua mambo yatakayotukia wakati ujao.—Linganisha Isaya 42:14.

Yehova anasababisha mapenzi yake yatendeke. Jambo hilo linahusianaje na uwezo wake wa kutabiri wakati ujao? Isaya 46:10 inaeleza hivi: “Tangu mwanzo ninatabiri matokeo, na tangu zamani za kale mambo ambayo bado hayajafanywa. Ninasema, ‘Uamuzi wangu utasimama, nami nitafanya jambo lolote ninalopenda.’”

Hivyo, sababu moja ambayo inafanya Yehova aweze kutabiri wakati ujao ni kwamba ana nguvu za kusababisha mambo yatukie. Hapeleki wakati mbele ili kuona kitakachotukia wakati ujao kana kwamba matukio ya wakati ujao tayari yameshatukia, kisha Yehova anayatazama kimbele. Badala yake, Yehova anaweza kuamua kwamba jambo fulani litatukia kwa wakati fulani hususa, kisha asababishe jambo hilo litukie wakati huo ukifika.—Kut. 9:​5, 6; Mt. 24:36; Mdo. 17:31.

Kwa sababu hiyo, Biblia inatumia maneno kama vile “nimelitayarisha,” “nimelitengeneza,” na “nimekusudia” ili kufafanua kile ambacho Yehova anafanya inapohusu baadhi ya matukio ya wakati ujao. (2 Fal. 19:25; maelezo ya chini; Isa. 46:11) Maneno hayo yanatafsiriwa kutoka katika neno la lugha ya awali ambalo linahusiana na neno linalomaanisha “mfinyanzi.” (Yer. 18:4) Kama tu ambavyo mfinyanzi mwenye ustadi anaweza kutengeneza chombo maridadi kutokana na udongo wa mfinyanzi, ndivyo ambavyo Yehova anaweza kutengeneza au kuongoza mambo ili kutimiza mapenzi yake.—Efe. 1:11.

Yehova anaheshimu zawadi ya uhuru wa kuchagua. Hapangi kimbele mambo yatakayompata kila mtu; wala hasababishi watu wanyoofu wafanye mambo yatakayowaongoza kwenye uharibifu wao. Anaruhusu watu wote wachague njia watakayofuata, na anawahimiza wachague njia sahihi.

Fikiria mifano miwili. Mfano wa kwanza unawahusu wakaaji wa jiji la Ninawi. Yehova alitabiri kwamba jiji hilo lingeharibiwa kwa sababu ya uovu wao. Lakini wakaaji wa jiji hilo walipotubu, Yehova “akafikiria upya kuhusu msiba aliosema kwamba angewaletea, naye hakuuleta.” (Yona 3:​1-10) Yehova alibadili uamuzi wake kuhusu jambo alilotabiri kwa sababu Waninawi walitumia uhuru wao wa kuchagua na kutubu walipopata ujumbe wa onyo ambao Yehova alikuwa ametuma.

Mfano wa pili ni unabii kuhusu Koreshi aliyeshinda vita vingi, ambaye angewaweka huru Wayahudi kutoka utekwani na kuagiza hekalu la Yehova lijengwe upya. (Isa. 44:26–45:4) Mfalme Koreshi wa Uajemi alitimiza unabii huo. (Ezra 1:​1-4) Hata hivyo, Koreshi hakumwabudu Mungu wa kweli. Yehova alimtumia Koreshi kutimiza unabii huo bila kuingilia uhuru wake wa kuchagua yule ambaye angemwabudu.—Met. 21:1.

Bila shaka, hayo si mambo yote yanayohusika Yehova anapoamua kutumia uwezo wake wa kutabiri. Ukweli ni kwamba hakuna mwanadamu anayeweza kuelewa kikamili njia za Yehova. (Isa. 55:​8, 9) Hata hivyo, mambo ambayo Yehova amefunua yanaimarisha imani yetu kwamba sikuzote Yehova anafanya yaliyo sawa—kutia ndani anapotabiri kuhusu wakati ujao.